
Wewe Makengeza,
Wewe kwa kweli unakuwa kipofu. Katika kulilia mavi ya kale unashindwa kuona mazuri yaliyopo. Si binadamu tu wanaobadilika kulingana na wakati, hata nchi inapaswa kufanya hivyo, bila unafiki, bila kificho.
Hebu tuchukue mfano wa katiba yetu iliyopitwa na 
wakati.  Yaani bado inatangaza kwamba tunafuata siasa ya Ujamaa na 
Kujitegemea.  Nani anadanganyika na uongo huo?  Labda vijana ambao 
wanafikiri Azimio la Arusha linahusu ujenzi wa barabara mjini na kwamba 
ujamaa maana yake ni kusaidiana kukwapua yanayokwapulika.  
Ujamaa ni hujumaaa!  Bila kusahau kwamba 
kujitegemea ni kutafuta wafadhili na mafedhuli wengi iwezekanavyo kutoka
 nje.   Haisaidii!
Kwa hiyo, si vizuri kuendelea kuwa na maneno tata 
ndani ya katiba.  Lazima kuwa na dira ya kutuongoza na hata kututongoza 
tukubali kujitoa na kujitosa katika maendeleo ya nchi yetu changa ya 
macho.
Ndiyo.  Hebu angalia uchaguzi unavyoendelea kwa 
sasa kupata wajumbe wa mabaraza ya kata.  Ni wajumbe tu wa mabaraza ya 
kata wenye lengo la kutoa mawazo kuhusu katiba yetu iweje.   Lakini 
badala ya watu kujinadi kwamba wana mawazo haya au yale kuhusu katiba, 
wanatwangana ngumi kwa misingi ya makundi ndani ya chama hiki au kile.
Waliofanikiwa kuchaguliwa kwenye ngazi ya mtaa 
wanadaiwa rushwa ili wapite kwenye ngazi ya kata na kadhalika.   Bila 
kuhonga, hata nafasi ya kuchangia Katiba Mpya huwezi kupata.
Kwa hiyo, waliofikiria kwamba Katiba ni suala la 
kuwatafuta watu wenye mawazo chanya ili kuwa na Katiba ambayo itatulinda
 sisi wa kizazi hiki pamoja na vizazi vijavyo vyote wanajidanganya.   Au
 tuseme kwamba wanaogombea nafasi hizo za kuingia kwenye mabaraza ya 
kata wameelewa kitu cha msingi sana kuliko wasomi wote wanaobwatia 
nadharia.  Mchakato wa katiba ndiyo dira ya Katiba.  
Bila rushwa, nchi yetu haiwezi kuendelea.  Naamini
 kwamba wananchi wote wameelewa hivyo ndiyo maana wanaendelea kubariki 
mtindo huu wa kupata wajumbe na mambo mengine yote ndani ya jamii yao.  
Msingi huo ni wazi pia.  Nikilinyamazia jambo fulani maana yake 
nimelikubali.
Kwa hiyo napenda kutangaza kwamba katika misingi 
ya taifa inayoorodheshwa ndani ya Katiba, itangazwe rasmi kwamba 
‘Tanzania ni nchi ya rushwa na kujitafutia’.   Kwa njia hiyo,  tunakuwa 
mfano bora wa uwazi na ukweli na pia tunaweza kuwashughulikia watu 
wahafidhina kama wewe mnaotaka kurudisha nyuma maendeleo ya nchi.  
Hebu tutafakari kidogo.  Juzi, nilipanda daladala 
kwenda vijijini. Wakati tunaanza safari jamaa mmoja alikuwa anamcheka 
mwimbaji maarufu eti analalamika kwamba wimbo wake hauchezwi na kituo 
cha redio kwa kuwa hajatoa hela.
Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog