Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi CUF Maalim Seif Sharif Hamad ameelezea
 kuchukizwa kwake na vitendo vya vurugu na uvunjifu wa amani 
vilivyotokea hivi karibuni visiwani Zanzibar.
Amesema
 vitendo hivyo vimeigharimu Zanzibar katika Nyanja mbali mbali zikiwemo 
za kiuchumi, kisiasa na kijamii, sambamba na kuitia doa katika jamii ya 
kimataifa.
Akihutubia mkutano wa 
hadhara wa chama hicho katika viwanja vya demokrasia Kibandamaiti mjini 
Zanzibar, Maalim Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar
 amevilaumu vyombo vya dola kwa kutochukuwa hatua zinazostahiki katika 
kudhibiti vitendo hivyo.
Amesema hatua 
zilizochukuliwa katika kurejesha amani baada ya kutokea kwa vurugu hizo 
hazikuwa muafaka, kwani zimekuwa zikiwadhalilisha na kuwanyanyasa 
wananchi wasiokuwa na hatia pamoja na kuhujumu mali zao.
Amesema
 yeye binafsi amechukizwa na kitendo cha kuuliwa kwa askari polisi 
katika eneo la Bububu, Koplo Said Abrahmani lakini bado serikali na 
vyombo vya dola vina jukumu la kulinda haki za raia kwa kuwasaka 
wanaohusika na tukio hilo, na sio kuwanyanyasa raia wasiokuwa na hatia.
“Nazungumza
 haya kwa unyonge sana leo, sikufikiria kuwa vitendo hivi vingetokea 
Zanzibar katika wakati huu tunaotekeleza maridhiano ndani ya serikali ya
 umoja wa kitaifa”, alieleza Maalim Seif na kuongeza: “Sipendi kuisema 
serikali yangu na Rais wangu hadharani, lakini inanibidi niseme ‘Rais 
wangu Dkt Shein unatuangusha’ kwa kuwa wewe ndiye mwenye jukumu kubwa 
zaidi la kulinda amani ya nchi hii” alieleza.
Ametahadharisha
 kuwa huenda vitendo hivyo vimepangwa kuvuruga umoja wa Wazanzibari 
ambao umeiletea sifa kubwa Zanzibar, na kuwataka wananchi kutokubali 
kuingizwa katika mtego utakaopelekea kuvunjika kwa umoja na mshikamano 
uliopo miongoni mwa wananchi.
Katibu 
Mkuu huyo wa CUF alienda mbali zaidi kwa kudai kuwa vikundi 
vinavyolalamikiwa kufanya vurugu vikiwemo vya ‘Ubaya ubaya, Mbwa mwitu 
na Janjawid vilikuwepo kabla ya tukio hilo na kwamba vimetokana na kundi
 kubwa la vijana la JANJAWID lililoahidiwa kupewa ajira na Serikali.
Katika
 hatua nyengine Maalim Seif ameitaka Tume ya mabadiliko ya katiba 
kufanya kazi kwa uadilifu na kuheshimu mawazo ya wananchi wanayoyatoa 
bila ya kuonyesha upendeleo kwa baadhi ya watu au makundi fulani.
“Tume
 hii inaonekana kuanza kuwa na ‘bias’ kwa baadhi ya watu na makundi 
fulani, lakini tunamwambia Jaji Warioba tume yake iheshimu mawazo ya 
wananchi”, alitanabahisha.
Katika 
risala ya wanachama wa chama hicho kwa wilaya sita za Unguja iliyosomwa 
na Katibu Mtendaji wa vijana CUF taifa Khalifa Abdallah walitahadharisha
 juu ya uwezekano wa kuwepo kwa ajenda ya siri ya kuvuruga Serikali ya 
Umoja wa Kitaifa. 
Amesisitiza kuwa 
Serikali ya Umoja wa Kitaifa bado inahitajika katika kupata ukombozi wa 
kweli wa Zanzibar, sambamba na kuendeleza umoja na mshikamano wa 
Wazanzibari.
Naye Kaimu wa Kaimu Naibu 
Katibu Mkuu wa CUF Bw. Salim Bimani amewasisitiza wananchi kuendelea 
kujitokeza kwa wingi kutoa maoni yao juu ya mabadiliko ya katiba, na 
kuiomba Tume inayohusika na ukusanyaji wa maoni kuwapa fursa wananchi 
kutoa maoni yao kwa uwazi.
“Wananchi msikubali kuchokozeka, nendeni mkatoe maoni kwani hii ni fursa pekee ya kupata katiba tuitakayo” alisisitiza Bimani.