Facebook Comments Box

Thursday, August 29, 2013

ASKOFU DR SHAO ASEMA WACHAGGA KUZIKANA KWAO NI UTARATIBU WA HOVYO

Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini, Dk Martin Shao, amekosoa utamaduni wa wakazi wa mkoa wa Kilimanjaro, ambao wengi ni Wachaga, wa kuzikana nyumbani (vihamba) na kusema ni utaratibu wa hovyo.

Akifafanua kauli hiyo juzi, Askofu huyo alielezea hofu ya kupotea kwa mashamba ya mibuni mkoani humo, kutokana na utamaduni uliosababisha ongezeko la makaburi kwenye mashamba hayo.

“Naomba Serikali mkoani, iweke utaratibu wa kudumu wa maeneo ya maziko badala ya watu kuzikwa ovyo majumbani… ardhi hii ni ndogo, lakini bado tunaimega kwa kuzika, hapo baadaye hatutakuwa na 
mashamba ya mibuni,” alisema.

Askofu huyo aliiomba Serikali kuelimisha wakazi hao, ili wabadili mfumo wa kugeuza makazi na mashamba yao  sehemu ya kuzika ndugu zao, ili kutotumia vibaya ardhi ndogo iliyopo.

Alisema hayo wakati wa harambee ya kuchangia Sh milioni 95 za ujenzi wa Kanisa la Usharika wa Nanjara  wilayani Rombo na kusisitiza umuhimu wa Serikali kuweka utaratibu wa maeneo ya kudumu ya maziko.

Kwa mujibu wa Askofu Shao, licha ya hatari ya kupunguza mashamba ya kahawa ambayo ndiyo nguzo ya uchumi wa mkoa, lakini pia utaratibu wa sasa wa kuzikana majumbani, utaathiri vizazi vijavyo na kusababisha vikose maeneo ya ujenzi wa makazi.

Alisema kutokana na mkoa kubuni miradi mikubwa ukiwamo wa soko la biashara la kimataifa la Lokolova na mji wa kitalii wilayani Siha, ni matumaini ya Kanisa kuwa pia Serikali itaandaa utaratibu wa kila wilaya, kutenga maeneo ya maziko ya jumuiya.

Dk Shao alisema iwapo mpango wa kila wilaya kutenga maeneo hayo utashindikana, Kanisa litakuwa tayari kununua ardhi kwa ajili ya waumini wake.

Akijibu ombi hilo, Naibu Waziri wa Nchi, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Aggrey Mwanri, alisema amelisikia na atalifikisha kwa Kamati ya Ushauri ya Mkoa ili ufumbuzi upatikane.

Mwanri pia alishukuru Kanisa kwa kutambua mchango wa Serikali kuleta maendeleo ya wananchi. Katika harambee hiyo, Sh milioni 35.5 zilipatikana. --- Imenukuliwa kutoka kwenye gazeti la HabariLeo


Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU