Facebook Comments Box

Tuesday, August 26, 2014

WAKONGWE WA REAL MADRID WAKIELEKEA KUPANDA MLIMA KILIMANJARO

Wakongwe wa Klabu ya Real Madrid ya nchini Hispania wakipiga picha za kikundi cha ngoma kilichokuwa kikiwatumbuiza mara baada ya kuwasili Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro kabla ya kuelekea Mlima Kilimanjaro.


MAGAZETI YA LEO: JUMANNE 26/08/2014

 



UFARANSA YAVUNJA SERIKALI YAKE

Rais wa Ufaransa Francois Hollande akitoa hotuba huko katika jumba la Elysee

Rais wa Ufaransa Francois Hollande amevunja serikali yake. Waziri Mkuu Manuel Valls amewasilisha hati za kujiuzulu kwa serikali yake ya kisoshalisti Jumatatu na Bw. Hollande amekubali na kumwamuru waziri mkuu huyo kuunda serikali mpya ifikapo Jumanne.


Monday, August 25, 2014

MAMBO MATANO NILIYO YAONA KATIKA MECHI YA ARSENAL NA EVERTON


Arsenal tumecheza mechi mbili katika ligi kuu ya Uingereza na tumecheza mechi ya awali katika ligi ya mabingwa na timu ya  Besiktas,lakini bado kumeonekana kuna tatizo kidogo katika timu. Kuna matumaini kidogo ya timu kuimarika yalionekana juzi wakati wa mechi na Everton. 

Hapa watu ndio wanapokuwa hawanielewi vizuri wanashangaa haya matumaini yanatoka wapi. Wengi wakidhani naongea kishabiki zaidi kuliko kitaaam. Hebu tukumbuke ile hamasa ya kishambuliaji ambayo wachezaji wetu walikuwa nayo msimu uliopita, kumbuka mchezo mzuri tulio onesha wakati wa mechi ya ngao ya hisani dhidi ya Manchester City pale Wembley.

Kwahiyo ninavyomjua Wenger sasa atakuwa ameusoma mchezo tulio ucheza pale Goodison Park na kwasasa atakuja na njia sahihi na nzuri katika mechi kubwa na ngumu na zingine zifuatazo.

Kuna mambo matano ambayo tumejifunza katika mechi ile:

Hata kama anatupa hasira na machungu kutokana na magoli ya wazi ambayo kuna wakati anayakosa bado hatakiwi kukosa katika kikosi kwa kuwa kwasasa yeye ndio mshambuliaji wetu tumaini kwasasa na huyu si mwingine bali ni  Olivier Giroud. Ukiangalia kipindi cha kwanza katika mechi yetu na Everton utaona ni kiasi gani tulikosa kushambulia na hivyo kuwaacha watushambulie muda wote.

Pili, Aaron Ramsey bado kidogo hajarudi katika hali yake ya kawaida. Bado mashuti na pasi zake si nzuri kihivyo. Bado tunamkosa katika mechi ya jumatano kutokana na kadi nyekundu na kuna uwezekano akakosekana kwenye mechi na Leicester mwisho wa wiki maana huwezi jua kwani nani alijua kuwa atapewa kadi nyekundu. Lakini pamoja na yote bado ni mchezaji wetu ambae anaweza akaingia kwa nguvu kwenye kumi na nane na kufunga goli kwa juhudi binafsi. Na kama utakumbuka kurudisha kwetu magoli kulianza na yeye na goli lake ndio lilioipa uhai timu yetu. Nina imani atarudi na kuwa bora na tumaini letu katika msimu huu.

Calum Chambers ni beki mzuri ila anahitaj kujua anapocheza na Per Mertesacker anatakiwa acheze vipi. Nina matumaini huu utakuwa wakati muafaka kwa Arsene Wenger kujaribu kumuweka Chambers acheze na Koscielny ili kuweka ulinzi imara na sio Per Mertesacker.
Chambers na imani ni beki mzuri na anaweza akaitendea haki nafasi ya beki vizuri kama akiwekwa na mtu sahihi ambae uchezaji wake unaenda. Ana makosa madogo madogo ambayo sio ya hatari sana kwa timu.

Alexis Sanchez ni mchezaji mzuri ila anahitaji muda ili aweze kuendana na mchezo na ligi ya uingereza. Najua amekuwa akijaribu sana kufanya hivyo na kuonesha kuwa hakusajiliwa kimakosa na ile gharama timu iliyoingia ni sahihi kwake. Ni vizuri ila anatakiwa asiwe na pupa sana atulie na aisome ligi hii, maana ni ligi ngumu na ndefu ambayo katikati ina mashindano mengi ambayo huchosha sana wachezaji. Mfano ni dhahiri katika wiki moja Arsenal tumecheza klabu bingwa ulaya na mechi ya ligi. Sitaki hii iwe kisingizio cha kutoa suluhu mbona Manchester United hawapo katika mashindano makubwa wamefungwa na kutoa suluhu?

Kwa hii mechi na Everton naweza kusema kwa mwisho pamoja na kuwa Arsenal bado hatujaonesha makali yetu ila bado tumeonesha muelekeo mzuri na tumeonesha Dira ya nini tunataka na kuhitaji. Sitakuwa mmoja wa watu wanao shangaa kama tutanyanyua kikombe kikubwa mwezi wa tano ujao.


MCHEZAJI APIGWA NA KITU KIZITO NA KUFA AWANJANI

Mchezaji mmoja wa soka raia wa Cameroon amefariki baada ya kupigwa na kitu katika kichwa chake kilichorushwa kutoka kwa mashabiki mwishoni mwa mechi katika ligi ya Algeria.

Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 24 Albert Ebosse aliyekuwa akiichezea kilabu kubwa ya JS Kabylie alikuwa ameifungia timu yake bao la pekee katika mechi ambayo timu hiyo ilishindwa kwa mabao mawili kwa moja na kilabu ya USM Alger.
Kitu kilichomgonga kichwani kilirushwa baada ya mechi kukamilika,wakati ambapo wachezaji walikuwa wanarudi katika chumba cha kujianda.
Waziri wa maswala ya ndani nchini Algeria ameagiza kuanzishwa
uchunguzi kuhusu mauaji hayo

 CHANZO: BBC SWAHILI


MAGAZETI YA LEO: JUMATATU TAREHE 25/08/2014




Sunday, August 24, 2014

CUF WALAANI UNYAMA WALIO FANYIWA VIONGOZI WA UAMSHO

Chama cha wananchi CUF kimetoa taarifa ya kulaani vikali madai ya vitendo visivyo vya kiungwana walivyofanyiwa viongozi wa Uamsho
na jeshi la Polisi.

Madai ya kudhalilishwa kwa watuhumiwa hao yalitolewa wiki hii na Sheikh Farid katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, mbele ya
Hakimu Mkazi, Hellen Riwa, wakati kesi ya tuhuma za ugaidi inayowakabili ilipokuwa ikitajwa.

Wakili wa Serikali Mwandamizi, Peter Njike, alidai kesi ilikuja kwa ajili ya kutajwa, upelelezi haujakamilika na wanaomba hati ya kuwachukua washtakiwa saba, akiwamo Sheikh Farid kwa ajili ya mahojiano.

Hakimu Riwa alikubali maombi hayo na kuahirisha kesi hadi Septemba 3, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa. Hali hiyo ilisababisha
washtakiwa kuomba kutoa maelezo yao.
“Mheshimiwa wametuomba kwenda kutuhoji tena, mara ya kwanza tulipohojiwa, polisi hawakutumia ustaarabu wala ubinadamu, ni
ushenzi na ukatili, walituhoji uchi wa mnyama na kutupiga.

“Kiongozi Mkuu wa Uamsho, Sheikh Mselem Ally Mselem, mwenye heshima,mfasiri wa Kur’ani, alinihadithia alipohojiwa walimfanya nini tumepigwa na hatukutibiwa, magereza wamejitahidi, lakini hawana nyenzo za matibabu.
 
“Watu wameumizwa vibaya, mengine hayasemeki, wanajisaidia haja ndogo damu wiki moja hadi mbili, tunaomba tufanyiwe uchunguzi
wa afya zetu, ipo siku mahakamani italetwa maiti.

“Tumekamatwa sababu hatutaki Muungano, hiyo ndiyo kesi ya msingi, tunawaambia ukweli katika mihadhara na watu wanatuamini, tunaomba Sheria ya Mabadiliko ya Katiba iletwe mahakamani tuijadili,” alidai Sheikh Farid.
Mshtakiwa wa 12, Salum Alli Salum aliomba mahakama imwite daktari ili aweze kufanyiwa uchunguzi wa afya yake kwani ameingiliwa kijinai kwa nguvu. “Mheshimiwa tunalazimishwa kutoa
maelezo wanayoyataka wao, wanatuingilia kinyume cha maumbile, wanaingiza majiti,chupa, wengine wanavuja nyuma,kama unaweza hakimu twende faragha nikakuonyeshe.

“Askari ameniingilia kisha akaniingiza jiti mpaka likakatika kungekuwa na sehemu ningekuonyesha, Jeshi la Polisi la kwanza
kuvunja sheria, waliofanya madhila haya wanawatukanisha Watanganyika na kufanya waonekane wabaya,” alidai mshtakiwa huyo.
 
Baada ya washtakiwa hao kutoa malalamiko yao, mahakama iliwaahidi washtakiwa hao waende wakahojiwe na muda wotewatakuwa katika mazingira salama. Sheikh Faridi nawenzake 19 wanashtakiwa kwamba kati ya Januari 2013 na Juni 2014 maeneo mbalimbali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania,walikula njama ya kutenda kosa la kuingiza watu nchini kufanya ugaidi.

Shtaka la pili linawakabili washtakiwa wote, wakidaiwa kuwa katika kipindi hicho walikubaliana kumuingiza Sadick Absaloum na Farah Omary nchini ili kushiriki kutenda makosa ya ugaidi. Katika shtaka la tatu linalomkabili SheikhFarid, anadaiwa kati ya Januari 2013 na Juni 2014 maeneo mbalimbali ya Jamhuriya
Muungano wa Tanzania, huku akijua ni kosa, alimuingiza nchini Sadick na Farah kufanya ugaidi. Sheikh Farid pia anadaiwa kuwahifadhi Sadick na Farah, huku akijua watu hao walitenda vitendo vya kigaidi.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Jamal Swalehe, Nassoro Abdallah, Hassan Suleiman, Anthari Ahmed, Mohammed Yusuph, Abdallah Hassani, Hussein Ally na Juma Juma.
Wengine ni Saidi Ally, Hamisi Salum,Saidi Amour Salum, Abubakar Mngodo, Salum Ali Salum, Salum Amour Salum,Alawi Amir, Rashid Nyange, Amir Hamis Juma, Kassim Nassoro na Said Sharifu.
 
Wakati huohuo, kesi nyingine ya ugaidi inayomkabili Kiongozi Mkuu wa JUMIKI,Sheikh Mselem Ali Mselem na mwenzake,Abdallah Said
Ali, imeahirishwa Septemba 3, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa kwa sababu Sheikh Mselem hakuwapo anaumwa.

Taarifa kamili ya chama hicho isome hapo chini:-
TAARIFA KWA UMMA NA VYOMBO VYA HABARI
TAREHE 23/08/2014
 
UNYAMA WA JESHI LA POLISI KWA MAHABUSU
 
CUF Chama cha Wananchi kinalaani vikali uukatili na ushenzi uliofanywa na jeshi la polisi dhidi ya viongozi wa Jumuiya ya Uamsho
na wenzake 19 . Kwa mujibu wa walivyoeleza watuhumiwa hao Shekh Farid Had Ahmed na wenzake Jeshi la polisi limewafanyia ukatili wa hali ya juu usiostahili kwa binadamu.

Mahabusu hao wanadai kulawitiwa na na asakri wa jeshi la polisi, kuwekewa vitu vyenye ncha kali kwenye sehemu za haja kubwa na mateso maengine mengi ikiwa ni pamoja na kupigwa hadi kuumizwa.

Hata kama ni wakosaji matendo haya ni kinyume na haki za binadamu. Inashangaza kuona vitendo vilivyokuwa vinafanywa na Makaburu dhidi ya Watu weusi wa Afrika Kusini sasa Vinafanywa na Vijana wa Kitanzania dhidi ya Watanzania wenzao kwa kisingizio cha Ugaidi.
CUF hatuoni mantiki ya uvunjaji wa Haki za Binadamu kwa kiasi hiki kwa watu wanaotuhumiwa kwa kile kinachoitwa kujishirikisha na Matendo ya Kigaidi. Hatakama watuhumiwa hao watiwa hatiani kwa makosa hayo, bado hukumu yao haitakua kulawitiwa kama ilivyoelezwa na mmoja kati ya Watuhumiwa hao mbele ya Mahakama.

Matendo hayo yanafanywa na Jeshi la Polisi dhidi ya Viongozi wa Dini , hivi tunataka wafuasi wao na Familia zao wafanye nini? CUF-Chama cha Wananchi kina mtaka Rais kutoa kauli na Msimamo wa Serikali dhidi ya unyanyasaji na udhalilishaji huu uliofanywa na Jeshi la.Polisi ili Wananchi wapate kujua hatua zitazo chukuliwa na Serikali sambamba na kukubali Ombi la Watuhumiwa la kufanyiwa uchunguzi wa Afya zao kama lilivyo wasilishwa kwenye Mahakama inayosikiliza Kesi hiyo.

Tunatoa wito kwa Taasisi zinazoshughulikia mambo ya Uvunjwaji wa.Haki za Binaadamu kufuatilia kwa Karibu suala hili na kuchukua hatua zinazostahili. Watuhumiwa hao wamelalamika kwamba mpaka hivi sasa wale
waliojeruhiwa bado wanauguliwa maumivu na hawajapewa matibabu .Wapo ambao mpaka hivi sasa kutokana na vitendo vya kishenzi waliofanyiwa bado mpaka leo hii hawajapata matibabu yoyote.

CUF Chama cha Wananchi kinawaomba tunawaomba Familia na Waislamu wote kua na subira na kufuatilia suala hili kwa njia za Sheria
ili kuweza kupata ufumbuzi wa tatizo hili la udhalilishaji uliofanywa na Jeshi la Polisi dhidi ya Familia zenu na Viongozi wetu.
 
Imetolewa na
Abdul Kambaya
Naibu Mkurugenzi Habari na Uenezi


WAZEE WA MADRID WAWAONESHA WAZEE WENZAO WA TANZANIA KUWA MPIRA NI KAMA BAISKELI UKIJUA UMEJUA




Tanzania eleven na wageni wao Madrid walipokuwa uwanjani jana.
Mdau wa Kitongoni akiwa jukwaani kupata burudani hiyo hapo jana.
Heka heka langoni mwa Tanzania eleven 

kitongoni Taifa:

Mechi ilikuwa nzuri kila timu ilicheza vizuri japo real Madrid walionekana wana mazoezi na hawana vitambi kwa kuwaangalia ni wazee ila mpira wanaucheza vizuri. Mpira ni kama basikeli ukijua umejua tu.

Kwa upande wa Tanzania eleven Kalimangonga Ongala na Athuman china walicheza vizuri na walionekana kuisumbua sana ngome ya wazee wa madrid maana kuna wakati Kalimangonga alitolewa ikabidi arudishwe Maana timu ilipwaya.

Kwa upande wa makipa wote wawili Mohamed Mwameja na Peter Manyika walidata vizuri na wanaonesha bado ni hazina kubwa kwa Taifa letu maana ujuzi hauzeeki bwana asikwambie mtu.

Ila jambo nililojifunza katika mtanange ule ni kwamba Wazee.wetu wana akili ya mpira na control kuliko vijana wa sasa maana vijana mambo mengi mpira unataka vitu vitatu tu Control, Pass and Move mambo mengine ya nini.




Saturday, August 23, 2014

KIBONZO: ISRAEL NA UMOJA WA MATAIFA DHIDI YA PALESTINA




SAMAHANI KWA PICHA: WEZI WACHOMWA TABATA LIWITI

Chini ni picha ya mmoja ya wezi ambao hufanya wizi kwa kutumia pikipiki. Inasemekana vijana hao wawili walikuwa kwenye pikipiki maarufu kama bodaboda walimnyang'anya mkoba binti mmoja leo alfajiri.
Watu walijitokeza na kuwakamata baada ya hapo waliwakata mikono na kuwachoma moto.
 Polisi walifika eneo la tukio na kuchukua miili ya watu hao.
 Tumeweka picha chache  kwa tahadhari nyingine zipo katika hali mbaya kiasi ambacho hatuwezi kuziweka hapa.

Miili ya wezi hao ikiteketea kwa moto
Polisi wakiwa wamefika kuchukua miili



VIFAA MAALUM VYA KUGUNDUA EBOLA VYAINGIA NCHINI: KUTUMIKA VIWANJA VYA NDEGE

Picha inayoonyesha moja ya kifaa (kamera) nne
zilizoagizwa na Serikali kupimia dalili za ugonjwa wa Ebola maeneo ya viwanja vya ndege. Kifaa hicho kina uwezo wa kutunza picha na kumbukumbu za msafiri, muda , joto la
msafiri, tarehe aliyoingia nchini pia uwezo wa kupata takwimu kutoka kwenye hali ya majimaji au jasho la Binadamu pindi kinapoelekezwa kwake.
Naibu Waziri wa Afya Dkt. Kebwe Steven Kebwe akiongea na waandishi wa habari eneo la uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere wakati wa kupokea na kukabidhi vifaa vya kupima dalili za ugonjwa wa Ebola. Wengine ni Mkurugenzi Msaidizi wa Kitengo cha Dharula
na Maafa (kulia) na Kaimu Mkurugezi wa Bohari ya Dawa (MSD), Cosmas Mwaifani.

Naibu Waziri wa Afya Dkt. Kebwe Steven Kebwe
akiangalia kwa karibu taarifa zilizorekodiwa na moja ya kifaa (kamera) nne zilizoagizwa na Serikali kupimia dalili za ugonjwa wa Ebola maeneo ya viwanja vya ndege.
Picha na Aron Msigwa –MAELEZO.
========= ======= ========
Sehemu ya vifaa vya kubaini hatua za awali za ugonjwa wa Ebola kwa kupima hali ya joto la mwili kwa wasafiri kutoka nje nchi wanaotumia viwanja vya ndege vilivyokuwa vimeagizwa na Serikali vimewasili jijini Dar es salaam.
Vifaa hivyo vinavyohusisha kamera 4 zenye uwezo wa kubaini joto la mwili wa msafiri kwa umbali wa mita 100 bila kumgusa muhusika vimewasili leo katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar
es salaam kutoka nchini Afrika ya Kusini vilikonunuliwa.

Akikabidhi vifaa hivyo kwa wataalam wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dkt. Kebwe Steven Kebwe amesema kuwa kuwasili kwa vifaa hivyo ni moja ya juhudi za Serikali za kuhakikisha kuwa wananchi wanakuwa salama kwa kuuzuia ugonjwa huo kuingia nchini.

Amesema vifaa hivyo vitapelekwa katika maeneo ya viwanja vya ndege na maeneo yanayotumiwa na raia wa kigeni kuingia nchini vikiwemo vya Dar es salaam, Zanzibar, Kilimanjaro,Mbeya na Mwanza. Ameongeza kuwa Serikali inaendelea na mpango wa kuagiza vifaa zaidi vya kuwezesha shughuli ya upimaji wa afya kwa wasafiri wanaotembea (scanners) zitakazowezesha kubaini afya za wasafiri wengi zaidi kwa wakati mmoja bila kulazimu kuwasimamisha.
Aidha, amewataka wataalam hao wa afya kufanya kazi zao kwa weledi mkubwa kwa kuhakikisha wanawapima abiria wote wanaotoka nje ya nchi bila kujali hadhi walizonazo ili kuweza kubaini kama wana maabukizi au dalili za ugonjwa wa Ebola.

“Nataka mfanye kazi yenu kwa kuzingatia weledi wa taaluma yenu na kwa kuzingatia yale mliyojifunza,mvitumie vifaa hivyo kupima kila abiria ili kubaini joto lake bila kujali cheo wala hadhi yake maana janga hili ni kubwa” Amesema Dkt. Kebwe.
Kuhusu utunzaji wa vifaa hivyo amewataka wataalam hao kuhakikisha wanavitunza vifaa hivyo ili viweze kudumu na kutimiza malengo yaliyokusudiwa ya kuwasaidia wananchi kutokana na vifaa hivyo kugharimu fedha nyingi kila kimoja.

Katika hatua nyingine Mh. Kebwe amefafanua kuwa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii inaendelea na shughuli ya utoaji wa Elimu ya Afya kuhusu ugonjwa wa Ebaola ili kuwawezesha wananchi kuchukua tahadhari na kuzielewa
dalili za ugonjwa huo na namna ya kujingika endapo utagundulika nchini.
Amesema tayari kamati mbalimbali za wataalam
zimeshaundwa ili kuwezesha zoezi la utoaji wa elimu na mafunzo kwa wataalam wa ndani ili kuwajengea uwezo wa kukabiliana na janga hilo.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Bohari ya Dawa nchini (MSD), Cosmas Mwaifwani ambaye ofisi yake imehusika katika uagizaji wa vifaa hivyo nchini Afrika ya Kusini amesema kuwa mahitaji ya vifaa hivyo kwa sasa yameongezeka kutokana na umuhimu wake na jinsi vinavyofanya kazi kwa ufanisi mkubwa.
Amesema upimaji kwa kutumia vifaa hivyo unatumia teknolojia ya kubaini mionzi ya joto kutoka katika mwili wa binadamu pindi vinapoelekezwa katika maeneo ya macho na masikio ya mwili wa binadamu.

Amefafanua kuwa vifaa hivyo vinauwezo wa kutunza picha na kumbukumbu za msafiri, muda , joto la msafiri na tarehe aliyoingia nchini na kuongeza kuwa vifaa hivyo vina uwezo wa kupata takwimu kutoka kwenye hali ya majimaji
au jasho la Binadamu pindi kinapoelekezwa kwake.

Mwaifwani ameeleza kuwa MSD inaendelea kuimarisha uwezo wake kwa kuongeza vifaa zaidi kutoka Ubelgiji na China na kufafanua kuwa Bohari hiyo imejiandaa kukabiliana na ugonjwa wa Ebola kwa kujenga uwezo wa kuwa na dawa za kutibu hali ya magonjwa yanayoambatana na homa hiyo.

Naye Mkurugenzi wa Viwanja vya ndege nchini, Moses Malaki akizungumza kwa niaba ya Viwanja vya ndege nchini ameielezea hali hiyo ya upatikanaji wa vifaa katika maeneo hayo kuwa itaongeza ufanisi wa uchunguzi wa afya kwa wasafiri na kuondoa usumbufu kutokana na uwezo wa vifaa hivyo kumpima msafiri akiwa mbali.


 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU