
Na. Emmanuel J. Shilatu
Mara
 baada ya kufanikiwa kuziondoa tawala mbovu, nyonyaji na za kidhalimu za
 Wakoloni hapa nchini, aliyekuwa akiongeza harakati hizo ambaye pia ni 
Baba wa Taifa letu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alisema ya kuwa 
“tumefanikiwa kuwaondoa wakoloni na hivyo tupo huru na Uhuru ni kazi”. 
Hapa Mwalimu Nyerere alikuwa na maana ya kuwa ili tuweze kupiga hatua 
kimaendeleo ni lazima tuutumie huu uhuru wetu vilivyo kwa kufanya kazi 
kwa bidii na maarifa yote ili kuleta maboresho katika Nyanja zote za 
kimaisha yaani uchumi, kijamii na kisiasa.
Na ndio maana yeye kama kiongozi alianza kuonyesha mfano wa  dhahiri
 kwa kuanzisha mapambano kwa vitendo dhidi ya maadui zetu watatu ambao 
ni ujinga, maradhi, na umaskini. Sehemu ya mafanikio yake ni kwa kupitia
 kuanzisha maazimio, mashirika, kauli mbiu na sera mbalimbali. Hayo 
yoote (yaani tangu kusaka uhuru wa Tanganyika) aliweza kufanikiwa 
kutokana na kufanya mambo kwa matendo zaidi kuliko maongezi (porojo) 
zisizoisha.
Pia
 Mwalimu Nyerere alikuwa na falsafa (dhana) ya kimaendeleo ambapo 
aliamini kuwa maendeleo sahihi hayawezi yakapatikana nje ya uwepo wa 
mambo manne ambayo ni“Watu”, “ardhi”, “siasa safi”na “uongozi bora”
Ndio
 “Watu”ni kiungo kimojawapo cha hakikisho la maendeleo chanya yeyote 
yale ndani ya familia, jamii na Taifa kwa ujumla. Kama tutakuwa na 
miundombinu bora ni watu wamechangia uwepo wake; kama tutakuwa na mazao 
ya kutosha kwa ajili ya chakula, kiada na biashara ni watu ndio 
wamechangia hayo; Endapo kuna amani na utulivu nchini basi ujue watu 
wamechangia hayo; ama taifa likiwa na wasomi wa kutosha ni watu 
mbalimbali ndio wamechangia hilo.
Licha
 ya kwamba Taifa letu Tanzania lina watu zaidi ya Milioni 45 lakini hao 
watu wamekuwa ndio kikwazo kikubwa katika uletaji wa maendeleo ya kweli 
na ya dhahiri. Tatizo lililopo ni uibukaji wa umaskini mkubwa wa 
utegemezi na utajiri mkubwa wa porojo ndani ya jamii na kila Mwana jamii
 ni mwathirika wa hili si Kijana wala Mzee awe ni Mwanamke au Mwanaume.
Utakuta
 vijana wengi kutwa wanashinda kwenye kucheza “pool table” na kukaa 
vijiweni tu; Wazee ama akina Baba nao kutwa wanacheza “bao” ama “draft” 
tu; na akina Mama nao kila kukicha wapo vibarazani wakisutana na 
kupashana umbea tu. Hayo ndio maisha ya kila siku ya baadhi ya wanajamii
 ya kutokupenda kufanya kazi kwa bidii.
Jamii inachojua ni utegemezi pekee. Kivipi? ... Kwa
 jinsi tuanavyoishi utadhani tunawangojea baadhi ya watu kutoka nje ili 
waje watuletee maendeleo yaani imefika kipindi kwa mtu hata kutandika 
kitanda chake mwenyewe anacholalia imekuwa ni kazi kuubwa kwake. Pia 
suala la maendeleo ya nchi yetu wenyewe tumewaachia viongozi pekee huku 
tukijiengua katika kapu la dhana ya neno“Serikali” wakati kiuhalisia na 
kikatiba pia ni kwamba Serikali inaundwa na viongozi pamoja na Wananchi.
Hii
 yote inatokana na jamii kuziasi mitazamo miongozo na falsafa za Mwalimu
 Nyerere (mathalani ile ya “Uhuru ni kazi”) hali inayosababisha kiwango 
cha idadi ya watu maskini kuzidi kukua nchini licha ya kujaariwa 
rasilimali na mali za asili kwa kuyachakachua maendeleo yetu wenyewe. 
Kisa? Porojo kutawala maisha yetu.
Hali
 hii tuliyonayo ya kutaka kuongea ongea ovyo huku parojo zikituendesha 
katika masuala ya kimsingi ya maisha yetu, tunataka tuwaambukize hata na
 viongozi wetu. Imefika kipindi kigezo ama kipimo cha uwezo wa Kiongozi 
unapimwa na utokeaji wa mara kwa mara kwenye vyombo vya habari ama 
uongeaji, uropokaji na ubwatukaji wa mara kwa mara kwenye jumba letu 
tukufu la kutunga sheria na wala si utendaji wake kazi na uletaji wa 
maendeleo katika jamii yaani ni usanii, usanii mtupu. Hii ni hatari 
sana.
Hivi
 tunachotaka kutoka kwa Kiongozi ni mazungumzo pekee ama matendo yake ya
 kimaendeleo? Ama uwezo wa kiongozi bora upo kwenye mazungumzo tu ama 
utakelezaji wa kimaemdeleo? Hivi uhodari wa mbunge wangu unatoka na 
amezungumza mara ngapi Bungeni ama amenipunguziaje zigo langu la 
matatizo ya kimsingi? Bila shaka majibu ni hapana ila ajabu ya firauni 
ni kuwa kwa miaka ya hivi karibuni kumeibuka dhana mfu ya  kupima
 uwezo wa Kiongozi si kwa uletaji wa maendeleo bali ugwiji wake wa 
kuzungumza Bungeni kwa kuchangia hoja kuulizwa maswali ya msingi na 
kadhalika.
Mtazamo
 huu unaonyesha kuwa kiongozi bora anapimwa kwa uwezo wake wa kuongea 
Bungeni na si utetaji wa maendeleo; Pili, wanawafundisha viongozi wetu 
tabia mbaya ya kuwa wawe ni wazungumzaji tu na si watendaji; Tatu, 
inavyoonyesha hawaijali thamani ya maisha ya Mtanzania bali ya Yule 
anayeiwasha vipaza sauti mara kwa mara pale mjengoni. 
Katika
 kipindi fulani cha nyuma tafiti mojawapo nchini walitoa matokeo yao ya 
utafiti ambapo waliueleza Umma kuwa Mh. Edward Ngoyai Lowassa ndiye 
anayeongoza pale Bungeni kwa kutokuongea pale Bungeni tangu 2005. Jamani
 hivi ni kweli?
Lowassa
 wanayemzungumzia ni yule yule ambaye alikuwa Waziri Mkuu wa kwanza 
katika serikali hii ya awamu ya nne kwa takribani miaka miwili. 
Kikatiba, Waziri Mkuu ndiye Kiongozi wa shughuli nzima za Serikali 
Bungeni. Hivi inawezekana vipi kwa kiongozi mkubwa kama huyo (Waziri 
Mkuu) kutokuongea lolote lile kwenye mikutano na vikao vya Bunge? Amu 
hoja au maswali mazito yahusuyo serikali yakiwashinda Mawaziri, M/Waziri
 au Mwanasheria Mkuu huwa yanatolewa ufafanuzi na nani?
Suala
 la kuongea mno Bungeni sio hoja ya kuwaletea neema ya kimaendeleo bali 
Wapiga kura wanahitaji matendo na wala sio maneno matupu . Wapo Wabunge 
ambao sio waongeaji lakini kwenye majimbo yao wameleta neema ya ajabu 
kupitia uongozi wao.
Mathalani
 Mh. Nimrod Mkono ambaye ni Mbunge wa Musoma Vijijini katika kipindi cha
 ubunge wake amewaletea neema kubwa Wapiga kura wake. Amewajengea shule 
ya sekondari kubwa na ya kisasa na kuikabidhi kwa Serikali, amejenga 
maabara ya kisasa  iliyojitosheleza kila kitu mihimu, 
amejenga nyumba za walimu. Pia amewanunulia gari la kubebea wagonjwa kwa
 wana wa jimbo la Musoma vijijini na kadhalika. Pamoja na kutokuongea 
kwake Bungeni lakini Wapiga kura wake hauwaelezi kitu kwani ni Mkono, 
Mkono tu. Hivyo kutokuongea Bungeni sio tatizo.
Pia
 mwangalie Mohamed Dewji “MO” (Mbunge wa Singida Mjini) ambaye yeye si 
muongeaji lakini nyakati zote ameonyesha nia ya dhati ya kuwapenda na 
kuwathamini wapiga kura wake. “MO” amejitolea kwalipia ada ya vyuoni 
wale wote wa jimbo lake waliobahatika kupata elimu ya juu (chuoni), kwa 
wale pia ambao wana vigezo amewaahidi kuwapa ajira za kudumu kupitia 
makampuni yake, hata hivyo pia amekamilisha miradi mingi ya maendeleo 
ambayo ilikuwa inasuasua.
Hao
 ni baadhi tu ya wale ambao sio waongeaji lakini ni watendaji haswaa 
ambao Wapiga kura wao wanajivunia nao. Lakini wapo wale ambao ni mafundi
 wa kuongea hadi kuwa wabwatukaji pale Bungeni lakini uongeaji wao huo 
haujawasaidia lolote lile Wapiga kura wao.
Licha
 ya ufundi wao wa kuongea lakini wameshindwa kuwatatulia kero za maji, 
umeme, hospitali, shule ama masoko kwa ajili ya bidhaa zao; wengine 
waliahidi kuwajengea majosho ya kuogesha ng’ombe wao, kuwajengea 
machinjio ya kisasa na hata wengine wameshindwa kuikamilisha mradi wa 
ujenzi wa kawaida cha kusindika Tangawizi tu. Wengine ndio wameua kabisa
 sekta ya kilimo katika majimbo yao hali ambayo inawafanya Wananchi 
waishi maisha magumu na yasiyoelezeka. 
Nimelazimika
 kuyaeleza haya kutokana na mitazamo isiyo na tija kwa jamii inayozaa 
matukio ya uletaji ushabiki wa kisiasa kwenye chombo muhimu cha kutunga 
sharia za nchi ambapo Wabunge wanawatelekeza wapiga kura wao kwa 
kutokupigania maslahi yao na badala yake wanaendekeza ushabiki wa 
kichama ndani ya Bunge.
Ni
 aibu isiyoelezeka kumuona Mbunge anawasha kipaza sauti na kuanza kutoa 
maneno ya kebehi kwa kufuata utashi wa kisiasa. Huko ni kuwapotezea muda
 wapiga kura wao.
Dhana
 ya hiyo ya kushabikia waongeaji ndani ya Bunge imewafanya Wabunge wengi
 wasiwe watiifu mbele ya kiti cha Spika kwa kujiamulia kuwasha vipasa 
sauti na kila mmoja kuanza kuzungumza na hatimaye kuligeuza Bunge kuwa 
gulio na si tena mhimili wa dola.
Utoto
 wa Wabunge haustahili kuvumiliwa hata kidogo kwa kuwa wao ni Watu 
wazima na watu wamewaamini kiasi cha kuwapatia madaraka. 
Endapo
 Mbunge atakuwa anatumia muda mwingi kwa ajili ya kuzomea zomea ndani ya
 Bunge ama kutoa lugha za kebehi na dharau ndani, atapata wapi wasaa wa 
kuwasemea matatizo ya Wapiga kura wao? Je, sisi Wananchi wa kawaida 
tunanufaikaje na matokeo hayo ya kitoto yanayofanywa na Wabunge wetu 
tuliowachagua?
Kimsingi,
 umaarufu wa Mbunge hauji kwa kuzunumza kwa jazba wala kutoa lugha za 
maudhi awapo Bungeni, umaarufu wa Mbunge utatokana na kutekeleza ahadi 
ahadi ya kukidhi matarajio kwa waliomchagua.
Ni
 vyema Wabunge wakatambua ya kwamba fursa na uhuru waliopewa na watu 
waliowaamini una mipaka na una mwisho wake, ni vyema wakautumia huo 
uhuru kabla wakati haujawapita kwani wakati ni ukuta, wakishindana nao 
wataumia.
Ndugu
 zangu, kuna haja kubwa ya kuwa makini sana wakati wa upigaji kura ili 
kuepukana na wabunge wasijali maslahi ya Wananchi bali maslahi yao na ya
 chama chao, kuwaepuka viongozi watovu wa nidhamu dhidi ya kanuni na 
utaratibu husika. Bila ya hivyo, tutazidi kuwa maskini!
 















