Miaka 20 iliyopita,
mwaka 1993 Rais Mstaafu wa awamu ya pili wa serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar Mzee Aboud Jumbe Mwinyi aliandika mfululizo wa makala katika
gazeti la kila wiki la Mwananchi wakati huo. Aliziita makala zake,
Tuishi bila kubaguana kidini.Mzee
Jumbe akieleza katika makala zake kuwa, aliamua kuchukua uamuzi wa
kuandika makala hizo ili wananchi pamoja na viongozi waweze kuchukua
hatua juu ya suala la udini ambalo lilikuwa likitishia uhai na umoja wa
Taifa letu.
Aliyoyaongelea Mzee Jumbe sasa yameanza kuonekena
katika jamii yetu. Tatizo la udini linazidi kukua badala ya kupungua.
Wanasiasa wanaongelea udini, viongozi wa dini wanaongelea udini,
wanaharakati nao pia wanaongelea uwepo wa udini. Kila mahali utakapopita
siku hizi, katika mada zitakazojadiliwa, moja wapo ni mada inayohusu
udini.
Kabla sijaendelea na makala yangu haya, ni vema nikanukuu beti za shairi lililotungwa na Kiongozi wetu huyo alilolipa jina la
Tanzania ni ya Watanzania wote.
|
|
Wito huu nautoa, kwa wote watanzania Naona hatari yaotea, twendako yangojea Wajibu wote kuijua, tuchange kuiondoa Enyi watanzania jueni, Tanzania yetu sote.
Huu si usaliti, pia si uchochezi Ni onyo tena la dhati, Nilitoalo kwa wakati Wazeni enyi wananchi, Msije kukosa bahati. Enyi Watanzania jueni, Tanzania yetu sote.
Umoja na amani, usawa kwa wote nchini. Akataaye ni nani, mkorofi, adui kisirani. Aseme wazi hadharani, ya nini chini chini Enyi Watanzania jueni, Tanzania yetu sote.
Kweli na haki kote, uwe mwendo wa wote Hadaa au dhuluma yoyote, iwe karaha kwa sote Hii nchi yetu sote, tufaidike nayo wote. Enyi Watanzania jueni, Tanzania yetu sote.
Namaliza sikudhulumu, wenyewe mhukumu, Uhuru na umoja kudumu, bila ya usawa vigumu Hilo wazi mfahamu, je haki au dhuluma? Enyi watanzania jueni, Tanzania yetu sote
|
Watu
wengi wamekuwa wakiongelea uwepo wa udini hapa nchini lakini pindi
unapowauliza nini hasa maana ya udini wamekuwa wakishindwa kutoa jibu
lililo sahihi. Si ajabu ukaambiwa kuwa “jamaa Fulani ni mdini kwa kuwa
tu anasali sala tano na muda wote anavaa kanzu na tas’bihi mkononi
haimuondoki. Au pia, fulani ni mdini kwa kuwa muda wote amevaa rozali na
kuwa hana starehe yoyote zaidi ya kusikiliza kwaya na kusoma Biblia.
Wakati
nafikiria kuandika makala haya, niliamua kwanza kutafuta maana ya neno
udini. Kitabu cha kwanza kabisa kukikimbilia ilikuwa ni kamusi ya
Kiswahili sanifu, toleo la pili ya mwaka 2004. Kwa bahati mbaya, nadhani
inaweza kuwa imetokana na kusahaulika au kutokana na makosa ya mchapaji
neno udini halipo katika orodha ya maneno katika kamusi hiyo.
Jitihada
za pili katika kutafuta maana ya maneno haya niliipeleka katika kazi za
wanazuoni mbalimbali ambapo niliamini kuwa lazima watakuwa
wamezungumzia neno hilo katika kazi zao. Bahati nzuri maana ya neno
udini nililipata kutoka kwa viongozi wawili wa kidini hapa Tanzania.
Hawa ni Mwinjilisti Kamara Kasupa na Sheikh Mohamed Issa.
Katika
pitia pitia zangu katika maandiko ya Mwinjilisti Kamara Kasupa, yeye
aliutafsiri udini kuwa ni Ubaguzi unaoendeshwa katika misingi ya kidini,
na aliendelea kufafanua kuwa udini una kawaida nyingine mbaya, nayo ni
ubinafsi wa kubinafsishwa katika misingi ya kidini, una kawaida nyingine mbaya nayo ni ubinafsi wa kubinafsisha kila kitu.
Tafsiri
ya pili ya dhana ya udini niliipata kwa mwanazuoni maarufu wa kiislamu
Sheikh Mohamed Issa. Katika mada yake iliyoitoa katika msikiti wa Haq
mkoani Morogoro, aliutafsiri udini kuwa ni kupendelea dini yako kiasi
cha kuwadhulumu watu wa dini nyingine, na bila kujali taratibu.
Akaelezea zaidi kuwa ni kupendelea dini yako na kuwadhibiti watu wa dini
nyingine wasije wakapata mafao, mafanikio na maendeleo kama ya dini
yako.
Baada ya kupata tafsiri hizo, niliamua kumfuata kiongozi
wangu wa dini na kukaa nae huku tukijadili masuala mbalimbali
yanayoendelea katika nchi yetu. Katika mazungumzo yetu nilimuuliza,
uislamu unatutaka tuishi vipi na wasiokuwa waislamu?
Alinijibu kuwa, katika Quran Tukufu Surat AN-Nisaa aya ya 36
mwenyezi Mungu anasema “Muabuduni Mwenyezi Mungu wala msimshirikishe na
chochote.
Na wafanyieni ihsani wazazi wawili, na jamaa na mayatima na masikini na
jirani walio karibu na jirani walio mbali, na rafiki wa ubavuni (mwenu)
na msafiri aliye haribikiwa, na wale iliyowamiliki mikono yenu ya kulia
(kuume). Bila shaka Mwenyezi Mungu hawapendi wenye kiburi wajivunao”.
Funzo
kubwa nililolipata katika aya hii ni kuwa muislamu wa kweli hatakiwi
kubagua. Anatakiwa kutenda wema kwa wote bila kujali dini, kabila au
utajiri wa mtu. Migogoro ya kidini, nini hasa chanzo chake na kwa nini
hasa waislamu ndo wanaonekana kama wapenda fujo na vurugu? Hili ndio
hasa nataka kulijadili na pia kutoa mbinu za kuiepuka migogoro hii ili
isije kuliangamiza taifa hili.
Mwalimu wangu wa chuo Kikuu,
Profesa Mwesiga Baregu alipokuwa akitufundisha somo lililohusu Utatuzi
wa migogoro na ujenzi wa amani (Peace making and conflicts resolution)
alikuwa akisisitiza suala la kusikiliza, kutafakari na hatimaye
kuchukua hatua stahiki katika kutatua matatizo. Na baada ya hatua
kuchukuliwa ni vema kuwarudishia majibu walalamikaji na walalamikiwa.
Tatizo
kubwa tulilonalo sisi ni kwamba tumekuwa wagumu sana kusikiliza
malalamiko hasa yanayotolewa na waislamu, na hata ikitokea malalamiko
yao yamesikilizwa basi yamekuwa yakitolewa majibu mepesi sana.
Nimekuwa
nikijiuliza, kwa nini hasa malalamiko ya waislamu huwa hayapewi uzito
sana, huwa nakosa jibu. Labda huwa tunawaangalia watoa malalamiko, kwa
kuwa labda wengi wao wanavaa kanzu zilizo chakaa na makubadhi au hata
yeboyebo zilizo chakaa, hivyo tunadhani hata akili zao zimechakaa kama
kanzu na yeboyebo wanazovaa.
Hili ni tatizo, maana siku hizi mtu
mwenye akili anapimwa kwa vitu alivyovaa au anavyomiliki au usafiri
anaotumia na hata wapi anaishi. Anayetumia VX huonekana ana akili sana
kuliko anayeendesha baiskeli au mtembea kwa miguu. Anayeishi Masaki au
Mikocheni na Oysterbay jijini Dar es salaam au Uzunguni, Area C na Area D
mkoani Dodoma huonekana kuwa ana akili sana na amestaarabika kuliko mtu
anayeishi Mbagala, Manzese hapo hapo Dar au pia anayeishi Chang’ombe
mjini Dodoma.
Tumejenga tabia ya kuthamini hata mavazi na lugha.
Anayevaa suti na kuongea kiingereza huonekana ana akili sana na
amestaarabika kuliko anayevaa kaniki na kuongea Kiswahili.
Kuna
suala moja ambalo mimi binafsi limekuwa likinikera sana na ninahisi kwa
kila mpenda amani na usawa huwa anakereka. Suala hili ni kuwaita
viongozi wa dini kuwa ni wahuni. Hili ni tusi kubwa hasa unapomuita
kiongozi wa dini ambaye anaongoza mioyo na imani za watu. Tumeshuhudia
watu kama akina Sheikh Ponda, Sheikh Farid na wengine wengi wakiitwa
majina ambayo yanaonesha dharau kubwa si kwao pekee bali pia kwa dini
yao na taasisi wanazoziongoza.
Lakini sababu ya pili inayowafanya
waislamu waonekane kama wapenda fujo na wapenda machafuko kwamba
wamekuwa katika harakati za kuitetea dini yao ambayo wanadhani kuwa
imekuwa ikdharauliwa na pengine kutothaminiwa kabisa.
Hili
nitalielezea. Kwa sasa kumekuwa na wanaharakati wengi na wanasiasa ambao
wamekuwa katika harakati za kuhamasisha na kufanya mabadiliko
mbalimbali katika mifumo yetu hasa sheria, mabadiliko ambayo kwa njia
moja ama nyingine yataathiri imani na ibada za waislamu.
Mathalani,
unapoanzisha vuguvugu la kuwepo kwa sheria moja ya mirathi, kitu
ambacho kitaleta upinzani mkubwa kutoka katika jamii za waislamu kwa
kuwa tayari wana mfumo wao wa mirathi, ambao umeelekeza namna gani
mirathi igawanywe na nani apate nini na kwa nini apate hivyo.
Udini
umekuwepo siku nyingi sana hapa nchini kwa sura tofauti. Vichwani mwa
watu wamekuwa na dhana za ubaguzi wa kidini bila wenyewe kujijiua. Watu
wanaoamini katika dini ya kiislamu wamekuwa wakidharauliwa na kukejeliwa
sana. Mfano, ukitazama vyombo vya habari hasa magazeti. Mfano, ili
kufikisha ujumbe kwa wasomaji, wachora wa picha za magazetini huwatumia
sana wazee wenye muonekano wa kiislamu katika kuonesha watu
wasiostaarabika.
Utakuta unapotaka kumchora mchawi, mganga wa
kienyeji ama mtu anayependa sana kula katika sherehe au misiba,
atamchora mzee aliyevaa kanzu, makubadhi, amevaa baraghashia na ameshika
bakora vitu ambavyo hutumiwa sana na waislamu ingawa pia katika baadhi
ya jamii kama za wahaya mavazi hayo ni mavazi ya heshima kwa wazee bila
kujali dini.
Utendaji wa baadhi ya taasisi nao umekuwa ukiibua
hisia za kidini. Hii ilidhihirika miaka michache iliyopita wakati hakimu
mmoja jijini Dar es salaam ilipoamua kumfunga kifungo cha miezi sita,
muislam mmoja aliyehudhuria mahakamani kwa kuwa tu alikataa kuvua kofia
aina ya baraghashia. Aliadhibiwa kwa kosa la kudharau mahakama.
Pia
upo ubaguzi katika makazi na maeneo. Maeneo mengi ambayo kiasili
yamekuwa yakikaliwa na waislamu yamekuwa yakipewa majina yasiyo na
nidhamu kama vile uswahilini, uswazi nakadhalika na yamekuwa yakisifika
sana kwa sifa ya uchawi, kitu ambacho kimejengwa ndani ya vichwa vya
watu na hutokea mpaka wageni kuogopa kuishi ama kuwekeza katika maeneo
hayo na hivyo kuyafanya yaendelee kuwa duni siku hadi siku.
Kwa
mtu yeyote, ukimueleza maeneo kama Ujiji na Gungu mkoani Kigoma, Isevya
mkoani Tabora, Bagamoyo , Rufiji na Tanga, taswira inayojengeka kichwani
mwake moja kwa moja ni kuwa, hii ni miji iliyojaaa wachawi na
washirikina. Na hii imejengeka kiasi kwamba, iwapo inatokea mtu
amekosewa na mwenzake, tishio huwa ni kwamba, nitakuendea Ujiji kama
siyo Bagamoyo, Rufiji na Kilwa.
Si rahisi kukuta mfanyakazi wa
serikali aliyepangwa kufanya kazi mkoani Kigoma, kukubali kuishi Ujiji
au Gungu hata kama ataambiwa bei ya pango kwa nyumba nzima ni Tsh 50,000
kwa mwezi. Mtumishi huyo yupo radhi kuishi Mjimwema ambako atalipa Tsh
200,000 kwa mwezi na ukimuuliza kwa nini hasa hataki kuishi Ujiji ama
Gungu, atakueleza kuwa anaogopa kurogwa. Huu pia ni ubaguzi.
Profesa Mahmood Mamdani ametunga kitabu chake alichokipa jina la Good Muslim, Bad Muslim.
Katika kitabu hicho anaelezea jinsi waislamu walivyogawanywa katika
makundi. Kwa hapa Tanzania Good Muslim ni wale waislamu walio chini ya
BAKWATA, ambao wanaiona BAKWATA kama mtetezi na mlinzi wa waislamu na
Bad Muslim ni wale wote ambao hawataki msimamo wa BAKWATA na pia
hawataki kuitambua BAKWATA, ambao wanaiona BAKWATA kama mnyonyaji na
mkandamizaji wa haki za waislamu. Bad Muslims hawasikilizwi na muda wote
wamekuwa wakiitwa walalamishi.
Lakini sasa kuna hili suala la
kamatakamata ambalo limekuwa likiendeshwa na jeshi la polisi katika
kudhibiti viongozi wa dini ambao wanahubiri “uchochezi”. Jambo hili
lisipofanywa kwa umakini, linaweza kuingilia uhuru wa watu wa kuabudu.
Majuzi nilikuwa natazama kipindi fulani katika TV. Mwanaharakati mmoja
kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binaadamu (LHRC) alilalamikia
matumizi ya maneno kama vile “kafir” na kuelezea kuwa si vizuri kuyatumia.
Tukumbuke
kuwa neno hilo lipo katika kitabu kitukufu cha waislamu, , Quran na
kulalamikia kutumika kwa neno hilo ni sawa na kusema liondolewe au
lisitumike, kitu ambacho nina uhakika kuwa hakitawezekana kwani kwa
mujibu wa mafundisho ya uislamu, dini yao ilikwisha kamilika na hakuna
marekebisho yoyote ambayo yanaweza kufanyika.
Lakini pia,
niwashukuru viongozi wetu wa dini, kama alivyosema Sheikh Alhad Mussa
Salum, Sheikh mkuu wa BAKWATA wa Mkoa wa Dar es Salaam na Muadhama
Askofu Kardinali PolycaRp Pengo, kuwa kuna haja ya kukutana kwa viongozi
wa dini ili wajadili kwa kina, chanzo hasa cha migogoro na namna ya
kuitatua. Na vikao hivyo ni vema vikianzia katika ngazi za vitongoji
mpaka ngazi ya taifa.
Nimalizie makala yangu haya, kwa kuwaomba
viongozi wetu na watendaji wa serikali kutopuuzia malalamiko ya watu
wao. Wayafanyie kazi bila kujali, nani ameyaleta na huyo aliyeyaleta ana
miliki nini au ana elimu gani. Na pia nikumbushe maneno ya rais wa
zamani wa Iran Mohammed Khatami aliyeelezea majadiliano baina ya tamaduni (Dialogue among Civilizations) kama njia ya kuelewana na kuzuia machafuko yanayojiegemeza katika tamaduni.
Alicho kisisitiza Mzee Aboud Jumbe ni TUEPUKE UDINI KWA KUTENDA HAKI