Facebook Comments Box

Wednesday, July 31, 2013

BAADA YA KUTEMWA NA KLABU YAKE KASEJA AFANYA MAZUNGUMZO NA FC LUPOPO YA DRC

 

Nahodha wa timu ya taifa ya Tanzania, (Taifa Stars), Juma Kaseja Juma maarufu kama (Juma K. Juma) amesema kwamba amefanya mazungumzo na wakala wa klabu ya St. Eloi Lupopo ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), lakini bado hajaingia Mkataba na klabu hiyo ya Lubumbashi.
 
  Kaseja amesema kwamba mtu aliyejitambulisha kwake kama wakala wa Lupopo alimfuata wakafanya mazungumzo na kufikia makubalino juu ya dau la usajili, mshahara na mambo mengine ya msingi.

Hata hivyo, kipa huyo namba moja Tanzania amesema kwamba baada ya mazungumzo hayo na maafikiano, wakala huyo amepeleka majibu Lupopo ambao wakiafiki ndipo masuala ya Mkataba yatafuatia.

“Nimezisikia hizo habari, kwamba mimi tayari ni mchezaji wa Lupopo, hapana, si kweli. Ni kwamba tumefanya mazungumzo tu na wakala wao na tumefikia makubaliano, nasubiri hadi nisaini Mkataba ndipo nitajihesabu tayari ni mchezaji wa Lupopo,”alisema Kaseja.

Pamoja na Simba SC kutomuongezea Mkataba Kaseja, ameendelea kuwa kipa chaguo la kwanza timu ya taifa mbele ya kocha Mdenmark, Kim Poulsen.
 
Iwapo Kaseja atafanikiwa kuingia Mkataba na Lupopo atakwenda kuwa mpinzani mkuu wa wachezaji wenzake wa Taifa Stars, Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu wanaochezea Tout Puissant Mazembe ya Lubumbashi.
 
Kaseja alicheza pamoja na Samatta na kiungo Mganda wa Mazembe, Patrick Ochan katika klabu ya Simba mwaka 2010 kabla ya 2011 wachezaji hao kuuzwa DRC.     
Source:Bin Zubeiry


Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU