Katika siku za hivi karibuni, kumekuwapo na mjadala kuhusiana na hatua ya 
klabu ya Yanga kupinga udhamini wa Ligi Kuu ya Tanzania unaotarajiwa 
kufanywa na Azam Media.
 Tumeona ni vema tukatoa msimamo wetu wa pamoja kuhusiana na hatua hiyo ya wenzetu kwa lengo la kuweka rekodi sawa. Tunataraji hatua hii ya vilabu hivi 13 itafunga mjadala huu na 
tungependa wana habari, kama mtaamua kuuendeleza, basi muundeleze katika
 mlengo ambao wadau, yaani sisi vilabu vinavyoshiriki mashindano hayo, 
zimeamua kuufuata.
 Tunapenda kukumbusha kwamba kwa muda mrefu, kilio cha vilabu vya Ligi 
Kuu ya Tanzania kilikuwa ni ukosefu wa wadhamini na kwa bahati nzuri 
kuna dalili kwamba Mungu ameanza kukisikia kilio hicho msimu huu. 
 Kwa faida ya umma, tungependa kutoa takwimu za nchi jirani 
zinazotuzunguka. Kenya, kila klabu hupata Sh milioni saba za Kenya (sawa
 na Sh milioni 125 za Kitanzania) kwa mwaka –fedha ambazo zimeifanya 
ligi ya Kenya kuwa na uwiano na ushindani wa kweli (fedha hizo ni 
mjumuisho wa gharama za matangazo ya televisheni na udhamini wa bia ya 
Tusker). 
 Tanzania leo tunajivunia kuwazidi Kenya kutokana na udhamini wa Azam 
ambapo kwa mwaka huu, kila klabu itapata zaidi ya Sh milioni 170 (Jumla 
kutoka milioni 100 za Azam na milioni 70 za Vodacom).  
 Hatuna sababu ya kutaja viwango vya udhamini kwa nchi nyingine jirani 
kama Uganda, Burundi, Rwanda, Zambia nk kwa vile zote zina udhamini wa 
chini kuliko Kenya. SuperSport, ambao wanaliliwa na baadhi yetu, udhamini wao kwa ligi ya 
Uganda ni dola 350,000 ambazo ni pungufu kulinganisha na dola milioni 
moja zilizotolewa na Azam Media hapa nchini.  
 Ni imani yetu kwamba udhamini huu utaifanya ligi ya Tanzania kuwa bora 
kuliko zote za Afrika Mashariki. Hili litasaidia kutengeneza timu bora 
ya Taifa ya Tanzania. Tungependa kutoa ufafanuzi wa masuala machache ambayo yaliongelewa na wenzetu wa Yanga kama sababu za kupinga udhamini huu. 
 BODI YA TPL
Kwa mujibu wa Katiba za FIFA, CAF na TFF, Haki za Televisheni zipo chini ya FA ya nchi husika. TFF iliamua kukasimu shughuli ya majadiliano kwa Kamati ya Ligi ambayo ilishirikisha vilabu vyote 14, ikiwamo Yanga na wawakilishi wake walihudhuria mchakato mzima hadi mwisho.
Kwa mujibu wa Katiba za FIFA, CAF na TFF, Haki za Televisheni zipo chini ya FA ya nchi husika. TFF iliamua kukasimu shughuli ya majadiliano kwa Kamati ya Ligi ambayo ilishirikisha vilabu vyote 14, ikiwamo Yanga na wawakilishi wake walihudhuria mchakato mzima hadi mwisho.
 Hoja ya Yanga kuwa bodi haina nguvu/Mamlaka kisheria kwa kuwa ni ya 
mpito inakosa mashiko kwa sababu kimsingi ni TFF ndiyo iliyoingia 
mkataba kwa sababu ndiyo iliyopewa mrejesho na Kamati ya Ligi kwamba 
mchakato umekwenda sawasawa. 
 Hoya ya kuwa Bodi ya TPL iliyoko sasa hivi haina mjumbe hata mmoja 
aliyeteuliwa kutoka YANGA. Hili si kweli hata kidogo. Mmoja wa wajumbe 
wa TPL ni Seif Ahmed almaarufu Seif Magari; ambaye vyeo vyake ndani ya 
Yanga vinajulikana.  
 Kama alikuwa hahudhurii vikao vya TPL, hilo ni suala la Wanayanga 
wenyewe kumuhoji kwanini alikuwa hahudhurii hivyo na hivyo kuinyima 
klabu yake ushiriki katika mijadala muhimu kwa maslahi ya soka hapa 
nchini. Ifahamike pia kwamba TPL haikuhodhi mchakato huu bali ilitoa fursa kwa 
vilabu vyote vya Ligi Kuu kushiriki ambapo Yanga ilikuwa ikiwakilishwa 
na Makamu Mwenyekiti wake, Clement Sanga na Katibu Mkuu, Lawrance 
Mwalusako.  
 Hii maana yake ni kwamba hoja kuwa Yanga haikushirikishwa ni mfu. Yanga walitumia neno UTARATIBU WA DUNIA NZIMA wakisema eti hakuna 
mahala duniani ambapo kampuni yenye klabu inayocheza ligi husika kupewa 
mkataba wa udhamini au urushwaji wa matangazo. 
 Inaonekana Yanga hawakufanya utafiti kwani ligi ya Afrika ya kusini ina
 timu inayoitwa Super Sports United na inarushwa na kituo cha TV 
chaSupersports. Pia majirani zetu Kenya wana timu inayoitwa Tusker FC huku ligi hiyo ikidhaminiwa na bia ya Tusker.  
 Tunawashauri Yanga kuwa ni vema kufanya utafiti kabla ya kuibuka na hoja za namna hii ili kuepuka kuwapotosha wanachama wao. Yanga pia katika hoja zao wamepinga utaratibu wa kugawana mapato sawa. 
Hoja hii ni ya msingi na majadiliano yetu yalilitazama hili kwa kina 
lakini tukaona kwa mazingira ya Tanzania na uchanga wa ligi yenyewe kwa 
sasa ni heri kugawana sawa ili pesa kwa usawa ili itoke kwa wakati na 
kusaidia vilabu kujiendesha. 
Yanga wanakosea wanaposema eti wao 
wanastahili kupewa zaidi kwa sababu ni klabu kubwa na yenye mashabiki 
wengi kwa kuwa sababu hii haitumiki sehemu yoyote duniani. 
 Tuchukulie mfano wa nchi ya England ambako ingawa Liverpool ina 
washabiki wengi kuliko Manchester City na Chelsea, imezidiwa kwenye 
mapato ya televisheni na timu hizo. 
 Hii ni sababu kinachoamu mapato mwisho wa siku ni kiasi cha mechi za 
timu ambazo zimeonyeshwa na televisheni kwenye msimu husika na nafasi ya
 timu kwenye msimamo wa ligi. 
 Hata hivyo, ikumbukwe kwamba nchini England, malipo haya hufanyika 
baada ya msimu kumalizika na hapo ndipo watu hukaa chini na kupigiana 
hesabu za nini kilipatikana. Sasa ukitumia mfumo huu, ina maada timu 
zitalazimika kusubiri ligi iishe ili kuangalia msimamo ya ligi kisha 
kugawana mapato. Sote tunajua jinsi timu zinavyoteseka kwa kukosa nauli,
 posho, mishahara, pesa za kambi nk.  
 Kwa mazingira yetu ya Tanzania kwa sasa, mfumo kama huu haufai. Hii ni 
kwa sababu timu zinahitaji fedha kuanzia kwenye maandalizi ya mechi ya 
kwanza na hazikopesheki fedha kwenye mabenki. Tanzania inachohitaji kwa sasa ni ligi yenye ushindani tofauti na sasa 
ambapo ushindani uko kwa timu chache zenye uwezo wa kifedha.  
 Tukizijengea uwezo timu zote taifa litakuwa na ligi nzuri na hatimaye 
timu nzuri ya taifa. Pia itawezesha wadhamini wengi zaidi kuingia kwenye
 mpira na hivyo timu nyingi zaidi kufaidika. 
 Tukifikia huko, tunaweza kukaa chini na kutazama mfumo wa kugawana mapato utakaokuwa bora zaidi wakati huo.
 Mambo ya Kuzingatia.Tangu ligi ianze hapa nchini takribani miaka 50 
iliyopita, hakuna timu iliyowahi kulalamikia mfumo wa kugawana mapato 
sawa kwa kila mechi ambao umekuwa ukitumika. Mfano mapato ya mlangoni 
tumekuwa tukigawana sawa na Yanga haijawahi kulalamika, Pesa za udhamini
 wa Vodacom tangia ilipokuwa ikidhaminiwa na TBL hadi leo hii  tumekuwa 
tukigawana sawa na Yanga haijawahi kulalamika kutaka kupata zaidi kwa 
kuwa eti ina mashabiki wengi, pia hata pesa za haki ya matangazo ya 
Televisheni zilizowahi kutolewa huko nyuma nailiyokuwa ikiitwa GTV, na 
Star TV kwa nyakati tofauti pesa ziligawiwa sawa kwa kila timu.
 Hii ni kwa sababu kikanuni, timu zote zinazoshiriki kwenye ligi ni sawa na zote zinaweza kuwa bingwa au kushuka daraja. Ni mdudu gani huyu aliyeingia kwenye soka ya Tanzania na kuanza kuleta 
siasa za kubaguana? Baba wa Taifa alipata kutuasa kwamba dhambi ya 
ubaguzi ni sawa na kula nyama ya mtu. Ikianza, haitaishia kwenye ligi 
pekee na itakwenda hadi mahali tusipotaka. 
 MGOGORO WA MASLAHI. 
 Yanga imekuwa ikilalamikia uwepo wa kiongozi mwandamizi wa makampuni ya
 Bakhresa kwenye bodi ya Ligi na kusema inaleta mgongano wa maslahi.  Sisi vilabu tunaamini kwamba uwepo wa kiongozi huyu ndiyo umesaidia 
makampuni yake kuwekeza fedha kwenye mpira. Na mifano ipo hai tukianzia 
na michuano ya Vijana ya Uhai Cup, ujenzi wa kituo cha michezo cha 
Chamazi ambacho kinatumiwa na timu nyingi za Tanzania.  
 Na sasa tunafaidika na udhamini huu mnono ambao haujapata kutokea katika historia ya Tanzania. Tungependa viongozi wengi zaidi wa makampuni yanayoheshimika hapa 
nchini wakijitokeza kuongoza mpira badala ya kuanza kuwapinga. Kwa mfano tungependa kuona Mkurugenzi wa Benki ya CRDB akiwa kiongozi 
wa Ashanti, bosi wa Barrick akiongoza Mbeya City na Mkurugenzi wa Tanga 
Cement akiongoza Coastal Union.  
 Hivi ndivyo namna mpira unavyoweza kuvutia wawekezaji. Ndiyo maana tulifurahi wakati Yusuf Manji, alipoomba uongozi Yanga. 
 Bado tunataraji kwamba naye atajitosa kuingiza fedha zake kwenye ligi 
ya Tanzania (mpira) kama alivyofanya Bakhresa ambaye pamoja na kutumia 
fedha zake Azam FC, bado ameamua kusaidia na timu nyingine kwa ujumla. Tunapenda kumuahidi Yusuf Manji kwamba iwapo naye atataka kudhamini 
Ligi Kuu iwe kibiashara au kiufadhili, sisi tutamuunga mkono na 
hatutajali suala la mgongano wa maslahi. 
 UPOTEVU WA MAPATO 
Wenzetu Yanga wamedai kwamba kwa kuonyesha mechi kwenye televisheni, mapato yake ya mlangoni yatapungua.
Wenzetu Yanga wamedai kwamba kwa kuonyesha mechi kwenye televisheni, mapato yake ya mlangoni yatapungua.
 Hili pia halikufanyiwa utafiti wa kutosha. Katika siku za karibuni, 
mechi zilizoingiza mapato makubwa zaidi ya milangoni ni zile ambazo 
zilionyeshwa Live kwenye televisheni za ndani na nje ya nchi. Mifano ni mechi za watani wa jadi msimu uliopita zilizoonyeshwa Live na
 SuperSport na mechi za Kombe la Kagame zilizoonyeshwa wakati huo.  
 Hata mechi ya Taifa Stars na Ivory Coast iliyoonyeshwa Live pia, 
ilijaza uwanja. Ulaya ambako karibu kila familia inamiliki televisheni 
na umeme wa uhakika, bado watu wanajaa katika viwanja vya soka. Mpira kuonyeshwa kwenye televisheni unaufanya utangazike zaidi na watu 
watake kuona. Kuna faida nyingi za mpira kuonyeshwa kwenye televisheni 
kuliko hasara moja ya kufikirika ambayo Yanga wanaiona. 
 Ingekuwa vema iwapo Yanga wangetoa takwimu za kuonyesha ni kwa namna 
gani mechi kuonyeshwa kwenye televisheni kuliwahi kupunguza mapato ya 
milangoni. Kwa faida ya umma, mpira kuwa kwenye televisheni kuna faida zifuatazo; 
jezi kuongezeka thamani na hivyo kuvutia makampuni makubwa kutaka 
kudhamini klabu wakitumia fursa ya kutangaza bidhaa zao, matangazo ya 
viwanjani (touchline fence) kuwa na thamani zaidi ambapo kwa sasa vilabu
 havipati chochote, kuchochea michezo ya kubahatisha, kutabiri matokeo 
na kupata habari kupitia simu za mkononi na hivyo vilabu vitaanza 
kutengeneza fedha za kutosha. 
 Ulaya wamesonga mbele kutokana na televisheni. Anayekataa mpira 
kuonyeshwa kwenye televisheni ni sawa na mtu anayegoma kutumia mfumo wa 
digitali katika ulimwengu wa leo.
 UWAZI KWENYE MCHAKATO WA KUUZWA KWA HAKI ZA MATANGAZO
Yanga wameandika kwenye taarifa yao rasmi eti hakukuwa na uwazi kwenye mchakato wa kuipata kampuni ya kurusha matangazo ya Televisheni. Sote tunajua kuwa vituo vya televisheni vilivyopo nchini kama Star TV ambayo iliwahi kurusha mechi kadhaa msimu uliopita vilikuwa vikijua kuwa kuna nafasi hiyo na TFF mara kadhaa wamekuwa wakitangaza hilo kupitia idara ya Habari ya TFF.
Yanga wameandika kwenye taarifa yao rasmi eti hakukuwa na uwazi kwenye mchakato wa kuipata kampuni ya kurusha matangazo ya Televisheni. Sote tunajua kuwa vituo vya televisheni vilivyopo nchini kama Star TV ambayo iliwahi kurusha mechi kadhaa msimu uliopita vilikuwa vikijua kuwa kuna nafasi hiyo na TFF mara kadhaa wamekuwa wakitangaza hilo kupitia idara ya Habari ya TFF.
 TFF kwa mfano walikwenda mbali kwa kuialika Supersports kuja kuonesha 
mechi bure kwa kilichokuwa kikiitwa Super Week ili kuwashawishi waje 
kuwekeza na mara ya mwisho ni Yanga hawa hawa walioongoza harakati za 
kuikataa Supersports kuonesha mechi bure wakisema kuwa kama ni kuwavutia
 inatosha. Katika mazingira kama haya tunastaajabishwa na ukigeugeu wa Yanga leo 
kusema eti tenda haikuwekwa wazi. Sote tunajua kuwa ni Super Sports 
pekee tuliokuwa tukiwategemea na kuwashawishi ambao hawakuonesha 
kuhitaji kuja kuwekeza. Kwa nini leo tuikatae Azam TV?  
 Yanga wanaposema eti TFF/Kamati ya Ligi imeipa haki za matangazo 
kampuni ambayo haina ofisi wala kituo cha televisheni kilicho hewani kwa
 sasa wanasahau kuwa huko nyuma TFF iliwahi kuwapa haki za matangazo GTV
 ambao hawakuwa na ofisi wala kituo cha TV na baada ya miezi michache 
walifungua ofisi zao na kuleta vingamuzi na kuaza kurusha mechi zetu.  
 Vilabu vilifaidi udhamini ule kabla ya ile kampuni kufilisika. Kwa hiyo
 hii si mara ya kwanza kwa jambo hili kufanyika na kama Azam TV 
hawataonesha mechi za ligi hiyo sisi kama vilabu haituhusu kwani ni 
hasara yao.  
  Tunachowaomba Azam Media sisi kama vilabu ni kuhakikisha wanatulipa 
pesa zetu kwa haraka ili zitusaidie kwenye maandalizi,Tunawaomba Yanga 
wasichafue hali ya hewa kwa kuwa wao hawana shida ya Pesa.  
 Sisi Umoja wa Vilabu 13 vinavyoshiriki Ligi Kuu ya Tanzania tunapinga, 
kwa nguvu zote, madai ya Yanga kwamba hatukushirikishwa kama vilabu 
kwenye mchakato huu. Mfumo wa ugawanyaji wa mapato tuliouchagua, tuliuchagua wenyewe bila 
kushurutishwa na yeyote na tunadhani ndiyo mfumo unaotufaa kwa sasa hadi
 hapo ligi yetu itakapokuwa na nguvu maana kwa sasa inaruhusiwa klabu 
kupata fedha mwanzoni kulingana na hali halisi ya vilabu vyetu. 
 Tunawashauri wenzetu wa Yanga waanze kuamini kwenye kitu kinachoitwa 
Uwajibikaji wa Pamoja (Collective Responsibility). Mambo yanayoamuliwa 
kwenye vikao hayapaswi kupingwa nje ya vikao. Kama hoja ililetwa kwenye vikao na ikazidiwa nguvu na hoja nyingine, 
hakuna sababu ya kuikataa kwa sababu tu hukubaliani nayo. Mfumo wa 
kidemokrasia una kanuni moja kuu; Wengi Wape.
 Imetolewa na
Vilabu 13 vya Ligi Kuu ya Tanzania
Vilabu 13 vya Ligi Kuu ya Tanzania
Simba SC, Azam FC, Ashanti United, JKT Ruvu, Ruvu Shooting Stars, Mgambo JKT, JKT Oljoro, Rhino Rangers, Mbeya City, Tanzania Prisons, Mtibwa Sugar, Coastal Union na Kagera Sugar.
Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog