Mbunge
 wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba (kushoto) akizozana na wabunge wa 
Chadema, Mchungaji Peter Msigwa(kulia)mbunge wa Nyamagana, Ezekiah Wenje
 (wa pili kulia) na Mbunge wa Musoma Mjini, Vicent Nyerere (wa pili 
kushoto) baada ya kukutana nje ya ukumbi wa mikutano wa St Gasper,Dodoma
 jana wakati wa semina ya wabunge ya kuhusu UKIMWI. (picha: Fidelis 
Felix/MWANANCHI)
 
 
Mbunge
 wa Jimbo la Iringa Mjini (CHADEMA), Mchungaji Peter Msigwa na mbunge wa
 Iramba Magharibi (CCM), Mwigulu Nchemba jana nusura wachapane makonde 
baada ya kutupiana maneno ya kashfa, wakituhumiana kuhusika na mlipuko 
wa bomu uliotokea Jumamosi iliyopita mkoani Arusha.
Tukio hilo 
lilitokea katika viwanja vya Hoteli ya St Gasper nje kidogo ya mji wa 
Dodoma, walipohudhuria semina ya wabunge wapambanaji na UKIMWI, ambapo 
baadhi ya wabunge wa CHADEMA walihudhuria.
Malumbano hayo 
yanatokana na Nchemba kuituhumu CHADEMA kuhusika na mlipuko wa bomu huko
 Soweto, Arusha (kwenye mkutano wao wa kufunga kampeni za Uchaguzi wa 
Madiwani katika Kata za mkoa huo, siku ya Jumamosi ya Juni 25, 2013), 
Juni 20 mwaka huu wakati akichangia hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali ya 
mwaka 2013/2014, akisema chama hicho kilipanga kulipua bomu hilo ili 
kuwafanya Watanzania waamini kuwa Serikali ya CCM ndiyo inayohusika na 
tukio hilo.
Msigwa akiingia katika ukumbi huo akiwa ameongozana 
na Mbunge wa Nyamagana (CHADEMA), Ezekiah Wenje, walikutana uso kwa uso 
na Nchemba ambaye alikuwa akizungumza na Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA, 
Said Amour Arfi. Baada ya Nchemba kumwona Msigwa alimkaribisha mchungaji
 huyo akisema; 
  
  
  
“Karibu sana bwana, salama lakini?”
Hata
 hivyo, badala ya kujibu salamu hiyo ya Nchemba, Msigwa alikuja juu na 
kumtuhumu Nchemba kwamba anatoa kauli zinazoweza kuvuruga amani ya 
nchi: “Wewe ni mtu hatari sana, haya yote yanasababishwa na wewe, mnatumia damu za watu kutafuta madaraka,” alisema Msigwa akimtupia maneno Mwigulu.
Baada ya kauli hiyo Nchemba alihoji akisema: “Ki-vipi? Hayo mambo tuyaache, Msigwa achana na haya mambo!”
Baada
 ya Nchemba ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa CCM kujibu, Msigwa 
alimsogelea karibu na kumnyooshea kidole, huku akiendelea kumtuhumu kuwa
 ana siasa chafu zinazopandikiza chuki kwa jamii.
Malumbano
 hayo pia yaliingiliwa na Mbunge wa Musoma Mjini (CHADEMA), Vicent 
Nyerere ambaye alimuunga mkono Msigwa, huku akimtuhumu Nchemba kuwa ni 
mtu mbaya katika siasa za Tanzania.
Katika kile kilichoonekana 
kutaka kuweka mambo sawa, Wenje alimvuta Msigwa na kumpeleka ukumbini 
ili kuepusha shari baada ya wabunge hao kuzidi kurushiana maneno. Hata 
walipoingia ndani ya ukumbi huo wabunge hao waliendelea kulumbana, 
lakini wakatulizwa na baadhi ya wabunge waliokuwa karibu yao.
Alipotakiwa kueleza sababu za mzozo huo na Nchemba, Mchungaji Msigwa alisema, “Achana
 na yule mpuuzi, mimi siwezi kuzungumza na mtu mnafiki, mkatili na yeye 
ndiye alihusika na mipango mibaya dhidi ya CHADEMA hata mlipuko wa 
Arusha hivyo kutesa watu wa CHADEMA.”
Alisema
 kuwa yeye haoni sababu ya mtu mwenye mipango mibaya na wananchi wa 
Tanzania pamoja na chama chake (CHADEMA), kuwafuata na kujikomba.
Kwa
 upande wake Nchemba alipoulizwa alisema kuwa alichokizungumza ni 
mtazamo wake na kwamba ikiwa kuna mtu anayeona kuwa alizungumza uzushi, 
ajitokeze na kupinga: “Nilichokizungumza ndicho kilichofanyika kwa matukio yote niliyoeleza bungeni,”alisisitiza Nchemba.