Facebook Comments Box

Friday, August 29, 2014

BAADA YA KUWA NA MGOGORO NA YANGA OKWI RASMI SIMBA

NA BIN ZUBERY

STAILI ile ile waliyotumia Yanga SC kumpata mshambuliaji Emannuel Arnold Okwi ndiyo ambayo klabu yake ya zamani, Simba SC inatumia kumrejesha kundini Mganda huyo.

Akizungumza na Waandishi wa Habari jioni hii mjini Dar es Salaam,
Okwi amesema kwamba amesaini Simba SC mkataba huru wa muda, baada ya Yanga SC kumpa barua ya kusitisha mkataba naye
jana pamoja na kumshitaki Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

Okwi amesema ameamua kuomba kuichezea Simba SC kipindi hiki
ambacho ana matatizo na Yanga SC ili kulinda kipaji chake, kwa
kuwa hata FIFA haitaki mchezaji akae bila kucheza.“Sasa wakati Yanga wanaendelea na kesi yao, mimi ninaomba nichezee Simba SC ili kulinda kipaji changu. Nimewaandikia barua TFF na FIFA pia na nina matumaini usajili wangu utaidhinishwa, kwa sababu mimi si tatizo katika hili,”amesema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC,
Zacharia Hans Poppe amesema kwamba wamemsaini mchezaji huyo baada ya kupitia kwa kina suala lake na Yanga SC na kugundua haki ipo upande wa mchezaji.

“Baada ya kulipitia suala lake na Yanga kwa undani kabisa na vielelezo ambavyo mchezaji mwenyewe ametupatia, tumejiridhisha tuko sahihi kumsaini ili acheze mpira kunusuru kipaji chake kipindi
hiki ambacho ana matatizo na Yanga SC,”amesema Poppe.



Tayari Simba SC imetuma jina la mchezaji huyo katika usajili wake
TFF na ataungana na Mganda mwenzake, Joseph Owino, Warundi
Pierre Kwizera na Amisi Tambwe na Mkenya, Paul Kiongera katika wachezaji watano wa kigeni.

“Tumewaandikia barua TFF kuomba kumtumia mchezaji huyu kwa
muda wakati kesi yake na Yanga inaendelea, tume ambatanisha na
barua yake ambayo yeye anatuomba kucheza kwetu kulinda kipaji
chake,”amesema Poppe.

Okwi aliichezea Simba SC tangu mwaka 2009 kabla ya Januari mwaka jana kuuzwa kwa dola za Kimarekani 300,000 Etoile du Sahel ya Tunisia. Etoile haikulipa fedha hizo Simba SC na baadaye ikaingia kwenye mgogoro na Okwi, aliyedai hakulipwa pia mishahara yake kwa miezi mitatu.

Okwi akawafungulia Etoile kesi FIFA na akaomba wakati mgogoro
wao unaendelea, aruhusiwe kuchezea timu yoyote kulinda kipaji chake, ndipo akajiunga na SC Villa ya kwao. Akiwa SC Villa ndipo aliposaini Yanga SC Desemba mwaka jana na pamoja na mapingamizi yaliyoanzia ndani, na baadaye klabu yake, Etoile- lakini Okwi aliidhinishwa kuichezea timu hiyo ya Jangwani.

Okwi aliichezea Yanga SC mechi 11 na kuifungia mabao matano- lakini kuelekea mechi tano za mwisho za Ligi Kuu msimu uliopita akaingia kwenye mgogoro na klabu hiyo. Okwi alisusa kushinikiza amaliziwe fedha zake za usajili na mgogoro wao umeendelea huku mchezaji huyo akiwa amesusa tangu Machi, miezi minne tu baadaye tangu asajiliwe.

Vikao kadhaa vimekwisha fanyika baina ya Okwi na Yanga SC tangu hapo kutafuta suluhu ya suala hilo na kikao cha mwisho leo baina ya mchezaji huyo na Mwenyekiti wa klabu hiyo, Yussuf Manji matokeo yake ni nyota huyo kurejea Msimbazi.

Kuhusu deni lao la dola 300,000 kumuuza mchezaji huyo Etoile, Poppe amesema haihusiani kabisa na usajili wake huu wa sasa. “Ile
kesi yetu ya madai ya fedha zetu kule FIFA ilikwishamalizika na vielelezo vyote vilipelekwa, bado kutolewa hukumu tu,” amesema.


Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU