MAELEZO NA HOJA BINAFSI  YA KUPENDEKEZA BUNGE LIJADILI NA KUPITISHA 
MAAZIMIO YA HATUA ZA HARAKA ZA KUBORESHA UPATIKANAJI WA MAJI SAFI NA 
USHUGHULIKIAJI WA MAJI TAKA KATIKA JIJI LA DAR ES SALAAM KWA MUJIBU WA 
KANUNI YA 54 FASILI YA (1) YA KANUNI ZA KUDUMU ZA BUNGE TOLEO LA MWAKA 
2007
Mheshimiwa Spika; Awali ya yote niungane na wote wenye 
mapenzi mapema katika kuomba ulinzi wa Mwenyezi Mungu wakati tukitimiza 
wajibu wa kibunge kwa mujibu wa ibara ya 63 ya Katiba ya Jamhuri wa 
Muungano wa Tanzania wa kuwawakilisha wananchi, kuisimamia serikali, 
kuidhinisha mipango na kutunga sheria.
Mheshimiwa Spika; Aidha,
 kwa namna ya pekee ni kushukuru wewe binafsi na uongozi mzima wa Bunge 
kwa kunipa fursa hii adimu na adhimu ya kuwasilisha hoja binafsi kwa 
mujibu wa kanuni ya 54 fasili ya (1) ya kupendekeza bunge lijadili na 
kupitisha maazimio ya hatua za haraka zaidi za kuboresha upatikanaji wa 
maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar es salaam.
Mheshimiwa Spika; Maji
 ni uhai, hivyo matatizo ya upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji 
wa maji taka katika Jiji la Dar es salaam na nchini kwa ujumla kama 
hatua za haraka zisipochukuliwa yatageuka kuwa janga la taifa. Katika 
kila watanzania katika Jiji la Dar es Salaam na nchini; kwa wastani 
mmoja hapati huduma ya maji safi na salama na hali ni mbaya zaidi kuhusu
 ushughulikiaji wa maji taka.
Wakati baadhi ya nchi duniani 
zikielezwa kwenye kitabu cha hivi karibuni cha Mnukuzi Maalum wa Umoja 
wa Mataifa (UN Special Rapporteur) kuwa katika mwelekeo unaostahili 
kuhusu kuhakikisha haki ya maji na usafi wa mazingira (On the right 
track; Good practices in realizing the rights to water and sanitation: 
2012), hali ni kinyume kwa taifa letu. 
Ripoti ya Taasisi ya 
Kimataifa inayoshughulikia masuala ya maji (WaterAid: 2011) imeiweka 
Tanzania katika kundi la nchi ambazo haziko katika mwelekeo unaostahili 
wa kuboresha upatikanaji wa maji safi, ushughulikiaji wa maji taka na 
usafi wa mazingira (Policy Report: Off Track, Off Target; why 
investments in water, sanitation and hygiene is not reaching those who 
need the most). 
Mheshimiwa Spika;Hoja hii inalengo la
 kuibua mjadala wa hatua za haraka. Kimsingi hatua hizi za haraka 
hazitanufaisha Mkoa mmoja pekee kwa kuzingatia kuwa Mpango Maalum wa 
kutatua tatizo la maji katika Jiji la Dar es salaam ni kwa ajili pia ya 
maeneo mengine ya miradi iliyo sehemu ya mpango huo ya Morogoro mpaka 
Pwani. Aidha, kujadiliwa na kupitishwa kwa mapendekezo ya hoja hii 
kutaongeza pia msukumo wa miradi katika maeneo mengine ya mijini na 
vijijini katika mikoa mbalimbali nchini. 
Shukrani zangu za dhati
 ziwafikie wabunge wenzangu wa vyama vya upinzani na wa chama tawala kwa
 maoni na mapendekezo yenu yaliyoniwezesha kuirekebisha hoja hii pamoja 
na ushauri wa Katibu wa Bunge Dr Thomas Kashillilah na  maafisa na 
watendaji katika ofisi ya bunge, kambi rasmi ya upinzani na ofisi ya 
mbunge wa Jimbo la Ubungo mlioboresha hoja hii kwa manufaa ya Jiji la 
Dar es Salaam na Taifa kwa ujumla. 
Mheshimiwa Spika;Nitumie
 pia nafasi hii kuwashukuru Watanzania wenzangu wa kada, hadhi na ngazi 
mbalimbali katika taasisi na maeneo mengi ndani na nje ya nchi 
mnaoendelea kuniunga mkono kwa hali na mali katika kutimiza majukumu 
yangu ya kibunge na nafasi nyingine ninazozitumikia. 
Nawashukuru
 sala zenu wakati wa kesi ya msingi na rufaa ya kupingwa kwa matokeo ya 
ushindi wetu Jimbo la Uchaguzi la Ubungo; kwa pamoja tumeshinda, 
tuendelee na kazi. 
Aidha, pamoja na mjadala huu wa bungeni 
natarajia kupokea maoni na mapendekezo yenu kuhusu hoja hii kwa njia 
mbalimbali za mawasiliano ikiwemo kupitia mtandao wa 
http://mnyika.blogspot.com kwa hatua zaidi. Kaulimbiu yetu ni ile ile: AMUA; Maslahi ya Umma Kwanza. 
MAELEZO YA HOJA: 
Mheshimiwa Spika; Maji ni mojawapo ya mahitaji ya msingi 
ya binadamu, maji ni uhai. Upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama 
ni sehemu ya muhimu ya maendeleo ya nchi na maisha ya wananchi. Maji ni 
lazima kwa matumizi ya majumbani, maji ni muhimu ni moja ya malighafi 
muhimu katika kazi za uzalishaji iwe ni za viwanda, kilimo, mifugo na 
shughuli zingine za kiuchumi. 
Mheshimiwa Spika; Tanzania
 ni nchi ambayo imejaliwa vyanzo vingi vya maji, vinavyohusisha mito, 
mvua, maziwa na bahari; kuwepo kwa vyanzo hivi vya maji ni wazi kuwa 
nchi yetu inaweza kuepukana na shida ya maji inayoikumba jamii ya 
Tanzania iwapo tutaondoa udhaifu uliopo. Aidha, udhaifu huo unahusisha 
pia kuziweka vyanzo vyenyewe pia mashakani kwa matendo ya binadamu yenye
 kuathiri endelevu wa matumizi hali itayozua migogoro katika siku za 
usoni iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa. 
Mheshimiwa Spika;Upatikanaji
 wa maji safi na salama kwa urahisi wa bei unachangia katika kupunguza 
gharama za maisha; upatikanaji wa maji safi na salama karibu na makazi 
husaidia jamii, hususan wanawake, kutumia nguvu na muda katika 
uzalishaji na hivyo kuchangia katika kupunguza umaskini. Upatikanaji wa 
maji safi na salama ni nyenzo ya kulinda utu na afya; kinyume chake 
kuenea kwa magonjwa na maisha duni. 
Ifahamike kuwa kadiri ya 
Tathmini ya Hali ya watu na Afya ya mwaka 2010 (Demographic and Health 
Survey 2010); ni asilimia 4.8 tu ya kaya zilizopo vijijini ndiyo 
zinazopata maji katika eneo lao la kaya (water on premises) wakati ni 
asilimia 19.4 tu ya kaya kwa mijini ndizo zenye maji katika kaya zao.  
Hivyo kaya nyingi za Tanzania zinawekwa katika mazingira hatarishi kwa 
magonjwa ya mlipuko na mengine ambayo si ya mlipuko kutokana na uhaba wa
 maji, hali ikiwa tete zaidi katika maeneo yasiyopimwa yenye msongamano 
mkubwa wa watu katika Jiji la Dar es Salaam (slums).
Mheshimiwa Spika;Katiba
 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, toleo la mwaka 2005 
haijataja haki ya kupata maji safi na salama; huu ni kati ya upungufu 
ambao wananchi wa mijini na vijijini wanapaswa kuutolea maoni katika 
mchakato wa katiba mpya kwa kurejea mfano wa Katiba ya Afrika Kusini, 
Ghana na katiba mpya ya Kenya. 
Katika hatua ya sasa haki hii 
inapaswa kulindwa kupitia Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiuchumi, 
Kijamii na Kiutamaduni (“The International Covenant on Economic, Social 
and Cultural Rights”, ICESCR) wa 1966.   Mkataba huu unataja haki za 
kijamii na hivi karibuni Umoja wa Mataifa (UN) umeutafsiri kuwa ni 
pamoja na haki ya kupata maji safi na salama ambayo inapaswa kutiliwa 
mkazo katika nchi yetu. 
Suala la upatikanaji wa maji safi na 
kuweza kushughulia maji taka ni sehemu ya makubaliano ya kimataifa 
ambayo nchi yetu imeridhia kuingia  mathalani Malengo ya Milenia (MDGs);
 lengo namba saba (7) shabaha 10; la kupunguza nusu ya watu waoishi bila
 maji na safi ya kunywa na usafi wa msingi. Hatua za haraka za kuboresha
 upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka ni muhimu kama 
sehemu ya haki za binadamu lakini lina tija pia katika uzalishaji na 
uchumi wa nchi kwa kuwa tafiti zinaonyesha kwamba kudumu kwa matatizo 
hayo kunazigharimu nchi za Afrika, Tanzania ikiwemo wastani wa asilimia 
sita (6) ya pato la taifa (Gross Domestic Product).
Utafiti 
uliofanywa kwa Stockholm Environment Institute kwa kushirikiana na Benki
 ya Maendeleo Afrika mwaka 2006 kuhusu uhusiano kati ya maji na umaskini
 Afrika kwa kutumia mfano wa nchi yetu (Water and Poverty Linkages in 
Africa: Tanzania Case Study) umebainisha namna ilivyo vigumu kupima 
Tanzania inavyosonga mbele katika utekelezaji wa malengo ya maendeleo ya
 milenia yanayohusu maji. Aidha, utafiti huo umeeleza namna ambavyo bila
 kushughulikia kwa haraka matatizo ya maji jitihada za kupambana na 
umaskini zitakwama. 
Mheshimiwa Spika; Jiji la Dar es 
Salaam ni letu sote, ni mahali ambapo wabunge wote tunaishi kwa nyakati 
mbalimbali hususan wakati wa vikao vya kamati za kudumu za Bunge hivyo 
adha ya maji katika Jiji hili kila mmoja anaifahamu na anawajibu wa 
kushiriki katika kuipatia ufumbuzi. 
Kwa mujibu wa Sensa ya Watu 
na Makazi mwaka 2002 Mkoa wa Dar es salaam ulikuwa na jumla ya wakazi 
2,497,940 huku ukikadiriwa kuwa na kasi ya ongezeko la watu ya asilimia 6
 kwa mwaka; ikiwa ni juu ya wastani wa kitaifa wa asilimia 4.5, lakini 
kasi ya upatikanaji wa maji na ushughulikiaji wa maji taka ikiwa ndogo. 
Bunge ikiwa ni chombo cha juu cha kuisimamia Serikali linapaswa 
kuitafakari hali hii kwa upekee wake kwa kuwa itakuwa na athari kwa 
taifa kwa sasa na baadaye ikiwa hatua za haraka hazitachukuliwa. 
Hadi
 kufikia mwaka 2011 Jiji la Dar es Salaam linakadiriwa kuwa na watu 
zaidi milioni nne na laki tano likiwa na takribani nusu ya waajiriwa 
wote wa viwandani nchini. Hivyo kwa kurejea takwimu za ujumla za sensa 
zilizotolewa mwezi Desemba 2012 kwamba Tanzania kwa sasa ina watu zaidi 
ya milioni 44.9; hoja hii inalenga kupendekeza kwa bunge kujadili kuhusu
 mustakabali wa zaidi ya asilimia 10 ya Watanzania, lakini kwa kurejea 
utangulizi wangu maazimio ninayopendekeza yapitishwe yatakuwa na maslahi
 sio kwa wakazi wa Dar es salaam bali kwa taifa kwa ujumla mijini na 
vijijini. 
Mheshimiwa Spika; Upatikanaji wa maji 
katika Jiji la Dar es salaam miaka michache baada mwaka 1961 ulikuwa 
zaidi ya asilimia 68; hivi sasa miaka 50 baada ya uhuru tumerudi nyuma 
na upatikanaji ni kwa wastani asilimia 55 tu tena kwa mgawo. 
Zipo
 hisia kwamba Dar es salaam inapata huduma maji safi na maji taka kuliko
 miji na mijiji mengine nchini, lakini uhalisia unaonyesha kwamba hali 
ni bora kwa wachache wakati walio wengi hususan waoishi kwenye maeneo ya
 wananchi wa kipato chini hali ya upatikanaji wa maji ni duni kuliko 
miji na majiji mengine nchini. 
Jiji la Dar es Salaam ni la 
mwisho kwa kigezo cha wastani wa kitaifa wa upatikanaji wa maji 
ukilinganisha na majiji mengine ambayo yanafikia asilimia 75; hivyo 
hatua za haraka zinahitajika kurekebisha hali hiyo. 
Hatua hizo 
zitawezesha kupunguza kwa haraka tatizo hilo na kuelekeza nguvu zote 
katika maeneo ya vijijini palipo na shida kubwa badala ya mfumo wa sasa 
ambapo kwa miaka zaidi ya kumi, rasilimali zinatumika lakini 
kunakosekana ufumbuzi endelevu maeneo yote.  
Hatua za haraka 
zinapaswa kuchukuliwa kuhusu hali hii kwa kuzingatia kuwa idadi ya watu 
katika Jiji la Dar es salaam inaendelea kukua kwa kasi likiwa ni jiji la
 tatu kwa ongezeko kubwa la watu barani Afrika na la tisa duniani; 
matatizo ya upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka 
katika jiji kutokana na msongamano wake wa watu ni bomu la wakati. 
Mheshimiwa Spika; Mkoa
 wa Dar es Salam unapata maji kutoka mito na visima kwa matumizi ya 
nyumbani, viwanda, bustani, mifugo, usafi na Mazingira. Sehemu ya Jiji 
inayopata maji inahudumiwa na Kampuni ya DAWASCO (Dar es salaam Water 
Supply and Sewerage Company) ambayo imepewa mkataba na Mamlaka ya Maji 
Safi na Maji taka Dar es Salaam, DAWASA (Dar es Salaam Water Supply and 
Sewerage Authority) na maeneo yasiyo na mtandao wa DAWASA hupata maji 
kutoka visima vinavyoendeshwa na vyombo vya watumia maji, Taasisi na 
watu binafsi. 
Mheshimiwa Spika; Kwa upande wa Jimbo 
la Ubungo kama sehemu ya Jiji la Dar es salaam katika kufuatilia masuala
 ya maji nilianza kwa kufanya Kongamano la Maji mwanzoni mwa mwaka 2011 
ili kuwakutanisha wananchi, mamlaka husika na wadau wengine katika 
kuunganisha nguvu kupata ufumbuzi. Nikiri kwamba katika hatua za awali 
ushirikiano kutoka DAWASA, DAWASCO na Wizara ya Maji ulikuwa mdogo kwa 
kiwango cha kuamua kuwaunganisha wananchi kupitia ‘maandamano ya maji’ 
kwenda DAWASCO. Toka wakati huo ushirikiano umeongezeka kwa upande wa 
DAWASCO ambapo nimeshafanya nao ziara ya kikazi ya kata mbalimbali ya 
kutembelea maeneo yenye matatizo na hatua zimechukuliwa ambazo 
zimewezesha baadhi ya maeneo kuanza kutoka maji. Wakati wa hatua hizo 
tumewaonyesha DAWASCO biashara haramu ya maji iliyokuwa ikiendelea na 
baadhi ya maeneo wamechukua hatua ikiwemo kwa watendaji wao; hatua zaidi
 zinahitajika. 
Mheshimiwa Spika;Baada ya mwito wa 
mara kadhaa hapa bungeni; nashukuru pia Waziri wa Maji Prof. Jumanne 
Maghembe alifika Jimboni Oktoba 2012 kwa ajili ya uzinduzi wa visima 
katika maeneo ya King’ongo, Kilungule na Mavurunza na kuona hali halisi 
ya ugumu wa upatikanaji wa maji katika Mkoa wa Dar es salaam. 
Natambua
 pia jitihada zinazofanywa na wadau wengine wa maendeleo Jimboni Ubungo 
katika masuala ya maji hususani Shirika la Kibelgiji (BTC) katika maeneo
 ya Kwembe na Kibamba. Hata hivyo, yapo bado maeneo mengi yenye matatizo
 makubwa ya maji ikiwemo ya Msumi, Makabe, Msakuzi, Malambamawili, 
Msingwa, Goba na mengineyo mengi katika Jiji la Dar es salaam. Na hata 
yale yenye miundombinu ya maji kama Sinza, Manzese, Makurumla na mengine
 nayo hali ni tete. Hali iko hivyo katika Manispaa zote tatu za Ilala, 
Kinondoni na Temeke. 
Mheshimiwa Spika; Hata katika 
maeneo ya umma ya kuuzia maji, bei ipo juu kwa kuwa mamlaka zetu za 
kuratibu na kusimamia masuala ya bei kama EWURA imekuwa na udhaifu 
katika kusimamia na kuratibu bei elekezi wanazozitoa. Kwa mfano jiji la 
Dar es Salaam: vituo vingi vya kutoa huduma za maji chini ya 
DAWASCO/DAWASA maarufu kama “vioski vya maji” vimekuwa vikiongeza bei 
tofauti na bei elekezi toka EWURA ya Tsh 1 kwa lita moja yaani ndoo ya 
lita 20 kwa Sh 20 kinyume na waraka nambari 10-017 (Order No.10.017) wa 
Juni 8, 2010, agizo lililopaswa kuanza kutekelezwa Juni 15, 2010. 
Utafiti
 wa Shirika lisilo la kiserikali la Twaweza uliofanywa katika maeneo 
mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam uliopewa jina; “Bei ya maji Dar es 
Salaam Je, wanaoendesha maghati ya maji wanazingatia bei walizopangiwa?”
 uliweza kubainisha kukithiri kwa bei zilizoongezwa kinyume na taratibu 
na agizo hilo la EWURA katika maghati ya maji. Hata baada ya 
kurekebishwa kwa agizo hilo na bei kuongezwa kiasi bado maeneo hayo ya 
kuuzia maji kwa umma yamekuwa yakipandisha bei kupindukia. 
Mheshimiwa Spika; Kero
 kubwa zaidi iko wa wauzaji binafsi ambapo mazingira ya upungufu na 
ukubwa wa mahitaji umefanya maji yauzwe kama bidhaa ya anasa bila 
mamlaka EWURA kutunga kanuni wala kudhibiti bei, na kuachia soko holela 
yenye kuambana na hujuma za miundombinu katika baadhi ya maeneo ili 
kuongeza uhaba. 
Wananchi ambao wengi wao ni wa kipato cha chini 
hupata huduma ya maji kwa gharama kubwa ambayo huuzwa kwa kati ya Tsh 
300 hadi Tsh 500 kwa ndoo ya lita 20 kwa maeneo ya Dar es salaam. 
Kuwapo
 pia kwa watoa huduma wasio rasmi husababisha bei ya maji kuwa kubwa 
ambapo inakadiriwa kuwa 68% ya wakazi wanaoishi maeneo ya mjini yenye 
msongamano mkubwa hupata maji kutoka kwa wauzaji wasio rasmi. 
Hatua
 za haraka zinahitajika kudhibiti ongezeko kubwa la bei ya maji kwa 
wananchi wa kipato cha chini wanaotegemea kupata maji kutoka sekta 
binafsi ambapo wanaonunua maji kwa madumu hununua bei ambayo ni 
takribani mara 15 ya bei ya mteja anayepata huduma ya maji ya bomba. 
Mheshimiwa Spika; Kwa
 nyakati mbalimbali katika kipindi cha kati ya mwaka 2000 mpaka 2012 
Serikali imekuwa ikitoa ahadi bungeni ya kumaliza tatizo la majisafi na 
majitaka katika Jiji la Dar es Salaam bila utekelezaji sahihi, kamili na
 wa haraka. 
Malengo ya Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kuondoa 
Umaskini wa kwanza (MKUKUTA I) yaliyoingizwa pia katika ilani ya 
Uchaguzi wa CCM ya mwaka 2005-2010 hayakuweza kutekelezwa. 
Malengo
 mengine yameingizwa katika ilani ya CCM na Mkakati wa Kukuza Uchumi na 
Kuondoa Umaskini awamu ya pili (MKUKUTA II) ya kuboresha upatikanaji wa 
maji safi na usafi wa mazingira ifikapo mwaka 2015; nayo tukiwa mwaka 
2013 mwelekeo unaonyesha kwamba hayatafikiwa iwapo hatua za haraka 
zisipochukuliwa. 
Mara baada ya kupitishwa kwa Mpango Maalum wa 
Maji katika Jiji la Dar es salaam mwaka 2011, Rais alitangaza kwamba 
tatizo la maji kuwa historia mwaka 2013; ambapo ni mwaka huu. Hata 
hivyo, utekelezaji wa mipango hauashirii ahadi hiyo kutekelezeka na kwa 
mwelekeo wa sasa tatizo litaendelea mpaka baada ya mwaka 2016 iwapo 
hatua za haraka hazitachukuliwa. 
Mheshimiwa Spika;Mabomba ya ‘mchina’ bila maji na miradi hewa katika maeneo ya wananchi wa kipato cha chini Jijini Dar es Salaam: Kati
 ya mwaka 2003 mpaka 2010 Serikali ilitekeleza Mradi wa ukarabati na 
upanuzi wa miundombinu ya Majisafi na Majitaka Jijini Dar es salaam na 
maeneo ya Bagamoyo na Kibaha (Dar es salaam Water Supply and Sanitation 
Project-DWSSP). 
Mradi huo uliotumia dola milioni 164.6 hata 
hivyo mpaka sasa katika maeneo mengi mtandao wake maarufu kama mabomba 
ya wachina hautoi maji huku kukiwa na upungufu katika uzalishaji, 
upotevu wakati wa usafirishaji, udhaifu katika usambazaji na tuhuma za 
ufisadi katika matumizi. 
Hali hii ni kati ya matatizo yanayokera
 wananchi wa Jiji la Dar es salaam kwa kuwa na mabomba yasiyotoa maji 
kwa muda mrefu hata kwa mgawo maarufu mitaani kama mabomba ya ‘mchina’. 
Serikali
 ilieleze bunge lako sababu ya mabomba hayo kutokutoa maji mpaka hivi 
sasa, lini mabomba hayo yataanza kutoa maji katika maeneo ambayo maji 
hayatoki mpaka sasa na hatua gani zimechukuliwa wa waliotekeleza mradi 
huo bila kuzingatia maandalizi ya msingi. 
Ni muhimu hatua 
zikachukuliwa kwa wahusika kwa kuwa kitendo cha mabomba hayo kukaa muda 
mrefu bila kutoa maji inafanya miundombinu hiyo kuanza kuharibika au 
kuharibiwa ambayo ni hasara kwa taifa kwa kuwa pamoja na fedha 
zilizotumika kuweka mabomba hayo kupotea, fedha nyingine zitatumika 
katika hatua ya baadaye kufanya matengenezo kwenye maeneo 
yaliyoharibika. 
Aidha, yapo pia malalamiko ya kwamba yapo maeneo
 ambayo yalitoa maji mara chache kati ya mwaka 2009 na 2010 lakini baada
 ya hapo maeneo hayo hayajatoa maji tena mpaka sasa, Serikali itoe 
maelezo ya kitaalamu kwa bunge na kwa wananchi kuhusu sababu za maji 
hayo kutoka wakati huo na kutokutoka tena na hatua zinazochukuliwa 
kurekebisha hali hiyo. 
Mheshimiwa Spika; Kasoro 
katika mradi wa ukarabati na upanuzi wa miundombinu ya Majisafi na 
Majitaka Jijini Dar es salaam na maeneo ya Bagamoyo na Kibaha (Dar es 
salaam Water Supply and Sanitation Project-DWSSP); hazielezwi na 
wananchi pekee bali pia hata watafiti mbalimbali. 
Ripoti ya 
karibuni kabisa mwaka 2012 ya Shirika la Kimataifa la Water Aid ya 
utafiti uliofanywa ukihusisha wataalamu kutoka Overseas Development 
Institute na Chuo kimoja cha nchini Uingereza (SOAS) iliyofuatilia 
uwekezaji wa miradi ya maji mijini katika nchi za Ghana, Burkinafasso na
 Tanzania ( Stregthening pro poor targeting of investments by African 
utilities in urban water and Sanitation) ikiwemo namna miradi 
ilivyoshindwa kuwajali maskini na maeneo na kiwango cha hali ya maji 
kutokupatikana kinyume na malengo yaliyowekwa wakati wa kuanza kwa 
mradi. 
Mheshimiwa Spika; Matatizo ya kuwa na mabomba 
yasiyotoa maji hayapo tu katika mabomba waliyofungiwa wananchi majumbani
 bali pia kwenye visima na ‘vioski’/maghati ya jumuiya. Kuna udhaifu wa 
kuanzisha miradi ya jamii na kuacha kusimamia uendelevu (sustainability)
 wake na hatimaye baada ya muda mfupi miradi hiyo iliyotumia fedha za 
umma inabaki kuwa ‘miradi hewa’. 
Utafiti wa vituo vya maji 
uliofanywa June 2009 na Overseas Development Institute (ODI) chini ya 
udhamini wa shirika la Water Aid hapa nchini ulibainisha ni asilimia 54 
tu ya vituo vya maji vilivyopo ndivyo vinatumika kwa kutoa huduma ya 
maji. 
Hivyo kwa wastani baada ya miaka miwili tu ya kujengwa 
karibu nusu ya visima na vioski huwa haviendelei tena kufanya kazi.  
Utaratibu wa kukimbilia kutumia fedha za miradi ya maji kwa mwaka wa 
kibajeti mpya bila kuzingatia taarifa za utekelezaji na ufuatiliaji wa 
miradi ya nyuma ni hatari kwa uendelevu wa kuwepo kwa huduma ya maji kwa
 siku zijazo kama hatua za haraka hazitachukuliwa kuzingatia matatizo 
yaliyojitokeza katika miradi iliyopita na kuzingatia ubora na ufanisi 
katika miradi ya maji nchini. 
Mheshimiwa Spika; Utafiti
 uliofanywa na Economic and Social Research Foundation, umebaini 
utofauti wa utekelezaji wa miradi ya serikali na mashirika binafsi 
katika kauhakiki ubora wa matumizi ya fedha na huduma kwa jamii. Utafiti
 ulibaini kuwa katika miradi iliyofadhiliwa na mashirika ya maendeleo, 
wastani wa asilimia 67 ya vioski vilionekana kufanya kazi; wakati miradi
 ambayo imefadhiliwa na Serikali ni wastani wa asilimia 45 ya vioski vya
 maji vilikuwa vikifanya kazi katika maeneo hayo hayo. Utafiti huo 
ulihusu Mikoa ya Singida na Dodoma. 
Hali ni mbaya zaidi kwa 
upande wa Dar es Salaam ambapo kwa mujibu wa utafiti mwingine wa Shirika
 la Water Aid uliobainisha kuwa asilimia 85 ya vioski vilivyounganishwa 
Jijini Dar es Salaam havitoi maji, Asilimia 10 vinatoa maji kwa kusuasua
 na asilimia 5 tu ndivyo ambavyo vinatoa maji kwa uhakika. 
Mheshimiwa Spika;Kasoro katika utendaji na uwajibikaji wa mamlaka na vyombo vinavyohusika na utoaji na udhibiti wa huduma ya maji: Majukumu
 ya utoaji wa huduma ya maji jijini Dar es salaam na baadhi ya maeneo ya
 Kibaha na Bagamoyo yanafanywa na Mamlaka ya Majisafi na Majitaka 
(DAWASA) ambayo ni mmiliki, mkodishaji na msimamizi wa utoaji wa huduma 
ya majisafi na maji taka na ina wajibu wa kupanga na kugharamia 
utekelezaji wa miradi ya miundombinu, kuiendeleza na kugharamia 
matengenezo ya dharura na makubwa. 
Mwaka 2005 DAWASA iliingia 
mkataba wa miaka kumi (10) wa uendeshaji na Shirika la Maji Safi na Maji
 Taka Dar es Salaam (DAWASCO). Chini ya mkataba huo majumu ya DAWASCO ni
 kuendesha mitambo, kusimamia usambazaji wa maji na uondoshaji wa maji 
taka, kuuza maji kwa wateja , kutoa ankara kwa wateja, kukusanya 
maduhuli, kulipia gharama za uendeshaji, kutekeleza matengenezo makubwa 
yanayogharamiwa na DAWASA na kutekeleza uunganishaji wa maji kwa wateja 
wapya kwa kutumia mfuko wa maji. 
Kisheria na kimkataba DAWASA 
ina wajibu wa kuisimamia DAWASCO iliyoingia nayo mkataba; hata hivyo kwa
 kuwa yote ni taasisi na mashirika ya umma ambayo bodi zake na watendaji
 wake wakuu huteuliwa na mamlaka zile zile na kuripoti kwa watu wale 
wale, hali ambayo ina athari kwenye utendaji na uwajibikaji. 
Wakati
 umefika sasa wa mkataba huo kati ya DAWASA na DAWASCO kuwekwa wazi kwa 
umma; kufanyiwa tathmini ya miaka zaidi ya mitano iliyopita ya 
utekelezaji; kufanyiwa marekebisho kwa ajili ya kipindi kilichobaki na 
maandalizi kuanza ya mfumo bora unaopaswa kuanza kuandaliwa baada ya 
kuisha kwa mkataba huo mwaka 2015. 
Utoaji wa huduma ya maji 
unamhusu pia mdhibiti ambaye ni Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma ya Nishati
 na Maji (EWURA) yenye mamlaka ya kudhibiti utoaji wa huduma, 
kuidhinisha bei ya huduma ya maji safi na uondoaji wa maji taka pamoja 
na kutoa leseni za uendeshaji. Hata hivyo, EWURA imekuwa ikitoa 
kipaumbele zaidi kwenye kutumia mamlaka yake kudhibiti kwa karibu sekta 
ya nishati, huku udhibiti kwenye sekta muhimu ya maji hususan kwa upande
 wa watoa huduma binafsi ukiachwa uwe katika mfumo wa soko holela na 
kuchangia katika ongezeko la bei ya maji pamoja na ubovu wa huduma. 
Wakati
 umefika sasa wa Bunge kusimamia kwa karibu utekelezwaji wa  The Energy 
and Water Utilities Regulatory Authority Act (Sura ya 414) kifungu cha 6
 ambayo inaelekeza bayana kwamba wajibu wa EWURA ni pamoja na kulinda 
maslahi ya walaji na kuhamasisha upatikanaji wa huduma inazozidhibiti 
ikiwemo maji wa watumiaji wakiwemo wa kipato cha chini na walio 
pembezoni au katika mazingira magumu (low income and disadvantaged 
consumers). 
Aidha kwa mujibu wa kifungu cha 7 cha sheria hiyo 
majukumu ya EWURA ni pamoja na kupanga viwango cha ubora, viwango vya 
ugavi, kufuatilia utendaji ikiwemo uwekezaji na upatikanaji, kudhibiti 
bei na tozo na kushughulikia malalamiko na migogoro. 
EWURA 
itumie mamlaka yake pia kwa kutumia vifungu vya 16, 17, 18 na 19  
kuhakikisha kwamba masuala ya udhibiti wa bei hashaishii tu katika 
mamlaka za umma na pia ianze yenye uchunguzi juu ya kuporomoka kwa kiasi
 na kiwango cha huduma za maji katika Jiji la Dar es salaam na nchi kwa 
ujumla na kupendekeza hatua za ziada za haraka zaidi kuweza kuchukuliwa.
 
Mheshimiwa Spika; Mwaka 2011 Mkaguzi Mkuu wa Hesabu 
za Serikali (CAG) alifanya ukaguzi wa ufanisi (performance audit) kuhusu
 usimamizi wa usambazaji wa maji katika maeneo ya mijini ikiwemo Dar es 
salaam, hata hivyo taarifa yake ya Januari 2012 baada ya kutajwa bungeni
 miongoni mwa hati zilizowasilishwa; hatua za kutekeleza mapendekezo 
yake hazikupata usimamizi wa kutosha wa kibunge. 
Hivyo, ipo haja
 kwa kamati ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa niaba ya Bunge ipokee
 maelezo ya Serikali kuhusu utekelezaji wa mapendekezo yaliyomo kwenye 
ripoti hiyo ambayo yalilenga kuboresha utendaji wa DAWASA, DAWASCO na 
Mamlaka zingine za maji katika mikoa yote nchini na hatimaye kamati hiyo
 iwasilishe maoni na mapendekezo yake bungeni kwa ajili ya hatua zaidi. 
Mfumo duni wa ushughulikiaji wa maji taka ni bomu la wakati katika Jiji la Dar es salaam: Mheshimiwa Spika;Hali
 ni mbaya zaidi kuhusu uondoaji wa maji taka ambapo ni chini ya asilimia
 10 tu ya makazi ndiyo yaliyounganishwa katika mtandao wa maji taka na 
hivyo kuleta uchafuzi wa mazingira hususani katika maeneo yasiyopimwa. 
Hata katika maeneo yaliyopimwa Jijini Dar es salaam, mitandao ya maji 
taka haijakarabatiwa na kupanuliwa kwa wakati kwa kuzingatia ongezeko la
 watu suala ambalo lisipochuliwa kwa uzito unaostahili madhara yatatokea
 katika siku za usoni. 
Kwa mujibu wa ripoti ya EWURA ya mwaka 
2009, viwango vya huduma za uondoaji maji taka katika asilimia vimewekwa
 katika mabano Mwanza (3.1%), Moshi (5.8%) Arusha (7.0%), Dodoma 
(11.6%), Tabora (1.3%) na Tanga (9.3%). 
Taarifa hiyo inaeleza 
kuwa kwa upande wa Dar es salaam huduma za mtandao wa maji taka ni kwa 
kiwango cha asilimia 4.8 katika Jiji lenye msongamano mkubwa wa watu 
ambapo hata katika kata zilizopimwa kama ya Sinza na nyinginezo hali ni 
tete. 
Matokeo yake ni kuwawapo wakazi ambao hukiuka sheria na 
kusubiri mvua zinyeshe na kutiririsha maji taka hali ambayo ni hatari 
kwa afya za wananchi; kwa upande wa vijijini unafuu unapitakana katika 
ukubwa wa maeneo ya kuweza kuchimba vyoo, kinyume na mijini ambapo 
kadiri gharama za kukodi magari ya maji taka kwa sekta binafsi 
zisizodhibitiwa zinavyozidi kuongezeka ndivyo hatari zinavyozidi katika 
maeneo wanayoishi wananchi wa kipato cha chini. 
Udhaifu wa kiutendaji katika miradi ya maji inayosimamiwa na Halmashauri, kamati na jumuiya za watumia maji: Katika
 baadhi ya Halmashauri nchini ikiwemo za Jiji la Dar es salaam 
yamekuwepo matumizi mabaya na udhaifu wa kiutendaji katika miradi ya 
maji inayosimamiwa na Halmashauri kwa kushirikiana na kamati za maji au 
jumuiya za watumia maji. 
Kushindwa kushughulikiwa kwa matatizo 
ya kimfumo kuhusu uendeshaji wa miradi ya maji, kutokutekelezwa kwa 
wakati kwa vipaumbele vya maji kwa mujibu wa bajeti za Halmashauri 
iliyopitishwa na madai ya ufisadi katika miradi inayosimamiwa na kamati 
za maji au jumuiya za watumiaji katika baadhi ya maeneo kumesababisha 
wananchi kukosa huduma ya maji. 
Hata hivyo, pamoja na wananchi 
kuwasilisha malalamiko yao Wizara ya Maji na Ofisi ya Waziri Mkuu 
(Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa- TAMISEMI) ili kutimiza wajibu wa 
usimamizi na ufuatiliaji hatua za haraka zimekuwa hazichukuliwi hali 
inayohitaji mjadala na usimamizi wa kibunge. 
Katika mjadala 
utakaotokana na hoja hii, naamini wabunge wenzangu mchangia uzoefu wenu 
katika maeneo mnayotoka; naomba kwa upande wangu nitoe mfano wa Manispaa
 ya Kinondoni kuhusu mradi wa maji kata ya Goba. 
Tatizo la maji 
katika kata ya Goba limedumu sasa kwa kipindi cha miaka  zaidi ya 
mitano, pamoja na kwamba serikali inaowajibu kulinda maslahi ya walaji 
na kuhamasisha upatikanaji wa huduma ya maji kwa watumiaji wakiwemo wa 
kipato cha chini na walio pembezoni au katika mazingira magumu mamlaka 
zinazohusika hazijaweza kutimiza wajibu ipasavyo kuhusu kata ya Goba. 
Jitihada
 nyingi zimefanywa zilizofanywa na wakazi wenyewe kama njia mbadala ya 
kupata huduma hiyo muhimu kwa maisha ya Binadamu lakini zimekuwa 
zikikwamishwa na baadhi ya watendaji wa Halmashauri kwa kushindwa 
kusimamia kwa kurejesha na kupanua huduma hiyo muhimu kwa wananchi hata 
baada ya kupokea malalamiko katika nyakati mbalimbali . 
Mnaweza 
mkajiuliza sababu za suala hili kuvuka mipaka ya Baraza la Madiwani wa 
Manispaa ya Kinondoni, mpaka Bungeni; ni muhimu ifahamike mapema kwamba 
jitihada katika ngazi hizo kwa miaka mingi hazijaweza kuleta ufumbuzi 
hali inayohitaji chombo cha juu zaidi kwa niaba ya wananchi; yaani Bunge
 kujadili kwa kuwa Wizara ya Maji nayo imeshindwa kuchukua hatua 
zinazostahili kwa wakati. 
Historia ya tatizo hili inaonesha  
kuwa wakazi wa Goba wameshawahi kuandika barua kwa Waziri wa Maji  barua
 ya tarehe 15/10/2009 ikieleza kero ya maji kwa wananchi na wakimtaka 
alipatie ufumbuzi tatizo hilo na nakala ya barua hiyo ilipelekwa kwa 
mkuu wa mkoa wa Dar es salaam, na mkuu wa wilaya ya Kinondoni pamoja na 
hayo bado tatizo linaendelea kutopatiwa ufumbuzi huku wakazi wa Goba 
wakiendelea kukosa haki yao ya msingi kwa kuwa hakuna maisha bila maji. 
Kushindwa
 kulipatia ufumbuzi tatizo hilo kulipelekea wananchi pia kuandika barua 
 ya wazi kwa waziri mkuu mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda 
wakilalamikia mradi wa maji wa muda mrefu, pamoja na barua hiyo hakuna 
jitihada kamili zilizofanyika za makusudi kuondoa tatizo hilo. 
Utendaji
 mbovu na usimamizi mbovu wa miradi ya maji kwa manispaa ya Kinondoni  
chini ya kamati za maji zilizosababisha maji kukatwa kwa nyakati 
mbalimbali kati ya mwaka 2007 na 2011  ndiyo chanzo cha ukosefu wa maji 
kwa kipindi chote hicho. 
Katika kipindi cha karibuni, kamati ya 
maji Goba baada ya kukatwa kwa maji ilimwandikia barua mkurugenzi wa 
Manispaa ya Kinondoni tarehe 30/08/2011 yenye kumbukumbu namba 
G/WP/GOBA/VOL013/11 ikimuarifu Mkurugenzi kuhusu kusitishwa kwa huduma 
ya Maji kwa Wananchi wa Kata ya Goba. 
Katika barua hiyo ambayo  
mbunge nilipatiwa nakala yake, wananchi hao walimlalamikia mkurugenzi 
kwa kutozifanya kazi barua zao wakionesha mfano barua ya tarehe 
22/05/2011 na kumuomba Mkurugenzi kuchukua hatua za haraka ili huduma ya
 maji irejeshwe hata hivyo Manispaa ilizembea kuchukua hatua 
zinazostahili. 
Mnamo tarehe 21/03/2011, nilimwandikia barua 
Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni yenye namba : KUMB:OMU/MJ/005/2011  
yenye kichwa cha barua “Hatua za Haraka zinahitajika kuhusu mradi wa 
Maji Goba” . 
Kutokana na hatua stahili kutochukuliwa niliandika 
barua nyingine kwa Mkurugenzi  yenye kumb. OMU/MJ/008/2011  na 
kupendekeza hatua za haraka kuchukuliwa ikiwa ni pamoja na kuhakikisha 
fedha kutoka mfuko wa Jimbo Tsh 3,000,000.00 zinapelekwa haraka  katika 
Akaunti ya maji Goba ikiwa ni sehemu ya kuchangia katika wajibu wa 
manispaa za kujenga uwezo wa mradi husika na kuhakikisha wananchi 
wanapata huduma ya maji. 
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa 
ya Kinondoni  alifanya ziara Goba tarehe 31/01/2012 katika ziara ile 
mkurugenzi aliwaahidi wakazi wa Goba kurejesha huduma ya Maji ndani ya 
wiki moja lakini hadi sasa ni zaidi ya  mwaka wananchi bado  hawajapata 
huduma hiyo. 
Tarehe 18/03/2012 niliwaandikia barua tena DAWASA 
yenye kumbukumbu namba OMU/MJ/006/2012 kuhusu hatua ambazo DAWASA 
imechukuakuhusu matatizo ya maji katika kata ya Goba, katika barua hiyo 
nilitaka kujua hatua ambazo DAWASA imechukua kushughulikia matatizo ya 
maji Goba hususani juu ya kufanya majadiliano na Manispaa ya Kinondoni  
ili kuwa na mfumo endelevu zaidi wa utoaji wa huduma ya maji katika kata
 ya Goba ambayo ina ongezeko kubwa la wakazi, makazi na mahitaji mengine
 mengi kwa sasa. 
Wizara ya Maji na mamlaka zingine za kiserikali
 zinapaswa kuharakisha uchunguzi na kuchukua hatua dhidi ya wote 
waliohusika kusababisha uvunjwaji wa haki za watumiaji wa huduma ya 
maji, udhaifu wa usimamizi wa miradi ya maji na ukosefu wa huduma ya 
maji katika kata ya Goba kwenye Manispaa ya Kinondoni Jijini Dar es 
salaam ili kutoa fundisho kwa maeneo mengine.  
Kwa kufanya 
hivyo, Serikali ifuatilie mpaka Manispaa ya Kinondoni, DAWASA na DAWASCO
 wawezeshe huduma ya maji kurejea kwa wananchi, kupanua kwa dharura wigo
 wa upatikanaji wa maji kwa wananchi wa Kata ya Goba pamoja na kuboresha
 mfumo mzima wa upangaji, utekelezaji na usimamizi wa miradi ya maji 
katika Manispaa ya Kinondoni, DAWASA na DAWASCO. 
Aidha ili 
kupata ufumbuzi wa kudumu Wizara ichukue hatua za ziada ili kata ya Goba
 itoke katika kupatiwa huduma ya maji chini ya Manispaa ya Kinondoni na 
badala yake ihudumiwe na  DAWASA pamoja na DAWASCO ili kuwezesha 
uboreshaji mpana wa miundombinu. 
Mheshimiwa Spika;Upungufu katika usimamizi wa Sheria za maji na haja ya kuharakisha utungaji wa kanuni na marekebisho ya sheria husika: Hatua
 kuhusu uboreshaji wa huduma ya maji safi na uondoaji wa maji taka 
katika Jiji la Dar es salaam zinasimamiwa na sheria mbalimbali 
zilizotungwa na Bunge hili. 
Baadhi ya Sheria hizo ni pamoja na 
Sheria ya usimamizi wa rasilimali za maji ya mwaka 2009, Sheria ya maji 
safi na usafi wa mazingira ya mwaka 2009, sheria ya mamlaka ya udhibiti 
wa nishati na maji ya mwaka 2001 na sheria ya mamlaka ya maji safi na 
maji taka Dar es salaam ya mwaka 2001. Hata hivyo kumekuwa na upungufu 
wa kusimamia utekelezaji wa sheria hizo ikiwemo katika kutunga kanuni na
 kuchukua hatua kwa wakati. 
Serikali inapaswa kutoa maelezo 
bungeni ni kwanini mpaka mwezi Julai mwaka 2012 ilikuwa haijakamilisha 
kutunga kanuni zinazohusu uendeshaji wa Mfuko wa Taifa wa Uwekezaji wa 
Maji (National Water Investment Fund) toka Sheria husika itungwe mwaka 
2009. Bunge lijadili hoja hii ili pamoja na mambo mengine liisimamie 
Serikali mfuko huu uweze kufanya kazi kwa manufaa ya wananchi wote wenye
 kuhitaji uwekezaji toka mfuko huu kuondoa matatizo ya maji nchini 
ikiwemo Dar es salaam. 
Mheshimiwa Spika; Aidha, 
katika utekelezaji wa sheria umeonekana pia upungufu mwingine wa ziada 
unaohitaji marekebisho ya sheria mbalimbali. Mfano, ukiondoa maeneo ya 
mijini ambapo huduma za maji zinasimamiwa na mamlaka za maji safi na 
maji taka kwa upande wa Dar es salaam ikiwa ni DAWASA; maeneo ya 
vijijini kote nchini yanayohudumiwa na Halmashauri ikiwemo maeneo ya 
pembezoni ya Dar es salaam yanayohudumiwa na Manispaa, mifumo ya 
usimamizi ina udhaifu kutokana na upungufu wa kisheria. 
Kutokana
 na hali hiyo kwa nyakati mbalimbali limetolewa pendekezo na wabunge 
kwamba paundwe Wakala wa Maji (TANWATER) kama ilivyo Wakala wa Barabara 
(TANROADS) hata hivyo Serikali mpaka sasa haijatekeleza pendekezo hilo 
ambalo utekelezaji wake utahusisha pia marekebisho ya sheria mbalimbali.
 
Mheshimiwa Spika; Sheria ya Mamlaka ya Maji Safi na 
Maji Taka Dar es salaam ya mwaka 2001 nayo inahitaji kufanyiwa 
marekebisho makubwa. Kati ya mambo yanayohitajika kufanyika ni pamoja na
 kurekebisha ramani ya awali iliyopitishwa ikiwa ni sehemu ya sheria 
husika kuhusu eneo ambalo kwa mujibu wa sheria linapaswa kuhudumiwa na 
DAWASA (designed area) ili kuendana na ukuaji wa jiji pamoja na maeneo 
jirani ya Kibaha na Bagamoyo. 
Aidha, marekebisho mengine 
yanahitajika katika utaratibu mzima wa DAWASA kutoa mikataba kwa 
makampuni mengine kuendesha huduma ya maji kwa niaba yake ili kuepusha 
kasoro zilizojitokeza wakati wa mkataba wa City Water na kasoro nyingine
 zinazoendelea hivi sasa katika mkataba baina ya DAWASA na Kampuni ya 
Maji Safi na Maji Taka (DAWASCO). 
Marekebisho yanayohitajika 
kufanyika ni pamoja na ya kubadili muundo wa Bodi ya DAWASCO ikiwemo 
kuwezesha uwakilishi wa Halmashauri za Manispaa za Dar es salaam katika 
bodi ya DAWASA. 
Kwa upekee wa muundo wa Mkoa wa Dar es salaam, 
Halmashauri ya Jiji la Dar es salaam inafanya kazi ya uratibu tu wakati 
ambapo sehemu kubwa ya taratibu za ardhi, mipango miji na ujenzi ziko 
katika Halmashauri. Halmashauri za Manispaa ndizo ambazo zinahusika kwa 
kiwango kikubwa katika utekelezaji wa miradi ya maji ukiondoa ya DAWASA 
katika kata na mitaa mbalimbali ya Jiji la Dar es salaam. 
Hata 
hivyo, wakati halmashauri ya Jiji la Dar es salaam inawakilishwa kati 
bodi ya DAWASA, Manispaa zote tatu hazina uwakilishi hali ambayo 
inapunguza kiungo cha mawasiliano na kuathiri nguvu za Halmashauri 
katika kufuatilia miradi ya maji inayotekelezwa katika maeneo yao na 
wakati mwingine kuchelewesha miradi husika. 
Marekebisho ya 
sheria ya DAWASA yanapaswa kuhusisha pia kurekebisha adhabu zinazotokana
 na makosa ya uharibifu wa miundombinu ya maji, wizi wa maji safi na 
uunganishaji kinyemela wa mabomba ya maji taka; kwa kuwa adhabu zilizopo
 kiwango chake kimepitwa na wakati na hakilingani na kukithiri kwa 
makosa ya biashara haramu ya maji na hujuma katika miundombinu ya maji 
katika jiji la Dar es salaam. 
Kasoro katika upangaji na utekelezaji wa Mpango Maalum wa kutatua tatizo la Maji katika Jiji la Dar es salaam: Ikumbukwe
 kuwa katika kutafuta ufumbuzi Mwezi Machi 2011 Baraza la Mawaziri 
lilipitisha Mpango Maalum wa Maji Dar es salaam na Pwani wenye mgawanyo 
wa fedha ufuatao: 
Mahitaji ya fedha Mpango Maalum 
 
  | 
   
              Mahitaji ya fedha Mpango Maalum 
 | 
 
  | 
   
Na. 
 | 
  
   
Kazi
  zitakazotekelezwa 
 | 
  
   
Gharama 
2010-2013 
(SH.BILIONI) 
 | 
  
   
Makadirio
  kila mwaka wa fedha  (sh. bilioni) 
 | 
 
  | 
   
2010/11 
 | 
  
   
2011/12 
 | 
  
   
2012/13 
 | 
  
   
2013/14 
 | 
 
  | 
   
1 
 | 
  
   
Upanuzi
  wa mtambo wa Ruvu Juu 
 | 
  
   
17.25 
 | 
  
   
0.45 
 | 
  
   
6.00 
 | 
  
   
6.00 
 | 
  
   
4.80 
 | 
 
  | 
   
2 
 | 
  
   
Upanuzi
  wa mtambo wa Ruvu Chini 
 | 
  
   
122.50 
 | 
  
   
9.38 
 | 
  
   
24.28 
 | 
  
   
56.98 
 | 
  
   
31.88 
 | 
 
  | 
   
3 
 | 
  
   
Kazi
  ya visima vya Kimbiji na Mpera 
 | 
  
   
133.15 
 | 
  
   
10.35 
 | 
  
   
70.90 
 | 
  
   
29.25 
 | 
  
   
22.65 
 | 
 
  | 
   
4 
 | 
  
   
Ujenzi
  wa bwawa la Kidunda 
 | 
  
   
174.75 
 | 
  
   
3.00 
 | 
  
   
7.80 
 | 
  
   
83.70 
 | 
  
   
80.25 
 | 
 
  | 
   
5 
 | 
  
   
Upanuzi
  wa mtandao wa mabomba ya maji safi 
 | 
  
   
82.40 
 | 
  
   
- 
 | 
  
   
24.05 
 | 
  
   
37.15 
 | 
  
   
21.20 
 | 
 
  | 
   
6 
 | 
  
   
Uchimbaji
  na ukarabati wa visima katika maeneo yasiyo na maji. 
 | 
  
   
4.00 
 | 
  
   
1.50 
 | 
  
   
2.50 
 | 
  
   
- 
 | 
  
   
- 
 | 
 
  | 
   
7 
 | 
  
   
Kuimarisha
  utoaji wa huduma ya maji  
 | 
  
   
18.00 
 | 
  
   
- 
 | 
  
   
5.00 
 | 
  
   
6.00 
 | 
  
   
7.00 
 | 
 
  | 
   
8 
 | 
  
   
Kuboresha
  uondoaji wa majitaka (upanuzi wa mtandao na ujenzi wa mitambo mitatu ya maji
  taka) 
 | 
  
   
100.60 
 | 
  
   
- 
 | 
  
   
- 
 | 
  
   
50.30 
 | 
  
   
50.30 
 | 
 
  | 
   
9 
 | 
  
   
Miradi
  mingine 
 | 
  
   
0.20 
 | 
  
   
0.20 
 | 
  
   
- 
 | 
  
   
- 
 | 
  
   
- 
 | 
 
  | 
   
10 
 | 
  
   
Elimu
  kwa umma 
 | 
  
   
1.00 
 | 
  
   
0.50 
 | 
  
   
0.20 
 | 
  
   
0.20 
 | 
  
   
0.10 
 | 
 
  | 
   
 
 | 
  
   
Jumla Kuu 
 | 
  
   
653.85 
 | 
  
   
25.38 
 | 
  
   
140.73 
 | 
  
   
269.58 
 | 
  
   
218.18 
 | 
 
Katika kutekeleza mpango huu maalum, natambua kwamba upanuzi wa 
mfumo wa maji wa Ruvu Juu ikiwemo ujenzi wa wa Tanki la Kibamba na Bomba
 mpaka Kimara utafanyika na fedha za ujenzi huo kiasi cha dola milioni 
132 zimepatikana ikiwa sehemu ya mkopo wa dola milioni 178 kutoka 
Serikali ya India. Nafahamu pia kwamba ujenzi wa kupanua intake na 
machujio mapya ya maji unaendelea kwa udhamini wa Shirika la Milenia 
(MCC) wa kiasi cha dola za kimarekani milioni 36.8. Naelewa pia kuwa 
ujenzi wa bomba kutoka Ruvu Chini hadi Dar es Salaam utakaogharimu 
shilingi bilioni 122.5 za walipa kodi wa Tanzania umeanza.
Hata 
hivyo, kiwango cha uwekezaji huo hakijaweza kufikisha malengo 
yaliyopitishwa na Baraza la Mawaziri na Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano 
uliopitishwa na Bunge hili; kwa kuwa jumla mpaka mwaka wa fedha 
2012/2013, zilipaswa kuwa zimetumika au walau zimetengwa kiasi cha 
shilingi bilioni 435.67 ikiwa ni hatua ya haraka ya kuboresha 
upatikanaji wa maji safi na uondoaji wa maji taka katika Jiji la Dar es 
salaam na mikoa mingine inayoguswa na miradi hiyo ikiwemo ya Morogoro na
 Pwani. 
Mheshimiwa Spika; Hivyo, pengo hilo linapaswa
 kuzibwa kwa haraka kupitia nyongeza ya fedha katika Mpango wa Maendeleo
 na Bajeti ya mwaka 2013/2014 kwa kuchukua hatua za haraka. Serikali 
ieleze bungeni imefikia wapi katika kupata fedha za kulipa fidia ya 
maeneo ya hifadhi ya maji ya Kimbiji na Mpera kiasi cha shilingi bilioni
 27 ambayo ilipaswa kuwa imelipwa tangu mwaka 2011 na lini hasa ujenzi 
utaanza. 
Serikali ieleze iwapo ujenzi wa Bwawa la Kidunda Mkoani
 Morogoro unaokadiriwa kugharimu shilingi bilioni 175 utaingizwa katika 
vipaumbele vya taifa kwa mwaka 2013/2014 kwa kuzingatia umuhimu wa bwawa
 hilo katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi ambayo 
yenye kufanya upatikanaji wa maji kutokuwa na uhakika katika mto Ruvu 
kipindi chote cha mwaka na kusababisha uhaba wa maji kwa wananchi wa 
Pwani na Dar es Salaam. 
Hatua hizi zote zitakuwa na tija kwa 
wananchi wengi zaidi iwapo zitaambatana na ujenzi wa mfumo wa usambazaji
 wa maji katika maeneo ambayo hayakufikiwa katika awamu iliyopita; 
maeneo ambayo wananchi huyaita ‘yaliyorukwa katika uwekezaji wa mabomba 
ya mchina’ na ukarabati wa mifumo chakavu ya usambazaji wa maji. 
Serikali inapaswa kueleza ni lini maeneo hayo yatawekewa mtandao wa 
mabomba ambayo yanakisiwa kuhitaji jumla ya shilingi bilioni 82.4. 
Mheshimiwa Spika; Kwa
 upande mwingine, ili kuondokana na ‘bomu la wakati’ serikali ione 
umuhimu wa kutafuta fedha kwa haraka kiasi cha shilingi bilioni 100.6 
kwa ajili ya kuboresha huduma za maji taka kama ilivyoahidi kwa nyakati 
mbalimbali. 
Fedha hizi zinaonekana ni nyingi lakini ni matokeo 
ya udhaifu wa miaka mingi katika mipango miji katika Jiji la Dar es 
salaam hali inayosababisha gharama za usambazaji wa huduma ya maji safi 
na uondoaji wa maji taka kuwa kubwa. Upo umuhimu wa Wizara ya Ardhi, 
Nyumba na Maendeleo ya Makazi kutambua kwamba ongezeko la zaidi ya 
asilimia 70 ya maeneo ya makazi ambayo hayajapimwa katika Jiji la Dar es
 Salaam ikilinganishwa na wastani wa asilimia 30 wa miji mingine mikuu 
ya mikoa ni hali yenye kuathiri kwa kiwango kikubwa uchumi wa nchi na 
maisha kwa wananchi kwa ujumla. 
Ujenzi wa miundombinu hiyo mipya
 na ukarabati wa ile chakavu ya usafirishaji hautakuwa na maslahi tu kwa
 wananchi kwa kuwawezesha kupata huduma bali pia utakuwa na tija kwa 
nchi kwa kupunguza upotevu wa maji mpaka asilimia 25 na hivyo kudhibiti 
hasara ambayo inalikumba taifa hivi sasa kutokana na kiwango cha maji 
kinachopotea kwa Jiji la Dar es Salaam pekee. 
Bajeti ndogo ya sekta ya maji na utegemezi wa fedha kutoka nje: 
Mheshimiwa Spika; Fedha zinazotengwa kwa ajili ya miradi 
ya maendeleo kwenye sekta ya maji ni kidogo na hata hizo zinazotengwa 
utegemezi wa wahisani kutoka nje ni mkubwa kwa kiwango cha kuathiri 
miradi katika Jiji la Dar es salaam na nchi kwa ujumla. 
Kujibu 
wa ripoti ya Hali ya Umaskini na Maendeleo ya Watu mwaka 20112 (PHDR) 
Fedha za ndani za kutekeleza bajeti ya Sekta ya Maji imekuwa ikishuka 
mwaka hadi mwaka toka 57% katika mwaka wa fedha 2005/06 hadi 10% kwa 
mwaka wa fedha 2011/12. 
Hali hii imesabababisha kukithiri kwa 
utegemezi katika vyanzo vya mapato toka nje na kwa wabia wa maendeleo 
kuwezesha miradi ya maji; fedha ambazo hazipatikani kwa wakati na kwa 
kiwango kinachokidhi mahitaji. 
Kwa mwaka 2011/12 tumeshuhudia 
kutokutimizwa kwa azimio la serikali la kutenga kiasi cha Dola za 
Kimarekani 128 milioni kutekeleza Programu ya Kuendeleza Sekta ya Maji 
(WSDP) huku bajeti pangwa ikiwa ni dola za kimarekani 28 milioni tu kwa 
mwaka huo 2011/12. 
Tufahamu kwamba kupungua huku kwa kiwango cha
 bajeti katika sekta ya maji kunapingana hata na azimio la Sharm el 
Sheikh la nchi za Umoja wa Afrika la mwaka 2008 la kutaka dhamira na 
azma ya kuongeza kipaumbele cha kisiasa katika utengwaji na kuwekwa wazi
 kwa bajeti kwa ajili ya sekta ya maji safi na maji taka. 
Mheshimiwa Spika; Utekelezaji
 wa bajeti ya mwaka 2012/2013 umeendelea kuonesha upungufu katika utoaji
 wa fedha za miradi ya maendeleo katika sekta ya maji, taarifa 
zinaonyesha kwamba katika kipindi cha miezi sita ya kwanza Jumla ya 
Shilingi Bilioni 29 tu ndizo zilitolewa ikiwa ni sawa na asilimia 36 
katika fedha za ndani. Hali hii ni kidogo ikizingatiwa kiwango 
kilichoidhinishwa na tume ya mipango kikiwa ni shilingi 48,326,792,184 
kwa kipindi cha robo ya kwanza pekee. 
Mheshimiwa Spika, Mapungufu
 yanayojitokeza katika utekelezaji wa mipango ya serikali hususani 
katika ugawaji wa rasilimali fedha ambazo zimeidhinishwa na bunge katika
 huduma muhimu za jamii kama maji, matokeo yake ni kuwa na huduma mbovu,
 hivyo napendekeza bunge lijadili hali hiyo na kupitisha hatua za haraka
 ambazo zitanufaisha nchi kwa ujumla ikiwemo Jiji la Dar es Salaam. 
Hatua
 hizo zitawezesha  fedha za miradi ya maendeleo ya maji kutolewa kwa 
wakati katika miezi iliyobaki ya mwaka wa fedha 2012/2013 na kupewa 
kipaumbele katika Mpango wa Mwaka wa Maendeleo na Bajeti kwa mwaka 
2013/2014. 
Mheshimiwa Spika; 
Udhaifu katika utekelezaji wa Programu ya Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini: Tangu
 mwaka 2000 Bunge hili limekuwa likipewa ahadi za utekelezaji wa 
Programu ya Maji na Usafi wa Mazingira vijijini (RWSSP). Wakati maelezo 
ya kuanza kwa mpango huo yalipoletwa bungeni mwaka 2003, wakati huo 
ukiitwa mpango wa vijiji kumi (quick wins), yapo maeneo katika Jiji la 
Dar es salaam ambayo yalikuwa na vijiji na yaliingizwa katika mpango 
huo. Hata hivyo, mpaka leo miaka takribani kumi baadaye mwaka 2013 
maeneo hayo yakiwa yameshapanda hadhi na kuwa mitaa miradi hiyo 
haijatekelezwa kwa ukamilifu wake. 
Maeneo hayo yamekosa maji kwa
 pande zote, hayajahudumiwa na DAWASA na DAWASCO kwa kuwa yapo kwenye 
vijiji kumi; na mradi huo wa vijiji kumi haujaweza kuwafanya wananchi 
hao wapate huduma ya maji. 
Hali hii haihusu Halmashauri za 
Manispaa za Jiji la Dar es Salaam za Ilala, Kinondoni na Temeke; inahusu
 halmashauri zote nchini ambazo mpango huo ulipaswa kutekelezwa. Naamini
 kujadiliwa kwa hoja hii kutawezesha wabunge wenzangu kueleza pia uzoefu
 katika maeneo yenu ya vijijini na mijini hatimaye kutokana na 
mapendekezo ya hoja hii; Bunge likapitisha maazimio ambayo yataweza 
kuchangia katika kurekebisha hali hii. 
Mheshimiwa Spika; Programu
 hii ya Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini ilipaswa kutekelezwa kwa 
awamu nne, ambapo utekelezaji wa awamu ya kwanza baada ya kucheleweshwa 
toka mwaka 2003 ulipaswa kuanza mwaka 2005/2006 na kukamilika mwaka 
2010/2011. Kwa maneno rahisi ni kwamba hadi kufikia hivi sasa ilipaswa 
tayari maji yawe yameshapatikana katika vijiji kumi vya kila halmashauri
 nchini, hata hivyo ukomo wa muda wa awali ukiwa umeshapita kwa zaidi ya
 mwaka mmoja; utekelezaji katika maeneo mbalimbali nchini haukufanyika 
hata robo. 
Hali iko hivyo, wakati ambapo fedha zimetumika bila 
maji kupatikana; katika hatua hiyo ya kwanza jumla ya shilingi bilioni 
96.4 zimetumika kwenye “quick wins” hadi kufikia mwanzoni mwa mwaka 2012
 huku maji kwa sehemu kubwa kukiwa hakuna; hali ambayo ni matumizi 
mabaya ya rasilimali za umma. 
Mheshimiwa Spika; Katika
 ufuatiliaji wangu kuhusu masuala ya maji katika Manispaa za Jiji la Dar
 es salaam, katika halmashauri zingine na katika Wizara ya Maji 
nimebaini kwamba hali hiyo ilisababishwa na mikataba mibovu yenye dalili
 za ufisadi, kukosekana kwa uwajibikaji miongoni mwa makampuni 
yaliyopewa zabuni katika mazingira ya utata na udhaifu katika mchakato 
mzima wa zabuni na usimamizi wa miradi. 
Matokeo yake watafiti na
 wachimbaji binafsi wengi wao wakiwa hawana uwezo wa vifaa na wataalamu 
walipewa kazi na kulipwa fedha bila hata ya mchakato kukamilika; badala 
ya kuwekwa mfumo wa watafiti kuhusika pia na uchimbaji na kulipwa kwa 
kadiri na matokeo na hatua iliyofikiwa. Anafanya utafiti mwingine, 
anachukua fedha zake anakwenda; anayekwenda kufanya uchunguzi ni 
mwingine naye anachukua fedha zake anakwenda; anayejenga miundombinu ni 
mwingine, naye anaelekezwa eneo na baadaye kueleza kwamba hakuna maji 
huku hasara ikiwa imeshapatikana. 
Ripoti ya Tathmini (Appraisal 
Report) ya Programu ya Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (Rural Water 
Supply and Sanitation Program) ya mwaka 2010 inaonyesha namna ambavyo 
awamu ya kwanza katika ya mwaka 2007 mpaka 2010 ilivyoshindwa 
kutekelezwa kwa ufanisi. Usimamizi wa kutosha wa kibunge unahitajika 
kuhakikisha awamu ya pili (RSSWP Phase II), ambayo awali ilipangwa 
ifanyike kuanzia mwaka 2011 mpaka 2014 inafanyika kwa kuanzia na kufanya
 ukaguzi wa awamu iliyopita. 
Bunge lako lijadili hali hii na 
kupitisha maazimio yenye kuwezesha ukaguzi maalum ufanyike kwenye 
matumizi ya bilioni 96.4 za mradi wa maji safi na mazingira vijijini 
katika Jiji la Dar es salaam na Halmashauri zote nchini ili kasoro  hizo
 zisijirudie katika awamu ya pili ya programu hiyo inayotarajiwa kuanza 
mwezi Juni mwaka 2014. 
Mheshimiwa Spika; Baada ya 
maelezo hayo sasa naomba kuwasilisha hoja kwa mujibu wa kanuni ya 54 
fasili ya (1) (2) na (3) ya kupendekeza bunge lijadili na kupitisha 
maazimio ya hatua za haraka zaidi za kuboresha upatikanaji wa maji safi 
na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar es salaam. 
MABADILIKO
 KATIKA HOJA  KUHUSU HATUA ZA HARAKA ZA KUBORESHA UPATIKANAJI WA MAJI 
SAFI NA USHUGHULIKIAJI WA MAJI TAKA KATIKA JIJI LA DAR ES SALAAM (Kwa mujibu wa Kanuni 55 (10) ya  Kanuni za Kudumu za Bunge) 
Kwa
 kuondoa maneno kuanzia “KWA KUWA, kati ya mwaka 2003….. (yaliyo kuanzia
 katika ukurasa wa 42 na kuendelea mpaka ukurasa wa 45 yanapoishia 
maneno maneno)…….. mapendekezo ya mpango wa taifa” 
Na kuingiza maneno: “
KWA KUWA,
 Programu ya Maji Safi na Mazingira Vijijini ikiwemo katika Manispaa za 
Jiji la Dar es Salaam ilipaswa kutekelezwa kuanzia mwaka 2005/2006 na 
kukamilika mwaka 2010/2011 kwa kugharimu dola za kimarekani milioni 292 
hata hivyo tathmini ya miaka miwili na nusu ya utekelezaji (mid term 
review) imebanisha kasoro nyingi katika utekelezaji. 
KWA KUWA,
 Kati ya mwaka 2003 mpaka 2010 Serikali ilitekeleza Mradi wa ukarabati 
na upanuzi wa miundombinu ya Majisafi na Majitaka Jijini Dar es salaam 
na maeneo ya Bagamoyo na Kibaha (Dar es salaam Water Supply and 
Sanitation Project-DWSSP) uliotumia dola milioni 164.6 hata hivyo mpaka 
sasa katika maeneo mengi mtandao wake maarufu kama mabomba ya wachina 
hautoi maji huku kukiwa na upungufu katika uzalishaji, upotevu wakati wa
 usafirishaji, udhaifu katika usambazaji na tuhuma za ufisadi katika 
matumizi. 
NA KWA KUWA, Wizara ya Maji iliandaa waraka 
maalum wa kuiomba Serikali kutenga kiasi cha shilingi bilioni 653.85 
Mpango Maalum 2011-2013 wa kuboresha huduma za majisafi na uondaji wa 
majitaka katika Jiji la Dar es salaam na kupitishwa na Baraza la 
Mawaziri mwezi Machi 2011 lakini utekelezaji wake unaelekea 
kucheleweshwa mpaka mwaka 2016. 
NA KWA KUWA, katika mwaka
 wa fedha 2011/2012 na 2012/13 Serikali haikutenga kiwango kamili cha 
fedha kwa kuzingatia Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano 
ulioidhinishwa na Bunge na kwa kuzingatia mgawanyo wa Mpango Maalum wa 
Maji Safi na Maji Taka katika Jiji la Dar Es Salaam na kauli ya Serikali
 ya tarehe 7 Novemba 2012. 
NA KWA KUWA, kwa mujibu wa 
ibara ya 62 (2)  na (3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 
mwaka 1977 , Bunge ndicho chombo kikuu chenye madaraka, kwa niaba ya 
wananchi, kuisimamia na kuishauri Serikali na vyombo vyake vyote katika 
utekelezaji wa majukumu. 
NA KWA KUWA, kwa mujibu wa ibara
 ya 63(3) katika utekelezaji wa madaraka yake bunge laweza kujadili na 
kuidhinisha mpango wowote wa muda mrefu au wa muda mfupi unaokusudiwa 
kutekelezwa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kutunga sheria 
pale utekelezaji unapohitaji kuwapo sheria. 
NA KWA KUWA, 
Malengo ya Kitaifa yalikuwa ni kuwapatia wakazi wa Mjini maji kwa 
asilimia 90 ifikapo mwaka 2010 na kwamba malengo hayo kwa Jiji la Dar es
 Salaam yamesogezwa mbele na kuwekwa malengo mapya ya upatikanaji wa 
huduma ya maji safi kufikia asilimia 90 na uondoaji wa maji taka kufikia
 asilimia 30 ifikapo mwaka 2015. 
KWA HIYO BASI, Bunge 
linaazimia kwamba Serikali ichukue hatua za haraka zaidi za kuboresha 
upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la 
Dar es salaam: 
NA KWAMBA, Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za 
Serikali (CAG) afanye ukaguzi  maalum wa matumuzi ya fedha matumizi ya 
bilioni 96.4 za mradi wa maji safi na mazingira vijijini katika Jiji la 
Dar es salaam na Halmashauri zingine na kuwezesha hatua za ziada 
kuchukuliwa. 
NA KWAMBA, Kufuatia kauli iliyotolewa 
bungeni tarehe 7 Novemba 2012 kuhusu Mpango Maalum wa kutatua tatizo la 
maji katika Jiji la Dar es salaam uliopitishwa mwezi Machi 2011 Serikali
 izingatie makisio ya awali ya gharama za mpango huo na kuingiza 
mahitaji yaliyobaki kwenye Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Mwaka 
2013/2014 na Bajeti ya mwaka 2013/2014. 
NA KWAMBA, Mpango
 wa dharura wa kupunguza kero ya maji ulionza kutekelezwa na Wizara ya 
Maji kwa kushirikiana na DAWASA kuanzia Juni 2010 unaohusisha uchimbaji 
wa visima 29 uliopaswa kukamilika Oktoba 2011 uwekewe muda wa ukomo wa 
kukamilika kwa dharura katika maeneo ambayo miradi haijakamilika mpaka 
hivi sasa ikiwemo iliyozinduliwa Oktoba 2012 yenye kuhitaji miundombinu 
ya ziada kufikia wananchi zaidi. 
NA KWAMBA, Mkaguzi Mkuu 
wa Hesabu za Serikali (CAG) afanye ukaguzi wa thamani ukilinganisha na 
ufanisi (Value for Money) wa Mradi wa ukarabati na upanuzi wa 
miundombinu ya Majisafi na Majitaka Jijini Dar es salaam na maeneo ya 
Bagamoyo na Kibaha (Dar es salaam Water Supply and Sanitation 
Project-DWSSP) kwa kurejea ukaguzi wa kiufundi (technical Audit) 
uliofanywa na kampuni ya Howard Humphreys. 
NA KWAMBA, 
EWURA ifanye ukaguzi wa kiufanisi (performance audit) wa miradi ya 
visima vya maji takribani 200 ambavyo vilichimbwa na serikali na 
kukabidhiwa kwa DAWASCO, jumuiya za wananchi na taasisi mbalimbali 
lakini haitoi huduma inavyostahili kwa kadiri ya malengo ya awali. 
NA KWAMBA,
 EWURA iharakishe kukamilisha mchakato ulioanza wa kutunga kanuni za 
udhibiti wa ubora na bei ya huduma ya maji kwa upande wa sekta binafsi 
katika Jiji la Dar es salaam. 
NA KWAMBA, Kamati husika ya
 Bunge ijadili taarifa ya ukaguzi wa ufanisi kuhusu usimamizi wa 
usambazaji wa maji katika maeneo ya mijini (performance audit report on 
the management of water distribution in urban areas) ya Januari 2012 ili
 maoni na mapendekezo yazingatiwe wakati wa kujadili na kushauri kuhusu 
mapendekezo ya mpango wa taifa na bajeti ya nchi. 
NA KWAMBA,
 Serikali iwasilishe bungeni haraka iwezekanavyo muswada wa sheria ya 
marekebisho ya sheria mbalimbali za majisafi na majitaka (Water Supply 
and Sanitation Miscellaneous Amendment Bill) ili kushughulikia upungufu 
uliojitokeza katika utekelezaji wa sheria zilizopo na kuweka mfumo 
thabiti wa usimamizi wa sekta ya maji nchini.” 
Naomba kuwasilisha. 
………………… 
John John Mnyika(Mb) 
Jimbo la Uchaguzi-Ubungo