
 

 

 
 
WAKATI mbunge wa Iringa Mjini (CHADEMA), Mchungaji Peter Msigwa, 
akimtuhumu Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki, 
kuibeba kampuni ya uwindaji ya Leopard Tours Ltd, mwenyewe amejibu 
mapigo akidai mbunge huyo hajafanya utafiti.
Msigwa aliwaambia 
waandishi wa habari jana mjini Dodoma kuwa Kagasheki alitumia nafasi 
yake kuiarifu kampuni hiyo kuipatia ekari tano kwa gharama ya dola za 
Kimarekani 30,000 nusu ya gharama za kawaida dola 60,000 kwa ekari kumi.
Mbunge
 huyo ambaye pia ni msemaji mkuu wa kambi ya upinzani kwa wizara hiyo, 
alisema kuwa Kagasheki anaendesha wizara kwa kukiuka sheria na taratibu 
akitumia mamlaka vibaya.
Msigwa alisema kuwa Kagasheki tangu 
alipoingia madarakani na kuivunja Bodi ya Mamlaka ya Hifadhi ya 
Ngorongoro (NCAA), sasa hifadhi inaendeshwa bila bodi jambo ambalo ni 
kinyume.
Alidai kuwa waziri huyo alifanya maamuzi hayo ya kuibeba
 kampuni hiyo ya uwindaji bila kuzingatia sheria na kanuni za ugawaji wa
 vitalu na kwamba alivunja sheria kwa kufanya uamuzi wa moja kwa moja na
 Leopard Tours wa kushusha viwango vilivyowekwa kisheria bila kutoa 
tangazo la serikali.
Msigwa pia aliibua tuhuma nyingine akidai kuwa Kagasheki ama kwa makusudi au kutokujua kuwa ana 
  
 
 
  
maslahi binafsi
 ya mahusiano na mbunge wa viti Maalumu wa Mkoa wa Arusha, Catherine 
Magige (CCM), na kumkingia kifua ili taasisi yake ya Catherine 
Foundation ipate msaada wa sh milioni 10 kutoka NCAA.
“Msaada
 huo si tu ulikiuka kanuni za msaada ambao unaelekezwa katika shughuli 
za msaada wa kijamii kupewa kiasi kisichozidi sh milioni 2 lakini mradi 
huo wa Catherine ulipewa fedha hizo huku dokezo la maombi ya msaada huo 
likionyesha watendaji wa NCAA wakilalamika. Walitoa mapendekezo mara 
mbili, kwanza kwa kupitia meneja wa maendeleo ya jamii kuwa hakuna 
bajeti ya kusaidia msaada huo kutoka idara ya maendeleo ya jamii labda 
wafikiriwe kupitia fungu la donesheni,” alieleza Msigwa.
Aliongeza kuwa nyaraka zinaonyesha kwamba kaimu mhifadhi wa Ngorongoro, alimjibu meneja maendeleo ya jamii kuwa fungu la donesheni halina fedha za kutosha, hivyo ni bora Magige ajibiwe na asubiri mpaka mwaka wa fedha ujao.
Msigwa
 alifafanua kuwa dokezo hilo lilisainiwa Desemba 14 mwaka jana: “Jambo 
la kushangaza na kutia walakini ni kuwa kaimu mhifadhi kwa shinikizo 
alimuelekeza mhasibu kuilipa Catherine Foundation kiasi cha milioni 10 
kwa ajili ya ununuzi wa madawati 18 Juni, mwaka huu, ukiwa ni mwaka wa 
fedha wa 2012/13 kinyume na mapendekezo yake ya awali.”
Alisema
 kuwa wanataka kujua kaimu mhifadhi alitumia kigezo gani kuilipa taasisi
 hiyo fedha hizo za msaada wa ununuzi wa madawati tofauti na kiwango 
kilichowekwa cha sh milioni 2.
Kagasheki ajibu
Akijibu
 tuhuma hizo, Kagasheki alisema kuwa anamfahamu Msigwa kwa vile hiyo si 
mara yake ya kwanza kutoa tuhuma za uongo dhidi yake: “Msigwa alishawahi
 kusema nijiuzulu kwamba nimeshindwa kushughulikia ujangili kwa kuwa eti
 nashughulika na watu wadogo (dagaa) na kuwaacha mapapa (viongozi),” 
alisema.
Kagasheki alifafanua kuwa 
tatizo analoliona kwa Msigwa ni kukurupuka bila kufanya utafiti wa kina 
na kuanza kutuhumu watu kwa sababu binafsi anazozijua yeye: “Msigwa ana 
chuki na mimi na hii ilitokana na yeye kuondolewa kwenye Kamati ya Bunge
 ya Ardhi, Maliasili na Mazingira; anadhani nilishawishi aondolewe kumbe
 yalikuwa matakwa ya Spika,” alisema.
Alisisitiza
 kuwa kwa vile Msigwa amejitokeza kuisemea Ngorongoro ni dhahiri sasa 
anaamini tetesi zilizopo dhidi yake kuwa anatumika kuwatetea vigogo 
walioondolewa kwa tuhuma za ufisadi: “Ngorongoro kuna ufisadi wa 
kutisha, subirini kidogo ripoti yake inakamilika mtajionea hao watu 
anaowatetea walifanya nini huko,” alisema.
Kuhusu
 madai ya kuibeba kampuni ya uwindaji, Kagasheki alisema kuwa mwindaji 
huyo amekuwa nchini akifanya kazi zake kihalali na kutoa ajira kwa 
wazawa na kwamba uamuzi wake ulikuwa wa busara kwani NCAA walitaka 
kumchakachua: “Huyu aliomba eneo kujenga kambi lakini lililopatikana 
halikufikia hata nusu sasa wakawa wanataka kumuuzia kila kilomita kwa 
dola 60,000 ndipo nikaagiza auziwe kwa nusu yake. Hapa nilifanya kosa 
gani wakati nilidhibiti ufisadi?” alihoji.
Alisisitiza
 kuwa tayari anazo taarifa za Msigwa kutumiwa na kundi linalompiga vita 
ndani ya wizara hiyo na kaapa kwamba kamwe hawatashinda.
Kuhudu
 madai ya kuishinikiza NCAA kumpa msaada Magige, waziri huyo alisema 
maneno hayo ni ya kitoto zaidi kwani kama angetumia wadhifa wake 
kumkingia kifua asingepewa fedha kidogo kiasi hicho: “Ni kweli Magige 
ana taasisi yake na wamekuwa wakiomba fedha maeneo mengi kusadia yatima 
na wahitaji wengine lakini sina taarifa kama hata aliomba fedha NCAA; 
Msigwa ana ajenda yake,” alisema.
Magige awaka
Akizungumzia
 tuhuma hizo, Magige alisema taasisi hiyo ni kama zingine na hivyo 
kumshangaa Msigwa kuihusisha na mahusiano binafsi ya watu.
Alikiri
 kuomba msaada NCAA na kupewa kiasi hicho cha sh milioni 10 lakini 
akasema huo ni uamuzi wao kwani hawakuwapangia kiwango.
“Tuliandika
 barua ya maombi tukapeleka; ikakaa muda mrefu lakini baadaye wakatuita 
na kutupa msaada huo. Mimi nadhani kungelikuwa na shinikizo la waziri 
ningepewa fedha nyingi zaidi ya hizo! Msigwa ni mchungaji, sisi 
tunapaswa kujifunza ukweli kutoka kwake sasa iweje anasingizia watu na 
kuwazulia mambo ya uongo jamani? Amekumbwa na nini?” alihoji Magige.
Source: 
wavuti