Facebook Comments Box

Wednesday, August 21, 2013

WAMBURA AJITOA KWENYE KINYANG'ANYIRO CHA UCHAGUZI TFF


Aliyewahi kuwa mgombea wa Uchaguzi Mkuu Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) uliosimamishwa na Fifa, Michael Wambura, amesema hatashiriki tena kwenye uchaguzi ujao wa shirikisho hilo, Oktoba 27.
 
Awali Wambura, aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa FAT (sasa TFF), aliwania nafasi ya Makamu Rais katika uchaguzi uliosimamishwa na Shirikisho la Soka Ulimwenguni (Fifa), kutokana na kuwepo malalamiko kutoka kwa watu  walioenguliwa akiwamo yeye.
 
Jana TFF ilitangaza majina ya wagombea 58 wote ikiwa ndiyo siku ya mwisho  kurejesha fomu, lakini bila kuwepo kwa jina la Wambura ambaye  alipoulizwa na Mwananchi sababu ya kutogombea tena alisema: “Siwezi  kujisafisha na majitaka.”
 
“Nimeamua kupumzika, nilipigania haki imepatikana kwa kamati mbili kuundwa. Bila mimi kamati hizo zisingekuwapo, lakini jambo muhimu ni kwamba siwezi kujisafisha na majitaka,” alisema Wambura.
 
“Mfumo wa uongozi TFF ni mbovu, kumejaa siasa za majitaka, hizo kamati  zilizoundwa hazitafanya kazi kwa vile tu Wambura hayupo, ningekuwepo  zingepata kazi ya kufanya,” alitamba Wambura.
 
Nafasi ya Makamu wa Rais inawaniwa na Iman Madega, Ramadhan Nasib na  Walace Karia, huku wajumbe waliomba kuwakilisha kanda mbalimbali ni Abdallah Mussa, Kaliro Samson, Jumbe Magati, Mugisha Galibona, Vedastus  Lufano, Samwel Nyalla, Epaphra  Swai, Mbasha Matutu, Stanslaus Nyongo, Ally Mtumwa, Elley Mbise na Omari Walii. ni Ahmed Mgoyi, Yusuf Kitumbo, Ayoub Nyaulingo, Blassy Kiondo, Nazarius Kilungeja, Ayoub  Nyenzi, Cyprian Kuyava, David Lugenge, Elias Mwanjala, Eliud Mvela, John  Kiteve, James Mhagama, Kamwanga Tambwe na Stanley William Lugenge, Athuman Kambi, Francis Kumba, Zafarani Damoder.
 
Charles Komba, Hussein Mwamba, Stewart Masima, Farid Nahdi, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’, Riziki Majala, Twahil Twaha Njoki, Davis  Mosha na Khalid  Mohamed. Alex  Kamuzelya, Juma Pinto, Muhsin Balhabou, Omar Abdulkadir, Shaffih Dauda na Wilfred  Kidao. Kwa upande wa TPL Board waliojitokeza kuwania uongozi wa juu ni wawili Hamad Yahya (Mwenyekiti) na Said Muhamad Said (Makamu Mwenyekiti).Walioomba nafasi za ujumbe wa TPL Board ni Kazimoto Muzo, Michael  Kaijage, Omari Mwindadi, Salum Rupia na Silas Magunguma.
CHANZO:SHAFFIH DAUDA


TIMU ZOTE 14 ZAKABIDHIWA VIFAA KWA AJILI YA LIGI KUU YA VODACOM INAYOTARAJI KUANZA JUMAMOSI YA TAREHE 24/08/2013


Wadhamini wakuu wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Kampuni ya Vodacom Leo imekabidhi vifaa kwa timu zote 14 vyenye thamani ya Shilingi milioni 400.

Akizungumza kabla ya zoezi la kukabidhi vifaa hivyo kuanza, Mkurugenzi wa Mashindano wa TFF, Saad Kawemba pamoja na kuishukuru Vodacom kwa kutekeleza majukumu yake ya kimkataba amevitaka vilabu vya ligi kuu kuu ya Vodacom kuheshimu chapa ya mdhamini wakati wote wa mechi za ligi.

“Ninatoa wito kwa vilabu vyote kutumia jezi zenye nembo ya mdhamini kama kanuni zinavyo sema, pia ninawaomba viongozi wote tuwe na Ushirikiano katika kuhakikisha ligi inafanikiwa kama inavyotakiwa,”

Wawakilishi wa timu mbalimbali zinazoshiriki ligi kuu ya Vodacom Tanzania Bara, wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kukabidhiwa vifaa vya michezo na mdhamini wa ligi hiyo kampuni ya Vodacom tayari kwa ajili ya kuanza kwa msimu wa ligi kuu 2013/2014. Pamoja nao katika picha ni Mkuu  wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano wa kampuni  hiyo Kelvin Twisa,(Aliyeshikilia mpira) na Mkurugenzi  wa Mashindano wa TFF, Saad Kawemba.

Kama mzazi tusingependa kutumia kanuni na sharia kuadhibu klabu inayokwenda kinyume tunapenda kuona kila mmoja akimtendea haki mdhamini kama ambavyo nayeye anavyotimiza haki yake ya kutupatia vifaa hivi.”

Kwa upande wake Mkuu wa kitengo cha Masoko na Mawasiliano wa Vodacom, Kelvin Twissa alisema kuwa vifaa hivyo viko tayari na anaamini timu zote zimejiandaa vya kutosha na tayari kuingia katika mtanange wa ligi.

“Tunajisikia furaha sana kufikia hapa leo na kukabidhi vifaa hivi tukitekeleza matakwa ya mkataba wa udhamini, ni imani yetu kwamba timu zineshajiandaa vizuri na sasa tupo tayari kuanza msimu mpya wa 2013/2014.’Alisema Twissa

Twissa aliongeza kuwa vifaa vipya vilivyo kabidhiwa ni pamoja na seti za jezi mbalimbali, viatu vya mazoezi na mechi, soksi, vilinda ugoko (shin guards), nguo za mazoezi, nguo za kawaida, gloves na vifaa vingine.

Aidha, Pamoja na kukabidhi vifaa hivyo wao kama wadhamini wa ligi kuu pia wamefarijika kuona timu zote zimefanya maandalizi ya kutosha.

 “Hii ni  ishara tosha kuwa siku hadi siku ligi yetu imeendelea kuimarika na kuwa na ushindani mkubwa zaidi hakika tunajivunia kuwa sehemu ya mafanikio ya soka nchini,” alisema.

Twissa alihitimisha kwa kutoa wito kwa wadau wengine wenye malengo ya kukuza soka la Tanzania kujitokeza na kuongeza udhamini katika ligi ili kuleta tija zaidi huku akiendelea kuwakumbusha wanahabari wajibu wao wa kuitangaza ligi hususan vipaji.

CHANZO:BIN ZUBEIRY


KIM POULSEN AMEWAITA KAMBINI WACHEZAJI 24 KUIVAA GAMBIA



PICHA NA MAKTABA:

Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen amewaita kambini wachezaji 24 kujiandaa kwa mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia dhidi ya Gambia itakayochezwa Septemba 7 mwaka huu nchini humo.

Wachezaji hao wanatakiwa kuripoti kambini Agosti 29 mwaka huu kabla ya saa 1 kamili usiku. Kambi ya Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager itakuwa kwenye hoteli ya Accommondia jijini Dar es Salaam.

Makipa walioitwa katika timu hiyo Juma Kaseja (Huru), Mwadini Ali (Azam), Ally Mustafa (Yanga) na Aishi Manula (Azam). Mabeki ni Aggrey Morris (Azam), Kelvin Yondani (Yanga), Shomari Kapombe (Simba), Nadir Haroub (Yanga), Erasto Nyoni (Azam), Vincent Barnabas (Mtibwa Sugar) na David Luhende (Yanga).

Viungo Khamis Mcha (Azam), Salum Abubakar (Azam), Said Dilunga (Ruvu Shooting), Frank Domayo (Yanga), Athuman Idd (Yanga), Haruna Chanongo (Simba), Amir Kiemba (Simba), Mrisho Ngasa (Yanga), Simon Msuva (Yanga), John Boko (Azam), Thomas Ulimwengu (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo), Mbwana Samata (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo) na Juma Liuzio (Mtibwa Sugar).
CHANZO:TFF


SERIKALI YA RWANDA YATUPILIA MBALI USHAURI WA TANZANIA.


Mushikiwabo alisema wako tayari kuwapokea na kuwalinda wote waliofukuzwa Tanzania kwa kisingizio kuwa ni wahamiaji haramu, akieleza kwamba anasikitishwa kwa kuwa Tanzania haikufanya jitihada yoyote kuwasiliana na Rwanda kuhusu suala hilo kabla ya kuchukua uamuzi huo (HM).


"Ni uamuzi ambao umeshachukuliwa, hatukushirikishwa kwa namna yoyote na jukumu letu kama serikali na taifa ni kuwahakikishia ulinzi wote wanaokuja, na hili ndilo suala tunalolishughulikia kwa sasa," alisema.

Kwa mujibu wa gazeti la New Times, Mushikiwabo aliwaeleza waandishi wa habari kwamba agizo hilo la Rais Kikwete pamoja na ushauri wa kuitaka Serikali ya Rwanda kuzungumza na wanamgambo hasimu wa FDLR waliopo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), hayatayumbisha uhusiano imara baina ya Watanzania na Wanyarwanda.

"Sisi si majirani tu, tuna mfungamano imara baina ya watu wetu pia, tuna mfungamano wa damu, wa kibiashara, na mengine mengi ya kutufanya tuendelee kuwa pamoja," alisema na kutumia fursa hiyo kuwakaribisha Watanzania nchini Rwanda.

Watanzania wanaweza kuishi hapa kwa umri wowote wanaotaka. Tunawachukulia kuwa ni watu wetu muhimu kwenye fungamano la Jumuiya ya Afrika Mashariki," alisisitiza.

Rais Kikwete wakati akihitimisha ziara yake mkoani Kagera alitoa agizo la kuwataka wanaomiliki silaha kinyume cha sheria na wahamiaji haramu ama kuondoka au kuhalalisha ukazi wao, huku akitoa wiki mbili kwa zoezi hilo kutekelezwa, kabla ya kuanza kwa operesheni ya kuwasaka watu hao.

Kauli hiyo ilitokana na kushamiri vitendo vya kihalifu katika eneo la Kanda ya Ziwa, Rais hakutaja jina la nchi ya wahamiaji hao. Kwa ukanda huo Tanzania inapakana na Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi na DRC.

Pia, Rais Kikwete katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi alizungumzia kusikitishwa na kauli za shutuma, kejeli na udhalilishaji zilizotolewa na Rais Paul Kagame wa Rwanda dhidi yake.

Mvutano baina ya Rwanda na Tanzania ulianza kuwekwa hadharani Mei mwaka huu, baada ya Rais Kikwete kuishauri Rwanda kukaa na kuzungumza na FDLR wenye makao yao DRC, hatua ambayo haikuifurahisha Serikali ya Rwanda.

Wakati Rwanda ikieleza hayo jana Katibu Mkuu Kiongozi, Ombeni Sefue alizungumza na gazeti hili, na kutaka majibu ya kauli hiyo ya Rwanda yatolewe na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje, Mkumbwa Ally alisema kauli iliyotolewa na Rais Kikwete ilikuwa ni ushauri, kwamba Rwanda wanaweza kuukubali ama la.

"Kilichomkasirisha Rais Kikwete ni lugha za matusi zilizokuwa zikitolewa na viongozi wa Rwanda, ila kwa hicho walichokisema sidhani kama kitakuwa na tatizo kwetu," alisema Mkumbwa.

Alifafanua kwamba, alipokuwa mkoani Kagera Rais Kikwete hakutoa agizo la Wanyarwanda kufukuzwa, bali alitoa agizo la kuanza kwa operesheni ya kuwakamata wahamiaji haramu, wale wanaomiliki silaha kinyume na taratibu.

"Rais alizungumzia masuala ya jinai 'Criminal Element', siyo kuwafukuza Wanyarwanda," alisisitiza.

Hatutazungumza na FDLR
Waziri wa Mambo ya Nje, Louise Mushikiwabo, aliendelea kusema sera ya Rwanda kuhusiana na makundi ya aina hiyo, iko wazi na haitabadilika, kauli ambayo amekuwa akiirudia kila mara na kuwataka wote wanaofikiria kuhusu Rwanda kuzungumza na FDLR kwa namna yoyote kusahau wazo hilo.

"Kama umehusika kwa namna yoyote na maangamizi, wewe utakuwa adui wa kila mtu. Ni wazi kwamba Wanyarwanda wote watakuwa kwenye majonzi iwapo kwa namna yoyote kutakuwa na mawasiliano ya FDLR," alifafanua.

Kundi la FDLR ambalo ni kifupisho cha Democratic Forces for the Liberation of Rwanda, linaundwa na watu walioshiriki kwenye mauaji ya kimbari yaliyowalenga watu wa kabila la Watutsi mwaka 1994, na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 800,000 kwa miezi mitatu.

Kundi hilo ambalo limeweka makazi yake mashariki mwa DRC, linadaiwa kufanya mashambulizi kadhaa yakiwamo ya milipuko ya mabomu nchini Rwanda, ambapo mwezi uliopita shambulio la aina hiyo mjini Kigali lilisababisha vifo vya watu watatu na kujeruhi watu kadhaa.

Uhusiano wa kihistoria
Familia za Rwanda zikiwamo zilizoishi Tanzania tangu miaka ya 1950, zimeelezwa kuwa zimekuwa zikiwasili nchini humo kupitia mpaka wa Rusumo baada ya agizo la Rais Kikwete kuwataka wawe wameondoka ndani ya wiki mbili, kabla ya kuanza kwa operesheni rasmi ya kuwaondoa.

Kwa mujibu wa mamlaka nchini Rwanda, mamia ya Wanyarwanda waliokuwa wakiishi mkoani Kagera ambako ndiko Tanzania inapopakana na Rwanda wamekuwa wakirejea kwa wingi, ambapo hadi juzi, zaidi ya watu 300 walikuwa wameshaorodheshwa kwenye ofisi za Uhamiaji. CHANZO:MWANANCHI

KATIBU MTENDAJI MPYA WA SADC APOKELEWA KWA SHANGWE WIZARA YA MAMBO YA NJE


Mhe. Bernard K. Membe (Mb.), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa akimlaki kwa furaha Katibu Mtendaji mpya wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC),  Mhe. Dkt. Stergomena Lawrence Tax mara baada ya kuwasili Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
Mhe. Membe akimkabidhi shada la maua Dkt. Tax kwa niaba ya Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje mara baada ya kuwasili Wizarani hapo.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. John Haule nae akimkarisha Dkt. Tax kwa furaha Wizarani.
Mkurugenzi wa Kitengo cha Sheria katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Irene Kasyanju akimpongeza kwa shada la maua Dkt. Tax mara nbaada ya kuwasili Wizarani.

Dkt. Tax akipongezwa na kukaribishwa Wizarani na Naibu Katibu Mkuu, Balozi Rajabu Gamaha.
Balozi mpya  wa Tanzania nchini Ethiopia, Mhe. Naimi Aziz, nae pia aliungana na Wafanyakazi wa Wizara kumpongeza dkt. Tax. Anayeshuhudia pembeni ni Bw. Ali Mwadini, Katibu wa Naibu Waziri. 
Dkt. Tax akipongezwa na Bw. Omar Mjenga, Mkurugenzi Msaidizi, Idara ya Asia na Australasia huku Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Mipango, Bw. James Lugaganya (kushoto) akishuhudia.
Balozi Bertha Semu-Somi, Mkurugenzi wa Diaspora akimlaki kwa shangwe Dkt. Tax wakati wa mapokezi.
Mkurugenzi wa Idara ya Mashariki ya Kati, Balozi Simba Yahya nae akitoa pongezi zake za dhati kwa Dkt. Tax
Maafisa mbalimbali wa Wizara nao pia walikuwa mstari wa mbele kumpongeza Dkt. Tax.
Dkt. Tax akisaini Kitabu cha Wageni mara baada ya mapokezi makubwa aliyoyapata kutoka kwa Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, huku Mhe. Membe akishuhudia.
Mhe. Membe akifurahia jambo na Makatibu Wakuu wakati Dkt. Tax akisaini Kitabu cha Wageni.Picha na Reginald Philip.


MSANII WA BONGO FLEVA NASEEB ABDULMALIKI a.k.a DIAMOND ATAJWA SAKATA LA MADAWA YA KULEVYA




Utajiri, safari zake nje ya nchi vyatiliwa shaka
*Ahusishwa na mtandao hatari wa Masogange


KWA mara ya kwanza tangu lilipoibuka sakata la watu maarufu kujihusisha ama na utumiaji au usafirishaji wa dawa za kulevya, jina la mwanamuziki anayeaminika kuwa na ukwasi mkubwa kwa sasa hapa nchini, Nasseeb Abdulmaliki, maarufu zaidi kwa jina la Diamond, limeanza kutajwa kuwa ni miongoni mwa vigogo wa dawa hizo.

Tayari mjadala mkubwa wa chini chini umeibuka kwa watu mbalimbali wakiwemo mashabiki wake, na taarifa ambazo zimelifikia MTANZANIA Jumatano kutoka vyanzo mbalimbali zimedai kuwa, mwenendo wa maisha ya Diamond sasa unachunguzwa na baadhi ya maofisa wa vyombo vya dola vya ulinzi na usalama.

Kutajwa kwa jina la Diamond katika sakata hili, kunatiwa nguvu zaidi na mwenendo binafsi wa maisha wa msanii huyo maarufu wa muziki wa kizazi kipya, unaokwenda sambamba na ukwasi mkubwa alioupata katika kipindi kifupi.

Kama hiyo haitoshi, safari za nje ya nchi za mwanamuziki huyo unaohusisha ziara zake nchini Afrika Kusini na Uingereza, pia ni mambo ambayo yamechochea wingu la mashaka lililofikia hatua ya jina lake kuingizwa katika mtandao huo ambao katika siku za karibuni, umewagusa pia baadhi ya watu wenye majina makubwa katika jamii.

Kuhusu ziara hizo, kilicholeta mshtuko na dukuduku dhidi yake ni kuwapo kwa taarifa kwamba, katika moja ya ziara hizo za nje ya nchi, Diamond alifikia hatua ya kusafiri akitumia chumba kinachotumiwa na wageni mashuhuri (VIP), badala ya njia ya wasafiri wa kawaida.

Mbali na hilo, taarifa nyingine zinaeleza kwamba, mizigo ya msanii huyo ambaye mara kadhaa amekuwa akisafiri na kundi la wacheza shoo wake, imekuwa ikipita pasipo kupitishwa katika hatua za ukaguzi kwa namna ile ile ilivyokuwa kwa mabinti wawili wa Kitanzania walionaswa nchini Afrika Kusini baada ya kuruka mfumo wa ukaguzi wa JNIA.

Aidha, ukaribu wa kimahusiano kati ya Diamond na baadhi ya Watanzania wanaoishi nchini Afrika Kusini na ambao majina yao pia yameanza kuhusishwa na biashara hiyo ya mihadarati, ni jambo jingine ambalo limechochea harakati za kufuatiliwa kwa karibu kwa nyendo za Diamond.

Taarifa zaidi kutoka JNIA zinaeleza kwamba, miongoni mwa watu wanaoweza wakawa wamemponza Diamond ni wale ambao walionekana kuwa karibu na Agness Gerald ‘Masogange’ (25) na Melisa Edward (24), siku walipokuwa wakisafiri kwenda Afrika Kusini kabla hawajanaswa katika uwanja wa Ndege wa Oliver Thambo jijini Johannesburg nchini Afrika Kusini, wakiwa na shehena ya dawa za kulevya.

Mwenendo wa watu hao unatiliwa shaka kuwa huenda ni miongoni mwa wafanyabiashara wakubwa wa dawa za kulevya wenye maskani yao nchini Afrika Kusini, kwa sababu mbali na ukaribu na wasichana hao, pia walihusika kwa karibu kuusafirisha mwili wa mwanamuziki Albert Mangwair, aliyefia huko huko Afrika Kusini ambaye taarifa za kufa kwake ziligumbikwa na matumizi ya dawa za kulevya.

Alipoulizwa jana na MTANZANIA Jumatano kupitia simu yake ya kiganjani kuhusu taarifa hizo na iwapo amekwishahojiwa na vyombo vya dola baada ya jina lake kuanza kutajwa kuwa miongoni mwa orodha ya wasanii wa muziki wanaosafirisha dawa za kulevya, Diamond alikiri kuwa na pesa za kutosha kuishi maisha anayoyataka, lakini akakana kujihusisha na biashara hiyo.

Akifafanua tuhuma moja baada ya nyingine kwa mpangilio aliokuwa akiulizwa na gazeti hili, Diamond alisema katika maisha yake, hajawahi kujihusisha na utumiaji au usafirishaji dawa za kulevya, lakini madai hayo yamekuwa yakitolewa dhidi yake na watu ambao hawajui siri ya mafanikio yake.

“Kazi ngumu siku zote inalipa, sasa napata matunda ambayo yanatokana na kile nilichokifanya, iweje watu wanitilie mashaka, Watanzania ni mashahidi wangu wananiona navyochumia juani, nitaendelea kulia kivulini tu kwani nakula kwa jasho langu.

“Siyo kweli kwamba mizigo yangu haikukaguliwa na kama haikukaguliwa na ingekuwa na kasoro, basi Uingereza wangenitia hatiani, nilipita na nilikaguliwa.” Alisema Diamond.

Alipoulizwa kuhusu taarifa za kuwa mwanamtandao wa kundi la Masogange, pia alikanusha kwa kueleza kuwa hata siku aliyosafiri kwenda Afrika Kusini alikwenda peke yake uwanja wa ndege na kuongeza kuwa alikwenda huko kwa shughuli za kimuziki, ambapo safari nzima iligharimu zaidi ya Dola 30,000 za Kimarekani.

“Afrika Kusini nimekwenda kufanya kazi zangu na safari hiyo imenigharimu zaidi ya Dola 30,000, nilikwenda kurekodi nyimbo yangu mpya inayoitwa namba moja ambayo itaanza kusikika hivi karibuni.

“Unajua Watanzania sasa hivi wanajua mtu hawezi kufanikiwa au kupata maendeleo bila kuuza ‘unga’, hili si sawa juhudi za mtu ndizo zinamfikisha alipo, na mimi juhudi zangu ndio zinanifikisha hapa, watu waache kunijadili vibaya.” Alisema Diamond.

Kuibuka kwa taarifa hizi kumekuja ikiwa ni takribani miezi miwili sasa tangu Watanzania wawili, Agness Gerald ‘Masogange’ (25) na Melisa Edward (24), waliokuwa na uhusiano wa karibu na baadhi ya wanamuziki maarufu hapa nchini, kukamatwa nchini Afrika Kusini wakiwa na dawa za kulevya aina ya Crystal Methamphetamine zenye thamani ya Sh bilioni 6.8.

Mbali na kuwa na uhusiano wa karibu na wanamuziki, Edward anadaiwa kuwa alikuwa mfanyakazi katika mgahawa mmoja maarufu jijini Dar es Salaam, unaomilikiwa na mmoja wa vijana matajiri hapa nchini ambaye hata hivyo gazeti hili halijafanikiwa kumpata ili kufanya naye mahojiano.

Wakati huo huo, tayari hatua za kinidhamu zimekwishaanza kuchukuliwa dhidi ya wafanyakazi wa JNIA waliohusika kupitisha kilo 150 za dawa za kulevya, ambao Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, ametaja majina yao hivi karibuni na kuonyesha kwa waandishi wa habari ushahidi wa kuhusika kwao.

CHANZO:JAMII FORUMS



 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU