Wednesday, July 10, 2013
TAARIFA YA MAAMUZI YA KIKAO CHA KAMATI KUU YA CHADEMA

MUHTASARI
Ili kukabiliana na vitendo vya fujo vinavyofanywa na vijana wa CCM dhidi ya wagombea, Wanachama na viongozi wa CHADEMA, Kamati Kuu imeagiza kwamba kitengo cha ulinzi cha Chama “Red Brigade”kiimarishwe zaidi kwa kuhakikisha kuwa vijana wote wa Red Brigade Nchi nzima wanapewa mafunzo maalum ya UKAKAMAVU yatakayoandaliwa katika Makambi maalum katika mikoa yote.
RIPOTI KAMILI
TAARIFA
 KWA UMMA KUHUSU MAAMUZI YA KIKAO CHA KAMATI KUU YA CHAMA KILICHOFANYIKA
 TAREHE 06-07/07/2013 KATIKA HOTEL YA BLUE PEARL, DAR ES SALAAM.
Kamati
 kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo ilikutana katika Kikao cha 
dharura kuanzia tarehe 06-07/07/2013 katika Hotel ya Blue Pearl Dar es 
salaam kujadili pamoja na mambo mengine Rasimu ya Katiba mpya na hali ya
 Siasa nchini.
Kamati kuu imejadili na kuyatolea maamuzi mambo mbalimbali kama ifuatavyo:
1:0. Hali ya Siasa Nchini.
Kamati kuu imepokea taarifa ya hali ya siasa nchini na kuzingatia mambo yafuatayo:
a) Shambulio la Bomu Arusha.
 Kamati Kuu imesikitishwa na kulaani kwa nguvu zote tukio la Bomu Arusha
 lililosababisha watu wanne kuuwawa na zaidi ya watu 70 wengine 
kujeruhiwa vibaya.
 Kamati Kuu imeridhika kwamba shambulio hilo 
lililenga kuwaua viongozi wakuu wa CHADEMA akiwamo Mwenyekiti wa Taifa 
Mheshimiwa Freeman A. Mbowe na Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini na Mjumbe
 wa Kamati Kuu, Mheshimiwa Godbless J. Lema na viongozi na wanachama 
wengine wa CHADEMA waliohudhuria Mkutano wa kufunga kampeni za udiwani 
katika Jiji la Arusha pamoja na kuvuruga Uchaguzi huo na kuinyima 
CHADEMA ushindi mkubwa;
 Kamati Kuu imeridhika kwamba ushahidi 
uliopo wa vielelezo na wa mashuhuda wa shambulio unaonyesha ushiriki wa 
moja kwa moja wa Jeshi la Polisi katika shambulio hilo;
 Kamati 
Kuu imefadhaishwa na kauli ya Serikali bungeni iliyolenga kulikosha 
Jeshi la Polisi kwa kuhusika kwake na shambulio hilo dhidi ya CHADEMA na
 wananchi wa Jiji la Arusha na kuilaumu CHADEMA wakati CHADEMA ndio 
mhanga wa shambulio hilo;
 Kamati Kuu imeshangazwa na kitendo 
cha Serikali kupuuza maafa yaliyowafika wananchi wa Arusha kwa kushindwa
 kushiriki katika mazishi ya wahanga wa mauaji ya Soweto na 
kuwashambulia kwa mabomu ya machozi, vipigo na maji ya sumu waombolezaji
 waliokusanyika kuwaaga marehemu waliouawa kwenye shambulio;
 Kamati Kuu imesikitishwa na Rais Kikwete kuendelea kukaa kimya juu ya 
shambulio la Arusha na kushindwa kwake kuunda Tume huru ya Kimahakama 
kuchunguza kwa uwazi shambulio hilo. Aidha, Kamati Kuu inaamini kwamba 
ukimya huu wa Rais Kikwete na kushindwa kwake hata kuwatembelea wafiwa 
na wahanga wengine wa shambulio hilo ni ushahidi mwingine wa kuhusika 
kwa vyombo vya ulinzi na usalama vya Serikali katika kupanga na 
kutekeleza shambulio la Arusha;
 Kamati Kuu imefadhaishwa na 
kitendo cha Bunge la Jamhuri ya Muungano kuendelea na vikao vya Bunge 
kama kawaida; kukataa kutoa mchango wowote kwa wahanga na kushindwa 
kupeleka ujumbe wa Bunge kuwatembelea na kuwafariji wahanga na 
waathirika wa shambulio kinyume na utaratibu uliozoeleka wa Bunge 
kutambua na kushiriki katika majanga na misiba ya aina hii.
Kamati
 Kuu inautaka uongozi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano uwaeleze 
Watanzania kama maafa ya shambulio la Arusha yalikuwa na tofauti yoyote 
na maafa ya shambulio la bomu la Olasiti, au na maafa ya mabomu ya Gongo
 la Mboto, ajali ya MV Skargit au maafa mengine yaliyosababisha Bunge la
 Jamhuri kuahirisha shughuli zake, kutoa michango kwa waathirika pamoja 
na kupeleka ujumbe wa Bunge kuwafariji wafiwa na wahanga wa matukio 
hayo;
Kutokana na maelezo hayo hapo juu Kamati kuu imeazimia kuwa:
•
 Iwapo Rais ataendeleza msimamo wa kutokuunda tume huru ya kimahakama, 
Ushahidi uliopo juu ya tukio la kurushwa Bomu Arusha utawekwa wazi muda 
utakapofika kwa wananchi wa Tanzania; vyama na mashirika ya kiraia ya 
haki za binadamu hapa nchini na ya nje ya nchi; ofisi za kibalozi za 
mataifa rafiki na Tanzania pamoja na jumuiya ya kimataifa ili 
yaishinikize Serikali kuunda Tume huru ya Kimahakama kuchunguza 
shambulio hilo na matukio mengine ya mauaji yenye sura ya kisiasa ambayo
 yamehusishwa na Jeshi la Polisi na vyombo vingine vya usalama vya 
Serikali au vya Chama cha Mapinduzi;
2:0. Hali ya Wananchi wa Mtwara.
Kamati
 kuu imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa juu ya unyanyasaji, 
utesaji, ubakaji na uonevu wanaofanyiwa wananchi wa Mtwara hivi sasa na 
vyombo vya dola huku serikali ikikaa kimya juu ya jambo hili bila 
kukemea. Kamati kuu imejadili kwa kina namna wananchi wa Mtwara 
wanavyofanyiwa na vyombo vya dola na kufikia maazimio yafuatayo;
 Vyombo vya dola vitimize wajibu wake wa kulinda amani na mali ya raia 
na siyo kuwatesa na kuwapiga wananchi kwa kuwasababishia vifo kinyume na
 Haki za Binadamu.
 Serikali iwasikilize wananchi wa Mtwara na 
siyo kutumia ubabe, unyanyasaji, uonevu na mateso kama mbinu za 
kuhalalisha kukubalika kwake kwa wananchi.
 Rais Kikwete 
alitangazie taifa “hali ya hatari” kwa mkoa wa Mtwara kama anaona kuwa 
Mtwara ni hatari kwa kiasi hicho cha kulitumia JWTZ kuzunguka mitaani na
 silaha za kijeshi ili taifa liweze kujua,Aidha kama jeshi la polisi 
limeshindwa kutimiza majukumu yake kwa mujibu wa sheria atangaze 
kulivunja jeshi hilo mara moja.
 Serikali iunde tume huru ya 
kuchunguza matukio ya mauaji,ubakaji,utesaji na ukiukwaji wa haki za 
binadamu yaliyofanywa na vyombo vya dola na waathirika wote waweze 
kufidiwa kwa mujibu wa sheria.
3:0. Kauli ya Waziri Mkuu.
Kamati
 Kuu imejadili kwa kina kauli ya Waziri Mkuu Bungeni kwamba ni sahihi 
kwa Jeshi la Polisi nchini kuwapiga Wananchi wote wanaotumia haki zao za
 Kikatiba kupinga sera au maamuzi ya Serikali. Kamati Kuu imeazimia 
kuwa:
 Kauli ya Waziri Mkuu imekiuka Katiba na sheria za nchi 
yetu zinazokataza Jeshi la Polisi kutumia nguvu dhidi ya raia wasiokuwa 
na silaha na ambao wanatumia haki zao za kikatiba kufanya maandamano;
 Kamati Kuu inaamini kwamba kauli ya Waziri Mkuu inatoa Baraka kwa Jeshi
 la Polisi kuendeleza vitendo vya ukatili na mauaji dhidi ya wananchi 
ambayo yamelifanya Jeshi la Polisi la Tanzania kutangazwa kuwa moja ya 
majeshi katili ya polisi katika Afrika Mashariki;
 Kamati Kuu 
inaungana na wananchi, taasisi na mashirika ya kitaifa na kimataifa 
ambayo yamelaani vikali kauli hiyo ya Waziri Mkuu na inawataka wananchi,
 taasisi na mashirika hayo kuendelea kumlaani vikali Waziri Mkuu kwa 
kauli hiyo;
 Kamati Kuu inaamini kwamba Waziri Mkuu amepoteza 
sifa za kuendelea kuwa Waziri Mkuu na inaungana na wananchi na taasisi 
ambazo zimedai Waziri Mkuu awajibike au awajibishwe kutokana na kauli 
yake hiyo. Aidha, Kamati Kuu inawaelekeza Wabunge wote wa CHADEMA 
washirikiane na Wabunge wengine wote wenye mapenzi mema na nchi hii na 
ambao wanaamini katika utawala wa sheria waanzishe mchakato wa kumpigia 
kura ya kutokuwa na Imani Waziri Mkuu kupitia Bunge;
 Kamati Kuu
 imewataka Jeshi la Polisi kama sehemu ya jamii ya watanzania kupuuza 
kauli ya Waziri Mkuu katika utekelezaji wa kazi zao kwa kuwa kauli hiyo 
ni ya uvunjifu wa Katiba na Sheria na inachochea uvunjifu wa amani.
4:0. Uchaguzi wa Madiwani.
Kamati Kuu imepokea taarifa kuhusu ushiriki wa CHADEMA katika Uchaguzi wa Madiwani uliofanyika tarehe 16/06/2013 katika kata 22.
 Kamati Kuu imeipongeza Sekretarieti na uongozi wa Kanda mbalimbali za 
CHADEMA kwa maandalizi mazuri katika Uchagzuzi huo uliosababisha CHADEMA
 kuwapokonya CCM ushindi katika kata 4 ilizokuwa imeshinda katika 
Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010. Kamati Kuu imewapongeza wananchi kwa 
kuipatia CHADEMA kura asilimia (47.7%) dhidi ya CCM (49%) na (3.3%) za 
CUF.
 Kamati kuu imesikitishwa na vitendo vya fujo 
walivyofanyiwa viongozi, wagombea pamoja na Wanachama mbalimbali katika 
sehemu mbalimbali palipo fanyika Uchaguzi. Kamati Kuu imesikitshwa na 
kulaani vitendo hivyo vikiwemo vya watu kukatwa mapanga , kuchomwa visu 
na kubakwa kwa akina Mama na vijana wahuni walioandaliwa na Chama cha 
Mapinduzi.
 Kamati Kuu imelaani vitendo hivyo vya kinyama vilivyofanywa mbele ya jeshi la polisi na Wakuu wa Wilaya.
 Ili kukabiliana na vitendo vya fujo vinavyofanywa na vijana wa CCM 
dhidi ya wagombea, Wanachama na viongozi wa CHADEMA, Kamati Kuu imeagiza
 kwamba kitengo cha ulinzi cha Chama “Red Brigade” kiimarishwe zaidi kwa
 kuhakikisha kuwa vijana wote wa Red Brigade Nchi nzima wanapewa mafunzo
 maalum ya UKAKAMAVU yatakayoandaliwa katika Makambi maalum katika mikoa
 yote.
 Kamati Kuu imejadili maandalizi ya Uchaguzi wa madiwani 
katika kata nne (4) katika Jiji la Arusha. Kamati Kuu imepokea kwa 
masikitiko taarifa juu mipango inayofanywa na jeshi la polisi kwa 
kushirikiana na Mkuu wa Mkoa wa Arusha Magesa Mulongo na viongozi 
wengine wa CCM mkoani Arusha katika kuhujumu zoezi la Uchaguzi kwa 
kuwatisha wapiga kura kwa kutumia polisi na vijana wa Green Guard siku 
ya uchaguzi.
 Kamati Kuu inamtaka Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) 
kuchukua hatua stahiki kuzuia harakati za polisi na CCM za kuvuruga 
Uchaguzi na kutaka kujipatia ushindi kwa njia za hila. Aidha Kamati kuu 
imelitaka jeshi la polisi kuheshimu maadili ya uchaguzi yaliyosainiwa na
 Serikali, Tume ya uchaguzi na vyama vya siasa.
 Kamati Kuu 
imesikitishwa na Tume ya Uchaguzi kushindwa kuwazuia CCM kuendelea na 
kampeni za Uchaguzi huku wakiwa wamezuia kampeni hizo kwa vyama vingine.
 Kamati Kuu imeendelea kuwapa pole wananchi wa Arusha kwa matukio mabaya
 wanaofanyiwa na serikali ya CCM mkoani humo, na imewapongeza kwa 
kusimama kidete katika kulinda haki na ukweli.
 Kamati Kuu 
imewaomba wananchi wa Arusha wajitokeze kwa wingi siku ya kupiga kura 
tarehe 14 Julai 2013, na imewataka wabunge wote washiriki katika 
kusimamia zoezi la upigaji kura na uhesabuji kura siku ya Uchaguzi na 
wananchi wajitokeze kwa wingi kulinda kura bila hofu.
5:0. Rasimu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Kamati
 Kuu imejadili kwa kina sana maudhui yaliyomo katika Rasimu ya Katiba ya
 Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya 
Katiba;
• Kamati Kuu imetambua kazi kubwa iliyofanywa na Tume ya 
Mabadiliko ya Katiba katika kukusanya na kuchambua maoni ya wananchi na 
kuandaa Rasimu ya Katiba Mpya;
• Hata hivyo, Kamati Kuu imetambua
 na kuainisha mapendekezo mengine ya msingi ambayo yanastahili 
kuboreshwa zaidi katika Rasimu hiyo;
• Msimamo na maazimio ya 
Kamati Kuu juu ya Rasimu ya Katiba Mpya yameainishwa na kuchapishwa 
katika kijitabu maalumu ambacho kitazinduliwa katika Mkutano wa hadhara 
utakaofanyika siku, tarehe na mahali patakapo tangazwa hapo baadaye.
Imetolewa na:
……………………….
Freeman A. Mbowe, (MP)
Mwenyekiti Taifa
Subscribe to:
Comments (Atom)