Tarehe
 27 Desemba maelfu ya wananchi wa Mtwara waliandamana kudai gesi ya 
Mnazi Bay itumiwe kuendeleza viwanda katika mkoa wa Mtwara kabla ha
ijasafirishwa
 kwenda kutumiwa maeneo mengine ya nchi. Kwa muda mrefu CUF Chama cha 
wananchi kimekuwa kikisisitiza kuwa na sera zitakazohakikisha kuwa 
maliasili na rasilimali za nchi zinawanufaisha Watanzania wote kwa 
ujumla na hususani wananchi wanaoishi katika maeneo ambayo maliasili 
hiyo imegunduliwa.
Katika nchi nyingi utajiri mkubwa wa gesi na 
mafuta umeleta balaa badala ya kuleta neema. Nchini Nigeria katika delta
 ya mto Niger ambako ndipo mafuta yanachimbwa kuna ghasia kubwa za 
kisiasa kwa madai kuwa wananchi wa eneo hilo hawanufaiki na rasilimali 
yao.
Wananchi wa mikoa ya kusini wana sababu za msingi za kulalamika kuwa  kwa muda wa miaka 51 ya uhuru wa 
Tanzania Bara bado hawajatendewa haki. 
Serikali ya mkoloni wa Kiingereza ilijenga reli kuunganisha Nachingwea 
na Mtwara ilipoanzisha mradi wa kilimo cha karanga. Mradi huu 
haukufanukiwa. Badala ya kutafuta ufumbuzi wa matatizo na kuendeleza 
uzalishaji wa mazao mengine kama vile korosho, ufuta, alizeti, kunde na 
mbaazi, Serikali ya TANU baada ya kupata uhuru ikaamua kun’goa reli ya 
Nachingwea – Mtwara na kuihamishia Kilosa Mikumi.
Zambia
 ilipokuwa inakabiliwa na tatizo la kusafirisha mizigo yake isipitie 
Rhodesia iliyokuwa inatawaliwa na wazungu wachache, walipendekeza kwa 
serikali ya Tanzania kujenga reli kwenda Mtwara kwani bandari ya Mtwara 
ni nzuri, ina kina kirefu na haina msongamano. Shaba ya Zambia 
ingepakuliwa kwa haraka na kusafirishwa kwenda nchi za nje. Vile vile 
mizigo inayoagizwa kutoka nje ingepakuliwa haraka na kusafirishwa kwenda
 Zambia. Serikali ya Tanzania haikuafiki pendekezo la Zambia na 
ikasisitiza reli ya TAZARA iende Dar es Salaam.
Gesi
 ya Songosongo ilikuwa itumiwe kama malighafi katika kiwanda cha mbolea 
cha Kilwa Ammonium Company. Prof Cleophace Migiro alienda kusomea PhD ya
 Chemical engineering kwa maandalizi ya kuja kufanya kazi KILAMCO. Ardhi
 ya kujenga kiwanda ilinunuliwa Kilwa Masoko, kiwanja cha ndege 
kikatengenezwa, mpango wa kuimarisha bandari ya masoko ukaandaliwa. 
Mgogoro wa uchumi wa miaka ya 1980 ikatibua mambo.
Dr.
 Shija waziri wa Nishati na Madini katika kipindi cha kwanza cha Rais 
Mkapa alizungumzia umuhimu wa kufufua mradi wa KILAMCO lakini hakuna 
kilichotendeka. Gesi ilipoanzwa kuchimbwa Songosongo likajengwa bomba 
dogo la nchi 12 kusafirisha gesi chini ya bahari toka Songosongo hadi 
Somanga. Bomba la nchi 14  lilijengwa toka Somanga hadi Dar es Salaam.
Uwezo
 wa mabomba haya ni mdogo ukilinganisha na gesi inayopatikana Songosongo
 na mahitaji yake kwa shughuli ya kufua umeme na kutumia viwandani. 
Mkopo wa kujengea bomba la Songosongo hadi Dar es Salaam ulighubikwa na 
tuhuma za ufisadi za ujenzi wa kituo cha kufua umeme cha IPTL 
kinachotumia mafuta mazito ambacho gharama zake za kufua umeme ni za juu
 sana. Mkataba wa TANESCO na IPTL uliiwajibisha TANESCO kuilipa IPTL 
dola milioni moja kila mwezi hata kama haijazalisha umeme wowote. 
Mkataba huu ulidhoofisha sana hali ya fedha ya TANESCO.
Kampuni
 ya Artumas iligundua kuwepo kwa gas Mnazi Bay, Mtwara na kuanza 
utaratibu wa kuichimba mwaka 2006 na kuitumia kufua umeme wa Megawati 
18. Kabla ya mtikisiko wa sekta ya fedha na uchumi wa dunia wa mwaka 
2008, Artumas ilikuwa na mpango wa kuwekeza kwenye mtambo wa kufua umeme
 Mtwara wa Megawati 300 na kuunganisha Mtwara kwenye gridi ya taifa. 
Mpango huu ulikubaliwa na serikali na ukaingizwa katika Mpango Kabambe 
wa Taifa wa kufua na kusambaza umeme (National Power Development Master 
Plan). Mradi huu wa kufua umeme MW 300 Mtwara ulipangwa uwe umekamilika 
mwaka huu wa 2012.
Mtikisiko wa uchumi 
na fedha duniani wa 2008 uliikumba kampuni ya Artumas. Thamani ya hisa 
za Artumas iliporomoka katika soko la mitaji Canada na Norway. Artumas 
iliiomba serikali dola milioni 7 kunusuru Mradi wa Nishati wa Mtwara 
(Mtwara Energy Project). Uwezo wake wa kutekeleza mpango wa kufua umeme 
Mtwara ukatetereka pamoja na kuwa mradi huo una faida ya muda mrefu. 
Kampuni ya Artumas Group Inc. iliamua kubadilisha jina lake na kuwa 
Wentworth Resources Limited.
Wananchi 
wa Mtwara wanahitaji kujua kwa nini serikali haikutafuta njia mbadala ya
 kugharamia mpango wa kufua umeme na kuiunganisha Mtwara na gridi ya 
taifa?
Wentworth Resources wamefanya 
upembuzi yakinifu (feasibility study) na kubaini kwamba njia nzuri ya 
kibiashara na kiuchumi ya kutumia gas wanayoweza kuzalisha Mnazi bay 
hivi sasa ni kuanzisha kiwanda cha kutengeneza mbolea na kemikali 
nyingine Mtwara. Hata hivyo serikali imewamrisha kupeleka gesi 
watakayozalisha kwenye bomba la gesi la kwenda Dar es Salaam. Gazeti la 
Financial Time la London la tarehe 6 Desemba 2012 linaeleza
“Bob
 McBean, executive chairman of Wentworth Resources, which explores in 
Mnazi Bay, had been planning to use any gas finds together with an 
existing discovery to power a petrochemical plant to make Africa’s first
 home-produced fertiliser. “We can supply 80[bcf] right away but we’d 
have made more money with the plant,” anasema Bw.Mc Bean ambaye kampuni 
yake imetakiwa kusafirisha  gesi kwenda Dar es Salaam.
Kampuni
 inayochimba gesi inaamini kuwa kujenga kiwanda cha kutengeneza mbolea 
Mtwara kitakuwa na faida kubwa kwa kampuni yake. Isitoshe kiwanda hicho 
kitaongeza ajira kwa vijana wa Mtwara. Kitaanza kuijenga Mtwara kama 
kituo cha sekta ya gesi na viwanda vyake. Upatikanaji wa mbolea ya bei 
inayotengenezwa hapa nchini utasaidia kuendeleza kilimo na kuifanya 
kaulimbiu ya Kilimo Kwanza kutekelezwa kwa vitendo. Hatua ya serikali 
kuilazimisha Wentworth Resources kuipeleka gas ya Mnazi Bay kwenye bomba
 la gesi ili isafirishwe Dar es Salaam kunaathiri maendeleo ya Mtwara na
 Tanzania kwa ujumla.
Ujenzi wa bomba 
la Mtwara umeanza bila kuwa na mipango ya kuhakikisha kuwa kutakuwepo na
 gesi ya kutosha kuisafirisha hadi Dar es Salaam. Bomba hili litakuwa na
 uwezo wa kusafirisha futi za ujazo bilioni 200. Uwezo wa gesi ya Mnazi 
Bay kwa hivi sasa ni futi za ujazo bilioni 80. Hakuna mpango unaoeleweka
 wa kupata futi za ujazo bilioni 120 ili bomba la gesi liweze kutumiwa 
kikamilifu. Mpaka hivi sasa gesi kiasi cha futi za ujazo trilioni 33 
imegunduliwa hasa katika bahari yenye kina kirefu. Kuna uwezekano wa 
kugundua mafuta. Uchimbaji wa gesi hii bado haujaanza. Inaweza 
kuchukukua miaka 7 – 10 kabla ya shughuli ya uchimbaji wa gesi 
kukamilika na kuanza kuitumia ndani ya nchi au kuiuza nje ya nchi.
Upatikanaji
 wa mkopo wa masharti nafuu kutoka China wakujenga bomba la gesi ndiyo 
umeishawishi serikali kutekeleza mradi  huu haraka bila maandalizi ya 
uzalishaji wa gesi ya kutosha.Ni vyema serikali ingetekeleza mradi wa 
kufua umeme Mtwara na kuunganisha Mtwara na gridi ya taifa na kuruhusu 
kiwanda cha mbolea kuanzishwa Mtwara.
CUF
 Chama cha wananchi tunaitaka serikali kuzingatia kuwa, kwa kuwa mradi 
wa kujenga bomba la gesi uko katika hatua za mwanzo ni vyema serikali 
ikatathmini upya mantiki na faida za mradi huo. Mradi unaweza 
kutekelezwa kwa awamu. Awamu ya kwanza iwe kujenga bomba la gesi had 
Somanga Kilwa ili kuongeza uwezo wa kusafirisha gesi ya Songosongo kuja 
Dar es Salaam.
Kama nchi bado tuna 
udhaifu mkubwa wa kuandaa mipango na kusimamia utekelezaji wake. 
Serikali itufahamishe utekelezaji wa National Power Development Master 
Plan umefikia wapi? Vipi Mtwara development Corridor bado ipo?
Katika
 kusimamia sekta ya gesi tujifunze toka nchi ya Norway, Ili kuendesha 
shughuli za mafuta kwa ufanisi, Norway iliamua mapema kuwa makao makuu 
ya shughuli za mafuta utakuwa Stavange na siyo mji mkuu wa Oslo. Uamuzi 
huu umeufanya mji wa Stavange kukua na kuwa kituo cha biashara ya 
mafuta. Mtwara uwe mji mkuu wa shughuli zote za mafuta na gesi kwa 
sababu ina bandari asilia yenye kina kirefu na gesi imeanza kugunduliwa 
kanda ya kusini ya bahari ya Tanzania.
CUF
 tunasisitiza kwamba, malalamiko ya wananchi wa Mtwara ni ya msingi na 
wala hayaathiri umoja wa kitaifa. Maoni yao ya kuwa na viwanda 
vinavyotumia gesi Mtwara na maeneo mengine ya kusini yana mantiki ya 
kiuchumi. Serikali iwasikilize isiwabeze. Msimamamo wa CUF wa Dira ya 
Mabadiliko ni kuhakikisha kuwa maliasili na raslimali za nchi zinatumiwa
 vizuri kuleta neema kwa wananchi wote. Wananchi wa Mtwara wana haki ya 
kunufaika na neema ya gesi ya Mnazi Bay.
Mwisho Watanzania wote heri ya mwaka mpya – Happy New Year.
Imetolewa na
Mwenyekiti wa CUF-Chama cha wanachi, Taifa
Mhe. Prof. Ibrahim Lipumba