![]()  | 
| Bibi. Sarah Hermitage ambaye ni Mwanasheria raia wa Uingereza, mwanaharakati wa kupambana na rushwa na pia mwekezaji katika shamba la Silverdale. | 
Anapatikana @Chomachomp au http://thesilverdalecase.blogspot.com/
KATIKA hali inayoonyesha dharau 
kwa Watanzania na waumini wa Dini ya Kiislamu, Muingereza Sarah 
Hermitage, amefananisha Watanzania na nguruwe ambaye ni mnyama haramu 
kwa mujibu wa imani ya Kiislamu.
Sarah ambaye amekua akiwakashifu 
viongozi na wananchi wa Tanzania mara kwa mara alivuka mipaka na 
kufananisha Watanzania na nguruwe, baada ya kulalamikiwa kwa vitendo 
vyake vya kutoa maneno machafu kwa Watanzania katika mitandao ya 
kijamii.
Kauli hizo za Sarah amekua 
akizitoa kupitia mitandao ya twitter kupitia ukurasa wake 
wa https://twitter.com/Chomachomp kwa muda mrefu sasa bila 
kuchukuliwahatua zozote na viongozi wala watendaji wa serikali ya 
Tanzania.
Kauli ya Sarah kuita Watanzania 
ilianzia pale Mtanzania mmoja ambaye ni mwandishi wa habari mkongwe 
Mbaraka Islam, kulalamikia kitendo chake cha kutukana viongozi na 
Watanzania wote kwa ujumla wao bila kuwa na hoja zinazowahusu.
Huku akijua aliyewasiliana naye 
ni Muislamu, Sarah aliandika katika ukurasa wake kwamba “anga la 
Tanzania limejaa nguruwe wanaopaa, Mbaraka Islam, ni kupe wa mwezi”, 
akimaanisha kwamba Mbaraka Islam ni mmoja wa nguruwe wengi wanaoelea 
katika anga la Tanzania.
“Kwa maana yoyote anayotaka 
kuuaminisha umma na katika mazingira ya Tanzania na Dini yetu, 
haiwezekani kwamba Sarah hakujua kwamba ni kashfa nzito ya Kidini 
kumfananisha Muislamu na nguruwe kwa namna yoyote ile. Alijua mimi ni 
Muislamu alifanya hivyo kusudi.
“Huyu mama (Sarah) amefanya hivyo
 baada ya kuona Watanzania wamelala na hakuna anayethubutu kumgusa hasa 
viongozi wetu anaowatukana anavyotaka bila kuguswa na yeyote,” alisema 
Islam na kuongeza kwamba amechukua hatua kadhaa ambazo hajapenda 
kuziweka hadharani kwa sasa.
Kwa mujibu wa imani ya dini ya 
Kiislamu, mnyama nguruwe ni haramu na najisi na kwamba haruhusiwi kuliwa
 na unapomgusa unapaswa kujitakasa kwa kuoga mara saba moja ikiwa ni kwa
 kutumia mchanga.
Sarah alikerwa na makala aliyoandika Islam katika gazeti la Raia Mwema, ambayo  ilielezea kukerwa na maneno machafu anayoyatoa kwa Watanzania.
Katika makala hiyo, Islam alisema:
KWA takriban miaka mitano sasa, 
raia mmoja wa Uingereza, Sarah Hermitage amekuwa akiendesha kampeni ya 
kumchafua Rais Jakaya Kikwete, Serikali ya Tanzania, taasisi muhimu za 
nchi yetu kama vile mahakama, waandishi wa habari na hata Watanzania 
ambao wamekua wakimpinga.
Pamoja na kuwa kumekua na 
mapungufu katika serikali yake na vyombo vyake kama ilivyo kwa serikali 
nyingine Duniani ikiwamo ya Uingereza, Muingereza huyu amekua akitoa 
kashfa kwa kila jambo linaloandikwa ama kujadiliwa kuhusiana na viongozi
 wa Tanzania na taasisi zake na kwa kutumia lugha isiyo na staha.
Watanzania siku zote wakiwamo 
wanasiasa, waandishi wa habari na wanaharakati, wamekua wakiikosoa na 
hata kuishambulia serikali na vyombo vyake inapokosea jambo ambalo ni 
jema na linasaidia kuimarisha utawala bora, lakini kwa staili anayotumia
 Muingereza huyu ni kupitiliza mipaka na zaidi ya yote ni udhalilishaji 
usioweza kuvumilika kwa mtu mwenye mapenzi mema na nchi yake.
Dhumuni la Sarah Hermitage na 
washirika wake wakiwemo baadhi ya Watanzania ni kuzishawishi nchi za 
Magharibi wakianzia na Uingereza kusitisha misaada na uwekezaji katika 
Tanzania. Hilo angeweza kulifanya huko kwao kwa kuwasiliana na serikali 
yake, lakini badala yake amekuwa akitumia mitandao ya kijamii na barua 
pepe tena kwa kutumia lugha ya kukashifu na kudhalilisha.
Watanzania wote tuna jukumu la 
kutetea heshima ya nchi yetu, lakini wapo wale ambao tumewapa jukumu la 
kusimama mstari wa mbele. Jambo la kusikitisha ni kwamba ni watu 
wachache sana kama Mbunge wa Kigoma Kaskazini Zitto Kabwe ambaye ambaye 
amekua na ujasiri wa kumkabili Muingereza huyu, kwa kumwambia wazi 
kwamba kama ni misaada ana haki ya kuishawishi nchi yake kuzuia misaada 
kwa Tanzania lakini si kwa kudhalilisha Watanzania.
Zitto alienda mbali zaidi kwa 
kusema kwamba nchi nyingi tajiri duniani ikiwamo Uingereza, zimejengwa 
kwa kutumia rasilimali walizozipora katika nchi walizozitawala ikiwamo 
Tanzania na kwamba nchi hizo zinaweza pia kuendesha shughuli zake bila 
misaada ya dharau. Bahati mbaya sana watendaji wengine wengi ambao 
wanapaswa kutetea heshima yetu, hili suala limewapita, pengine kutokana 
na kutokua na taarifa sahihi ama kwa kutowajibika.
Jambo la kujiuliza, wale ambao 
miongoni mwa majukumu yao ya kila siku ni kutetea na kulinda hadhi na 
heshima ya nchi yetu wanafanya kazi gani? Sasa tunawalipa mishahara 
mikubwa na marupurupu ya nini kama hawawezi kututetea tunapodhalilishwa 
ama kutukanwa?
Hali hii inatufanya tukumbuke 
ujasiri wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, ambaye mara kadhaa 
aliwatunishia misuli viongozi wa mataifa makubwa walipotaka 
kuidhalilisha nchi yetu, sembuse raia mmoja ambaye amekua akitumia 
matatizo yake binafsi kutaka kuidhalilisha Tanzania na kutaka 
kuishinikiza serikali yake na nyingine kuichukia Tanzania.
Jinsi anavyotumia mtandao wa twitter kuchafua Tanzania
Sarah Hermitage amekua akitafuta 
katika taarifa za vyombo vya habari vya ndani na nje ya Tanzania 
vinavyoandika taarifa zozote kuhusu Tanzania na kuziongezea maneno ya 
kukashifu na kejeli.
Kwa mfano amekua amechukua 
taarifa inayomunukuu Raia Jakaya Kikwete akiitaka Taasisi ya Kuzuia na 
Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kupambana na rushwa hadi ndani ya Baraza 
la Mawaaziri, na yeye kuongezea maneno akisema, “kundi moja la majambazi
 linaliambia kundi lingine la majambazi kukamata mwizi”.
Akachukua taarifa iliyochapishwa 
katika vyombo vya habari ikimnukuu Waziri Mkuu, Mizengo Pinda 
akikaribisha wawekezaji katika kilimo na yeye kuongeza maneno akisema, 
“Mheshimiwa Pinda kitakachoendelea kukandamizi uwekezaji katika kilimo 
cha Tanzania ni uporaji wa ardhi ya wawekezaji katika mtindo wa Mugabe 
(Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe).”
Amekua akidiriki kukashifu hadi 
majaji wote wa Tanzania kwamba wana bei akisema, “sina hakika kama 
unaweza kupata jaji ambaye si mla rushwa. Wote wana bei,” kauli ambayo 
hata Watanzania wanakua wakiitoa kwa uangalifu maana hata kama kuna 
majaji ambao si waadilifu, haiwezekani wakawa ni wote, kama ilivyo 
katika taasisi nyingine.
Raia mmoja wa Kenya anayeishi Tanzania, aliyejitambulisha kwa jina la Marigi Patrick aliandika katika mtandao kwa kusema;
“Sisi Wakenya tuna matatizo yetu 
na tumekua na tofauti kubwa sana za wazi wazi, lakini anapotokea raia wa
 kigeni kumshambulia kiongozi wetu tena kama Rais wa nchi, tunaungana na
 kumshughulikia. Kuna wakati Wazungu walimshambulia Rais Mwai Kibaki, 
sote tukisaidiwa na wabunge wetu na vyombo vya habari tulimshambulia 
hadi akakoma kutudharau.”
Marigi ambaye anajihusisha na 
biashara ya bima, anasema Watanzania bado ni wachanga katika demokrasia,
 ama wanadharau kila kitu bila kujua madhara yake katika hadhi na 
heshima ya Taifa, na ndio maana wanashindwa kutofautisha kati ya 
demokrasia na udhalilishaji unaofanywa na raia wa nchi nyingine kama 
alivyo Sarah Hermitage.
Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
