Facebook Comments Box

Tuesday, April 9, 2013

YANGA WAKATAA MECHI ZAO KUONESHWA BURE NA SUPER SPORT

Siku moja baada ya shirikisho la soka nchini TFF kubadilisha ratiba ya baadhi ya mechi za ligi kuu ya Tanzania bara ili kuweza kufanikisha mpango wa kuonyesha mechi hizo kupitia kituo cha Supersport, klabu ya Yanga kupitia makamu wake mwenyekiti Clement Sanga imesema haikubaliani na mpango huo kwasababu haujafuata utaratibu na pia utaziingizia hasara kubwa klabu zinazohusika na mpango huo.

Akizungumza na mtandao huu Sanga alisema kwamba mpango huo wa kuonyesha mechi za ligi kuu bure kwenye Supersport haupo katika kuzinufaisha vilabu bali wahusika wengine wa mpango huo.

"Kwanza jambo muhimu kuhusu suala hili kumekuwepo na mfumo m'bovu wa mawasiliano baina ya TFF, Supersport na vilabu vyenyewe kama Yanga. Sisi kwa upande wetu tunaona kabisa huu mpango unatuingizia hasara sana, kwa mfano baada ya kubadilisha ratiba ya mechi zetu tutacheza mechi 3 ndani ya siku 8 wakati ilitakiwa ndani ya wiki tucheze mechi mbili na bado ukumbuke bado tunapaswa kusafiri kwenda Tanga hivyo kuna mambo ya gaharama na vitu vingine vingi tu. Lakini pia mechi ambazo wanataka kuzionyesha bure ni zile ambazo sie vilabu tunazitegemea sana kwenye suala zima la mapato na wao ndio wanataka kuzionyesha bure - na watanzania wengi wanaposikia hivyo mahudhurio uwanjani yanakuwa hafifu hivyo tunakosa mapato. Bora waonyeshaji wa mechi hizo wangekuwa wanatoa fidia kiasi fulani kutokana na matangazo ya kibiashara wanayopata ili kuweza kuzinufaisha klabu zetu, lakini si hivyo wanavyotaka wao. Nadhani kwenye hili TFF wangeliangalia vizuri liweze kutunufaisha sote na sio watu wachache kama ilivyo sasa," Aliongeza Sanga.

Alipoulizwa kama wameshawasilisha msimamo wao kwa uongozi wa TFF na kamati ya ligi Clement Sanga alisema, "Kwanza walipotuletea taarifa kuhusu jambo hilo kwa njia ya barua pepe tuliwajibu na baadae ikaja barua ambayo katibu wetu alijibu kutoa msimamo wetu juu ya suala hili, kinachojitokeza hapa TFF wanatumia mabavu yao kutupeleka peleka, sie tumeshika makali wao mpini. Sie tusipokubali kucheza jumatano kama wanavyotaka wao basi watachukua maamuzi ya kuigawia timu pinzani ushindi, la msingi sie tutakalolifanya hatutokubali mechi zetu zionyeshwe kwenye TV bila kupata fidia ya fedha. Sisi kama Yanga hatupo tayari kuona tunafanyishwa kazi bure. Supersport imeshafanya majaribio sana, sasa haya ya sasa nini? Viongozi wa soka tubadilike tuweke mbele maslahi ya soka letu kabla ya kujiridhisha nafasi zetu, haiwezekani watu wawili watatu waamue tu kwamba mechi kesho hakuna bila kujali hasara zitakazowagharimu wengine. Sie tulishajipanga kwamba Jumatano tunacheza na Oljoro, then tunasafiri kwenda Tanga kucheza na Mgambo then turudi Dar kwa ajili ya mchezo mwingine. Matayarisho ya mechi hizi tulishafanya wiki mbili kabla, tukalipia hotel na gharama nyingine, sasa haiwezekani ghafla kikundi cha watu fulani wenye nguvu za kimaamuzi kutubadilishia ratiba - je zile fedha tulizolipa mahoteli watatulipa akina nani, kwa sababu ni dhahiri unapolipia hotel unapewa na muda wa kuivitumia vyumba vile hivyo muda ule unapoisha fedha yako inakuwa imeenda. Nadhani hili suala linahitaji kuangaliwa vizuri, na viongozi wa vilabu tuwe na umoja kuweza kulipigania hili suala dhidi yetu. Tusiwe viongozi wa kuburuzwa ovyo ovyo."

Akizungumzia mahitaji wanayotaka ili wakubali mechi zao ziweze kuonyeshwa kwenye TV, Sanga alisema kwamba hicho kituo cha TV kinachotaka kurusha matangazo ya moja kwa moja ya mechi zao inabidi walete ofa ya kueleweka ambayo itaweza kufidia hasara ya kwenye mapato na gharama nyingine ambazo timu wataziingia ili kuweza kwenda sawa na ratiba zao. Pia akataka uwepo uwazi wa makubaliano yote ya kimsingi ili kuepusha migogoro ya namna hii.


Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU