Kamanda
 wa Polisi Mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) 
Liberatus Sabas akiwaonyesha waandishi wa habari bunduki aina ya SMG 
iliyokamatwa wilayani Ngorongoro hivi karibuni huku mkono wake wa kulia 
akiwa ameshika kifurushi chenye madawa ya kulevya aina ya Heroin 
yaliyokamatwa jana wilayani Arumeru. (Picha na Rashid Nchimbi wa Jeshi 
la Polisi Arusha) 
 
Na Rashid Nchimbi wa Jeshi la Polisi Arusha
 
Kuelekea
 katika kusherehekea Sikukuu ya Krimas, Jeshi la Polisi Mkoani hapa 
limeendelea kupambana na wahalifu wa madawa ya kulevya ambapo safari hii
 limefanikiwa kuwakamata watu wanne wakiwa na madawa ya kulevya aina ya 
Heroin. Tukio hilo limetokea jana tarehe 23.12.2014 muda wa saa 12:30 
jioni maeneo ya Elikyurei wilayani Arumeru.
 
Akizungumza
 na waandishi wa habari ofisini kwake, Kamanda wa Polisi wa Mkoani hapa 
Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Liberatus Sabas amesema 
kwamba tukio hilo limefanikiwa baada ya kupata taarifa toka kwa raia 
wema ambapo askari wa Jeshi hilo walikwenda katika eneo husika na 
kuwakuta watuhumiwa hao wakiwa ndani ya chumba cha mtuhumiwa mmojawapo 
huku wakiwa wanaendelea kufunga kete za madawa hayo na tayari walikuwa 
wamefunga kete 25.
 
Kamanda
 Sabas aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Seifu Bakari (28) na Hamid 
Makame wote ni wakazi wa Elikyurei wilayani Arumeru pamoja na wenzao 
ambao ni Evance Gidion (29) Mkazi wa Ngarenaro na Abraham Hamis (23) 
Mkazi wa Kaloleni jijini hapa.
 
Kamanda
 Sabas alisema kwamba madawa hayo yenye uzito wa gramu 100 yanakadiriwa 
kuwa na thamani ya Tsh 10 Mil. Mpaka hivi Jeshi hilo linaendelea 
kuwahoji watuhumiwa hao ili kufahamu undani zaidi na watafikishwa 
mahakamani pindi upelelezi utakapokamilika.
 
Kufuatia
 tukio hilo na mengine ya nyuma Kamanda Sabas alizidi kuwashukuru 
wananchi wa Mkoa huu kwa jinsi wanavyoonyesha ushirikiano kwa jeshi hilo
 juu ya kufichua vitendo vya uhalifu na wahalifu na kuahidi kuendeleza 
falsafa ya Polisi Jamii ambayo inaleta mafanikio makubwa katika suala 
zima la kuimarisha amani na utulivu Mkoani hapa.