KOCHA Msaidizi wa timu ya Simba, Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ amedai 
kuondolewa kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika kulitokana na maandalizi 
hafifu na wachezaji hawapaswi kutupiwa lawama.
 
Mabingwa hao wa Tanzania, walijikuta wakitolewa kwenye michuano hiyo 
na Recreativo de Libolo ya Angola kwa jumla ya mabao 5-0. Awali 
ilifungwa bao 1-0 nyumbani kabla ya kutandikwa 4-0 ugenini.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Julio alisema timu yake 
haikupata maandalizi ya kutosha kwa ajili ya kushiriki michuano ya 
kimataifa, tofauti na wenzao ambao waliipa umuhimu mkubwa michuano hiyo.
Alisema, hali hiyo ndiyo ilisababisha kikosi chake kuondolewa katika 
raundi ya kwanza tu, kitu ambacho ni cha kusikitisha na kutia uchungu 
kwa timu kubwa kama Simba.
Julio aliongeza kuwa kutokana na matokeo hayo, hakuna haja ya 
kuwatupia lawama wachezaji, kwani walijitahidi kutimiza majukumu yao kwa
 kucheza kwa kiwango kinachostahili, lakini walizidiwa na wapinzani wao.
Alisema matokeo yameshakuwa hayo, hivyo kwa sasa hawana budi kuachana 
nayo na kuelekeza nguvu zao Ligi Kuu Bara ili kuweza kujiweka katika 
mazingira mazuri zaidi.
“Tutahakikisha tunafanya maandalizi ya hali ya juu ili tuweze kushinda
 michezo yetu iliyobaki na hivyo kupata nafasi nzuri itakayotuwezesha 
kushiriki michuano ya kimataifa mwakani,” alisema.
Simba kwa sasa inashika nafasi ya tatu ya ligi hiyo ikiwa na pointi  
31 huku Azam FC ikiwa ya pili na pointi 36 na Yanga inayoshikilia 
usukani ina pointi 42.
Katika hatua nyingine, uongozi wa Simba jana ulikuwa na kikao na 
wachezaji kwa ajili ya kujadili mustakabali wa timu yao, ambayo imekuwa 
na mwenendo mbaya katika mechi zake za hivi karibuni, zikiwemo za 
mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Bara.
Habari zilizopatikana jana jioni zinaeleza kwamba, Kamati ya Utendaji 
ya Simba, pamoja na viongozi wa Kamati ya Ufundi, walikutana na 
wachezaji baada ya mazoezi ya jioni na kujadili kiini cha kufanya kwao 
vibaya.
Kiongozi mmoja wa Simba, aliliambia Tanzania Daima kwamba, lengo la 
kikao hicho ni kubaini tatizo ili kulitatua na hatimaye kuondokana na 
mwenendo mbaya.
Hivi karibuni, kumekuwepo na ‘sintofahamu’ ndani ya klabu hiyo, ambapo
 kuna taarifa za mgomo wa chini chini unaofanywa na wachezaji kwa madai 
ya kubaguliwa na baadhi ya viongozi, huku pia wakilalamikia benchi la 
ufundi.