Facebook Comments Box

Sunday, February 10, 2013

MSUYA ALAZWA KWENYE HOSPITALI YA KIFALME UINGEREZA

 
Rais Jakaya Kikwete akimjulia hali Waziri Mkuu Mstaafu, Cleopa David Msuya Hospitalini, kwa sasa amepelekwa Uingereza kwa matibabu zaidi 
WAZIRI Mkuu Mstaafu, Cleopa David Msuya aliyepelekwa nchini Uingereza hivi karibuni kwa matibabu, anatibiwa katika hospitali ya kifahari inayomilikiwa na familia ya Malkia Elizabeth wa Uingereza.
Msuya anatibiwa katika Hospitali ya ‘The King Edward the V11’s Sister Agnes’ ambayo ni binafsi inayoongoza kwa huduma bora na gharama nchini humo, ambayo mlezi wake mkuu ni Malkia Elizabeth wa Uingereza.
Waziri Msuya aliyekuwa amelazwa katika Hospitali ya Muhimbili kitengo cha Mifupa (MOI), alipelekwa nchini Uingereza Februari saba kwa ndege maalumu ya kukodi. Hata hivyo, gharama za kukodi ndege iliyomsafirisha Msuya kwenda Uingereza hazijajulikana, wala aliyemlipia.
Mwananchi Jumapili liliwasiliana kwa simu na hospitali hiyo ya The King Edward the V11’s Sister Agnes na kuzungumza na idara ya mapokezi, ambayo baada ya kupewa jina la waziri huyo kwa herufi moja moja, walimuunganisha mwandishi kwa simu hadi katika kitengo cha kuhudumia wagonjwa.
Simu ya pili ilipokelewa na msichana aliyehoji maswali kadhaa ambapo baada ya kuridhishwa na majibu ya mwandishi, alimuunganisha moja kwa moja na Msuya katika chumba alicholazwa .
Hata hivyo, baada ya kupokea simu ya mwandishi wa habari hizi, Waziri Mkuu huyo mstaafu hakuzungumzia lolote kuhusu hali yake ya kiafya, bali alimhoji mwandishi, akitaka kujua alikopata mawasiliano ya hospitali aliyolazwa.
“Habari yako, nani anazungumza?,?? Msuya aliuliza. Baada ya mwandishi kujitambulisha, Msuya alisema: “Nani aliyekupa ‘contact’ zangu za huku?.” Kisha akakata simu.
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Hussein Mwinyi alipohojiwa kuhusu gharama za matibabu ya viongozi nje ya nchi alisema kuwa zinalipwa na Serikali.
“Mawaziri wakuu wastaafu na waliopo madarakani wote ni wafanyakazi wa Serikali, hivyo gharama za matibabu yao zinalipwa na Serikali,” alisema Mwinyi na kuongeza:
“Hata hivyo Serikali hulipa gharama hizo kwa anayetibiwa nje iwapo kuna sababu ya kufanya hivyo, hii siyo kwa viongozi tu, bali kwa Mtanzania yoyote mwenye mahitaji.”
Ofisa Uhusiano wa Kitengo cha MOI , Almas Jumaa alisema kuwa Msuya alipewa ruhusa katika hospitali hiyo tangu Februari Nne, baada ya kupata nafuu. Hospitali ya Mfalme Edward wa Saba iliyopo katika Mtaa wa Beaumont, katika Jiji la Westmister, ilianzishwa mwaka 1899.
Mtoto wa mfalme wa Wales, ambaye baadaye alikuwa Mfalme, Edward wa V11, kimada wake Agness Keyser, pamoja na dada wa Agness, aliyeitwa Fanny, walianzisha huduma za matibabu kwa ajili ya maofisa wa jeshi.


Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU