Facebook Comments Box

Wednesday, March 27, 2013

MAHAKAMA YAAMURU MATOKEO YA URAIS KENYA YAHESABIWE UPYA KATIKA VITUO 22 KATI YA 33


Nairobi. Mahakama ya Juu (Supreme Court) ya nchini Kenya imeagiza kuchunguzwa kwa fomu 34 za matokeo ya uchaguzi wa rais kutoka katika vituo vyote 34,400, vilivyotumika kupigia kura katika Uchaguzi Mkuu wa nchi hiyo uliofanyika Machi 4, mwaka huu.
Kadhalika mahakama hiyo jana iliagiza kuhesabiwa upya kwa kura za urais katika vituo vya kupigia kura 22 kati ya elfu 33 vilivyolalamikiwa na aliyekuwa mgombea urais wa Muungano wa Cord, Raila Odinga.
Katika malalamiko yake yaliyowasilishwa katika mahakama hiyo kupinga Uhuru Kenyatta kutangazwa mshindi wa urais katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Machi 4, Odinga alidai kuwa vituo hivyo 22 kura zilizopigwa zinazidi idadi ya wapigakura walioandikishwa.
Akisoma uamuzi huo kwa niaba ya majaji wenzake watano, Jaji Smokin Wanjala alisema kwamba uhesabuji kura wa vituo hivyo utafanyika leo kuanzia saa 2.00 asubuhi kwa lengo la kubaini ukweli kuhusu madai hayo.
“Matokeo ya kura zitakazohesabiwa katika vituo hivyo 22 yawasilishwe katika mahakama hii Jumatano, saa 10.00 jioni,” alisema Jaji Wanjala.
 
Kikao hicho, ambacho Jaji Mkuu wa Tanzania, Mohamed Othman Chande amealikwa kama mwangalizi, ni cha awali kabla ya kesi hiyo kuanza kusikilizwa rasmi keshokutwa (Alhamisi) na kuendelea kwa mfululizo hadi kufikia uamuzi ikiwa madhumuni yake.
Lengo ni kupitia madai yaliyowasilishwa mahakamani hapo na pande zote zinazohusika na kuamua mwenendo wa kesi utakavyofanyika.
Ukiachilia mbali kesi iliyofunguliwa na Odinga kupinga Kenyatta kutangazwa mshindi wa uchaguzi huo wa tano tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi hapa Kenya, kuna kesi nyingine ambayo imefunguliwa na muungano wa mashirika yasio ya kiserikali, `The African Centre for Open Governance’ (Africog).
Katika kesi hiyo inayorushwa moja kwa moja na vituo kadhaa vya televisheni nchini Kenya, Africog inahoji uhalali wa uchaguzi huo.

“Kesi yetu haihusiani na nani ameshinda au kushindwa bali jinsi umma ulivyoshindwa, tumepoteza ahadi ya uchaguzi uliowazi,” alisema Gladwell Otieno, Mkurugenzi Mtendaji wa Africog.
Kesi ya tatu ambayo imefunguliwa na wajumbe wa timu ya kampeni ya Kenyatta, mwanaharakati katika mitandao ya kijamii Dennis Itumbi na Moses Kuria wanaopinga uamuzi wa Tume Huru ya uchaguzi na Mipaka (IEBC) ya kujumuisha kura zilizoharibika wakati wa kujumlisha kura za wagombea urais.
Katika uamuzi wake, mahakama iliamua kwamba kesi zote tatu zitaunganishwa kuwa moja, huku ile iliyowasilishwa na Odinga ikiwa ndiyo kinara wa kesi zote.
Pia mahakama iliamuru Muungano wa Vyama vya Siasa wa Cord na Jubilee kuteua mawakala 10 kila mmoja ambao watakula kiapo mahakamani hapo kabla ya kuanza kuhesabu upya kura hizo.
Katika uamuzi wake jana jioni, mahakama hiyo ilikubali ombi la Mwanasheria Mkuu wa Kenya, kushiriki katika kesi hiyo kama rafiki wa mahakama na siyo mdaiwa kama ilivyokuwa awali. Wakili wa Cord, George Oraro alikubali uamuzi huo licha ya kuupinga awali.


ALIYEMGONGA TRAFIKI ENEO LA BAMAGA NA KUMUUA AFIKISHWA MAHAKAMANI




 Jackson  Simbo anayedaiwa kumgonga kwa gari marehemu trafiki Elikiza Nko wiki iliyopita katika taa za kuongozea magari za Bamaga-Mwenge  jijini Dar ss Salaam amepandishwa kizimbani leo katika mahakama ya Wilaya ya Kinondoni. 

Mshitakiwa huyo ameachiwa kwa dhamana hadi kesi hiyo itakapo tajwa tena Aprili 15 mwaka huu.


MWANAFUNZI WA KITIVO CHA SHERIA UDSM AJINYONGA


Picha hii kwa hisani ya Maktaba:

  Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) mwaka wa pili Kitivo cha Sheria, Joseph Bernadina (25), amejinyonga kwa kutumia kamba na kukutwa ameifunga juu ya mti, katika eneo la Yombo chuoni hapo.

Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Utawala, Profesa Yunus Mgaya, alithibitisha  kutokea kwa tukio hilo na kwamba alipata taarifa hizo jana asubuhi.

Aliongeza kuwa Jumamosi iliyopita alipokea simu kutoka kituo cha polisi cha chuo hicho akielezwa kuwa kuna mwanafunzi alitishia kujiua, lakini aliwahishwa hospitali na kupatiwa ushauri kutoka kitengo maalum cha washauri wa chuoni hapo na kuruhusiwa Jumapili.

“Nilikuja tena kushituka leo asubuhi napokea simu kutoka kwa mshauri wa wanafunzi kuwa kuna wanausalama wamemkuta mwanafunzi akiwa amejinyonga juu ya mti huku akiwa na karatasi kwenye mfuko wa sharti ikimtambulisha pamoja na ujumbe uliosema, kifo chake kisihusishwe na mtu yeyote kwani amejiua kwa ridhaa yake --asisumbuliwe mtu yeyote kwani nimefanya hivi kwa maamuzi yangu mwenyewe pia nizikwe kwetu--” alisema.

Profesa Mgaya alisema taratibu za mazishi zinaendelea kufanywa na Uongozi wa chuo kwa kushirikiana na ndugu wa marehemu na kwamba Chuo kitagharamia kuusafirisha mwili kama alivyoomba katika ujumbe aliouacha wa kupelekwa wilayani Ludewa Mkoa wa Iringa.
 
Naye rafiki wa marehemu, Daniel Mwamlima, alisema marehemu hakuwahi kuzungumza chochote kilichoashiria kuwa ana matatizo wala mgogoro na mtu yeyote.  Alisema walimuacha hospitalini Jumamosi na kesho yake kumchukua, lakini  baadaye aliwatoroka.

“Sasa leo (jana) asubuhi tulipata taarifa za mwanafunzi kujinyonga mbaya zaidi tukakuta ni yeye,” alisema Mwamlima.

Waziri Mkuu wa Serikali ya Wanafunzi wa chuo hicho (DARUSO), Yasini Athumani, alisema wamezipokea taarifa hizo kwa masikitiko makubwa.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela, alithibitisha kutokea kwa tukio na alisema uchunguzi wa awali umebaini kwamba marehemu aliwahi kuwa na historia ya kwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa ajili ya kupata matibabu ya ugonjwa wa msongo wa mawazo.

Source: WAVUTI

 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU