Facebook Comments Box

Friday, September 9, 2016

TEMEKE WACHAPWA NA MBEYA AIRTEL RISING STARS

Timu ya Temeke ya wavulana imeshindwa kutamba mbele ya Mbeya baada ya kumkubali kichapo cha 2-0 kwenye mashindano yanayoendelea ya Airtel Rising Stars fainali za taifa zinazochezwa kwenye uwanja wa Karume Jijini Dar es Salaam.


Mchezajiwa timu ya Temeke Ismail Kovu (no 4) akimiliki mpira mbele ya mchezaji wa timu ya Mbeya Pius Griton (no 15) wakati wa mashindano yanaoendelea ya Airtel Rising Stars fainali za taifa kwenye uwanja wa Karume jijini Dar es Salaam. Mbeya ilishinda 1-0.
Kwenye mechi ya kwanza ya michuano hiyo iliyochezwa Jumatano 7 Septemba – timu ya wasichana ya Kinondoni iliifunga Arusha 4-0. Kwenye mechi ya kwanza iliyochezwa Jumanne 6 Septemba, Arusha waliwafunga Lindi 2-0. Magoli ya Kinondoni yalifungwa na Anna Audela dakika ya 35 kwa njia ya penati. La pili likifungwa na Maimuna Abasi dakika 39, la tatu Aisha Juma dakika ya 41 na la nne likifungwa na Vaileth Tadeo dakika ya 60.
Mchezajiwa timu ya Temeke Ismail Kovu (nyeupe) akitafutajinsi ya kuwatokamabeki wa timu ya Mbeya wakati wa mashindano yanaoendelea ya Airtel Rising Stars fainali za taifa kwenye uwanja wa Karume jijini Dar es Salaam. Mbeya ilishinda 1-0.
Kwenye mechi ya Mbeya na Temeke, timu ya Temeke ndio walianza na kasi baada ya kuwa wameshinda mchezo wa kwanza 4-1 dhidi ya Kinondoni, lakini mabeki wa Mbeya walisimama imara na kudhiti washambualiaji wa Temeke. Kwa dakika takribani 20 za kipindi cha kwanza, timu ya Temeke waliweza kuwadhiti vizuri Mbeya na hivyo kusababisha mpira kuchezwa nusu ya uwanja.
Hata hivyo, kadri muda ulivyokuwa unaenda, timu ya Mbeya iliweza kuanza mashambulizi taratibu na ilipofika dakika ya 45, Mbeya waliweza kuonana vizuri na kucheza pasi za uhakika ambapo Lameck Juma alitoa pasi nzuri kwa Ernest Kamange ambaye alimpiga beki wa Temeke na kuachia shuti lililomshindwa mlinda mlango wa Temeke na hivyo kuiandikia timu yake bao la kwanza. Timu zilienda mapumziko Mbeya ikiwa inaongeza 1-0.
Beki wa timu ya Temeke Ismail Kovu (nyeupe) akichuana na mshambuliaji wa timu ya Mbeya Biva Steven wakati wa mashindano yanaoendelea ya Airtel Rising Stars fainali za taifa kwenye uwanja wa Karume jijini Dar es Salaam. Mbeya ilishinda 1-0.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku Temeke wakitafuta bao la kuzawazisha bila mafanikio, Temeke waliendeleza mashambulizi lakini yote yaliishia kwa mabeki na kwa mlinda mlango ambaye alionyesha mpira wa kuvutia. Mpaka dakika ya 90 Temeke 0 Mbeya 2.

Beki wa timu ya  Temeke Ismail Kovu (nyeupe) akichuana na kiungo wa timu ya Mbeya SalumLuhinda wakati wa mashindano yanaoendelea ya Airtel Rising Stars fainali za taifa kwenye uwanja wa Karume jijini Dar es Salaam. Mbeya ilishinda 1-0.
Fainali za Airtel Rising Stars 2016 zilifunguliwa Jumanne 6 Septemba na Mkuu wa Wilaya ya Ilala Sophia Mjema kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda. Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Mkuu huyo wa Ilala alitoa Shukrani kwa kampuni ya Airtel Tanzania kuweza kuwekeza kwenye soka la vijana. ‘ Nataka nitoe pongezi za dhati kwa wenzetu wa Airtel kwa kudhamini mashindano haya. Hii inasaidia vijana kuweza kujipatia ajira kwani kwa wale watakaofanya vizuri watachanguliwa kujiunga na timu yetu ya vijana ya Serengeti Boys pamoja na Twiga stars, alisema Mjema.  Aliongeza kuwa Wazazi wanatakiwa wawape watoto uhuru wa kuchangua fani zao na kusimamia bega kwa bega kuwaunga mkono.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mawasiliano Airtel Tanzania Beatrice Singano alisema Airtel wataendelea kudhamini mashindano haya hapa nchini.


OKWI KUREJEA SIMBA?

Emanuel Okwi

Mshambuliaji Emmanuel Okwi ambaye uhamisho wake umekuwa ukizungukwa na maswali kila aendako, ameingia katika utata mwingine baada ya ripoti mpya kudai kwamba alisaini mkataba wa miaka mitano wa kuichezea timu ya SønderjyskE licha ya timu hiyo ya Denmark kutotoa hata senti kwa klabu yake ya Simba.

Utata huo mpya umefuatia Wadenmark hao kutaka kumrejesha Okwi Simba kwa mkopo wa miezi sita baada ya kukwama kuipata leseni yake ya uhamisho ya kimataifa (ITC), ambayo Simba imesema haitaitoa hadi itakapolipwa ada ya uhamisho dola 110,000 (sawa na Sh. milioni 220).

Kumekuwa na mitazamo kwamba kutolewa kwa mkopo kwa Okwi Simba kunaweza kuwa ni janja ya timu hiyo ya Denmark kuvizia Mganda huyo amalize mkataba wake Msimbazi unaomalizika Mei mwakani ili imchukue bure.

Hata hivyo, klabu kubwa kama ya Simba inatarajiwa kwamba ilisaini mkataba na SønderjyskE ambao unaifunga klabu hiyo ya Ligi Kuu ya Denmark kwamba lazima ilipe deni hilo, hata kama itamleta Msimbazi kwa mkopo.

Taarifa nyingine zinasema kuwa klabu hiyo ya Denmark imefikia uamuzi huo baada ya kumnasa mchezaji mwenye kiwango cha juu zaidi ukilinganisha na Okwi na gharama zake za usajili ni za chini.

Rais wa Simba, Evans Aveva, alisema kwamba kwa sasa wao wanachofuatilia ni kuhakikisha wanalipwa kiasi hicho cha fedha ndipo waruhusu usajili wa njia ya mtandao ufanyike.

Aveva aliweka wazi kwamba, walimuuza Okwi baada ya mchezaji kuangalia maslahi yake na sasa umefika wakati klabu kuhakikisha inapata haki yake na si kuona makosa yaliyofanyika huko nyuma yanajirudia.

Katika uongozi wa Mwenyekiti, Ismail Aden Rage, Okwi aliuzwa kwa klabu ya Etoile du Sahel kwa dau la Dola za Marekani 300,000 na baadaye mshambuliaji huyo alirejea klabu yake ya zamani ya SC Villa na muda mfupi alijiunga na Yanga.

Mganda huyo aliichezea Yanga katika kipindi kifupi na kurejea Simba kwa kueleza kuwa mabingwa hao wa Tanzania Bara hawakutimiza baadhi ya vipengele vilivyoko kwenye mkataba wake.

CHANZO: NIPASHE


NHC YAZUIWA NA MAHAKAMA KUZIPIGA MNADA MALI ZA MBOWE



Mahakama Kuu ya Tanzania, Kitengo cha Ardhi imeliamuru Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kutouza au kupiga mnada mali za Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), mpaka kesi ya msingi itakapomalizika.

Shirika hilo lilizichukua mali mbalimbali za kampuni za Mbowe ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Hai, wiki iliyopita kupitia mawakala wa kampuni ya Fosters Auctioneers katika jengo lililopo makutano ya mitaa ya Mkwepu na Indira Gandhi (Makunganya) jijini Dar es Salaam.

Hatua hiyo ya NHC ilitokana na mgogoro wa muda mrefu, wakimtuhumu Mbowe kushindwa kulipa deni la zaidi ya Sh. 1.3 bilioni, ikiwa jumla ya fedha za kodi ya kupangishwa kwenye jengo hilo.

Kutokana na mvutano huo, Mbowe alifungua kesi katika Mahakama Kuu, Kitengo cha Ardhi, kupinga hatua ya NHC kumuondoa katika jengo hilo, pamoja na kuchukua mali zake huku wakitangaza kuzipiga mnada baada ya siku 14 tangu kuzichukua.

Jana, Jaji Siyovelwa Mwangasi alitoa zuio na kuiamuru NHC kutouza wala kupiga mnada mali hizo za Mbowe mpaka mahakama hiyo itakapotolea uamuzi katika kesi ya msingi.

Katika kesi hiyo namba 722 ya mwaka 2016, Mbowe anawakilishwa na Mawakili  Peter Kibatala na Omary Msemo.

Jaji Mwangasi amesema kuwa, anakubaliana na maombi ya mlalamikaji na kutaka mali hizo zisiuzwe hadi hapo mahakama itakapofanyia uamuzi kesi ya msingi.
Hatua hiyo inakuja baada ya upande wa NHC kupitia mawakili wake Aloyce Sekule na Miriam Mungula kushindwa kuwasilisha hoja za msingi kueleza, ni kwanini zuio hilo lisitolewe hadi hapo kesi ya msingi itakapoanza kusikilizwa.

Awali, mawakili wa NHC, walidai kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza maombi ya Mbowe kwa kuwa hakuna kesi ya msingi ambayo imefunguliwa, hivyo maombi hayo yatupiliwe mbali.

Wakili Kibatala alijibu hoja hiyo kwa kusema, hatua ya kuwasilisha maombi hayo inalenga kubaini kama kweli Mbowe anadaiwa kodi ama la.

Kibatala alidai kuwa mahakama hiyo ina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo, hivyo inaweza ikatoa uamuzi wowote, na ndiyo maana wamewasilisha maombi hayo ili itolewe amri ya muda ya kuzuia mchakato huo.

Miongoni mwa hoja za Mbowe alizoziwalisha mahakamani hapo, ni pamoja na hoja kuwa, yeye (Mbowe) na shirika hilo walikubaliana kwamba atalikarabati na kulipanua jengo hilo kwa asilimia 100. Makubaliano ambayo yaliingiwa mwaka 1997.

Amedai kuwa katika makubaliano hayo yeye na NHC walikubaliana watamiliki jengo hilo kwa pamoja kwa muda wa miaka 99, huku Mbowe katika mgawanyo wa mapato akitakiwa kupata asilimia 75 na NHC ikitakiwa kupata asilimia 25.

Pia alieleza kuwa katika makubaliano hayo, licha ya mwenendo wa kibiashara kutokuwa mzuri, muda wote alikuwa akilipa asilimia hiyo 25, kwa mujibu wa makubaliano yao.

Hivyo kutokana na hatua ya NHC kuvunja mkataba huo kwa kumtoa kwenye jengo na kuchukua mali zake, anaiomba mahakama iliamuru shirika hilo limlipe fidia.
Mbowe aliondolewa kwenye jengo husika mnamo Septemba mosi kwa madai ya kushindwa kulipa deni la zaidi ya Sh. bilioni 1.3.

Mawakala wa NHC walifika katika jengo hilo saa 12:30 asubuhi na wafanyakazi zaidi ya 50 na kwenda moja kwa moja katika kampuni ya Free media pamoja na ukumbi wa Bilcanas na kuchukua vifaa mbalimbali ikiwemo, meza, viti na kompyuta.




YANGA HAWAKOSI SABABU


Kikosi cha Yanga

Timu ya Yanga ya Dar es Salaam kama ilivyo kawaida yao wakifungwa au kutoka sare huwa hawakosi sababu tayari wameweka hadharani sababu ya wao kutoka sare na Ndanda Fc wana Kuchele kuwa eti Wachezaji wao walikuwa na mgomo baridi.

Na imedaiwa kuwa timu haikufanya mazoezi ya kwa siku tatu mfululizo kabla ya mchezo huo wa ligi kuu yaVodacom Tanzania Bara jambo ambalo hata hivyo, Katibu wa Yanga, Baraka Deusdedit alilikana.

Imedaiwa wachezaji wa Yanga waligoma wakishinikiza kupewa mishahara yao ya mwezi Julai hadi walipokutana na Mwenyekiti, Yussuf Manji Jumatatu ambaye pia ni mfadhili ndipo wakasitisha mgomo wao.


Yanga ikasafiri Jumanne asubuhi kwenda Mtwara kwa ajili ya mchezo na Ndanda, uliomalizika kwa sare ya 0-0. Na waliingia kwenye mchezo wa huo baada ya mazoezi mepesi tu, tena ya siku moja Uwanja wa Nangwanda.  

Yanga ilicheza kichovu ikilazimishwa sare na Ndanda  kumbe kilichojificha nyuma ya hali hiyo ni timu kutofanya mazoezi kwa siku tatu.



Na inadaiwa huo ni mgomo wa pili ndani ya wiki mbili, baada ya awali wachezaji kugoma kuelekea mchezo wa mwisho wa Kundi A Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya TP Mazembe mjini Lubumbashi, DRC.

Inadaiwa waligoma kushinikiza kulipwa posho walizoahidiwa na Manji kwa kutwaa mataji matatu (Ligi Kuu, Kombe TFF na Ngao ya Jamii) msimu uliopita, kuwafunga mahasimu Simba mechi zote mbili na kufuzu hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho.



Hata hivyo, baadaye timu ilisafiri kwenda Lubumbashi, ambako ilichapwa mabao 3-1 na TP-MAZEMBE ya huko.



SOMA VICHWA VYA HABARI VYA MAGAZETI YA LEO IJUMAA TAR 09-09-2016 HAPA




















Monday, August 29, 2016

VITUO VIWILI VYA REDIO VYAFUNGIWA KWA MUDA USIO JULIKANA LEO



Waziri wa Habari, Utamaduni , Sanaa na Michezo Nape Moses Nnauye amezifungia radio mbili kwa muda usiojulikana kwa makosa ya kuandaa vipindi ambavyo vimerushwa hewani vikiashiria uchochezi.

 Nape amesema kuwa uamuzi wa kuvifungia vituo hivyo umefikiwa baada ya kujirdhisha kuwa kipindi cha Matukio kilichorushwa Agosti 25, 2016 muda wa saa 2 usiku hadi saa 3 na Radio 5 pamoja na kipindi cha Morning Magic katika kipengele cha Kupaka Rangi Agosti 17 vilikuwa na maudhui ya uchochezi ambao ungeweza kuleta uvunjifu wa Amani.

Amesema kuwa kufuatia tukio hilo amevifungia viyuo hivyo kwa muda usiojulikana kwani wamekiuka masharti ya kanuni ya 5 (a,b,c na d), kanuni ya 6(2a, b na c) na kanuni ya 218 ya huduma za utangazaji ya mwaka 2005.








PROF. LIPUMBA NA MAGDALENA SAKAYA WAVULIWA UANACHAMA CUF


Aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha CUF, Prof. Haruna Lipumba  
 
Chama Cha Wananchi (CUF) kimewasimamisha uanachama aliyekuwa Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba na Katibu Mkuu wa chama hicho upande wa Bara, Magdalena Sakaya.

Uamuzi huo umetolewa jana na Baraza Kuu la Chama hicho lililofanya mkutano wake visiwani Zanzibar kwa lengo la kuwajadili wanachama kadhaa wakiwemo vigogo hao. Sakaya amevuliwa nyadhifa zote ndani ya chama kabla ya kusimamishwa.

Taarifa kutoka ndani ya Mkutano huo zimeeleza kuwa Baraza hilo limewaadhibu wanachama 15 wakiwemo Sakaya ambaye pia ni mbunge wa Kaliua.

Mbali na vigogo hao, wengine waliopigwa rungu na Baraza Kuu la CUF ni pamoja na Katibu wa Baraza la Wazee, Shashi Lugeye, Thomas Malima na Naibu Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano, Abdul Kambaya.

Aidha, Baraza hilo limemsimamisha uanachama Mbunge wa Mtwara Mjini, Maftah Nachuma. Hatua hii inaweka matatani ubunge wa Sakaya na Nachuma kwani wakifikia hatua ya kufukuzwa watakosa sifa za kuendelea kuwa wabunge.

Lipumba na Sakaya hawakupata nafasi ya kujitetea kutokana na kutohudhuria mkutano huo wakati Shashi alipata nafasi ya kujitetea kutokana na uwepo wake lakini utetezi wake haukuzaa matunda. Katiba ya chama hicho haiwapi nafasi wabunge hao kukata rufaa kutokana na uamuzi wa Baraza hilo.

Uamuzi huo umekuja ikiwa ni siku chacha baada ya Mkutano Mkuu Maalum wa Chama hicho uliolenga kumchagua Mwenyekiti Mpya kuvunjika kutokana na kuwepo vurugu kubwa baada ya Profesa Lipumba kuingia ndani ya ukumbi huo na wafuasi wake wakitaka barua yake ya kutaka kurejea kwenye nafasi yake ijadiliwe na kukubaliwa.

Hata hivyo, kura zilizopigwa na wajumbe wote zaidi ya 800, ni kura 14 pekee zilizotaka Profesa Lipumba aendelee na nafasi ya uenyekiti.

KIKOSI CHA TIMU YA TAIFA STARS KITAKACHO SAFIRI KWENDA KUIVAA NIGERIA HIKI HAPA

Kocha Mkuu wa timu ya Mpira wa Miguu Tanzania ‘Taifa Stars’, Charles Boniface Mkwasa, ametangaza wachezaji 20 watakaounda kikosi kitakachosafiri mwishoni mwa mwezi huu kwenda Nigeria kwa ajili ya mchezo wa mwisho wa kuwania kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2017) dhidi ya timu ya Taifa ya nchi hiyo, Super Eagles.

Licha ya mchezo huo wa Septemba 3, 2016 kuwa sehemu ya mchuano wa kuwania nafasi ya kucheza fainali hizo za AFCON 2017 huko Gabon, lakini utakuwa ni wa kukamilisha ratiba baada ya Misri kufuzu kutoka kundi G ambalo mbali ya Nigeria na Tanzania, pia ilikuwako Chad ambayo iliyojitoa katikati ya mashindano.

“Tanzania hatuwezi kuupuuza mchezo huu, tunaupa umakini kabisa kwa sababu tunacheza ugenini ambako matokeo mazuri yanaweza kutusongesha mbele na kuingia ndani ya timu 99 bora katika viwango vya FIFA,” amesema Mkwasa.

Katika kikosi chake, Mkwasa ametangaza kutomjumuisha Mshambuliaji wa Kimataifa, Thomas Ulimwengu anayecheza klabu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) kutokana na majeruhi ya paja kama ilivyo kwa Juma Abdul wa Young Africans ambaye aliumia katika mchezo wa kuwania Kombe la Shirikisho dhidi ya Mo Bejaia ya Algeria.

“Timu ilitarajiwa kuingia kambini Agosti 28 siku ya Jumapili, mchezo huo ni wa kukamilisha ratiba ambapo Misri tayari wameshafuzu fainali za Afrika,” alisema Mkwasa na kuongeza kuwa kuna mchezaji wa Tanzania, Said Carte Mhando anamfuatilia ili ikiwezekana baadaye amwite kuchezea timu ya Taifa. Anachezea Klabu ya Brencia Calcio ya Italia.

Wachezaji walioitwa:

Makipa; Deogratius Munishi (Young Africans) na Aishi Manula (Azam FC)

Mabeki
Kelvin Yondani (Young Africans),Vicent Andrew (Young Africans)
Mwinyi Haji (Young Africans),Mohamed Hussein (Simba SC)
Shomari Kapombe (Azam FC) na David Mwantika (Azam FC)

Viungo
Himid Mao (Azam FC),Shiza Kichuya (Simba SC),Ibrahim Jeba (Mtibwa Sugar),Jonas Mkude (Simba SC),Muzamiru Yassin (Simba SC),Juma Mahadhi (Young Africans) na Farid Mussa (Tenerif ya Hispania)

Washambuliaji
Simon Msuva (Young Africans),Jamal Mnyate (Simba SC),Ibrahim Ajib (Simba SC),John Bocco (Azam FC) na Mbwana Samatta - CK Genk ya Ubelgiji

Wednesday, August 24, 2016

UVCCM WATARAJI KUFANYA MAANDAMANO YA AMANI AGOSTI 31, 2016 KWA AJILI YA KUELEZA UTENDAJI WA DKT. JOHN POMBE MAGUFULI



Kaimu Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Shaka Hamdu Shaka akizungumza na Waandishi wa habari Makao makuu ya Ofisi hizo jijini Dar es Salaam.

Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) wanatarajia kufanya maandamano ya Amani Agosti 31 kwa ajili ya kueleza utendaji kazi wa Rais Dk.John Pombe Magufuli kwa Watanzania.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Kaimu Katibu Mkuu wa Umoja huo, Shaka Hamdu Shaka amesema kuwa maandamano hayo wameshamwandikia barua mkuu wa jeshi la Polisi kwa ajili ya kupata ulinzi siku hiyo.
 
Amesema kuwa wasipopata ulinzi watafanya kwa kujilinda wenyewe ikiwa ni lengo la kufikisha ujumbe kwa wananchi juu ya utendaji kazi wa Rais Dk. John Pombe Magufuli.

Shaka amesema kuwa Rais Dk.John Pombe Magufuli amefanya watendaji kuwa na utii pamoja na maadili katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Aidha amesema kuwa maandamano hayo wanaawalika na vijana wa vyama vingine kushiriki kwa lengo moja tuu, la kuunga mkono utendaji wa Rais Dkt. John Pombe Magufuli.




 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU