Facebook Comments Box

Saturday, April 13, 2013

RUSHWA NI RAFIKI WA HAKI

 
Huu mjadala wa Katiba umeanza kusisimua kweli.  Laiti tungekuwa na muda zaidi, nadhani tungejifunza mengi.  Hebu ona barua hii.

Wewe Makengeza,
Wewe kwa kweli unakuwa kipofu.  Katika kulilia mavi ya kale unashindwa kuona mazuri yaliyopo.    Si binadamu tu wanaobadilika kulingana na wakati, hata nchi inapaswa kufanya hivyo, bila unafiki, bila kificho.
Hebu tuchukue mfano wa katiba yetu iliyopitwa na wakati.  Yaani bado inatangaza kwamba tunafuata siasa ya Ujamaa na Kujitegemea.  Nani anadanganyika na uongo huo?  Labda vijana ambao wanafikiri Azimio la Arusha linahusu ujenzi wa barabara mjini na kwamba ujamaa maana yake ni kusaidiana kukwapua yanayokwapulika.  
Ujamaa ni hujumaaa!  Bila kusahau kwamba kujitegemea ni kutafuta wafadhili na mafedhuli wengi iwezekanavyo kutoka nje.   Haisaidii!
Kwa hiyo, si vizuri kuendelea kuwa na maneno tata ndani ya katiba.  Lazima kuwa na dira ya kutuongoza na hata kututongoza tukubali kujitoa na kujitosa katika maendeleo ya nchi yetu changa ya macho.
Ndiyo.  Hebu angalia uchaguzi unavyoendelea kwa sasa kupata wajumbe wa mabaraza ya kata.  Ni wajumbe tu wa mabaraza ya kata wenye lengo la kutoa mawazo kuhusu katiba yetu iweje.   Lakini badala ya watu kujinadi kwamba wana mawazo haya au yale kuhusu katiba, wanatwangana ngumi kwa misingi ya makundi ndani ya chama hiki au kile.
Waliofanikiwa kuchaguliwa kwenye ngazi ya mtaa wanadaiwa rushwa ili wapite kwenye ngazi ya kata na kadhalika.   Bila kuhonga, hata nafasi ya kuchangia Katiba Mpya huwezi kupata.
Kwa hiyo, waliofikiria kwamba Katiba ni suala la kuwatafuta watu wenye mawazo chanya ili kuwa na Katiba ambayo itatulinda sisi wa kizazi hiki pamoja na vizazi vijavyo vyote wanajidanganya.   Au tuseme kwamba wanaogombea nafasi hizo za kuingia kwenye mabaraza ya kata wameelewa kitu cha msingi sana kuliko wasomi wote wanaobwatia nadharia.  Mchakato wa katiba ndiyo dira ya Katiba.  
Bila rushwa, nchi yetu haiwezi kuendelea.  Naamini kwamba wananchi wote wameelewa hivyo ndiyo maana wanaendelea kubariki mtindo huu wa kupata wajumbe na mambo mengine yote ndani ya jamii yao.  Msingi huo ni wazi pia.  Nikilinyamazia jambo fulani maana yake nimelikubali.
Kwa hiyo napenda kutangaza kwamba katika misingi ya taifa inayoorodheshwa ndani ya Katiba, itangazwe rasmi kwamba ‘Tanzania ni nchi ya rushwa na kujitafutia’.   Kwa njia hiyo,  tunakuwa mfano bora wa uwazi na ukweli na pia tunaweza kuwashughulikia watu wahafidhina kama wewe mnaotaka kurudisha nyuma maendeleo ya nchi.  
Hebu tutafakari kidogo.  Juzi, nilipanda daladala kwenda vijijini. Wakati tunaanza safari jamaa mmoja alikuwa anamcheka mwimbaji maarufu eti analalamika kwamba wimbo wake hauchezwi na kituo cha redio kwa kuwa hajatoa hela.
‘Hajui methali isemayo ‘Penya udhia tia rupia’!’

SOURSE: MWANANCHI


Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU