
KIKOSI 
cha timu ya Young Africans kitashuka dimba la Uwanja wa Taifa siku ya 
jumapili kupambana na Wajelajela, Timu ya Jeshi la Magereza,Tanzania 
Prisons kutoka jijini Mbeya ikiwa ni mchezo wa pili wa mzunguko wa 
kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania bara msimu wa 2014/2015.
Akiongea 
na tovuti rasmi ya klabu leo mara baada ya mazoezi, kocha mkuu wa Young 
Africans Mbrazil Marcio Maximo amesema vijana wake wako fiti kuelekea 
mchezo huo wa siku ya jumapili huku wakiwa wamejipanga kuhakikisha 
wanaondoka na pointi tatu muhimu.
        
Maximo 
amesema baada ya kupoteza mchezo wa awali dhidi ya wakata miwa wa Mtibwa
 Sugar, kikosi chake kimekua kikiendelea na mazoezi kila siku katika 
uwanja wa shule ya sekondari Loyola huku wakiyafanyia marekebisho makosa
 yaliyojitokeza katika mchezo huo wa awali.
Kuhusu 
timu ya Tanzania Prisons, Mbrazil Maximo amesema anatambua walishinda 
mchezo wa awali dhidi ya Ruvu Shooting hivyo wana morali bado ya 
kuendeleza ushindi siku ya jumapili, lakini pia kikosi chake kipo fiti 
kusaka pointi tatu muhimu.
Aidha 
Maximo amesema habari njema kwa wana Yanga ni kurejea dimbani kwa kiungo
 Andrey Coutinho pamoja na mshambuliaji Jerson Tegete ambao wanatarajiwa
 kuonekana kwenye mchezo huo na kuhakikisha wanaisaidia timu yao kupata 
ushindi.
Wachezaji
 watakaoukosa mchezo wa siku ya jumapili ni Oscar Joshua na Hussein Javu
 ambao wote ni majeruhi, wakisumbuliwa na maumivu ya nyama za paja, na 
jumatatu wanatarajiwa kuanza mazoezi mepesi baada ya kuwa kwenye 
matibabu chini ya usimamizi wa daktari wa timu Dr Suphian Juma.
Marcio 
Maximo amewaomba wapenzi, washabiki, wanachama na wadau wa soka kwa 
ujumla kujitokeza kwa wingi siku ya jumapili katika mechi dhidi ya 
Prisons kuja kuwapa sapoti vijana na kuwashangilia muda wote wa mchezo.
Chanzo:shaffihdauda
Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog