
Mtoto 
Kudra aliyekuwa ameunganika na kiwiliwili cha pacha mwenza, anaendelea 
vizuri na matibabu katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH).
Mtoto 
huyo alifanyiwa upasuaji Alhamisi iliyopita katika Taasisi ya Mifupa ya 
Muhimbili (Moi) na kulazwa katika wodi ya wagonjwa wanaohitaji uangalizi
 maalumu (ICU), lakini mwishoni mwa wiki iliyopita alitolewa katika wodi
 hiyo.
Mama 
mzazi wa mtoto huyo, Pili Hija, alisema hivi sasa Kudra ananyonya vizuri
 na kwamba amekuwa akitaka kufanya hivyo kila wakati .
"Kwa 
kweli kudra za Mwenyezi Mungu ndizo zimemweka hai mpaka leo hii, 
nilikuwa nimeshakata tamaa kuwa nampoteza mwanangu, nazidi kumuomba 
Mungu amwekee mkono wake apone kabisa," alisema Hija.
Daktari 
Bingwa wa Upasuaji wa Watoto katika Hospitali ya Muhimbili, Dk Zaitun 
Bokhary, alisema mtoto huyo anaendelea vizuri na mwishoni mwa mwezi huu 
atafanyiwa upasuaji mwingine.
"Tunamwacha
 achangamke kwanza, mwishoni mwa mwezi huu tutamfanyia upasuaji mwingine
 wa kumwekea njia ya muda ya kutolewa haja kubwa, kwa kumpasua ubavuni 
baada ya hapo ataruhusiwa kwenda nyumbani," alisema Dk Bokhary.
Kudra 
alipewa jina hilo Alhamisi usiku, saa kadhaa baada ya upasuaji kufanyika
 chini ya jopo la madaktari saba, walioongozwa na Dk Hamis Shaaban, 
mtaalamu wa Ubongo na Uti wa Mgongo kutoka Moi.
Alizaliwa
 Agosti 18, baada ya mwanamke huyo kujifungulia nyumbani watoto pacha, 
huku mmoja akiwa hajakamilika viungo vyote. Pia, kiwiliwili 
kilichoungana hakikuwa na kichwa, macho, maini, figo ila alikuwa na 
mshipa mmoja wa fahamu ambao ulikuwa umeshikana na mwenzake na 
kulazimisha madaktari hao kumfanyia upasuaji.
 
CHANZO:MWANANCHI
Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog