![]()  | 
| Kituo cha reli cha Kigoma | 
Mji wa Ujiji ulioko Magharibi 
mwa Tanzania una historia ndefu miongoni mwa miji ya kale ya Afrika 
Mashariki na Kati ukihusishwa na biashara ya watumwa kutoka Burundi, 
Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo.
Ni katika eneo hilo la Ujiji ndiko mvumbuzi wa 
kimataifa, Dr David Livingstone, alipofikia akiwa katika safari zake 
zilizomtoa pwani ya Afrika mashariki hadi Kongo. Kwa sasa kuna 
makumbusho maalum kwa heshima yake na kumbu kumbu ya vizazi vijavyo.
Lakini nusu karne baada ya uhuru wa 
Tanzania, umaarufu wa mji huo mkongwe umeporomoka na hali ya maisha ya 
watu wake imeendelea kuwa duni. Mwandishi wa BBC Baruan Muhuza 
ametembelea mji huo na kujionea hali ilivyo.
Kwenye kituo cha makumbusho ya Dr David 
Livingstone katika eneo la Mnazi Mmoja-Kabondo Ujiji ni eneo ambalo kuna
 majengo mazuri yenye vyumba kadhaa vilivyobeba alama za ujio wa 
Mvumbuzi huyo aliyechangia kukomeshwa kwa biashara ya utumwa, lakini pia
 kumbukumbu za asili za vitu na watu wa mji huo.
Kufifia kwa umaarufu wa eneo kongwe la Ujiji 
kulichangiwa na sababu nyingi, ikiwemo kuanzishwa kwa mji mpya wa 
Kigoma. Kurejea kwa Ndiyunze Msherwampamba aliyekuwa kiongozi wa watu wa
 kabila la wagoma kutoka Kongo kuliibua jina la mji mpya Kigoma.
Alhaj Mikdad bin Ibrahim Tawfiq Malilo mwenye 
miaka 79 mkaazi maarufu wa Ujiji, ameiambia BBC kuwa Msherwampamba 
alipokelewa pamoja na wafuasi wa kabila lake na wakapewa eneo la 
kujitawala ambalo wakati huo lilikuwa likiitwa Rusambo , na sasa ndilo 
linaloitwa Kigoma.
![]()  | 
| Mji wa ujiji unakumbwa na umaskini si haba | 
„Walipompokea Msherwampamba wakapewa kanchi, 
eneo lenyewe ni sehemu hivi sasa wanasema ikulu ndogo zamani tulikuwa 
tunasema Kaizahofu, eneo lote lile kabla ya hapo lilikuwa linaitwa 
Rusambo. 
Sasa wenyeji warundi ndiyo wanajiita wajiji 
wakawa wanakwenda kuwatembelea wanasema 'tugende kubagoma,' likaendelea 
likabadilika ndiyo ikawa Kigoma basi ndiyo kitovu cha mahala kuitwa 
Kigoma asili Rusambo”
Kwa miaka mingi nguvu za kiuchumi za wakazi wa 
mji huo imekuwa ikitegemea Ziwa Tanganyika kwa uvuvi na usafiri wa 
kwenda na kutoka maeneo mbali mbali ya mwambao wa ziwa hilo zikiwemo 
nchi jirani za Burundi, Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo.
Pamoja na kupoteza uimara wake, Mji wa Ujiji na 
Kigoma kwa ujumla umeibuka upya katika miaka ya karibuni kwa kutoa watu 
waliojipatia umaarufu mkubwa katika eneo lote la Afrika Mashariki na 
kati ikiwa ni pamoja na wasanii wa muziki wakiwemo Naseeb Abdul 
anaejulikana zaidi kama Diamond, Wanasoka wastaafu Kitwana Manara, 
Kassim Manara, Edibily Lunyamila na hata nahodha wa sasa wa Timu ya 
Taifa ya Tanzania Juma Kaseja .
Tangu enzi za Ukoloni watu kutoka maeneo 
mbalimbali ya Jamuhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, Burundi, Rwanda na 
Zambia waliingia mji wa Ujiji hasa kipindi cha utawala wa biashara ya 
watumwa.
CHANZO: BBC SWAHILI 
Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog

