Facebook Comments Box

Sunday, July 14, 2013

MAWAIDHA: SHEIKH RASHID AL-SHUKERY - MOYONI HADI MOYONI




SHEIKH WA WILAYA YA ARUMERU AMWAGIWA TINDIKALI

  
 
Sheikh Said Juma Makamba akiwa hospitali
Shekhe Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Said Juma Makamba amejeruhiwa vibaya kwa kumwagiwa maji yanayohisiwa kuwa tindikali na watu wasiojulikana juzi usiku akiwa nyumbani kwake jijini Arusha.

Shekhe Makamba, ambaye amelazwa katika Wodi ya Majeruhi kwenye Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru, amejeruhiwa vibaya maeneo ya usoni, kifuani na mgongoni huku akiendelea na matibabu.

Akizungumza kwa tabu, shekhe huyo alisema tukio hilo lilitokea saa 5 usiku wa kuamkia jana nyumbani kwake kwa Mromboo Arusha, wakati akijiandaa kulala baada ya kutoka kuswali Swala ya Tarawei.

Shekhe Makamba ambaye pia ni Imamu wa Msikiti wa Sekei mjini Arusha, alisema baada ya swala hiyo alirejea nyumbani kwake akisindikizwa na vijana wawili ambao walikuwa wakiswali pamoja na kuingia ndani ya nyumba yake ili kulala.

Alisema hata hivyo, kabla ya kulala alikwenda kujisaidia katika choo cha nje na kwamba wakati akirudi ili aingie ndani akipitia nyuma ya nyumba ghafla alimuona mtu akiwa amesimama jirani na mlango.

Alieleza kuwa wakati akitaka kumwangalia zaidi alishtukia mtu

 huyo akiinua mkono na kumwagia maji yaliyompatia maumivu makali usoni na kifuani.

‘’Wakati natoka msalani nikipitia uwani kwangu niliona kama mtu ameinama pembeni yangu wakati najaribu kumsogelea ili nijue ni nani nilihamaki mtu huyo akinimwagia maji yaliyonisababisha maumivu makali sana yenye asili ya moto na ngozi kuanza kubabuka,’’ alisema shekhe huyo.

Aliongeza kuwa baada ya tukio hilo alianza kupiga kelele kuomba msaada ambapo majirani walijitokeza na kumpa msaada wa kumpeleka hospitali, kwa vile wakati huo macho yake yalikuwa hayaoni na wakati wote alikuwa  akilia.

Pamoja na kujeruhiwa vibaya sehemu za usoni, kifuani na  mgongoni, pia ana majeraha  kwenye mikono na machoni na hali yake bado ni mbaya japo madaktari wanaendelea kumpatia matibabu.

Kaimu Katibu wa Bakwata Mkoa wa Arusha, Abdallah Masoud akizungumzia tukio hilo alieleza kushitushwa nalo akisema limefanana na lile la Katibu wa Bakwata Mkoa wa Arusha, Abdulaziz Jonjo ambaye mwaka jana alilipuliwa kwa bomu nyumbani kwake akiwa amelala.

Alisema kuwa matukio hayo yamekuwa yakijirudia huku wahusika wakishindwa kutiwa mbaroni na kudai kuwa matukio hayo yanahusiana na masuala ya kigaidi. Aliongeza kuwa pamoja na kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi, lakini wamekuwa hawapati matunda ya kukamatwa kwa watuhumiwa ingawa alisema wanajulikana.

Kwa upande wake,  Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas alisema polisi wameanza uchunguzi wa tukio hilo na kwamba taarifa zitatolewa pindi washukiwa watakapotiwa mbaroni kwani uchunguzi bado unaendelea na kwamba hakuna  mtu anayeshikiliwa hadi sasa.



FREEMAN MBOWE AVAMIWA NA POLISI USIKU WA MANANE

 
Freeman Mbowe
KUNDI la polisi wenye silaha za moto jana usiku walivamia nyumbani kwa Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe, kwa nia ya kumkamata.

Askari hao wanaokisiwa kufikia saba, wakiwa na silaha nzito katika gari la wazi waliwasili nyumbani kwa Mbowe majira ya saa saba na nusu usiku na kuwaamuru askari wanaolinda nyumbani kwake kumtoa Mbowe nje ili waonane naye.

Walinzi wa Mbowe walihoji uhalali wa ukamataji huo na kuwataka polisi wawaoneshe hati ya kumkamata, lakini hawakuweza kuionesha, hali iliyozusha wasiwasi kwa walinzi wa kiongozi huyo.

Hata hivyo walinzi hao waliwaambia polisi hao kuwa Mbowe ambaye pia ni kiongozi mkuu wa kambi ya upinzani bungeni alikuwa safarini, jibu ambalo lilipokewa kwa shingo upande na askari hao.

Polisi hao baada ya kuona wameshindwa kukamilisha kazi hiyo, waliwaachia walinzi hao namba ya simu 0754-085600 ya Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni, Ernest Kimola, wakiwaagiza 
kuhakikisha wanamwambia Mbowe awasiliane na kamanda huyo.

Hata hivyo, alipohojiwa na Tanzania Daima Jumapili kwa njia ya simu, Mkuu wa Upelelezi Kimola aligoma kuzunguzia suala hilo na kumtaka mwandishi kuwasiliana na mkuu wake wa kazi, ambaye ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Kamilius Wambura, akidai ndiye mwenye haki ya kutoa ufafanuzi wa jambo hilo.

“Unajua mimi si msemaji wa polisi, wasiliana na kamanda wa mkoa, maana ndiye mwenye uwezo wa kutoa maelezo,” alisema Kimola na kukata simu. Lakini alipopigiwa simu Kamanda Wambura aliruka kimanga, kwa mshangao, akidai kutojua lolote kuhusiana na polisi kuvamia nyumbani kwa Mbowe.

“Kwa kweli ndiyo napata taarifa hizo kutoka kwako, kuwa kiongozi huyo alifuatwa na polisi, maana silijui suala hilo hata kidogo,” alisema Wambura, naye kama alivyofanya Kimola akakata simu.

Lakini wakati Kimola akikataa kusema chochote, Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, alisema kuwa alizungumza kwa njia ya simu na Kimola kuhusiana na kitendo cha polisi kuvamia nyumbani kwa kiongozi huyo wa juu wa kisiasa, na kudai kupewa majibu ya kushangaza.

Akizungumza jana katika mkutano wa hadhara uliofanyika Manzese, Wilaya ya Kinondoni, Dk. Slaa alisema Kimola alijitetea akidai kwanza kukana kufika nyumbani kwa Mbowe usiku wa manane. Pili, alisema kuwa hawakwenda kumkamata Mbowe, isipokuwa kufanya naye mazungumzo na kisha wangemwacha.

Slaa alisema kitendo hicho kimewashitua na ni cha kinyama na kilichokiuka sheria za nchi na haki za binadamu. Aliongeza kwamba, daima wamekuwa wakilishutumu Jeshi la Polisi kwa kutumika vibaya kukandamiza wapinzani, lakini mara zote CHADEMA kimepuuzwa na sasa jeshi hilo limeamua kuvamia makazi ya viongozi wa kisiasa kwa madhumuni yasiyoeleweka.

Alisema haijulikani nini kingetokea ikiwa Mbowe angekuwa ndani, ikiwa walinzi wangeamua kugoma kumwachia kiongozi wao. “Tuna hofu kubwa na usalama wetu, maana pale wangeweza kufanya lolote, hata kumuua na kisha kutoa matamshi kuwa walikuwa wanajibishana kwa risasi, kama ambavyo imekuwa jadi ya askari polisi kutoa taarifa za uongo na upotoshaji wanapoua watu,” alisema Slaa.

Alisema ikiwa polisi walikuwa na shida ya kweli, wangemwita kwa njia sahihi na si kumvamia na kuingilia uhuru wake na wa familia yake kama wanakamata gaidi ama jambazi hatari.

Dk. Slaa alisema Mbowe anayo ofisi inayojulikana, na kama kweli hakukuwa na jambo baya lililopangwa na polisi hao wasingeweza kufanya uhuni kama walioufanya.

“Kama wanaweza kuvamia nyumbani kwa kiongozi mkubwa kama Mbowe wakiwa na silaha nzito, itakuwaje kwa viongozi wa kawaida na raia?” alihoji Slaa.

Kutokana na tukio hilo la kuogofya, CHADEMA imemtaka Rais Jakaya Kikwete kuwaeleza Watanzania maana ya matukio haya ambayo yamedhamiria kuleta vurugu kubwa nchini. Kadhalika, wamemtaka Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Said Mwema, kuueleza umma kile kilichokusudiwa na askari wake kuvamia nyumbani kwa Mbowe mithiri ya jambazi.

Itakumbukwa pia kuwa hivi karibuni askari polisi wa Mkoa wa Arusha walivamia nyumbani kwa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, wakiwa na silaha nzito na mbwa, na kumkamata, kisha kumtupa rumande kwa siku nzima.


---Imenukuliwa kutoka TANZANIA DAIMA


 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU