Facebook Comments Box

Thursday, September 12, 2013

WAGENI WOTE WATAKAO INGIA ZANZIBAR KUPIMWA MALARIA

KITENGO cha kupambana na Malaria Zanzibar (ZMPC) kimesema kinatarajia kuanza kampeni ya kuchunguza malaria kwa wageni wote watakaoingia nchini kupitia uwanja wa ndege na bandari ya Malindi.

Ofisa mwandamizi wa kitengo wa ZMPC, Mwinyi Mselem akizungumza na waandishi wa habari kuelezea mikakati ya kupambana na malaria nchini, alisema kitengo kimepanga kutekeleza mikakati hiyo, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha kwamba ugonjwa wa malaria unatokomezwa na hakuna njia za kuambukizwa kwa wananchi.

“Tunakusudia kuanzisha zoezi la kupima afya za wageni wote wanaoingia nchini kupitia njia za uwanja wa 
ndege pamoja na bandarini ili kujuwa afya za wageni wanaoingia nchini,” alisema.

Alisema mikakati ya kitengo cha kupambana na malaria ifikapo mwaka 2017 ni kuhakikisha ugonjwa huo umetokomezwa na siyo tishio tena kwa afya za wananchi. Kwa sasa Zanzibar imefanikiwa kushusha maambukizi ya ugonjwa huo kutoka asilimia 32 hadi kufikia asilimia moja na kupunguza vifo vya akinamama na watoto.

Hata hivyo, Mselem alisema katika kipindi cha miaka miwili sasa kumejitokeza maambukizi mapya ya malaria kutokana na kuongezeka kwa uchafuzi wa mazingira na hivyo kupelekea mbu kuzaliana zaidi.

Alisema kitengo cha kupambana na malaria kinatarajia kuanza kazi ya kupiga dawa majumbani pamoja na sehemu za mazalia ya mbu. Mselem alisema kazi hiyo inatarajiwa kuanza katika kipindi cha msimu wa mvua za vuli, ambazo huibuka kwa mazalia mengi ya mbu yanayosababisha ugonjwa wa malaria.

Zanzibar inatajwa mfano wa kupambana na ugonjwa wa malaria, ambapo hivi karibuni Rais mstaafu wa Marekani, Bill Clinton alizindua mradi wa kupambana na ugonjwa huo wa kupima damu hapo katika uwanja wa Amaan mjini hapa.

Khatib Suleiman
HabariLeo, Zanzibar


Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU