Facebook Comments Box

Tuesday, August 20, 2013

UDA YAPELEKA MABASI MIKOANI KWA AJILI YA WANAFUNZI: YAWEKA PIA MABASI KWA AJILI YA WANAWAKE NA WALEMAVU

Wanafunzi wa mikoa mbalimbali nchini wataondokana na kero ya usafiri wa daladala baada ya kampuni ya UDA kuingiza magari 10 kwa ajili ya kusafirisha wanafunzi ili kuwahi masomo.

Aidha, wanawake, wanaume na watu wenye ulemavu watakuwa na mabasi maalumu ambayo yatatoa huduma mikoani. 

Hayo yalisemwa jana Dar es Salaam na Ofisa Rasilimaliwatu wa UDA, Cyprian Malekela alipozungumza na waandishi wa habari jinsi kampuni hiyo inavyopambana na changamoto za usafiri ukiwamo uboreshaji wa huduma za usafiri mikoani.

Alisema kampuni hiyo kwa kuanzia, itatoa mabasi 10 ya wanafunzi kila mkoa na itaanza na Mwanza, Dodoma, Iringa, Mbeya na Arusha na sasa iko katika hatua ya mwisho ya mazungumzo na walimu wakuu wa shule za
msingi na sekondari ili kujua vituo watakavyopandia wanafunzi na muda wa kuwachukua na kuwarudisha.

Malekela alisema kampuni hiyo itakuwa na magari mengine 15 ya wanawake ambao hawawezi kugombania magari, 10 kwa ajili ya wanaume huku mengine sita yakiwa ni maalumu kwa watu wenye ulemavu.

"Kampuni imedhamiria kuboresha huduma zake kwa kuongeza idadi ya magari kwa ajili ya wanafunzi, wanawake, walemavu na wanaume lengo ni kutoa huduma za usafiri kila mkoa ili kuboresha huduma ya usafiri na kuondoa kero kwa wananchi wanaohitaji usafiri wa uhakika," alisema.

Aliongeza kusema kwamba awali kampuni hiyo kabla haijabinafsishwa ilikuwa ikimilikiwa na Serikali huku ikiwa na magari saba, lakini sasa iko mikononi mwa Mtanzania ambaye ameongeza idadi ya magari hadi 40.

Alisisitiza kuwa UDA imedhamiria kuboresha huduma za usafiri kila mkoa na kutoa rai kwa wamiliki wa kampuni na taasisi nchini kukodisha magari hayo ili yatoe huduma na hata madereva na wahudumu wa mabasi ya UDA wamepewa mafunzo maalumu ya kuhudumia abiria. -- HabariLeo



Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU