Facebook Comments Box

Wednesday, April 3, 2013

VIWANGO VIPYA VYA NAULI KWA MUJIBU WA SUMATRA.


IMG_6840
 
Kaimu Mkurugenzi wa SUMATRA Athman Kilima akizungumza na waandishi wa habari  katika makao makuu ya taasisi hiyo wakati akitangaza kupanda kwa viwango vya nauli ya mabasi ya mikoani na Daladala.
 
Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) imekamilisha mchakato na kuridhia viwango vipya vya nauli kwa ajili ya usafiri wa mijini na usafiri wa kwenda mikoani. Viwango hivi vipya vimefikiwa baada ya kufuata taratibu za kisheria na za kiutendaji ambazo SUMATRA kama msimamizi na mdhibiti wa sekta ya usafiri wa barabara inapaswa kuzifuata kabla ya kuridhia viwango hivyo. Viwango vipya vya nauli vitaanza kutumika kuanzia tarehe 12 Aprili, 2013.
 
SUMATRA ina wajibu kisheria kuhakikisha pamoja na mambo mengine kuwa maslahi ya watumiaji na watoa huduma za usafiri yanalindwa ili kuwepo na huduma endelevu ya usafiri ulio bora, salama na wenye kukidhi mahitaji. Aidha SUMATRA ina jukumu la kujenga na kulinda mazingira mazuri na ya kuvutia kwa watoa huduma ili huduma ya usafiri inayotolewa inakuwa katika kiwango na gharama zinazoendana na huduma zenyewe. 
 
Katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2011/2012, SUMATRA ilipokea maombi rasmi kutoka kwa wamiliki wa vyombo vya usafiri wa barabara yakiwemo makampuni ya usafirishaji abiria ya Cordial Transport Services P.L.C, Happy Nation Co. Ltd, ABC Trans na Mwesigwa Mtazaha Kazaula yakipendekeza mapitio ya viwango vya nauli za mabasi yanayotoa huduma za usafiri mijini (Daladala) na mabasi yanayotoa huduma katika Mikoa kufuatia ongezeko la gharama za uendeshaji kwa mujibu wa mawasilisho yao.
 
Wakati maombi ya wamiliki wa Daladala yalilenga katika kuongeza viwango vya nauli kwa 149% ya viwango vya sasa, wamiliki wa mabasi ya masafa marefu waliomba nyongeza kati ya 35% na 48.5%.
 
Kwa mujibu wa Kifungu Na 18 cha Sheria ya SUMATRA, 2001, SUMATRA iliwashirikisha wadau mbalimbali katika kujadili na kupata maoni yao kuhusu maombi ya wamiliki ya kuongeza viwango vya nauli kabla ya kufanya maamuzi ya mwisho.
 
Aidha Mamlaka iliridhia viwango vipya kwa mujibu wa kifungu cha 16 Cha Sheria ya SUMATRA ambacho kinaipa Mamlaka kufanya mapitio ya nauli mara kwa mara kwa kuzingatia gharama za kutoa huduma, maslahi ya watoa huduma, faida, maslahi ya watumia huduma ya kulipa nauli yenye uwiano na gharama za huduma inayotolewa.
 
Kwa kuzingatia hoja za waombaji, maoni ya wadau, uchambuzi wa menejimenti, haja ya kupunguza gharama zisizo za lazima za uendeshaji na udhibiti wa vitendo vya uvunjaji wa Sheria na taratibu za uendeshaji shughuli za usafirishaji, Mamlaka ya SUMATRA iliamua kuongeza viwango vya juu vya nauli za Daladala kwa wastani wa 24.46%.
 
Aidha kwa mabasi ya masafa marefu, viwango vimeongezwa kwa 20.3% kwa mabasi ya kawaida, 16.9% kwa mabasi ya daraja la kati na 13.2% kwa mabasi ya daraja la juu.
 
Mchanganuo wa viwango vipya vya nauli ni kama ifuatavyo:
  1. Nauli za Daladala – Jiji la Dar es Salaam

Umbali wa NjiaKiwango Kipya cha NauliMfano wa Njia
Kilomita kati ya 0 – 10 (Na mipaka ya Jiji Kati)Sh 400/=Ubungo – Kivukoni
Kilomita kati ya 11 – 15Sh 450/=Mwenge – Temeke
Kilomita kati ya 16 – 20Sh 500/=Tabata Chang’ombe – Kivukoni
Kilomita kati ya 21 – 25Sh 600/=Pugu Kajiungeni – Kariakoo
Kilomita kati ya 26 – 30Sh 750/=Kibamba – Kariakoo
Mamlaka imeandaa majedwali kwa njia zote za Dar es Salaam. Majedwali hayo yanaweza kupatika katika tovuti yetu www.sumatra.or.tz.
 
Nauli ya Mwanafunzi itakuwa Sh 200/= ambayo ni nusu ya nauli ya mtu mzima ya kiwango cha chini cha nauli ya Sh 400/=. Nauli hii itatumika kwa njia zote za Jiji la Dar es Salaam.
 
2.Nauli za Mabasi ya Masafa Marefu 
 
Daraja la BasiNauli ya zamani kwa km-abiriaNauli mpya kwa km-abiriaMfano wa kiwango kipya cha nauli kwa baadhi ya njia
Basi la Kawaida kwa njia ya lamiSh 30.67Sh 36.89DSM–Mbeya Km 833Sh 30,700
Basi la Kawaida kwa njia ya vumbiSh 37.72Sh 46.11S/wanga-KigomaKm 551Sh 25,400
Basi la hadhi ya kati (Semi LuxurySh 45.53Sh 53.22DSM–Mwanza Km 1,154Sh 61,400
Basi la hadhi ya juu (Luxury)Sh 51.64Sh 58.47DSM–Arusha Km 616Sh 36,000
Ili kuhakikisha kuwa kuna uwiano kati ya viwango vipya vya nauli na ubora wa huduma ya usafiri, Mamlaka imetoa maagizo kwa wamiliki wa mabasi ya masafa marefu kuboresha maeneo yanayohusiana na huduma ya usafiri kama ifuatavyo:
    1. Wamiliki wa mabasi kutokutumia wapiga debe katika kuuza tiketi za safari
    2. Wamiliki wa mabasi kuhakikisha wanafuata Kanuni za SUMATRA za Udhibiti wa Tozo na Nauli (SUMATRA Tarrif Regulations) ambazo zinahimiiza kuwepo kwa kumbukumbu sahihi za mahesabu ili kurahisisha mapitio ya viwango vya nauli
    3. Kufuata Sheria, Kanuni na Masharti ya Leseni ya usafirishaji abiria
    4. Kutoza nauli kwa mujibu wa daraja la basi lenye sifa kamili la daraja husika kama ilivyoainishwa katika Kanuni za Usalama na Ubora.
       
      Aidha kwa mabasi ya mjini, Mamlaka imetoa maelekezo yafuatayo:
    1. Kuhakiksha kuwa abiria wote wanapatiwa tiketi
    2. Kudhibiti vitendo vya ukiukwaji wa Sheria ikiwemo kutokamilisha safari maarufa kama kukata ruti, kubadili njia na unyanyasaji wa aina yoteyote kwa abiria
    3. Kutokutumia wapiga debe
    4. Wafanyakazi wa mabasi kuvaa sare nadhifu wakati wote.
Mamlaka ya SUMATRA inaendelea kuimarisha ushirikiano kwa kufanya kazi kwa karibu na Mamlaka zingine kama Wakuu wa Mikoa, Serikali za Mitaa, Mamlaka za Miji, Polisi, TBS, TANROADS, Kamisheni ya Bima na wananchi kwa ujumla, katika kuleta mageuzi kamili ya utoaji wa huduma za usafiri wa barabara kwa kiwango cha juu.
 
A.S.K. Kilima
KAIMU MKURUGENZI MKUU
2 Aprili, 2013


Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU