RIPOTI MAALUMU ya gazeti la JAMHURI
Kipindi
 cha uwindaji kinachoruhusiwa kisheria kinachoanza Julai hadi Desemba 
kila mwaka kimekwisha. Hii haina maana kwamba ulaji wanyamapori umekoma.
Nipo
 njiani naelekea mkoani Iringa. Kilometa 40 hivi kutoka mjini Morogoro, 
tunafika katika eneo linaloitwa Lugano. Hapa kunachomwa nyama za kila 
aina, lakini zinazotawala zaidi ni za mbuzi na swala. Kwa kutambua kuwa 
naweza kupata nyama ya swala, najenga urafiki na wauza nyama hawa. Nao, 
bila hiyana wanakuwa wachangamfu kwangu.
Swali
 langu la kwanza kwao ni, “Naweza kupata nyama ya swala?” Mmoja wa 
vijana hawa anajibu, “Sema jingine kaka, nyama umepata.” Nauliza swali 
la pili, “Naweza kupata nyama ya nyati au aina nyingine tofauti na 
swala?” Najibiwa, “Hapa nyati hupati, labda uende Mkata. Mkata ndiyo 
kwenye kila kitu.”
Naelekezwa
 kwamba kutoka hapa Lugano hadi Mkata ni mwendo kama wa kilometa 10 na 
ushei hivi. Maneno ya vijana hawa ya kwamba Mkata ndiyo kila kitu, 
yananifanya niwe na shauku ya kufika katika kijiji hicho. Kweli, napanda
 basi tayari kuelekea Iringa. Punde si punde, kwa msaada wa kondakta na 
kibao cha utambulisho, napaona Mkata. Naendelea na safari yangu hadi 
Iringa, lakini akili yangu inanisukuma niandae siku maalumu kwa ajili ya
 kufuatilia taarifa hizi.
Nasukumwa
 na ukweli kwamba vijiji kama Lugano, Mkata na Doma vipo jirani kabisa 
na Hifadhi ya Taifa ya Mikumi. Vijiji hivi vinapitiwa na barabara kuu ya
 Morogoro-Iringa. Wakubwa wanapita hapa kila siku. Kama hivyo ndivyo, 
iweje ujangili ushamiri kwa kiasi hiki cha kutisha?
Mwishoni
 mwa Desemba naamua kufunga safari kutoka Dar es Salaam kwenda Mkata na 
Doma. Kabla ya safari nampigia simu Kamanda wa Kikosi cha Kupambana na 
Ujangili katika Wizara ya Maliasili na Utalii, Faustine Masalu.
“Kamanda
 naelekea mkoani Morogoro kufuatilia taarifa za ujangili. Nakupa taarifa
 hizi kwa sababu huko naweza kukutana na mambo yasiyokuwa ya kawaida. 
Lakini kubwa itanipasa niweze kushiriki kununua nyamapori na hata 
kusafiri nayo bila kibali, kisheria nikikamatwa naweza kushitakiwa. 
Nakupa taarifa hii kama kinga kwa linaloweza kunipata,” huu ndiyo 
uliokuwa ujumbe wangu kwa Masalu, kabla ya kuanza safari kwa kutumia 
gari langu.
Muda ni 
saa tano asubuhi. Naanza safari ya kwenda Morogoro. Kwa kutambua ugumu 
wa kazi ninayokwenda kuifanya, namchukua mwandishi mwenzangu, Edmund 
Mihale.
Tunakwenda 
hadi Lugano. Hapa tunaegesha gari pembeni kwa ajili ya kuanza kazi. Mvua
 kubwa inanyesha. Majiko ya nyama ni mengi. Tunaomba tuuziwe nyamapori, 
lakini kwa hadaa, baadhi ya wauzaji wanatupatia nyama ya mbuzi. Wote 
tunashituka. Kuona hivyo, mmoja anatuelekeza kwenye jiko lake.
Kweli,
 tunakula nyama yenye ladha na sifa zote za swala. Kazi imeanza. 
Nakumbuka kwamba nilishaelezwa na hawa hawa vijana kwamba nyama za kila 
aina zinapatikana Mkata, mahali ambako sifa zake zinafanana na Mkata ya 
Handeni, mkoani Tanga, ambako kunauzwa nyama nyingi za mbuzi, lakini si 
swala na wanyamapori wengine.
Tunaanza
 safari kwenda Mkata. Si mbali. Baada ya kilometa tano hivi, tunakuta 
gari la Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) aina ya Land 
Rover likiwa limepinduka na kuwaumiza askari na raia waliokuwamo. Ni 
mali ya Kikosi cha 401.
Wanajeshi
 hawa walikuwa wakitoka kumzika mwenzao Kigamboni, Dar es Salaam, na 
sasa walikuwa njiani kurejea Songea. Kama ilivyo ada, tunashiriki kutoa 
huduma kwa wapiganaji na makamanda hawa. Magari mengi yanafika, 
yanasimama na kuuliza aina ya msaada unaotakiwa. Mwisho, majeruhi wote, 
isipokuwa mmoja, wanapelekwa Hospitali ya Mkoa wa Morogoro kwa matibabu.
Kuona
 hivyo, tunashawishika kuendelea na safari yetu. Vijana wawili wanaomba 
lifti. Nawauliza wanakokwenda. Wanajibu kwamba wao ni wakazi wa Mkata. 
Kusikia hivyo, haraka haraka nawakaribisha waingine katika gari. Njiani 
naanza kuwauliza kama wana uwezo wa kuniwezesha kupata nyama ya swala. 
Mmoja anajibu, “Sisi hatuuzi swala, lakini tunaweza kukupeleka kwa 
wanaouza.” Namwuliza kama naweza kupata aina nyingine ya wanyamapori.
“Hapo
 kila kitu utapata, hakuna wasiwasi,” anajibu kwa lafudhi ya Kimaasai. 
Baada ya kilometa kama saba hivi, tunafika Mkata. Nashangaa kuona magari
 mengi yakiwa yameegeshwa kando ya barabara. Nauliza kama kuna sherehe 
mahali hapa. Mmoja wa vijana hawa anajibu, “Siyo sherehe, watu wanakuja 
wote kula nyama hapa.”
Tunakwenda
 moja kwa moja hadi mahali kunakouzwa. Wenyeji wetu hapa hawana 
wasiwasi, pengine kutokana na hawa vijana wawili wenyeji waliotufikisha 
hapa. Tunawakuta wateja wengi wakila nyama. Jiko limejengwa ndani ya 
nyumba mbovu ya miti na kuezekwa kwa nyasi.
Anayechoma
 nyama hapa ni maarufu kwa jina la Mangi. Baadaye tunamwuliza jina lake 
halisi na anajitambulisha kuwa anaitwa Mrosso Anthony. Kuna nyama ya 
nyati, swala na pofu. Pande linauzwa kuanzia Sh 10,000. Mimi nasita 
kuchukua nyama kubwa, naomba atutengee ya Sh 5,000. Wateja wote 
tuliokutana hapa ni kama vile tulishaonana siku nyingi, maana wengine 
wanakata "kilaji" (bia). Wanatukaribisha tunywe. Ni katika mazingira 
ambayo watembezi huyaita “adventure”.
Upande
 wa pili wa nyumba hii, kuna nyama mbichi iliyotundikwa. Inavutia kweli 
kweli. Inavuja damu mbichi kabisa. Kuna miguu na mikono. Pembeni mwa 
hiyo nyama, kuna kijana mmoja mwenye uso uliojaa makovu. Anaitwa Pengo. 
Sijui kwanini anaitwa Pengo, pengine ni kutokana na kutokuwa na meno 
mengi mdomoni. Namwuliza; “Pengo, vipi bwana, mbona uso umeharibika, 
wewe ni mgomvi au ulikuwa ukipambana na nyati?” Anajibu kwa tabasamu, 
“Siyo nyati mkuu, hii kitu ndiyo imefanya yote haya,” anasema huku 
akinionesha pikipiki.
Wageni
 wanazidi kumiminika hapa, na nyama zinauzwa kwa kasi. Ghafla, Pengo na 
Mangi wanaonekana kuhamaki baada ya kuwaona wateja wengine wawili 
wasiowajua wakija mahali tulipo. “Wale nani?" Anahoji Mangi. Pengo 
anajibu, “Ni wateja tu, siyo watu wabaya.”
Nyama
 tuliyoilipia ipo tayari. Tunaanza kula, lakini ni ngumu. Yaelekea ni ya
 upande wa shingo.  Nimeshindwa kutelemka na kamera yangu kubwa. Hali 
hii inalilazimu nitumie kamera maalumu kupata picha za hapa na pale.
Ili
 nisiweze kushitukiwa, nauliza bei ya mguu wa pofu. Naambiwa kuwa bei 
yake ni Sh 120,000. Naomba niuziwe kipande cha Sh 20,000. Pengo 
anachukua mguu wa pofu. Anaupeleka nje kwenye gogo maalumu. Anakata. 
Kuona hivyo, walaji wenzetu nao wanaanza kununua. Wanakatiwa kadiri ya 
fedha zao. Wengine wanaingia wakiwa na bia zao kabisa. Nyama ni nyingi 
na hakuna mwenye wasiwasi.
Mwisho,
 nikiwa nimeshajiridhisha kuwa nyama inayouzwa ni ya pori, namwuliza 
Pengo wapi wanakopata nyama. “Hii nyama tunanunua kwa Waarabu wa 
Morogoro wanaokuja kuwinda huku.” Namwuliza, “Mbona muda wa kuwinda 
umekwisha?” Anakosa jibu.
Tumeshajiridhisha
 pasi na shaka kuwa hapa ni kwenye mnada wa wanyamapori. Tunaaga, lakini
 kabla ya kuondoka, Mangi anatupatia namba yake ya simu. “Chukua namba 
yangu ya simu, ukiwa unahitaji kabla ya kufika hapa wewe piga simu 
kabisa tukuandalie. Namba yangu ni 
0655 093795. Karibu sana,” anasema.
Ingawa
 mwanzoni alinieleza kwamba jina lake ni Mrosso Anthony, usajili wa 
namba hii unaonesha kuwa ni ya Christian Joseph. Hii inazidi kunipa 
shaka.
Baada ya hapo 
naanza uchunguzi wa hapa na pale. Najiridhisha kuwa pikipiki iliyopo 
hapa ni moja ya zana zinazotumika kusafirisha nyama. Naelezwa na mmoja 
wa vijana kwamba pamoja na kuwapo kundi la vijana wanaoendesha ujangili,
 baadhi ya nyama wanazipata kutoka kwa askari wanyamapori wa Mikumi.
Wiki
 ijayo naendelea kueleza vituo vingine vya uuzaji wanyamapori. Ushiriki 
wa maofisa na askari wanyamapori katika biashara hii haramu. Je, 
Mkurugenzi na mwenye dhamana ya kupambana na ujangili nchini, Paul 
Sarakikya; Kamanda Masalu, Mkuu wa KDU (Kikosi Dhidi ya Ujangili), Majid
 Lalu; Mkuu wa Hifadhi ya Mikumi; Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya 
Mvomero, Sarah Limuna; Ofisa Wanyamapori Mkoa wa Morogoro, Joseph Chuwa.
Nao,
 Askari Wanyamapori Wilaya ya Mvomero aliyepewa dhima ya kusimamia 
wanyamapori eneo la Doma, Peter Mayapila; Ofisa Uhusiano wa Mamlaka ya 
Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Paschal Shelutete; wanasemaje?  Je, 
kuwapo kwa huduma za mitandao ya simu hifadhini na katika mapori pamoja 
na kuruhusu matumizi ya bodaboda kunachangiaje wimbi la ujangili 
nchini?
...Usikose toleo lijalo la gazeti JAMHURI.