Facebook Comments Box

Tuesday, November 6, 2012

HII NDIO SIRI NDANI YA SIMBA



Kipa wa Simba,Juma Kaseja.

KOCHA MKUU wa Simba, Milovan Cirkovic ameapa kuendelea kumtumia kipa Juma Kaseja mechi zote huku bosi wa makipa, James Kisaka naye akiweka wazi hali ya mambo na kilichotokea Simba ikaondoka kileleni mwa Ligi Kuu Bara.

Milovan ametamka hivi: "Sijui kitu gani tumekutana nacho maana tunarekebisha makosa kwenye mazoezi wakiingia uwanjani kwenye mechi wanarudia tena, nashindwa kuelewa."

Lakini Kocha wa Makipa, Kisaka amesema bao alilofungwa, Juma Kaseja na Hussein Javu wa Mtibwa Sugar na timu yake kulala mabao 2-0 juzi Jumapili ni makosa yake na sasa kazi aliyonayo ni kurudisha imani kwa mashabiki wake ingawa amesisitiza hajashuka kiwango na kuwataka mashabiki wakumbuke fadhila.

Milovan amesema ataendelea kumtumia kwenye kikosi chake kwa sababu anaamini ndiye kipa bora zaidi ya wote. Kisaka amesema kutokana na uzoefu wake na idadi ya mabao 10, Kaseja aliyofungwa katika mechi za Ligi Kuu Bara ni uzembe wa mabeki na makosa ya kawaida.

"Wanaposema, Kaseja ameshuka kiwango siyo kweli kwa sababu aina ya mabao aliyofungwa si makosa yake ni safu nzima ya ulinzi. Kwanza Simba ilikuwa na tatizo la beki, mabao yaliyofungwa yalikuwa yanasababishwa na beki. Pili, kumekuwa na makosa ya kutoelewana kwa safu nzima ya ulinzi," alisema Kisaka.

"Lakini hili la pili tulilofungwa na Mtibwa linaweza kuwa ni makosa yake kwa sababu alienda kucheza mpira kwa kupiga chenga na adui akatumia udhaifu mwanya huo kumnyang'anya na kufunga.

"Unajua mashabiki wamekuwa wakisubiri kuona ubaya tu wazungumze na hawakumbuki fadhila ambazo Kaseja alizifanya kwa kipindi chote cha ushindi. Kaseja alifanya juhudi binafsi tukashinda beki ilikuwa haieleweki lakini hilo hawajui na kuangalia kosa hili la leo na kumpa wakati mgumu kufanya kazi ya ziada ili kurudisha imani kwa mashabiki wake.

"Naamini, Kaseja ndiye kipa bora zaidi ya wote kikosini ndiyo maana nampa nafasi ya kudaka mechi zote, makosa yanatokea ni hali ya kawaida hata hivyo nitaendelea kumtumia kwenye mechi zangu," aliongeza Milovan.
Hata hivyo, Kaseja aliyekuwa katika wakati mgumu na huzuni, aligoma kuzungumza lolote.

Matokeo hayo ambayo yaliipa Yanga mwanya wa kuongoza ligi yalimtoa machozi Kaseja haswa baada ya mashabiki kuonyesha kutokuwa na imani naye na kumuimbia nyimbo za kumdhihaki.

Hali halisi
Kwa mujibu wa duru za ndani ya Simba, uwezekano wa Milovan kukaa benchi la ufundi kwenye mzunguko wa pili wa ligi ni mdogo kwa kuwa hajatimiza malengo ambayo uongozi ulimtaka kushinda mechi zote nne dhidi Azam, Polisi Morogoro, Mtibwa na Toto African.

Aliishinda Azam mabao 3-1, akatoa suluhu na Polisi kabla ya kufungwa mabao 2-0 na Mtibwa juzi Jumapili na Jumapili ana kibarua cha Toto jijini Dar es Salaam.

Msimu uliopita Moses Basena alitimuliwa Simba baada ya kumaliza mzunguko wa kwanza akiwa na pointi 28 wakati Milovan akishinda mechi ya mwisho atamaliza na 26.

Habari zinapasha kuwa viongozi wa juu wa Simba jana Jumatatu walijadiliana hali ya mambo ingawa hawakutaka kutoa ufafanuzi wowote.

Hali ya kutoaminiana na pia kutopendana kwa baadhi ya wachezaji, chokochoko za ndani ya uongozi imedaiwa kuwa ni chanzo cha matokeo hayo ingawa wachambuzi wa mambo wanaeleza sare za Simba ni kutokana na uchakavu wa viwanja na morali ndogo ya timu.

Simba imetoka suluhu mechi mbili za Tanga dhidi ya Coastal Union na JKT Mgambo, kabla ya kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya timu dhaifu na inayochukia kushinda mechi ya Polisi Morogoro na juzi juzi huko huko Morogoro ikapigwa mabao 2-0 na Mtibwa.

Habari za ndani zinadai baadhi ya wachezaji wamekuwa wakiogopana kwa imani za kishirikina na wengine hawaongei kabisa wala kupeana pasi uwanjani.

Habari zinadai pia hata kucheza mechi nyingi kwa Kaseja peke yake hakuwafurahishi baadhi ya wachezaji ambao wanadai amechoka ndiyo maana inafika wakati anafungwa magoli laini ambayo Wilbert Mweta asingefungwa.

Suala la Kaseja limeonekana gumu kwani viongozi pamoja na makocha wanamkubali mno na wala hawana mpango wa kumweka benchi licha ya kelele za wanachama.

Jingine kubwa ni kwamba baadhi ya wachezaji wanadai kocha Milovan anaingiliwa na baadhi ya viongozi ambao wanamlalamikia kwa kutotoa nafasi kwa wachezaji wengi vijana na badala yake kuendelea kung'ang'ania walewale.


KATIBU WA MUFTI ZANZIBAR AMWAGIWA TINDIKALI

Watu mbalimbali wakiaangalia Katibu wa mufti Zanzibar Fadhili Soraga akipelekwa Hospitali baada ya kumwagiwa Tindikali na watu wasiojulika. Katibu alikuwa akifanya mazoezi kwenye viwanja vya mwanakwerekwe

Hapa akipelekwa kwenye chumba cha huduma ya kwanza hospitali ya mwanakwerekwe

Hapa akipandishwa kwenye gari ili awahishwe Muhimbili Hospital dar es Salaam


MUUWAJI WA KAMANDA BAROW ALIHUDHURIA MAZISHI YAKE

POLISI mjini Mwanza imebaini kuwa mmoja wa watuhumiwa wa mauaji ya aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Liberatus Barlow, alikwenda kuaga mwili wa Kamanda huyo katika uwanja wa Nyamagana sambamba na wananchi wengine. Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, Lily Matola jana alimtaja mtuhumiwa huyo kuwa ni Abdallah Petro ‘Ndayi’ (32) mkazi wa Mjimwema mjini hapa ambaye anashikiliwa Polisi. Kwa mujibu wa Kamanda Matola, Petro mbali na kutajwa kuhusika na mauaji hayo, pia anadaiwa kuwa na rekodi ya kufungwa miaka 30 jela katika gereza la Butimba kwa unyang’anyi wa kutumia silaha mwaka 2006. Alitoka gerezani mwaka 2010 baada ya kukata rufaa Mahakama Kuu ya Tanzania. Petro pia imebainika pia kuwa ni mdogo wa mtuhumiwa wa kwanza katika kesi hiyo, Muganyizi Peter. Vielelezo vyakamatwa Kamanda Matola alisema mbali na kuwa na uhusiano huo, Petro na mtuhumiwa mwingine, Abdurahim Ismail Athuman ‘Dula’ (28) mkazi wa Mkudi Ghana, pia mjini hapa, baada ya kukamatwa kwa nyakati tofauti Mjimwema na Kilimahewa mwishoni mwa wiki, waliwapeleka polisi mahali walikoficha baadhi ya mali za marehemu. Mali wanazodaiwa kuonesha polisi ni pamoja na redio ya mawasiliano ya Polisi na funguo za gari alilotumia kamanda Barlow siku ya tukio la mauaji yake. Kamanda Matola alisema watuhumiwa waliwapeleka polisi katika shimo la majitaka kwenye maeneo ya Nyanshana, jijini Mwanza walipokuwa wameficha vitu hivyo. Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Joseph Konyo alisema watuhumiwa baada ya kutimiza uhalifu, walitenganisha redio hiyo ya mawasiliano ili isipatikane. “Damu ya mtu haipotei bure, hayo yote ni pamoja na Mungu mwenyewe, kwani sisi peke yetu hatuwezi, wananchi mmetusaidia sana,” alisema Kamanda Konyo. Baada ya kuonesha polisi vitu hivyo ambavyo sasa vimechukuliwa kama vielelezo katika kesi ya mauaji ya Barlow, Kamanda Matola alisema watuhumiwa hao walipekuliwa na kukutwa pia na kadi tatu za simu za Vodacom na Airtel, simu ya mkononi, viatu vya ngozi na begi dogo. Pia walikutwa na kofia mbili za kijeshi aina ya bereti; moja ikiwa ya Polisi na nyingine ya kampuni ya binafsi ya ulinzi, sare za kampuni ya ulinzi, mtarimbo, bisibisi, mapanga, televisheni mbili, sub-hoofer na deki. Alisema walipohojiwa, walidai wamekuwa wakihifadhiwa na Ryoba Matiku ‘Mama Nyangi’ katika eneo la Nyakabungo Miembeni ambako mipango yote ya uhalifu imekuwa ikisukwa. Mama huyo anashikiliwa pia kwa mahojiano.

HATIMAYE SERIKALI YASEMA TPI WALITENGENEZA ARV FEKI

LICHA ya wamiliki wa kiwanda cha Tanzania Pharmaceutical Industries Limited (TPI) kukana kutengeneza na kusambaza dawa bandia za kupunguza makali ya UKIMWI, serikali imethibitisha kuwa kiwanda hicho ndicho kilitengeneza dawa hizo aina ya TT-VIR 30 yenye toleo Na OC.01.85. Kauli hiyo ilitolewa bungeni jana na Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Seif Rashid, akisema kuwa serikali itawachukuliwa hatua za kisheria wote waliohusika katika suala hilo. Alisema kuwa katika kuhakikisha kuwa suala hilo hatari linapatiwa ufumbuzi wa kudumu na kuzuia lisitokee tena, kabla ya kuchukua hatua hizo za kisheria uchunguzi unafanywa kupitia vyombo vya usalama. Dk. Rashid alikiri kuingia katika mzunguko kwa dawa hizo bandia lakini akawatoa hofu wagonjwa wote wanaotumia (ARV’s) kuwa dawa zinazopatikana kwenye vituo vya kutolea huduma hiyo kwa sasa ni salama na zenye viwango vinavyotakiwa. “Tunatoa wito kwamba waendelee kutumia dawa hizo kama wanavyoshauriwa na madaktari… kupitia Wizara ya Afya, serikali imehakikisha uwepo wa dawa za kutosha na kupunguza makali ya ukimwi katika vituo vyote vya kutolea huduma za afya,” alisema. Dk. Rashid alifafanua kuwa Wizara ya Afya hununua dawa hizo kupitia Bohari ya Dawa (MSD), ambayo imepewa jukumu la kununua, kuzitunza na kusambaza katika vituo vya kutolea huduma za afya. Alisema kwa hapa nchini kuna kiwanda kimoja tu cha TPI kinachotengeneza dawa hizo na kwamba zile za bandia zilibainika mwanzoni mwa Agosti mwaka huu katika ukaguzi wa kawaida wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) katika Hospitali ya Tarime. Alisema baada ya ukaguzi na uchunguzi kwenye vituo vyote vya huduma za afya katika mkoa wa Mara na nchi nzima ilibainika kuwa dawa yenye jina la biashara TT-VIR 30 toleo namba 0C.01.85 ni bandia. Alisema pia ilibainika kuwa nyaraka zilizokutwa katika Bohari ya Dawa (MSD) zinaonyesha kuwa TPI iliiuzia MSD dawa hiyo bandia toleo namba 0C.01.85. Naibu Waziri huyo aliongeza kuwa uchunguzi ulibaini kuwa dawa hiyo bandia ilikuwa na dawa zenye rangi tatu tofauti, njano, nyeupe na vidonge vya rangi mbili tofauti za pinki na nyeupe. Kwa mujibu wa Naibu Waziri huyo wa Afya, dawa zilizokuwa na rangi ya njano, zilikuwa na kiambata cha Efaverenz badala ya viambata aina ya Nevirapine, Lamivudine na Stavudine vinavyopaswa kuwemo. Aidha vidonge vyenye rangi nyeupe na vile vyenye rangi ya pinki na nyeupe vilikuwa na viambata vinavyotakiwa kuwepo yaani Nevirapine, Lamivudine na Stavudine kama ilivyokuwa kwenye lebo. Akielezea kuhusu hatua zilizochukuliwa na serikali baada ya matokeo hayo ya uchunguzi alisema ni pamoja na kusimamisha mara moja matumizi ya dawa hizo aina ya TT-VIR 30 toleo Na 0C.01.85. Hatua nyingine ni pamoja na kusitisha uzalishaji wa dawa zote katika kiwanda cha TPI Ltd hadi uchunguzi wa suala hilo utakapokamilika ikiwa ni pamoja na kujiridhisha tena ubora wa dawa inazozalisha. Alisema pia vigogo wa MSD akiwamo mkurugenzi wake walisimamishwa na kwamba wizara imeunda timu ya wataalamu kwa lengo la kufuatilia mwendelezo wa tiba na matunzo kwa wagonjwa wa UKIMWI.

 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU