Facebook Comments Box

Thursday, January 17, 2013

HUYU NDIO ALIO WAPELEKA SIMBA OMAN




Rahma al Kharoos ambaye hivi karibuni alichaguliwa kuwa mjumbe wa kamati ya utendaji ya simba, leo jioni alitembelea mazoezi ya Simba kwenye uwanja wa Oman Club
Rahma pia ndiye mmiliki wa RBP Oil, aliwahi kuwa mdhamini mkuu wa Twiga Stars, pia aliwahi kuwa mmoja wa wamiliki wa African Lyon..ni kati ya wapenda michezo.
Pia ndiye aliyeidhamini safari yote ya Simba hapa Oman kwa kuwalipia hoteli, tiketi pamoja na chakula kwa muda wote wa siku 14 watakazokuwa hapa.



PICHA NA SALEHE ALLY WA CHAMPION



HIZI NDIO MBINU ZA KUWATAMBUA WALIOFICHA FEDHA USWISI

 
Tutawatambuaje wenye mabilioni Uswisi? 

WAKATI Serikali na Bunge zikiwa kwenye mvutano kuhusu hatua za kufuatwa kurejesha mabilioni ya fedha za Kitanzania yaliyofichwa kwenye benki za nchini Uswisi, swali kubwa lililopo ni kwamba ni akina hasa ambao wana fedha huko.

Mtoaji wa hoja binafsi kuhusu suala hilo, Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA), Zitto Kabwe, amegoma kutaja majina ya vigogo wanaotajwa kuhifadhi fedha akitaka uchunguzi ufanyike na majina yafahamike wakati huo, huku serikali ikimtaka ataje majina ili ipate pa kuanzia kwenye uchunguzi huo.

Serikali kupitia Mwanasheria Mkuu, Jaji Frederick Werema, inataka kuendesha uchunguzi kuhusu madai hayo ya Zitto lakini kwanza inataka mbunge huyo ataje majina ya baadhi tu ya vigogo ambao ana ushahidi wamehifadhi fedha Uswisi.

Pamoja na hayo, swali moja ni lazima lipate majibu, leo au kesho. Swali lenyewe ni hili; ni akina nani waliokwiba fedha za Watanzania na kwenda kuzihifadhi ughaibuni?

Niseme mapema kwamba kuwa na akaunti nje ya nchi si dhambi. Dhambi inakuja pale inapofahamika kwamba fedha hizo zilipatikana isivyo halali.

Kwa mujibu wa ripoti ya Benki Kuu ya Uswisi iliyotolewa Juni mwaka jana, Watanzania wamehifadhi kiasi cha dola za 
Marekani milioni 178 (zaidi ya Sh bilioni 300) katika benki mbalimbali nchini humo. Ripoti hiyo haikutaja majina, wala kiwango walichonacho watu hao na kutokana na taratibu za kibenki za taifa hilo la Ulaya, ni lazima kuwepo na sababu nzito za wao kutoa taarifa zozote kuhusiana na wateja hao.

Hata hivyo, taarifa hiyo ya Benki Kuu ya Uswisi si ya kuaminika sana kwa vile taifa hilo linafahamika kwa kutoa taarifa zisizoaminika kuhusu kiwango hasa cha fedha kilichohifadhiwa na wateja wake.

Kwa mfano, wakati Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ilipodai fedha zilizoibwa na aliyekuwa rais wa taifa hilo, Mobutu Sesesseko, zilizokadiriwa kufikia dola bilioni tano, Waswisi walirejesha dola milioni nane tu wakidai ndiyo kiasi kilichokuwapo!

Hata hivyo, ripoti hiyo ya Benki Kuu ya Uswisi imesaidia tu kuthibitisha kwamba wapo Watanzania waliohifadhi mamilioni ya dola katika akaunti mbalimbali nchini humo.

Swali linakuja ni akina nani hao? Nimefanya utafiti kidogo na yafuatayo yanaweza kusaidia kupata majina ya wahusika.

1. Mazingira ya wizi

Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Kimataifa la Kupambana na Ufisadi (Global Financial Integrity, GFI), katika mataifa mengi ya kiafrika, fedha huibwa katika mazingira makubwa matatu- rushwa, ukwepaji kodi na mauzo ya bei za kurusha ya bidhaa au huduma mbalimbali.

Kuna maeneo mengine madogo kama vile ‘usafishaji’ wa fedha haramu, biashara ya silaha, dawa za kulevya na mambo mengine lakini GFI inaamini kwamba maeneo haya madogo yanafanya kazi zaidi katika mataifa ambayo yana serikali zisizo imara.

Kwa vile Tanzania ina serikali imara (walau), kulinganisha na nchi kama vile Somalia, sababu hizo tatu za awali kwa mujibu wa GFI ndizo zinazoweza kutoa picha kuhusu ni akina waliohifadhi fedha zao nchini Uswisi kutoka nchini mwetu.

GFI wametoa takwimu zinazoonyesha kuwa zaidi ya dola za Marekani milioni 148 (Sh bilioni 246) huibwa Afrika kila mwaka kutokana na rushwa. Dola milioni 50 (Sh bilioni 80) kwa ukwepaji kodi na dola milioni 30 (Sh bilioni 48) zinazotokana na misaada kutoka kwa wahisani. Je, wapi tuanzie kuchunguza?

2. Idara ya Usalama wa Taifa (TISS)

Kwa mujibu wa gazeti la The Guardian la Tanzania la Juni mwaka jana, katika kipindi cha kati ya mwaka 2001 hadi 2008, Tanzania imepoteza zaidi ya Tsh. trilioni 1.2 kutokana na mikataba mibovu, rushwa na ununuzi wenye kutia shaka.

Haya yote yamefanyika wakati Idara ya Usalama wa Taifa nchini ikiwa inatazama na katika hali ya kawaida haiwezekani kwa idara hii kutofahamu chochote kwenye kashfa kama za ununuzi wa rada ya mtumba, Meremeta, Deep Green, EPA na Richmond.

Kimsingi, serikali imeshindwa kutoa maelezo kuhusu mradi wa dhahabu wa Meremeta ikidai suala hilo lina maslahi ya taifa na vigogo kadhaa wa Idara ya Usalama wa Taifa wanatajwa kuhusika na mradi huo.

Mwanzoni mwa miaka ya 2000, serikali ya Uswisi ilirejesha nchini Peru kiasi cha dola milioni 180 (Sh bilioni 288) zilizodaiwa kuhifadhiwa humo na aliyekuwa Mkuu wa Usalama wa Taifa wa nchi hiyo, Vladimiro Montesinos, wakati wa utawala wa Rais Alberto Fujimori.

Kwa vyovyote vile, watu wetu wa usalama watakuwa wanajua kitu kuhusu ufisadi wote huu. Ipo imani kwamba makachero wa Tanzania ni miongoni mwa walio bora katika Bara la Afrika. Ni lazima TISS imulikwe ili ieleze iwapo ilikuwa na taarifa kuhusu ufisadi uliokuwa ukifanyika lakini taarifa hizo hazikufanyiwa kazi na watawala au yenyewe nayo ina mkono kwenye hilo.

Kwa sababu tayari tuna ushahidi wa Montesinos. Kwa sababu tayari serikali imekwishakutaja usalama wa taifa kwenye ufisadi wa Meremeta.

Kuna uwezekano mkubwa kuwa katika hizo trilioni 1.2 zilizoibwa katika kipindi cha miaka kumi iliyopita, nyingine zitakuwa zimeangukia Uswisi.

3. Mawaziri

KWA mujibu wa taratibu zilizopo nchini, Waziri wa Fedha anaruhusiwa kutoa misamaha ya kodi kwa kampuni au taasisi mbalimbali pale atakapoona inafaa.

Tayari mawaziri wawili wa zamani wa serikali ya awamu ya tatu, Basil Mramba na Daniel Yona Ndhira, wamefikishwa mahakamani kwa kuisababishia serikali hasara ya Sh. bilioni 11.2 kwa kutoa msamaha wa kodi kwa kampuni ya Alex Stewart.

Utafiti huu hauna haja ya kuwatia hatiani akina Mramba lakini kwa sababu GFI inasema sehemu ya fedha zinazoibwa hupatikana kwa misamaha ya kodi huu ni mfano mmoja wapo wa namna mtu anavyoweza kutumia mamlaka yake kujitajirisha.

Kama serikali imeweza kufungua mashitaka kwa mawaziri wawili tu wa zamani wa fedha ambao hasara waliyotia imefikia kiasi cha Sh. bilioni 11.2, je imepoteza kiasi gani kwa mawaziri wengine katika awamu tofauti za uongozi?

Kama kweli serikali inataka kufahamu ni akina nani wana fedha Uswisi, sehemu nzuri ya kuanzia ni hapa kwa mawaziri wa fedha na uchumi waliopita kwenye awamu tofauti hapa nchini.

Wengi wa vigogo wa nchi mbalimbali waliobainika kuhifadhi fedha Uswisi wanatoka katika nchi zenye utajiri wa maliasili kama Tanzania.

Serikali inaweza kuangalia zoezi zima la ugawaji wa vitalu kwa kampuni kubwa za mafuta zinazotafuta uwepo wa nishati hiyo hapa nchini na misamaha mbalimbali iliyowahi na inayoendelea kutolewa kwa makampuni ya madini hapa nchini.

Kuna taarifa kwamba baadhi ya makampuni makubwa ya kigeni hutumia rushwa ili wapewe vitalu vya gesi katika maeneo ambako kuna uwezekano mkubwa wa kupatikana gesi kuliko mengine. Wakipewa upendeleo huo, huweka fedha kwenye akaunti za waliowasaidia zilizo nje ya nchi.

Uchunguzi wa hili usiishie tu kwa mawaziri bali uende hadi kwa makatibu wakuu wao na maofisa wa ngazi za juu waliokuwa na ushawishi katika utoaji wa misamaha, vitalu na leseni mbalimbali za uchimbaji wa madini.

Humu ndimo wanapopatikana wengi wenye fedha chafu nchini Uswisi.

4. Jeshi la Polisi Tanzania

WAKATI ‘dili’ zinapofanyika na kubainika, watu wa kwanza kupewa taarifa ni Jeshi la Polisi kwa ajili ya kukamata watuhumiwa. Hawa ndiyo wanaoandaa mashitaka na hawa ndiyo wataamua kuwapo au kutokuwapo kwa kesi.

Aliyewahi kuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi la Afrika Kusini, Jackie Selebi, amefungwa jela hivi karibuni, kutokana na uhusiano wake na mhalifu maarufu nchini humo, Glen Agliotti. Mhalifu huyo alikuwa akimpa mkuu huyo zawadi mbalimbali na pia kumwekea fedha katika akaunti zake.

Tanzania kwa sasa ni miongoni mwa nchi zinazokamata sana dawa za kulevya ingawa kuna tuhuma kwamba magwiji wa biashara hizo wana mahusiano mazuri na baadhi ya vigogo wa Jeshi la Polisi.

Tukichunguza vizuri mabosi wa Polisi, tunaweza kupata kitu kuhusu akina nani wamehifadhi fedha zao Uswisi au popote duniani isivyo halali.

5. Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali 

KATIKA kashfa ya ununuzi wa rada, jina la aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Andrew Chenge, limeibuka mara nyingi na vyombo vya upelelezi vya Uingereza vinamtaja kama miongoni mwa wahusika wakuu wa kashfa hiyo.

Mwanasheria Mkuu wa serikali ndiye mshauri mkuu wa serikali kwenye mikataba minono (mikubwa) baina ya nchi na nchi au nchi na mashirika makubwa ya kimataifa.

Yeye ndiye anayeweza kuamua iwapo serikali iingie kwenye dili au la. Kama Chenge na baadhi ya wasaidizi wake walitajwa kwenye kashfa ya rada, ni wazi kwamba ofisi hii inatakiwa kumulikwa wakati serikali ikitafuta walioficha fedha Uswisi.

Kwa bahati nzuri, tayari inafahamika kuwa Chenge ana akaunti katika nchi za kigeni kama ilivyobainika wakati wa uchunguzi wa kashfa ya rada.

6. IKULU

Fujimori, Mobutu, Sani Abacha, Francosi Duvallier, Omar Bongo na Theodor Nguema wana mambo matatu yanayowafananisha; wote waliwahi kuwa marais katika nchi zao,  walifanya ufisadi wa kutisha na wote walificha mabilioni yao Uswisi.

Japo hii haimaanishi kuwa waliowahi kuwa marais wa Tanzania nao wana akaunti katika taifa hilo, sio vibaya kujiridhisha kwa kufanya uchunguzi ili kubaini kama wanaweza kuwa wameficha fedha Uswisi.

Kwa Tanzania, marais wenyewe wako wanne tu na hivyo kuchunguza si kazi ngumu.

Ikumbukwe kwamba rais pekee wa Tanzania kufungua ofisi ya biashara akitumia anuani ya Ikulu, Benjamin Mkapa, alipoumwa goti takribani miaka kumi iliyopita, alikwenda kutibiwa nchini Uswisi !

Labda tujiulize, angewezaje kuishi kule kwa miezi mitatu bila ya kuwa na akaunti katika mojawapo ya benki za huko? Je, ilikuw (ina) kiasi gani cha fedha?

Kwa mfano, Mkapa si ndiye aliyekuwa rais wakati wa ubinafsishaji? Serikali yake si ndiyo iliyopitisha misamaha mingi ya kodi kwa makampuni ya madini? Si mkitaka mnachunguza tu?

Tukiwa na nia ya kutaka kujua nani ana fedha Uswisi tutajua tu. Mimi nimetoa mchango wangu wenye pa kuanzia tu. Wengine wanaweza kutoa michango yao kwenye maeneo mengine.


KIBONZO KINACHO NANGA BARAZA LA VIJANA LA CHAMA KIMOJA




HII NDIO HALI YA HEWA YA DAR ES SALAAM ASUBUHI NA ADHUHURI YA LEO





 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU