Facebook Comments Box

Friday, August 2, 2013

TAARIFA YA TANESCO KWA UMMA

Picture: TANESCO Badra Masoud
Msemaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Badra Masoud (kushoto) akizungumza na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam katika ukumbi wa Idara ya Habari (Maelezo) juu ya mikakati ya shirika hilo katika kutekeleza miradi yake ili kupambana na tatizo la umeme nchini, kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Habari Bi. Zamaradi Kawawa. (Picha: Eliphace Marwa)
TAARIFA YA MKUTANO KATI YA WAANDISHI WA HABARI NA TANESCO 

1 AGOSTI, 2013

Ndugu zangu waandishi wa Habari napenda kuchukua nafasi hii adimu kabisa kwangu kuweza kuzungumza nanyi siku ya leo kuelezea shughuli mbalimbali zinazofanywa na Shirika letu la Umeme hapa nchini yaani TANESCO.

Kwanza kabisa napenda kuwakumbusha kidogo juu ya Shirika letu lilivyokuwa katika miaka ya 80 kwamba lilikuwa likisifika kama moja ya mashirika bora barani Afrika, na ni ukweli usiopingika kwamba katika kipindi hicho TANESCO ilifanya vizuri sana katika kila nyanja na hata kupata sifa hizo. Lakini kutokana na sababu mbalimbali za kiufundi na zisizo za kiufundi mwishoni mwa miaka ya 90 shirika hili lilianza kulalamikiwa na wateja wake kutokana na huduma kwa namna moja ama nyingine zinazodaiwa kutoridhisha huku maeneo makuu yaliyokuwa yakiangaliwa ni ufuaji, usafirishaji, usambazaji na uuzaji umeme.

Baadhi ya sababu hizo ni pamoja na kukatika umeme mara kwa mara kunakotokana na uchakavu wa miundombinu, huduma zisizoridhisha kutoka kwa baadhi ya watendaji wa Shirika, umeme kutowafikia watanzania walio wengi hasa maeneo ya vijijini na kasi ya kuunganisha wateja wapya kuwa ndogo.

Kutokana na changamoto hizo nilizozitaja, Shirika limeanza kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo ya kuboresha miundombinu ya umeme.

Maeneo yenye changamoto ya kukatika umeme
Pamoja na ukarabati huo unaofanywa katika miundombinu yetu, yapo maeneo ambayo umeme umekuwa 
unakatika mara kwa mara. Maeneo hayo ni  kama vile Bahari Beach, Kunduchi Beach, Mbezi Beach, Kimara  mpaka Mbezi mwisho Mbagala, Temeke na Kigamboni katika mkoa wa Dar es Salaam, Mererani mkoani Arusha, Kahama, Meatu, Bariadi, Kanda ya Ziwa.

Maeneo haya ukiangalia kwa makini utagundua kuwa miundombinu yake ilijengwa miaka mingi na ndiyo maeneo ambayo tunawekeza nguvu kubwa zaidi kuyaimarisha. Hivyo Shirika linapenda kuwaondoa hofu watanzania wa maeneo hayo kuwa kukatika umeme mara kwa mara katika maeneo hayo si mgao wa umeme na wala hakuna tishio lolote la mgao wa umeme kwa sasa, ni matatizo yanayotokana na udhaifu katika miundombinu yetu.

Hatua ambazo TANESCO inachukua kuondoa matatizo ya umeme katika maeneo yaliyotajwa
Bahari beach:
Bahari Beach kuna kituo kidogo cha kupooza na kusambaza umeme, kituo hiki kwa sasa kimezidiwa baada ya kuunganishwa kuhudumia wateja wengi kuliko uwezo wake.

Juhudi zinazofanyika ni kuimarisha Kituo cha kupoza na kusambaza umeme kilichopo Mbezi Beach ili kiwe na uwezo zaidi. Kazi hiyo inaendelea na itakapokamilika tutahamisha baadhi ya wateja kutoka katika Kituo cha Bahari Beach na kuwaunganisha kwenye kituo cha Mbezi Beach.

Mbezi Beach:
Kwenye kituo cha Mbezi Beach ilikuwepo transfoma moja ya MVA 15, transfoma hiyo ilishazidiwa na hivyo Shirika limeshafunga transfoma ya pili yenye uwezo mara dufu wa ile ya kwanza, hii ina MVA 30. Ina uwezo wa kuhudumia wateja wote wa Mbezi Beach na baadhi ya wateja tuliowahamisha kutoka Bahari Beach na hivyo kuondoa kabisa tatizo la umeme kwa wakazi wa Mbezi Beach na Bahari Beach.

Kimara mpaka Mbezi:
Kuna njia moja tu ya umeme wa msongo wa kilovolti 132 inayotoka Ubungo kupitia Kibo, Kimara, mpaka Mbezi barabara ya Morogoro. Likitokea tatizo lolote la kiufundi kwenye njia hiyo basi linaathiri maeneo yote haya inapopita njia hiyo.

Ili kuondokana na tatizo hilo, Shirika linafanya utaratibu wa kujenga kituo kingine eneo la Luguruni. Kituo hicho kitaweza kuhudumia maeneo yote ya Mbezi mwisho na hivyo kuacha njia nyingine kuhudumia Ubungo, Kibo na baadhi ya sehemu za Kimara. Hii itaondoa kabisa matatizo yote ya umeme katika maeneo haya.

Kahama:
Matatizo ya Kahama yanatokana na njia ya kusafirisha umeme kutoka Shinyanga hadi Kahama kuwa ndefu sana. Njia hii ina zaidi ya kilometa 200, urefu huu kitaalamu haukubaliki kwani umeme mwingi huwa unapotea njiani kulingana na umbali umeme huo unavyosafirishwa.

Aidha, Shirika linaweka kituo kikubwa cha kupooza na kusambaza umeme Buzwagi ili kufupisha njia ya kupeleka umeme kutoka Buzwagi mpaka Kahama. Kwa kufanya hivyo matatizo ya umeme yanayowakabili wateja wa Kahama yatakwisha ndani ya kipindi kifupi hiki.

Kanda ya Ziwa:
Kuna matatizo yanayojirudia rudia kutokana na umeme wenye nguvu ndogo unaotoka Mtera kupitia Dodoma mpaka Kanda ya Ziwa (low voltage).

Shirika kwa sasa linatekeleza mradi mkubwa unaoitwa ‘Backbone’. Mradi  huu utapandisha kiwango cha umeme unaosafirishwa kutoka kilovolti 132 hadi kilovolti 400. Makandarasi wameshapatikana na muda wowote wataanza ujenzi, na ujenzi wa mradi huu utakapokamilika matatizo ya umeme katika Kanda ya Ziwa yatakuwa madogo sana au yatakwisha kabisa.

Kwa Kanda ya Ziwa hadi sasa kituo kikubwa cha umeme kilichopo  Nyakato Mwanza kimejengwa, kituo hiki kina uwezo wa kuzalisha umeme  wa megawati 60, na umeme utakaozalishwa Nyakato utaingizwa kwenye gridi ya taifa na kupunguza kabisa tatizo la ‘low voltage’ umeme mdogo kwa Kanda ya Ziwa.

Kituo hiki tumekiweka makusudi ili kutoa huduma ya umeme wakati tukisubiri upanuzi wa njia ya kusafirishia umeme katika mradi wa ‘Backbone’ ulitajwa hapo juu.

Kituo hiki cha Nyakato kimekamilika na kitaanza kuzalisha umeme mwezi wa Januari, 2013. Shirika linawahakikishia wateja na wananchi wa Kanda ya Ziwa kwamba watapata umeme wa uhakika mwezi Januari, 2013.

Mererani - Arusha:
Mererani wanategemea umeme kutoka katika kituo cha Kiyungi kilichopo Moshi mjini, kutoka Moshi mpaka Mererani ni kilometa200, kwa umbali huu kitaalamu umeme unaosafirishwa unapungua nguvu njiani.

Ili kuondokana na tatizo hilo, TANESCO chini ya mradi wa TEDAP, imejenga kituo cha kupooza umeme eneo la Kilimanjaro International Airport (KIA) na sasa Mererani wanapokea umeme kutoka kituo cha KIA na mradi huu tunatarajia kuuzindua hivi karibuni.

Temeke, Kigamboni na Mbagala:
Tatizo la umeme la Temeke, Kigamboni na Mbagala halitokani na utendaji kazi wa TANESCO, tatizo kubwa katika maeneo haya yanatokana na wahujumu miundombinu ya Shirika. Kuna watu ambao hawapendi maendeleo, wanakwenda kwenye miundombinu ambayo tayari ipo, wanaiba mafuta ya transfoma na wanaiba nyaya za kopa. Wizi wa mafuta ya transfoma umeshamiri sana katika maeneo haya na hii ndio sababu kubwa ya wateja wetu kukosa umeme, kukaa gizani.

Aidha ili kuondokana na kero hii Shirika limeanza kutumia transfoma zisizo na mafuta katika maeneo hayo.

Shirika limeweza kudhibiti hali kama hii katika maeneo ambayo wizi wa mafuta ya transfoma ulikithiri, maeneo hayo ni kama Mbezi, Kinondoni Kaskazini na Kawe.

Lakini sasa wizi huu umehamiaTemeke, Shirika limefikia hatua ya kufunga aina hii ya transfoma isiyotumia mafuta ili kupunguza wizi na uharibifu ya miundombinu hii ambayo ni ghali sana.

MIRADI MIKUBWA ILIYO KATIKA HARAKATI ZA KUTEKELEZWA
  • Watanzania wategemee nini kutoka katika miradi hii?



Mradi wa ‘City Center’ Dar es Salaam:

Kuna mradi mkubwa unaotekelezwa kati ya Serikali ya Tanzania kupitia TANESCO na serikali ya Finland wenye thamani ya Euro milioni 25, mradi huu upo katika hatua za utekelezaji na utahusisha ujenzi wa kituo kikubwa cha kupoza na kusambaza umeme katika maeneo ya katikati ya jiji na kituo hicho kitajengwa eneo zilipo ofisi za UNICEF.

Kituo hiki kitakapokamilika kitaweza kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme katikati ya mji wa Dar es Salaam. Mradi huu utahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovolti 132 chini ya ardhi (underground cable) kwa ajili ya kuimarisha vituo vingine vilivyopo katikati ya mji na kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika.
Pamoja na kujenga nyaya za chini ya ardhi, tunategemea kuweka sakiti mzunguko (ring circuit), mfumo ambao utasaidia kuunganisha umeme kutoka kituo kimoja kwenda kingine iwapo kituo kimoja kitakuwa na hitilafu kwa vituo vyote vya kupooza na kusambaza umeme jijini Dar es Salaam.

Mradi huu tayari ameshakabidhiwa mkandarasi na ndani ya mwaka mmoja mradi huu tunatarajia utakuwa umekamilika na umeme wa uhakika utakuwa unapatikana.

Wakati mradi huo ukiendelea, Shirika linapenda kuwataarifu wakazi wa jiji la Dar es Salaam kuwa wamefunga transfoma kubwa mbili kubwa mpya katika Kituo cha Kupooza na Kusambaza umeme cha City Center za MVA 30 na hivyo kuimarisha upatikanaji wa umeme katikati ya jiji tofauti na ilivyokuwa hapo awali wakati ilipoungua transfoma ya MVA 15.

Vilevile Shirika limefunga transfoma mpya kwenye Kituo cha Kariakoo na Kituo cha Buguruni na kurekebisha miundombinu katika kituo cha Ilala zoezi ambalo limefanikisha kuimarika kwa hali ya upatianaji wa umeme katikati ya jiji la Dar Es salaam ambalo mahitaji yake yamepanda kwa kiasi kikubwa sana ukilinganisha na mwaka mmoja uliopita.

MRADI WA TEDAP
Mradi huu wa TEDAP tumeuelezea kwa ufupi hapo juu. Kusudi kubwa la mradi ni kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme jijini Dar na Arusha. Kwa Arusha, mradi unaendelea na kazi zote zinafanyika Njiro. Kwa Dar es Salaam, kazi kubwa ni kupeleka njia ya kusafirisha umeme (transimission line) mpaka Kurasini na kujenga kituo cha kupoza umeme kutoka Kilovolti 132 mpaka kilovolti 33, njia hii itatoka Kurasini hadi Mbagala ambapo kutakuwa na kituo kingine kikubwa cha kupoza umeme kutoka uwezo wa kilovolti 132 mpaka kilovolti 33 na kusambaza katika maeneo hayo ya Kurasini mpaka Mbagala.

Mradi huu unajenga njia nyingine kubwa ya kilovolti 132 kwenda Gongo la Mboto, ambapo kitajengwa kituo kingine kikubwa cha kupooza kutoka uwezo wa kilovolti 132 mpaka kilovolti 33 na kuunganisha hiyo sakiti na kituo cha Kipawa.

Kwa ufupi ni kwamba kutakua na sakiti mzunguko (ring circuit) kutoka Ubungo – Kurasini - Mbagala hadi Gongo la Mboto na kurudi Kipawa.

Mzunguko huu utatuhakikishia umeme wa uhakika kwa jiji zima la Dar es Salaam. Kama umeme ukikosekana eneo moja ni rahisi kuunganisha kwa kupitia upande wa pili na umeme ukaendelea kupatikana.

Hata hivyo kuna baadhi ya vituo vya zamani ambazo uwezo wake umekua ukipungua kadri mahitaji yalivyokuwa yanazidi kuongezeka. Vituo hivi ni kama vile Kituo cha Kipawa ambacho kwa sasa Shirika linafunga transfoma kubwa mbili zenye uwezo wa MVA 90, kazi hii itakamilika ndani ya mwezi mmoja, wananchi wanaokaa maeneo ya Tabata, Kisarawe na Gongo la mboto tayari watakua na uhakika wa umeme.

Umeme wa maeneo haya  yaliyotajwa unatoka Ilala, na pale kazi hii ya Kipawa itakapomalizika, umeme wa maeneo haya utakuwa unatoka Kipawa ambapo ni karibu na maeneo hayo na umeme utakua  ni wa uhakika zaidi.

Aidha tumefunga transfoma mbili kubwa katika Kituo Kikuu cha Kupooza na Kusambaza umeme cha Ubungo ambazo zimesaidia kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa umeme kwa jiji la Dar es Salaam.

MIRADI YA UZALISHAJI
Kwenye upande wa UZALISHAJI WA UMEME:

Mradi wa Bomba la Gesi kutoka Mtwara – Dar es Salaam
Wakati ujenzi wa bomba unaendelea TANESCO kwa kushirikiana na serikali inajitahidi kuhakikisha  kuwa mitambo ya kuzalisha umeme kwa kutumia gesi hiyo inakuwa tayari.

Kwa sasa tayari kuna mitambo mingi inayozalisha umeme kwa kutumia gesi asilia nyingi tofauti na kiwango cha gesi kinachozalishwa.

Mradi wa Kinyerezi
TANESCO ina mashine zenye uwezo wa kuzalisha zaidi ya megawati 150 zinazotumia gesi ambazo hatuwezi kuzitembeza kwa sababu hatuna gesi. Bomba litakapofika, pamoja na kuendesha mashine ya megawati 150 lakini pia tunaanza utaratibu wa ujenzi wa vituo ifuatavyo:
o    Tutakua na mtambo wa megawati 150 utakaojengwa Kinyerezi na taratibu za ujenzi wa mtambo huu zimeshaanza na muda sio mrefu jiwe la msingi litawekwa.
o    Tutakua na mradi wa meagawati 240, Megawati 300 na megawati 300 ambayo yote itajengwa pia Kinyerezi.
Hii miradi itakapomilika kati ya mwaka mmoja hadi miwili ijayo. TANESCO itakuwa na uhakika wa umeme usiopungua megawati 990 zinazotokana na gesi.

Mradi wa Kilwa Energy
Tuna mradi Kilwa, mradi huu unaitwa Kilwa Energy ukikamilika utatoa uhakika wa megawati 320, ni mradi wa mwekezaji binafsi na Shirika liko kwenye mazungumzo kuhakikisha mchakato wa mradi huu unakamilika. Bahati nzuri mazungumzo yamefikia hatua nzuri. Mradi huu utajengwa Kilwa na utaambatana na ujenzi wa njia ya msongo wa 240MV ‘double circuit line’  kutoka Kilwa mpaka Dar es Salaam.

Mradi wa kujenga mtambo wa umeme wa megawati 600 mkoa wa Mtwara utajengwa na Kampuni ya Symbion ya Marekani na kusafirisha umeme hadi Songea na Makambako na hatimaye kuunganishwa katika Grid ya taifa.

MIPANGO YA MIRADI YA USAFIRISHAJI
Ukijenga tu miradi hii ya kuzalisha umeme bila kujenga njia za kusafirisha umeme huo utakuwa haujakamilisha kazi.

Mipango iliyopo kwenye mikakati na ambayo imeshaingizwa katika mipango ya kitaifa ya kurekebisha miundombinu ya umeme ni pamoja na hii ifuatayo:
o    Mradi wa ‘North East Grid Transmission Line’ ya kutoka hapa Ubungo kwenda hadi Arusha, mradi una nia ya kuimarisha miundombinu ya umeme Kanda ya Kaskazini, Mikoa ya Tanga, Kilimanjaro na Arusha , mradi huu ni muhimu sana kwa sasa hivi ukiacha Kanda ya Ziwa ambapo ‘Backborne Projects’ imeanza kutekelezwa  eneo lingine ambalo miundombinu yake ni dhaifu sana ni Kanda hii ya Kaskazini na upotevu mwingi wa umeme unatoka huko.
o    Pia TANESCO kwa kushirikiana na ufadhili wa serikali ya Sweden chini ya shirika lake la SIDA, Shirika linaanza utekelezaji wa mradi kutoka Makambako mpaka Songea. Mwanzoni kulikuwa na mpango wa kuweka mradi wa kujenga njia ya kilovolti 220 mpaka Madaba na kilovolti 132 kutoka Madaba mpaka Songea. Sasa hivi  baada ya kuona maendeleo kwenye makaa ya mawe hasa maeneo ya Ngaka na Mchuchuma, tumeona ni vyema kuupanua mradi huu na kujenga njia ya kilovolti 220 badaala ya 132 kutoka Makambako hadi Songea. Mkandarasi ataanza kazi hii kabla ya mwisho wa mwaka huu.

o    Mradi mwingine wa usafirishaji umeme ambao upo katika hatua za utekelezaji ni mradi wa ‘North West Grid’ – ambao utasaidia upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa utatupa sasa uhakika kwa mikoa wa Mbeya, Rukwa na Katavi, Mpanda , Kigoma , Nyakanazi na kurudi kuunganisha na Kahama. Mradi huu ni muhimu sana, kwa kuwa utakapokamilika nchi nzima itakuwa imeunganishwa kwenye gridi ya Taifa.

o    Mwisho kabisa maeneo ya Lindi na Mtwara hayajasahaulika, tuna mipango mingi. Tunategemea Mtwara kuwa na mtambo wa megawati 320 ambao utaunganishwa na njia ya kusafirisha umeme ‘transmission line’ mpaka Kilwa, Lindi. Kituo hicho  pamoja na kujengwa kwa kituo hicho kitaunganishwa na gridi ya Taifa ya kutoka Mtwara kupitia Somanga na kutoa umeme Somanga na kuuleta  Dar es Salaam.

Kwa mikakati hii tutakua na uwezo wa kutoa umeme Mtera na Kihansi  na kuupeleka Kigoma, Mpanda n.k. na nchi nzamia itakua imeingizwa katika gridi ya Taifa.       

 Tunasisitiza kwamba miradi yote tuliyoieleza ni ya uhakika kwa kuwa taratibu za utekelezaji zimeanza kufanyika.



SIJAONA KOSA LA WAZIRI MKUU - DPP

MKURUGENZI wa Mashitaka (DPP), Eliezer Feleshi, amesema haoni mantiki yoyote au uhalali wa Kituo cha Haki za Binadamu (LHRC), kumshitaki Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

Alisema hayo janai wakati akijibu maswali ya waandishi wa habari, baada ya kufungwa kwa mkutano wa siku tatu wa mawakili wa Serikali wafawidhi, wakuu wa upelelezi wa mikoa na vikosi
vingine vya Polisi Alisema kauli aliyotoa Pinda bungeni, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Kilwa Kaskazini, Murtaza Mangungu kuhusu Polisi kutumia nguvu kwa wananchi, ililenga wanaokaidi kukamatwa na kufikishwa mbele ya sheria na si kupiga na kuua kama ilivyotafsiriwa na wengi.

“Sijapata taarifa kwa maandishi juu ya azma ya kumshitaki Waziri Mkuu, lakini Pinda hajavunja sheria kwa kauli yake aliyotoa,” alisema.

Alisema kwa jinsi alivyosikia maelezo ya Waziri Mkuu bungeni, kama LHRC wanamshitaki kwa jinai Waziri Mkuu, haoni uhalali wa mashitaka hayo.

Usahihi wa Pinda Alisema Waziri Mkuu alieleza hatua zinazochukuliwa dhidi ya mvunja sheria, na kufafanua kuwa Mtanzania yeyote ana haki kwa mujibu wa sheria, lakini pia ana wajibu, ndiyo maana vipo vyombo na kila chombo kimepewa mamlaka na wajibu wa kutekeleza.

Alifafanua, kwamba kilichoongelewa ni dhana ya mkusanyiko ambayo ni haki kwa mujibu wa Katiba, ikiwemo uhuru wa kukutana, kutoa mawazo na kufanya mawasiliano.

Hata hivyo, alikumbusha kuwa Sheria ya Jeshi la Polisi, inasema ili mkusanyiko ufanyike, lazima taarifa itolewe kwa kiongozi wa Polisi wa eneo husika.

Sheria hiyo inasema, kama mkusanyiko una nia ya kutenda kosa na ikafanyika hivyo, kuna chombo kilichopewa dhamana ya kuhakikisha mkusanyiko haramu unatawanyika na sheria hiyo inaruhusu Polisi kutawanya mkusanyiko haramu.

“Unatarajia nini kama kuna watu wanafanya fujo na polisi wana mamlaka ya kuwakamata waliofanya fujo?” Alihoji Feleshi na kuongeza kuwa dhana ya matumizi ya nguvu ni ya kisheria pia.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, akizungumza kwa simu na gazeti hili, alisema utaratibu wa Polisi kulazimika kutumia nguvu upo. Aliutaja utaratibu huo kwamba unatumika hasa katika mikusanyiko isiyotakiwa, ambapo Polisi hulazimika kutoa tangazo la angalizo mara kadhaa kutaka watu watawanyike.

“Tangazo linapotolewa, Polisi kwa kutumia kipaza sauti husema, tawanyikeni, tawanyikeni na kusisitiza hivyo mara kadhaa, hapo wanaopaswa kutawanyika wakikaidi, nguvu hutumika ingawa inaweza isiwe ya kupiga risasi, pengine virungu, yote hiyo si kupiga?

“Risasi ni kitu cha mwisho, labda uwe unashambuliwa wewe (polisi), hata ikiwa hivyo, ukipiga risasi kuna maeneo ya kupiga, si kichwani, polisi wana mafunzo ya kupiga maeneo ya miguuni, hivyo kutumia nguvu kwa polisi kupo,” alisema Jaji Werema.


 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU