Hatimaye
 Barack Obama, Rais wa Marekani anatembelea tena bara la Afrika. Hii 
itakuwa ni mara ya pili Obama kutembelea Bara hili alikotoka baba yake 
baada ya ziara yake ya kwanza mwaka 2009. Mwaka huo alitembelea Ghana na
 Misri ilhali mwaka huu anatembelea Senegali, Afrika Kusini na Tanzania.
 Ziara hiyo itakayoanza tarehe 26 mwezi Juni, itamfikisha Tanzania 
tarehe 1 Julai na kuondoka siku ya pili yake.
 
 Uchaguzi wa Obama
 kuwa Rais wa Marekani ulipokolewa kwa shangwe Afrika nzima. Wakati 
Waziri wa mambo ya nje wa Nigeria alilia kwa furaha, nchi ya Kenya 
ilitangaza siku ya mapumziko na Rais wa zamani wa Afrika Kusini ndugu 
Nelson ‘Madiba’ Mandela alisema ‘ushindi wa Obama unawafanya Waafrika 
wathubutu kuota ndoto (Jarida la The Economist). Hapa Tanzania kulikuwa 
kuna shamra shamra za kila namna na magazeti yaliweka vichwa vya habari 
kana kwamba ni Rais wa Tanzania aliyechaguliwa. 
 
 Waafrika walikuwa na matumaini makubwa sana na bwana Obama. Yamefikiwa?
 Ni vema ifahamike kuwa Barack Obama ni Rais wa Marekani na siku zote 
atalinda maslahi ya Marekani tu. Kuwa na matumaini makubwa kwamba labda 
yeye angeliweza kuiweka Afrika mbele sana ilikuwa ni kujifurahisha tu 
nafsi. Maslahi ya Marekani ni ya kipaumbele kuliko kitu kingine chochote
 kwa Rais Obama. Kwa wengi Obama amekuwa kama amewavunja moyo.
 
 
Tanzania inapokea kiongozi wa Taifa kubwa duniani wa pili sasa ndani ya 
kipindi cha miezi 3 tu. Kwanza alikuja Rais wa China na sasa wiki hii 
anakuja Rais wa Marekani. Maneno ya mtaani na kwenye mabaraza ya 
majadiliano ni kwamba viongozi hawa wanakuja kugombea maliasili tulizo 
nazo kama gesi asilia na madini. Nadhani haya ni maneno ya kusema katika
 kupiga soga maana kunyonywa kwa rasilimali hakuhitaji Rais wa Marekani 
aje Tanzania. Makampuni yote makubwa yanayochimba dhahabu hapa nchini ni
 makampuni ya nje na marais wao hawakuja ili waweze kupata mikataba 
minono ya kuvuna utajiri wetu.  Katika kitalu namba 2 cha utafutaji wa 
mafuta na gesi huko Bahari Kuu kampuni ya kimarekani ya ExxonMobil ina 
ubia na kampuni ya Norway ya StatOil. Kampuni hiyo haikusubiri Rais wa 
Marekani aje ili wapate mikataba.
 
 Kuna makampuni mengi sana ya 
kichina yanajenga barabara zetu hapa nchini yakiwa na mikataba minono 
sana. Kule Mchuchuma na Liganga kuna kampuni ya kichina inajiandaa na 
uchimbaji wa chuma na makaa ya mawe. Makampuni yote haya hayakusubiri 
Rais wao aje.
 
 Hoja inayojengwa hapa ni kwamba ujio wa Marais 
mbalimbali nchini ni ujio wa kujijenga kidiplomasia na wakati mwingine 
kama sehemu ya kutuma ujumbe Fulani kwa dunia. Nchi inayotembelewa pia 
inaweza kuona kuwa diplomasia yake inaheshimiwa na mataifa 
yanayoitembelea.
 
 Hata hivyo hii haiondoi ukweli kwamba Obama 
anakuja kwa ajili ya maslahi ya nchi yake kama ilivyo kwa wachina 
walivyokuja. Tumesikia Rais Obama ataambatana na mamia ya wafanyabishara
 kutoka Marekani kwa ajili ya kupata fursa za kuwekeza nchini. Pia 
tutasikia matangazo kuhusu msaada wa pili wa Millenium Challenge ambapo 
Wamarekani wanaendelea kumwaga pesa nchini kusaidia miundombinu lakini 
pia kushawishi kuungwa mkono na nchi zetu kwenye maamuzi Fulani Fulani 
jumuiya za kimataifa.
 
 Tumesikia Obama atakwenda kutembelea 
mitambo ya kampuni ya Symbion. Hii ni mitambo ambayo miaka 4 iliyopita 
ilipigiwa kelele kuwa ni mitumba na hivyo TANESCO wasiinunue. 
Hawakununua na badala yake kampuni hiyo ya kimarekani ikainunua, 
wakaingia  mkataba na TANESCO kuwauzia umeme unaozalishwa na mitambo 
hiyo hiyo chakavu. Wakati tunasuburi kulipa takribani tshs 105 bilioni 
kwa Dowans baada ya kutubwaga kwenye kesi, tunasubiri kuona wanasiasa 
watakaokwenda kumsindikiza Obama kwenye matembezi hayo ya kutembelea 
mitambo chakavu.
 
 Kampuni kubwa ya kutengeneza mitambo ya 
kuzalisha umeme ya GE imetangaza kuingia ubia na kampuni ya Symbion 
kuzalisha umeme nchini. Takribani 400MW zitazalishwa kutoka Mtwara na 
kuingizwa kwenye gridi ya Taifa. Pia sehemu kubwa ya umeme 
utakaozalishwa Mtwara tayari umepata soko kwenye kiwanda cha kuzalisha 
udongo ulaya (simenti) cha bwana Dangote kule Mtwara. Mtendaji Mkuu wa 
GE bwana Jeff Immelt ametangaza kuwa kampuni yake itauza mitambo ya 
kuzalisha umeme kwa kutumia gesi mingi zaidi Afrika Mashariki kuliko 
Marekani katika kipindi cha miaka mitatu ijayo. Ni biashara tu!
 
 Nishati naona ni kipaumbele kikubwa sana kwa ziara ya Rais Obama. Kwa 
nchi kama yetu yenye watu asilimia 21 tu wenye umeme, ni dhahiri 
kipaumbele hiki watu wengi watakiiunga mkono. Hata hivyo Obama ni lazima
 asimame kidete kuhakikisha kuwa kampuni za nchini mwake zinazopata 
miakataba hapa nchini ziweke wazi mikataba hiyo na kulipa kodi 
inavyostahili. Makampuni ya mafuta kutoka Marekani hayana historia nzuri
 duniani na hivyo ni lazima tulisisitize mapema kabisa. Uwazi wa 
mikataba na uwezo wa kupambana na ukwepaji kodi ni muhimu sana katika 
vita dhidi ya Ufisadi na ubadhirifu.
 
 Rais Obama atambue kuwa 
iwapo Tanzania ingekuwa inakusanya nusu ya kodi zinazokwepwa na 
makampuni makubwa yanayotumia mbinu kali, basi tungehitaji misaada ya 
Marekani na hapa nchini angekuja kama mbia wa kweli na sawa katika 
dunia. Hivyo ni vema aungane na Waziri Mkuu wa Uingereza kuhakikisha 
kuwa makampuni makubwa hayatumii ‘tax havens’ kukwepa kodi katika nchi 
kama Tanzania. Uwazi wa mapato yao na kilicholipwa kwa Serikali ni vema 
usisitizwe sana na Obama mwenyewe ili makampuni yao yasikie na yaache 
kupora utajiri wa Afrika kiujanja ujanja.
 
 Mwisho ni vema kama 
Rais Obama ataomba radhi kwa ushiriki wa Marekani kwenye mauaji wa 
Waziri Mkuu wa kwanza wa Kongo Patrice Lumumba. Hivi Tanzania 
inahangaika zaidi ya uwezo wake kupeleka majeshi huko mashariki ya Kongo
 kulinda amani. Waafrika wengi tunaamini kuwa mauaji ya Lumumba ilikuwa 
ni kama laana kwa Taifa lile na hivyo limekuwa ni taifa la vurugu na 
vita licha ya utajiri mkubwa ulioko nchini humo. Nyaraka za CIA 
zinaonyesha dhahiri kuwa Rais wa Marekani wa wakati huo Lyndon Johnson 
aliagiza kuuwawa kwa mwanamapinduzi Patrice Lumumba. Kuwaomba radhi 
Waafrika na hasa Wakongo kuhusu mauaji ya Lumumba ni jambo litakaloweza 
kusaidia sana kurejesha amani Kongo.
 Karibu Afrika, Karibu Tanzania ndugu Barack Hussein Obama.
 
 Zitto Z Kabwe
 
 Makala haya yanatarajiwa kutoka kwenye gazeti la MWANANCHI, mfululizo wa makala kuhusu ziara ya Obama.
Facebook Comments Plugin Enhanced by Kitongoni blog