Facebook Comments Box

Wednesday, July 31, 2013

MAMLAKA YA MAWASILIANO TANZANIA (TCRA) IMEZINDUA KAMPENI YA KUHAMASISHA MATUMIZI MAZURI YA MAWASILIANO

Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Profesa John S. Nkomo akizungumza mbele ya Wamiliki wa Blogs mbalimbali Tanzania na Waandishi wa habari katika Warsha ya kampeni ya kuzindua matumizi mazuri ya mitandao ya kijamii kwa ajili ya kuhamasisha maendeleo.

ProfesaNkomo amesema kuwa kwa sasa kumekuwepo na ongezeko kubwa la matumizi ya intanet kwa Watanzania walio wengi toka watumiaji laki tatu miaka mitatu iliyopita hadi watumiaji milioni 7.6 kwa takwimu za hivi karibuni.

Amesema kuwa wengi wa watumiaji wa intanet matumizi yao ni katika kujifunza na kujielimisha pamoja na matumizi ya mitandao ya kijamii kama vile Facebook, Twitter, BBM na Blogs zinazotoa habari mbalimbali kama vile habari za maendeleo, burudani na michezo.

Meneja uhusiano wa Mamlaka ya mawasiliano Tanzania Bw Innocent Mungi akiwakaribisha wadau mbalimbali wa habari na mitandao kuhusiana na uzinduzi wa kampeni hiyo.
Wadau wa mawasiliano ya kijamii, Blogs wakisikiliza hoja mbalimbali zilizokuwa zikitolewa na Mamlaka ya Mawasiliano katika uzinduzi wa matumizi mazuri ya mitandao kwa ajili ya kuhamasisha maendeleo ya Taifa kwa ujumla ambapo Mstari wa pili kulia mtu wa pili nyuma ni Muwakilishi wa kitongoni Blog Bw. Juma Kabange.
Wawakilishi wa TBC Bw. Elisha Elia na Bi. Daula Abdul
John Bukuku kutoka Full Shangwe Blog
Prof. John Nkomo akiwa na Mrisho Mpoto ambae ameimba wimbo maalum wa kampeni hiyo unaoitwa 'Delete Futa Kabisa' ukiashiria kufuta kabisa ujumbe mbaya utakaoupata katika simu yako au kwenye mtandao wako kabla hauja usambaza kwa wengine wengi.











JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEhfKhIZuVa-nyuNh8KCKIUzrysQRxIceLLTs1qM7cj2O5-yWGphgpY2g1BzmFgFW1Cq4Y5O-J1D3xIk0ckg7VcUXIyEUb3S-qKf4YALtgq4O4gFXns4pRd5bLxckQtXczoDRxpotjUu9e8/s1600/TCRA_logo4.jpg

MAMLAKA YA MAWASILIANO TANZANIA
Taarifa kwa VYOMBO VYA HABARI

KAMPENI YA KUHAMASISHA MATUMIZI MAZURI YA MAWASILIANO

Siku za hivi karibuni, ongezeko la huduma za mawasiliano nchini limekuwa kwa kasi sana. Huduma za mawasiliano nchini katika kipindi kifupi zimekuwa sana na kuwafikia Watanzania wengi zaidi. Kutoka laini za simu za mkononi  milioni tatu tu mwaka 2000 hadi kufikia laini 28,000,000.  

Watanzania walio wengi hivi sasa wanafaidika kwa huduma za mawasiliano, yakiwemo mawasiliano ya simu za mikononi, utangazaji. Vile vile huduma za ziada kama kutuma na kupokea fedha kwa kutumia mitandao na simu za mkononi zimeongezeka maradufu. Wananchi wengi wanapata huduma za kibenki kwa kutumia simu zao, wanawasiliana kwa kutumia simu zao kupitia sauti, SMS na kadhalika.

Hali kadhalika kumekuwa na ongezeko la matumizi ya intaneti kwa watanzania walio wengi kutoka watumiaji laki tatu miaka mitatu iliyopita hadi watumiaji milioni 7.6 kwa takwimu za hivi karibuni. Wengi wa watumiaji wa intaneti matumizi yao ni katika kujifunza na kujielimisha pamoja na matumizi ya mitandao ya kijamii kama vile Facebook, Twitter, BBM, LinkedIn na blog mbalimbali zinazotoa habari mbalimbali zikiwemo za kimaendeleo, burudani pamoja na michezo.

Matumizi haya ya intaneti yamewanufaisha watanzaia walio wengi kwani ni fursa murua ya kujifunza kupitia mitandao hiyo ya kijamii kwa kupata habari mpya, kujifunza na kuelimishana kuhusu shughuli za maendeleo na kuleta amani miongoni mwa watanzania.

Hata hivyo pamoja na maendeleo haya, kumekuwepo na baadhi ya watu wachache wanaotumia mawasiliano ya simu, mitandao ya kijamii, redio, TV na mawasiliano mengine kwa lengo la kuvuruga amani, kuchocheo vurugu, kuchonganisha watu, kusababisha ugomvi, kuwaumiza wengine kwa mambo yasiyo na ukweli, kupotosha jamii na hata kuvuruga maendeleo kwa ujumla.

Leo, Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) inazindua kampeni ya kuelimisha umma kuhusu matumizi mazuri ya mawasiliano na inawatahadharisha wananchi kwamba kutumia mawasiliano vibaya kama ilivyoainishwa katika sheria ya Mawasiliano ya Kielectroniki na Posta (EPOCA) ya mwaka 2010 ni makosa. Katika kampeni hii, Mamlaka inakusudia kuwasihi wananchi kuhakikisha wanatumia mawasiliano vizuri ili kudumisha amani, mshikamano na upendo miongoni mwa watanzania.

Katika uzinduzi huu, Mamlaka imewaalika baadhi ya watumiaji mahiri wa mitandao ya kijamii ambao wamekuwa mstari wa mbele kuhakikisha watanzania walio wengi wanafaidika na mawasiliano. Miongoni mwao wako wamiliki wa blog mbalimbali, wasimamizi wa makundi mbalimbali katika mtandao wa FB na mengineyo. Nia ya Mamlaka ni kuomba ushirikiano kwao ili waweze kushiriki katika kampeni hii na kuwahamasisha mashabiki wao kutumia vizuri mitandao ya kijamii ili kunufaisha Taifa letu kwa matumizi mazuri.

Watumiaji wa simu za mkononi na wananchi wote wanashauriwa kuunga mkono juhudi zinazofanyika ili kufanikisha kampeni hii kwa ajili ya kudumisha na kuendeleza amani na usalama na kuharakisha maendeleo ya sekta ya Mawasiliano inaendelea kuchangia uchumi wa Taifa na kuiweka Tanzania katika mazingira mazuri zaidi kijamii, kiuchumi na kisiasa.


Imetolewa na:

 MKURUGENZI MKUU
Mamlaka ya mawasiliano TaNzania

31 Julai 2013












Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU