Facebook Comments Box

Thursday, October 4, 2012

RAFU MBAYA YA BOBAN YAMPELEKA YONDANI HOSPITALI


Yondan wa pili kutoka kulia waliosimama katika kikosi cha Yanga jana
BEKI Kevin Yondan wa Yanga hajaamka mazoezini leo, kutokana na kuumizwa vibaya na kiungo wa Simba, Haruna Moshi ‘Boban’ katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Yanga wapo Uwanja wa sekondari ya Loyola, Mabibo hivi sasa wakifanya mazoezi, lakini Yondan anajiandaa kwenda hospitali kufanyiwa uchunguzi wa maumivu yake.
Habari kutoka Yanga, zimesema kwamba tangu jana beki huyo anasikia maumivu makali na hatima yake itajulikana baada ya vipimo hivyo.
Yanga jana ilitoka nyuma na kulazimisha sare ya kufungana bao 1-1 na wapinzani wao wa jadi, Simba SC katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, uliopigwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, kuanzia saa 1:02 usiku.
Habari kutoka ndani ya Simba, zimesema kwamba wachezaji waliahidiwa asilimia ya 60 ya mgawo wa timu kutokana na mapato ya milangoni na asilimia 20 ya kiwango hicho kuongezwa na Friends of Simba, lakini kwa sare hiyo, ahadi hiyo imeota mbawa.
Hata hivyo, uongozi wa Simba unafikiria kuwapa ‘kifuta jasho’ wachezaji wake kwa angalau kulinda hadhi ya klabu kwa kutokubali kufungwa na wapinzani wao hao wa jadi jana.
Yanga ambao walimaliza mechi hiyo wakiwa pungufu baada ya Simon Msuva kutolewa nje kwa kadi nyekundu dakika ya 77 kwa kumrudishia rafu Juma Nyosso, ndio waliohaha kusawazisha bao, baada ya kutanguliwa kwa bao la mapema la kiungo Amri Kiemba.  
Hadi mapumziko Simba walikuwa tayari mbele kwa bao 1-0, lililotiwa kimiani na kiungo Amri Kiemba dakika ya pili.
Simba walicheza vizuri kipindi chote cha kwanza wakigongeana pasi za uhakika na kuwazidi kasi uwanjani wapinzani wao, wakati Yanga pamoja na kuzinduka baada ya kufungwa bao, lakini makosa yalikuwa mengi.
Pasi zao zilikuwa nyingi hazifiki, walikuwa wanapokonyeka mipira kirahisi, wanazidiwa nguvu na wapinzani wao katika kugombea mipira na hata mashambulizi yao hayakuwa ya mpangilio, zaidi ya kuonekana kubahatisha zaidi.
Katika kubahatisha huko, Mbuyu Twite alifumua shuti zuri dakika ya 38 kutoka wingi ya kulia, ambalo lilitoka nje sentimita chache.    
Kabla hata ya dakika 45 za kipindi cha kwanza kumalizika, kocha Mholanzi Ernie Brandts alimtoa Hamisi Kiiza na kumuingiza Frank Domayo ili kuimarisha safu ya kiungo, ambayo ilionekana kuzidiwa na Simba inayofundishwa na Mserbia, Milovan Cirkovick.
Kipindi cha pili, Yanga walianza na mabadiliko, kocha Ernie Brandts akimtoa kiungo Nizar Khalfan na kumuingiza mshambuliaji Didier Kavumbangu, ambaye alikwenda kuongeza nguvu ya safu ya ushambuliaji ya timu hiyo.
Angalau, kipindi cha pili Yanga walionekana kucheza vizuri na kupeleka mashambulizi yenye uhai langoni mwa Simba, ingawa safu imara ya ulinzi ya Wekundu wa Msimbazi ilikuwa kikwazo.
Katika dakika ya 63, beki Paul Ngalema aliunawa mpira katika harakati za kuokoa na refa Mathew Akrama akaamuru penalti, ambayo ilikwamisha kimiani kiufundi na Said Bahanuzi ‘Spider Man’.
Katika dakika ya 77 Mathew Amkrama alimtoa nje kwa kadi nyekundu ya moja kwa moja Simon Msuva, baada ya kumkita Juma Nyosso, aliyemkanyaga ‘kwa bahati mbaya’. Msuva alichezewa rafu na Nyosso na tayari refa alikwishapuliza filimbi na kumpa kadi ya njano beki huyo wa Simba, lakini kiungo huyo wa Yanga akaponzwa na hasira za kitoto.
Pamoja na Yanga kubaki pungufu, waliendelea kucheza vema na mashambulizi yalikuwa ya pande zote mbili. Refa Akrama alishindwa kuumudu mchezo na maamuzi yake mengi yalikuwa chungu kwa Yanga, mfano Haruna Moshi ‘Boban’ alipomchezea rafu mbaya beki Kevin Yondan hadi akashindwa kuendelea na mchezo, na nafasi yake ikachukuliwa na Juma Abdul alimpoza kwa kadi ya njano.
Hakumchukulia hatua yoyote kipa Juma Kaseja aliyeonekana kupoteza muda tangu mwanzo, na alimpa onyo tu zaidi ya mara tatu.
Alipingia Abdul alikwenda kucheza beki ya kulia na Mbuyu Twite akahamia katikati kucheza na Nadir Haroub ‘Cannavaro’.
Baada ya mchezo huo, kocha wa Simba, Milovan alisema kwamba ulikuwa mchezo mzuri na Yanga walicheza vizuri, lakini timu yake ilicheza vizuri na anajivunia. Alisema Yanga imeimarika tofauti na ilivyokuwa awali na kwamba hizo ni dalili Ligi Kuu msimu huu itakuwa ngumu.
Kwa upande wake, kocha wa Yanga, mwanzoni hawakucheza vizuri, lakini baadaye walitulia na kucheza vizuri. “Hii ni mechi ya kweli ya upinzani, unaweza kuona rafu na kadi nyingi,”alisema Brandts.
Kwa matokeo hayo, Simba imefikisha pointi 13, ndani ya mechi tano na kuendelea kuongoza Ligi Kuu, wakati Yanga imefikisha pointi nane na kubaki nafasi ya tano, kwani Coastal Union imetoa sare ya 2-2 na JKT Oljoro mjini Arusha na kufikisha pointi tisa.   
SIMBA: Juma Kaseja, Nassor Chollo, Paul Ngalema, Juma Nyosso, Shomary Kapombe, Jonas Mkude/Haruna Moshi, Amri Kiemba, Mwinyi Kazimoto, Felix Sunzu, Edward Christopher/Daniel Akuffo na Mrisho Ngassa.
YANGA: Yaw Berko, Mbuyu Twite, Stefano Mwasyika, Nadir Cannavaro, Kevin Yondan/Juma Abdul, Athumani Iddi, Simon  Msuva, Haruna Niyonzima, Said Bahanuzi, Hamisi Kiiza/Frank Domayo na Nizar Khalfan/Didier Kavumbangu.


Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU