Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya 
Mrisho Kikwete leo, aliungana na mamia ya 
waombolezaji kumzika Mbunge wa Jimbo la Nyasa na msanii mahiri wa muziki
 nchini, Mheshimiwa Kepteni John Damiano Komba, kwenye makaburi ya 
Kanisa Katoliki katika Kijiji cha Lituhi, Wilaya ya Nyasa, Mkoa wa 
Ruvuma. 
Mara baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa 
Ndege wa Songea, akitokea Dar es Salaam, kiasi cha saa tano na robo 
asubuhi, Rais Kikwete alikwenda moja kwa moja Lituhi, karibu kiasi cha 
kilomita 140 kutoka mjini Songea, kwa ajili ya mazishi ya Mheshimiwa 
Komba ambaye pia alikuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya 
Chama cha Mapinduzi (CCM). 
Rais Kikwete alijiunga 
na waombolezaji akiwemo Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa 
Tanzania, Mheshimiwa Anne Semamba Makinda kiasi cha saa tisa mchana kwa 
ajili ya mazishi hayo. 
 
Shughuli za mazishi za kidini ziliongozwa na Askofu John Ndimbo wa 
Jimbo Katoliki Mbinga.
Mwili wa 
Marehemu Komba uliteremshwa kaburini saa 9:30 mchana huku ukishuhudiwa 
na mjane wa marehemu Salome Komba na watoto wake 11. 
Rais
 Kikwete ameondoka Lituhi mara baada ya mazishi kurejea mjini Songea 
kumalizia ziara yake ya siku mbili ya kikazi mkoani Ruvuma.