Nairobi.
 Mahakama ya Juu (Supreme Court) ya nchini Kenya imeagiza kuchunguzwa 
kwa fomu 34 za matokeo ya uchaguzi wa rais kutoka katika vituo vyote 
34,400, vilivyotumika kupigia kura katika Uchaguzi Mkuu wa nchi hiyo 
uliofanyika Machi 4, mwaka huu.
Kadhalika
 mahakama hiyo jana iliagiza kuhesabiwa upya kwa kura za urais katika 
vituo vya kupigia kura 22 kati ya elfu 33 vilivyolalamikiwa na aliyekuwa
 mgombea urais wa Muungano wa Cord, Raila Odinga.
Katika
 malalamiko yake yaliyowasilishwa katika mahakama hiyo kupinga Uhuru 
Kenyatta kutangazwa mshindi wa urais katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika 
Machi 4, Odinga alidai kuwa vituo hivyo 22 kura zilizopigwa zinazidi 
idadi ya wapigakura walioandikishwa.
Akisoma
 uamuzi huo kwa niaba ya majaji wenzake watano, Jaji Smokin Wanjala 
alisema kwamba uhesabuji kura wa vituo hivyo utafanyika leo kuanzia saa 
2.00 asubuhi kwa lengo la kubaini ukweli kuhusu madai hayo.
“Matokeo
 ya kura zitakazohesabiwa katika vituo hivyo 22 yawasilishwe katika 
mahakama hii Jumatano, saa 10.00 jioni,” alisema Jaji Wanjala.
Kikao hicho, ambacho Jaji Mkuu wa Tanzania, Mohamed Othman Chande amealikwa kama mwangalizi, ni cha awali kabla ya kesi hiyo kuanza kusikilizwa rasmi keshokutwa (Alhamisi) na kuendelea kwa mfululizo hadi kufikia uamuzi ikiwa madhumuni yake.
Lengo ni kupitia madai yaliyowasilishwa mahakamani hapo na pande zote zinazohusika na kuamua mwenendo wa kesi utakavyofanyika.
Ukiachilia
 mbali kesi iliyofunguliwa na Odinga kupinga Kenyatta kutangazwa mshindi
 wa uchaguzi huo wa tano tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi hapa 
Kenya, kuna kesi nyingine ambayo imefunguliwa na muungano wa mashirika 
yasio ya kiserikali, `The African Centre for Open Governance’ (Africog).
Katika
 kesi hiyo inayorushwa moja kwa moja na vituo kadhaa vya televisheni 
nchini Kenya, Africog inahoji uhalali wa uchaguzi huo.
“Kesi yetu haihusiani na nani ameshinda au kushindwa bali jinsi umma ulivyoshindwa, tumepoteza ahadi ya uchaguzi uliowazi,” alisema Gladwell Otieno, Mkurugenzi Mtendaji wa Africog.
Kesi
 ya tatu ambayo imefunguliwa na wajumbe wa timu ya kampeni ya Kenyatta, 
mwanaharakati katika mitandao ya kijamii Dennis Itumbi na Moses Kuria 
wanaopinga uamuzi wa Tume Huru ya uchaguzi na Mipaka (IEBC) ya 
kujumuisha kura zilizoharibika wakati wa kujumlisha kura za wagombea 
urais.
Katika
 uamuzi wake, mahakama iliamua kwamba kesi zote tatu zitaunganishwa kuwa
 moja, huku ile iliyowasilishwa na Odinga ikiwa ndiyo kinara wa kesi 
zote.
Pia
 mahakama iliamuru Muungano wa Vyama vya Siasa wa Cord na Jubilee kuteua
 mawakala 10 kila mmoja ambao watakula kiapo mahakamani hapo kabla ya 
kuanza kuhesabu upya kura hizo.
Katika
 uamuzi wake jana jioni, mahakama hiyo ilikubali ombi la Mwanasheria 
Mkuu wa Kenya, kushiriki katika kesi hiyo kama rafiki wa mahakama na 
siyo mdaiwa kama ilivyokuwa awali. Wakili wa Cord, George Oraro 
alikubali uamuzi huo licha ya kuupinga awali.
Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog
