Facebook Comments Box

Sunday, August 24, 2014

CUF WALAANI UNYAMA WALIO FANYIWA VIONGOZI WA UAMSHO

Chama cha wananchi CUF kimetoa taarifa ya kulaani vikali madai ya vitendo visivyo vya kiungwana walivyofanyiwa viongozi wa Uamsho
na jeshi la Polisi.

Madai ya kudhalilishwa kwa watuhumiwa hao yalitolewa wiki hii na Sheikh Farid katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, mbele ya
Hakimu Mkazi, Hellen Riwa, wakati kesi ya tuhuma za ugaidi inayowakabili ilipokuwa ikitajwa.

Wakili wa Serikali Mwandamizi, Peter Njike, alidai kesi ilikuja kwa ajili ya kutajwa, upelelezi haujakamilika na wanaomba hati ya kuwachukua washtakiwa saba, akiwamo Sheikh Farid kwa ajili ya mahojiano.

Hakimu Riwa alikubali maombi hayo na kuahirisha kesi hadi Septemba 3, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa. Hali hiyo ilisababisha
washtakiwa kuomba kutoa maelezo yao.
“Mheshimiwa wametuomba kwenda kutuhoji tena, mara ya kwanza tulipohojiwa, polisi hawakutumia ustaarabu wala ubinadamu, ni
ushenzi na ukatili, walituhoji uchi wa mnyama na kutupiga.

“Kiongozi Mkuu wa Uamsho, Sheikh Mselem Ally Mselem, mwenye heshima,mfasiri wa Kur’ani, alinihadithia alipohojiwa walimfanya nini tumepigwa na hatukutibiwa, magereza wamejitahidi, lakini hawana nyenzo za matibabu.
 
“Watu wameumizwa vibaya, mengine hayasemeki, wanajisaidia haja ndogo damu wiki moja hadi mbili, tunaomba tufanyiwe uchunguzi
wa afya zetu, ipo siku mahakamani italetwa maiti.

“Tumekamatwa sababu hatutaki Muungano, hiyo ndiyo kesi ya msingi, tunawaambia ukweli katika mihadhara na watu wanatuamini, tunaomba Sheria ya Mabadiliko ya Katiba iletwe mahakamani tuijadili,” alidai Sheikh Farid.
Mshtakiwa wa 12, Salum Alli Salum aliomba mahakama imwite daktari ili aweze kufanyiwa uchunguzi wa afya yake kwani ameingiliwa kijinai kwa nguvu. “Mheshimiwa tunalazimishwa kutoa
maelezo wanayoyataka wao, wanatuingilia kinyume cha maumbile, wanaingiza majiti,chupa, wengine wanavuja nyuma,kama unaweza hakimu twende faragha nikakuonyeshe.

“Askari ameniingilia kisha akaniingiza jiti mpaka likakatika kungekuwa na sehemu ningekuonyesha, Jeshi la Polisi la kwanza
kuvunja sheria, waliofanya madhila haya wanawatukanisha Watanganyika na kufanya waonekane wabaya,” alidai mshtakiwa huyo.
 
Baada ya washtakiwa hao kutoa malalamiko yao, mahakama iliwaahidi washtakiwa hao waende wakahojiwe na muda wotewatakuwa katika mazingira salama. Sheikh Faridi nawenzake 19 wanashtakiwa kwamba kati ya Januari 2013 na Juni 2014 maeneo mbalimbali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania,walikula njama ya kutenda kosa la kuingiza watu nchini kufanya ugaidi.

Shtaka la pili linawakabili washtakiwa wote, wakidaiwa kuwa katika kipindi hicho walikubaliana kumuingiza Sadick Absaloum na Farah Omary nchini ili kushiriki kutenda makosa ya ugaidi. Katika shtaka la tatu linalomkabili SheikhFarid, anadaiwa kati ya Januari 2013 na Juni 2014 maeneo mbalimbali ya Jamhuriya
Muungano wa Tanzania, huku akijua ni kosa, alimuingiza nchini Sadick na Farah kufanya ugaidi. Sheikh Farid pia anadaiwa kuwahifadhi Sadick na Farah, huku akijua watu hao walitenda vitendo vya kigaidi.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Jamal Swalehe, Nassoro Abdallah, Hassan Suleiman, Anthari Ahmed, Mohammed Yusuph, Abdallah Hassani, Hussein Ally na Juma Juma.
Wengine ni Saidi Ally, Hamisi Salum,Saidi Amour Salum, Abubakar Mngodo, Salum Ali Salum, Salum Amour Salum,Alawi Amir, Rashid Nyange, Amir Hamis Juma, Kassim Nassoro na Said Sharifu.
 
Wakati huohuo, kesi nyingine ya ugaidi inayomkabili Kiongozi Mkuu wa JUMIKI,Sheikh Mselem Ali Mselem na mwenzake,Abdallah Said
Ali, imeahirishwa Septemba 3, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa kwa sababu Sheikh Mselem hakuwapo anaumwa.

Taarifa kamili ya chama hicho isome hapo chini:-
TAARIFA KWA UMMA NA VYOMBO VYA HABARI
TAREHE 23/08/2014
 
UNYAMA WA JESHI LA POLISI KWA MAHABUSU
 
CUF Chama cha Wananchi kinalaani vikali uukatili na ushenzi uliofanywa na jeshi la polisi dhidi ya viongozi wa Jumuiya ya Uamsho
na wenzake 19 . Kwa mujibu wa walivyoeleza watuhumiwa hao Shekh Farid Had Ahmed na wenzake Jeshi la polisi limewafanyia ukatili wa hali ya juu usiostahili kwa binadamu.

Mahabusu hao wanadai kulawitiwa na na asakri wa jeshi la polisi, kuwekewa vitu vyenye ncha kali kwenye sehemu za haja kubwa na mateso maengine mengi ikiwa ni pamoja na kupigwa hadi kuumizwa.

Hata kama ni wakosaji matendo haya ni kinyume na haki za binadamu. Inashangaza kuona vitendo vilivyokuwa vinafanywa na Makaburu dhidi ya Watu weusi wa Afrika Kusini sasa Vinafanywa na Vijana wa Kitanzania dhidi ya Watanzania wenzao kwa kisingizio cha Ugaidi.
CUF hatuoni mantiki ya uvunjaji wa Haki za Binadamu kwa kiasi hiki kwa watu wanaotuhumiwa kwa kile kinachoitwa kujishirikisha na Matendo ya Kigaidi. Hatakama watuhumiwa hao watiwa hatiani kwa makosa hayo, bado hukumu yao haitakua kulawitiwa kama ilivyoelezwa na mmoja kati ya Watuhumiwa hao mbele ya Mahakama.

Matendo hayo yanafanywa na Jeshi la Polisi dhidi ya Viongozi wa Dini , hivi tunataka wafuasi wao na Familia zao wafanye nini? CUF-Chama cha Wananchi kina mtaka Rais kutoa kauli na Msimamo wa Serikali dhidi ya unyanyasaji na udhalilishaji huu uliofanywa na Jeshi la.Polisi ili Wananchi wapate kujua hatua zitazo chukuliwa na Serikali sambamba na kukubali Ombi la Watuhumiwa la kufanyiwa uchunguzi wa Afya zao kama lilivyo wasilishwa kwenye Mahakama inayosikiliza Kesi hiyo.

Tunatoa wito kwa Taasisi zinazoshughulikia mambo ya Uvunjwaji wa.Haki za Binaadamu kufuatilia kwa Karibu suala hili na kuchukua hatua zinazostahili. Watuhumiwa hao wamelalamika kwamba mpaka hivi sasa wale
waliojeruhiwa bado wanauguliwa maumivu na hawajapewa matibabu .Wapo ambao mpaka hivi sasa kutokana na vitendo vya kishenzi waliofanyiwa bado mpaka leo hii hawajapata matibabu yoyote.

CUF Chama cha Wananchi kinawaomba tunawaomba Familia na Waislamu wote kua na subira na kufuatilia suala hili kwa njia za Sheria
ili kuweza kupata ufumbuzi wa tatizo hili la udhalilishaji uliofanywa na Jeshi la Polisi dhidi ya Familia zenu na Viongozi wetu.
 
Imetolewa na
Abdul Kambaya
Naibu Mkurugenzi Habari na Uenezi


Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU