Facebook Comments Box

Tuesday, October 1, 2013

MKENYA ALIYE DAIWA KUMTEKA DR ULIMBOKA ATOZWA FAINI TSH 1, 000


Mtuhumiwa wa kutoa ushahidi wa uongo wa kumteka aliyekuwa mwenyekiti wa chama cha madaktari, Dk Steven Ulimboka, Joshua Muhindi akitoka katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam jana,mara baada ya kulipiwa faini ya Sh 1,000.
Dar es Salaam. 

Mkenya Joshua Muhindi aliachiwa huru baada ya kulipa faini ya Sh1,000 kwa kupatikana na hatia ya kuidanganya polisi kuwa alihusika kumteka na kumjeruhi Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk Steven Ulimboka.
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ilimhukumu kifungo cha miezi sita jela au kulipa faini hiyo. Mulundi alilipiwa faini hiyo na Mwandishi wa Habari wa Redio Times, Chipangula Nandule.

Hukumu hiyo imetolewa leo na Hakimu Mkazi, Aloyce Katemana baada ya Wakili wa Serikali Mwandamizi, Tumaini Kweka kusoma maelezo ya awali na mshtakiwa huyo kukiri alitoa taarifa ya uongo kwa polisi kuhusu tukio hilo.
Kabla ya hukumu hiyo, Mulundi aliomba Mahakama impunguzie adhabu kwa kuwa hilo lilikuwa kosa lake la kwanza. Pia alijitetea kuwa Juni 27, 2012 akiwa Arusha alitekwa na kupelekwa Dar es Salaam ambako alikuwa hana mwenyeji wala hakuwahi kufika.
Alisema kutokana na kutekwa huko alichanginyikiwa hivyo kukubali chochote alichoambiwa afanye kwa kuwa aliyemteka alikuwa na silaha na alimwelekeza mambo ya kuzungumza.
“Mheshimiwa kwa ajili ya vitisho hivyo, nilikwenda Kawe katika Kanisa la Ufufuo na Uzima lililoko kwenye eneo la Tanganyika Packers, mbele ya Mchungaji Joseph Malwa Kiliba na kuungama kuwa ni miongoni mwa watu waliomtesa Dk Ulimboka katika Msitu wa Pande,” alisema Mulundi na kuongeza.
“Siwalaumu Serikali, upande wa mashtaka wala polisi kwa kitendo cha kuniweka gerezani kwa muda mrefu, najilaumu mimi mwenyewe.” Kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo, Kweka aliiambia Mahakama kuwa hana kumbukumbu za uhalifu za mshtakiwa lakini aliomba apewe adhabu kali kutokana na mazingira ya tukio hilo.
Akitoa hukumu, Hakimu Katema alisema alifikia uamuzi huo kwa kuzingatia maombi ya mshtakiwa ya kupunguziwa adhabu.
CHANZO: MWANANCHI


Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU