Wajumbe wa Mabaraza ya Katiba Halmashauri ya Wilaya ya 
Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba, wametoa mapendekezo ya pamoja 
wakitaka mambo matano yaondolewe kwenye Muungano, yabaki kwenye Serikali
 washirika.
                
              
Waliyopendekeza yaondolewe ni Mambo ya Nje, Uraia 
na Uhamiaji, Sarafu na Benki kuu, usajili wa vyama vya siasa pamoja na 
ushuru wa bidhaa wakisema kwamba kama yataendelea kuwepo kwenye Muungano
 kama ilivyopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba yatasababisha 
Serikali shirikishi kuwa dhaifu.Wakizungumza baada ya kuwasilishwa kwa 
kazi za makundi yaliyopewa jukumu la kujadili suala la mihimili, wajumbe
 hao walisema mambo hayo matano ndiyo yanayoweza kuzipa nguvu Serikali 
shirikishi ambazo zitakuwa Tanganyika na Zanzibar.
Walitolea mfano wa mambo ya nje na kusema kuwa 
ikiwa Rais wa Serikali ya Tanganyika au Zanzibar ataondolewa jukumu la 
kuteua mabalozi na hata kuiwakilisha nchi nje ya nchi atakuwa 
ameondolewa meno. “Nchi washirika ziachiwe masuala ya mambo ya 
nje,”alisema Kassim Mohamed Kassi, mkazi wa Chimba akiwakilisha vijana.
Kuhusu Sarafu na Benki Kuu, walisema sababu za 
kupendekeza iondolewe katika muungano ni kuwa itadhoofisha uchumi wa 
nchi washirika.
Aidha kwa upande wa uraia na uhamiaji, 
walisisitiza kuwa kila nchi watu wake wana utamaduni usioingiliana na 
nchi nyingine washirika, hivyo kila upande uwe huru.
Ushuru wa bidhaa, wajumbe hao walipendekeza ubaki 
kwenye nchi washirika na siyo Muungano kama inavyopendekezwa kwa sababu 
ikiwa itaachwa hivyo sehemu kubwa ya kodi na ushuru kutoka nchi 
washirika zitashindwa kuwanufaisha watu wake.
Kuhusu usajili wa vyama vya kisiasa, wajumbe hao 
walisema hiyo ni moja ya kero za muungano iliyojitokeza baada ya kuingia
 kwa mfumo wa vyama vingi. Sheria ya chama ili kisajiliwe sharti kipate 
wanachama wa mikoa ya Tanzania bara na Zanzibar. Walitaka mambo ya 
muungano yabaki mawili tu ambayo ni Katiba na mamlaka ya Jamhuri ya 
Muungano wa Tanzania pamoja na Ulinzi na Usalama wa Jamhuri ya Muungano.
SOURSE:MWANANCHI
Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog