Facebook Comments Box

Thursday, September 19, 2013

TAZAMA PENNY ALICHOSEMA KUHUSU NASEEB ABDULMALIK 'DIAMOND PLATNUMZ'

Diamond na Penny
Penny 
Mwanadada anayewapandisha presha wadada wa mujini Penny Mungilwa 'sukari ya Diamond' ameongea nakueleza mengi kuhusu sukari wake huyo ambaye kwa sasa yupo nchini malaysia katika bonge la show.

Penny ambaye pia ni mtangazaji wa Tv hapa nchini tanzania amesema kwake hakuna wakati mgumu anaoupata kama Diamond akisafiri penny aliieleza kuwa anaumia sana kumkosa sukari wake huyo na mara nyingi hujikuta akiugua kabisa kama Diamond akimtajia safari.
Penny ameyasema hayo wakati Diamond akiwa nchini malaysia kikazi alikokwenda kupiga show na kumuacha Penny peke yake, "Kiukweli hakuna wakati mgumu na huwa naumwa kama diamond akisafiri yaani huwez  amini nimemzoea sana bby wangu jamani", alisema Penny. 

Muandishi wetu alimdadisi kutaka kujua kwanini aumwe au hamtakii mwenzie mafanikio maana mtu kama Diamond anaposafiri kikazi ujue ndio anaingiza mkwanja na pia anajitangaza yeye na nchi yetu kiujumla No, nafurahi anaposafiri na ninamtakia mafanikio mema ila nataka ujue tu kuwa nikutokana na jinsi tulivyoshibana na kuzoeana na sio mimi pekee yangu hata yeye nikisafiri hapati usingizi ni simu hadi kunakucha alisema mwanadada huyo.




SERIKALI YA MAPINDUZI ZANZIBAR (SMZ) YARUHUSU SHEIKH WA UAMSHO AZZAN KHALID HAMDANI KWENDA KUTIBIWA NJE YA NCHI

Sheikh Azzan Khalid Hamdani
Wizara ya Afya Zanzibar imeruhusu mshtakiwa wa nne, Kiongozi Mwandamizi wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislam (Jumiki), Sheikh Azzan Khalid Hamdani (56), kupelekwa nje kutibiwa baada ya kukosekana tiba ya maradhi yanayomsumbua visiwani hapa.

Sheikh Azzan alilazwa Hospitali ya Rufani ya Mnazi Mmoja kuanzia Septemba Mosi, mwaka huu baada ya kupoteza nguvu akiwa Gereza la Kiinua Miguu na imebainika anasumbuliwa na vijiwe kwenye figo.

Kuruhusiwa kwa Sheikh Azzan kupata tiba nje, kumethibitishwa na wakili wake, Salum Towfiq mbele ya Naibu Mrajisi wa Mahakama Kuu Zanzibar, Yesaya Kayange.

Wakili Towfiq alisema mteja wake hali yake siyo nzuri, amepata barua ya Wizara ya Afya Zanzibar kwamba maradhi yanayomsumbua hayatibiki Zanzibar na kutaka mwongozo.

Licha ya ombi hilo, Wakili Tawfiq aliwasilisha malalamiko kuwa wateja wake wananyanyaswa, ikiwamo kutopata nafasi ya kuwasiliana na familia zao kupitia simu na wanapokuwa kwenye mazingira ya Mahakama.

Alidai Chuo cha Mafunzo Zanzibar (Magereza) kimewawekea utaratibu wa kukutana na familia zao mara mbili kwa mwezi, huku akiomba Mahakama itoe mwongozo.

Pia, alidai hata wanafamilia wanapotaka kwenda mahakamani kusikiliza mwenendo wa kesi hukumbana na misukosuko na kushindwa kuingia ukumbini kutokana na kuimarishwa ulinzi na kuzuia njia za kuingia na kutoka.

Hata hivyo, Kayange alisema ombi la kwanza la matibabu ya mshtakiwa liko nje ya uwezo wake na kutaka liwasilishwe Mahakama Kuu. Pia, katika ombi la pili alikitaka Chuo cha Mafunzo Zanzibar kuwatendea haki washtakiwa kwa mujibu wa taratibu na sheria. Kayange aliahirisha kesi hiyo hadi Oktoba 7.


PAMBANO LA SIMBA NA MGAMBO LAINGIZA SHILINGI MILIONI 58


Mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Simba na Mgambo Shooting Stars iliyochezwa jana 18/09/2013 katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 58,365,000.

Watazamaji 10,241 walikata tiketi kushuhudia mechi hiyo namba 23 ya VPL msimu wa 2013/2014 iliyomalizika kwa wenyeji Simba kuibuka na ushindi wa mabao 6-0.

Viingilio katika mechi hiyo vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 13,839,327.45 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 8,903,135.59.

Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 7,036,946.16, tiketi sh. 2,548,890, gharama za mechi sh. 4,222,167.70, Kamati ya Ligi sh. 4,222,167.70, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 2,111,083.85 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 1,641,954.10.

MIKATABA YA MAKOCHA VPL, FDL YATAKIWA TFF

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limetoa siku 14 kwa klabu za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) na za Ligi ya Daraja la Kwanza (FDL) kuwasilisha mikataba ya makocha wao.

Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya TFF iliyokutana Septemba 12 mwaka huu imebaini klabu nyingi hazijawasilisha mikataba ya mabenchi yao ya ufundi, kitu ambacho ni matakwa ya kikanuni. Siku hizo 14 zimetolewa kuanzia Septemba 17 mwaka huu.

Kwa klabu ambazo zitashindwa kuwasilisha mikataba hiyo na vielelezo vingine ndani ya mudau huo zitachukuliwa hatua kwa mujibu wa kanuni.
Boniface Wambura Mgoyo
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)


JESHI LA POLISI KUFANYA OPERESHENI MAALUMU KATIKA MAKUTANO YA BARABARA ZOTE ZA DAR


Kamanda Kova

Jeshi la Polisi Kanda maalum ya Dar es salaam limetangaza operesheni maalum ya kuwaondoa ombaomba na wafanyabiashara katika makutano yote ya barabara kuu jijini Dar es salaam kutokana na kuwa kikwazo kiusalama wakati wa kupambana na wahalifu.

Kamishna wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es saalam DCP Suleiman Kova amesema uwepo wa watu wasiokuwa na shughuli maalum pembezoni mwa barabara katika makutano mbalimbali jijini kumekuwa kukikwamisha askari kutekeleza wajibu wao kama ipasavyo hasa vinapotokea vitendo vya uhalifu. 

Akizungumza jijini Dar es salaam baada ya kuwatunukia Nishani maofisa wa polisi waliotumikia jeshi hilo kwa zaidi ya miaka 35 kwa kanda maalum ya Dar es salaam Kamishana Kova amesema dhamira ya jeshi hilo ni kuacha wazi makutano yote ya barabara na kudhibiti uhalifu.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Said Meck Sadick amesema zoezi hilo la kuwaondoa ombaomba ni endelevu na linalenga kuliweka jiji la Dar es salaam katika hali ya usafi.


MNIGERIA ASHINDA MISS WORLD MUSLIMAH 2013

Binti wa kinigeria Obabiyi Aishah Ajibola mwenye umri wa miaka 21, jana ametangazwa kuwa mshindi wa shindano la Miss World Muslimah wa mwaka 2013 lililofanyika mjini Jakarta,Indonesia.

Mabinti 20 kutoka nchi sita ndio waliofanikiwa kuingia fainali ambapo washiriki wote walivaa hijabu na mavazi yaliyostiri maungo yao. 

Baada ya kuonesha watazamaji na wasomi wa kiislamu, jopo la majaji lilimchagua Obabiyi Aishah Ajibola kutoka Nigeria kuwa mshindi. 

Vigezo vilivyotumika kumpata mshindi ni Ufasaha wa kusoma Qurani na Maoni yao juu ya Uislamu katika Dunia ya kisasa. Baada ya kusikia jina lake kama mshindi Obabiyi Aishah Ajibola, alilia kwa furaha na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa yeye kuwa mshindi. “Jambo hili hasa si kushindana bali sisi tunajaribu tu kuonesha Dunia kwamba Uislamu ni mzuri” alisema Aishah.

Eka Shanti ambaye ndiye aliyeanzisha shindano hili miaka mitatu iliyopita, baada ya kupoteza kazi yake ya utangazaji wa Televisheni kwa kukataa kuvua Hijabu akiwa anatangaza, anasema, "Mwaka huu tumefanya makusudi lianze shindano letu kabla ya Miss World ili kuonesha kwamba kuna jambo mbadala na mfano wa kuigwa kwa wanawake wa kiislamu.”

Shindano hili lilianza mwaka 2011 likiwa na jina tofauti lilishirikisha waindonesia peke yake. Shanti anasema baada vyombo vya habari kulinganisha na Miss World tulibadilisha jina na tulikubali kuweka wagombea wa kigeni mwaka huu. Washiriki wa nje ya Indonesia, walitoka nchi za  Iran, Malaysia, Bangladesh, Brunei, na Nigeria.


ARSENAL YAPATA USHINDI UGENINI KWA KUWAFUNGA WENYEJI WAO MABAO 2 - 1





Wachezaji wa Arsenal Theo Walcott na Aaron Ramsey jana usiku waliiwezesha timu yao kupata ushindi mzuri ugenini pale walipokwamisha nyavuni mabao yao mawili dhidi ya moja la wenyeji wao Marseille na kuihakikishia timu yao ushindi wa mabao 2-1, katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Katika mchezo huo ambao ulikuwa na ushindani mkubwa, Arsenal ndiyo walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Walcott dakika ya 65 kabla ya kuongeza la pili dakika ya 83 lililofungwa na Ramsey.
Marseille walipata bao la kufutia machozi dakika ya 90 kwa njia ya penalti baada ya ndugu yake Andrew Ayew, Jordan Ayew kuangushwa kwenye eneo la hatari na Mwamuzi kuamuru adhabu ya Penati.


SIMBA YAONESHA MAKUCHA YAKE NA KUTOA KIPIGO CHA MBWA MWIZI KWA KUWACHAPA MGAMBO BAO 6 KWA SINIA.


Mshambuliaji wa Simba Betram Mwombeki akichuana na mlinzi wa Mgambo JKT Bakari Mtama wakati wa mchezo wa ligi kuu baina ya timu hizo uwanja wa taifa jijini Dar es Salaam hapo jana. Matokeo ya mchezo huo ni kama yanavyoonekana katika picha ya ubao wa matangazo hapo chini .



Timu ya Simba ya Dar es Salaam jana katika Uwanja wa Taifa imedhihirisha umwamba wake mbele ya Mgambo Shooting inayomilikiwa na JKT kwa kuicharaza mikwaju 6 - 0 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Soka Tanzania bara.  .



Magoli ya Simba yaliyo fungwa na Hamis Tambwe aliyefunga goli 4 na Haruna Chanongo goli 2 yameiwezesha Simba kushika usukani wa Ligi kwa kuishusha hadi nafasi ya pili timu ya JKT Ruvu ambayo  imecharazwa bakora 1 na Ruvu Shooting, bao la Ruvu liliwekwa kimiani na Cosmas Nyalusi "Baloteli".



Wakati Simba ikishangilia karamu hiyo ya Magoli imekuwa ni Mwiba kwa mahasimu wao Yanga ambapo wametoka sare kwa mara nyingine tena na Prisons "Wajelajela" baada ya kutoshana nao nguvu kwa bao 1 - 1.
 Yanga ikiwa bado na kumbukumbu ya kutoka sare mchezo wao na Watoto wa Mbeya Mjini "Mbeya City"ndiyo waliokuwa wakwanza kupata bao kupitia kwa Gerry Tegete kwa kifua baada ya kutokea piga nikupige kwenye lango la Prisons.

Ndani ya Chamazi Complex kama wanavyouita uwanja wao Azam FC nao wamepigwa na bumbuazi baada ya Ice-Cream zao kuyeyushwa na watoto wa mjini Ashanti United kwa sare ya 1-1. Wafungaji wa mabao hayo wakiwa ni Kipre Herman Chetche wa Azam na Anthony Matangalu wa Ashanti.


Huko Kwa wakata Miwa wa Kagera, ndani ya Kaitaba Bukoba, Kagera Sugar wamepata ushindi wao wakwanza baada ya kuifunga JKT Oljoro kwa bao 2 - 1, wafungaji wa mabao hayo ni Geofrey Aswile na Malegesi Mwangwa wa Kagera na Godfrey Nayopa wa Oljoro.


Mchezo mwigine ulio shuhudia sare ni ule wa Wakata Miwa wa Turiani Mtibwa Sugar iliyo toka sare ya bila kufungana na watoto wa Mbeya City.


Wagosi wa Kaya Coastal Union ya Tanga nayo imekutana na "wajeda" kutoka Tabora, Rhino Rangers na kutoka sare ya 1-1 wakiwa Mkwakwani.


Wednesday, September 18, 2013

KASEJA AJIUNGA NA ASHANTI AKITOKEA NDANDA FC YA DARAJA LA KWANZA

NAHODHA wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars Juma Kaseja amejiunga na timu ya Ashanti United ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara akitokea timu ya Ndanda FC inayocheza daraja la kwanza kama  kocha wa makipa wao na anatarajiwa kuanza kuichezea rasmi Januari mwakani, baada ya kuchelewa dirisha la usajili.
Kocha wa makipa wa timu hiyo ya Ilala, Dar es Salaam, Iddi Pazi ‘Father’ amesema jana kwamba Kaseja amejiunga na Ashanti United na amekwishaanza kazi.
Father, alisema kwamba pamoja na Kaseja, pia Ashanti imempata kipa mwingine mzoefu, Amani Simba SC ambaye naye amekwishaanza mazoezi.
“Nipo na Amani Simba na Juma Kaseja hapa Ashanti, naamini wote ni makipa wazuri na watachuana ili kurejea matawi ya juu. Nitawafanyia kazi na watakuwa makipa bora tena,”alisema Pazi, baba wa mshambuliaji wa Simba SC, Zahor Pazi.
Kaseja aliachwa Simba SC mwishoni mwa msimu baada ya kuitumikia timu hiyo tangu mwaka 2003 alipojiunga nayo akitokea Moro United.
Baada ya hapo, alipata ofa ya kwenda St. Eloi Lupopo ya DRC, lakini wakashindwa kuafikiana na kuamua kuangalia ustaarabu mwingine. Wakati wa maandalizi ya msimu mpya, Kaseja alikuwa akifanya mazoezi na Mtibwa Sugar iliyokuwa imeweka kambi Dar es Salaam.
Juhudi za kumpata Kaseja mwenyewe kuthibitisha kujiunga kwake na Ashanti hazikuweza kufanikiwa mapema.



WABUNGE WA NIGERIA WAPIGANA BUNGENI

Wabunge wa bunge la waakilishi Nigeria wamerushiana ngumi wakati wa vikao vya Jumanne baada ya kuzuka bungeni suitofahamu kuhusu mrengo wa wabunge waliojitenga na chama tawala. Taarifa hizi ni kwa mujibu wa vyombo vya habari nchini humo.

Kituo kimoja cha kibinafsi cha televisheni, pamoja na vituo vingine vilionyesha picha za mbunge mwanamke akimtosa kidole usoni kwa ghadhabu mbunge mwenzake wakati mbunge mwanamume akionekana akichukua kiti nusura kumgonga mwenzake.
Taarifa zinazohusiana

    Siasa

Wabunge wengine walionekana wakipigana ngumi.

Mgogoro inasemekana ulianza baada ya mwenyekiti wa mrengo wa wabunge waliojiondoa kutoka kwa chama tawala, Kawu Baraje, kuingia bungeni akiandamana na magavana wanaomuunga mkono.

Inaarifiwa spika wa bunge la waakilishi ,Aminu Tambuwal, aliambia wabunge kuwa Baraje aliomba ruhusa kuwahutubia wabunge wa mrengo wake kabla ya bunge kuanza vikao vyake.

Lakini kuwepo kwa wabunge hao bungeni kuliwaghabisha mno wafuasi wa chama tawala, PDP,kiasi cha kuzuka sokomoko bungeni kati ya pande hizo mbili na kumlazimisha bwana Baraje kukatiza hotuba yake kutokana na kelele bungeni.

Chama tawala PDP kina wabunge wengi zaidi bungeni wakiwa 23 kati ya wabunge wote 36

Aidha chama hicho kimetawala Nigeria tangu kupata uhuru mwaka 1999 lakini hivi kribuni kimezongwa na migogoro ya ndani ya chama pamoja na kukabiliwa na upizani wenye ushawishi.

Wananchi wanajiandaa kwa uchaguzi mwaka 2015, lakini wadadisi wana wasiwai ikiwa chama tawala kitakuwa kimesuluhisha migogoro yake, huku kikikabiliwa na upinzani mkali.

Mgogoro huu umekuwa ukitokota kwa miezi kadhaa huku baadhi ya wabunge wakitofautiana kuhusu ikiwa Rais Goodluck Jonathan aidhinishwe na chama kugombea urais kwa mara nyingine wakati kuna wanasiasa wengine wanaotaka kugombea urais.

Hii ni mara ya kwanza kwa wabunge wa Nigeria kurushiana ngumi bungeni.

CHQNZO: BBC SWAHILI


MWIMBAJI WA ZANZIBAR NJEMA MODERN TAARAB PRINCE AHMED MGENI AFARIKI DUNIA




AHMED MGENI WAKATI WA UHAI WAKE KATIKA PICHA TOFAUTI JUU HAPO



MSANII wa muziki wa Taarab Prince Ahmed Mgeni amefariki dunia alfajiri ya leo Visiwani Zanzibar.

Mgeni alikutwa na umauti huo baada ya kuugua TB ya tumbo kwa muda mrefu anatarajiwa kuzikwa leo visiwani humo.

Enzi za uhai wake msanii huyo aliyepata kuimba katika bendi mbalimbali sambamba na kutoa nyimbo kadhaa zilizoteka alikutwa na umauti huo Alfajiri saa kumi ya kuamkia leo alipokuwa amelazwa katika hospitali ya Mnazi mmoja, Zanzibar.

Mwezi April mwaka huu 2013 mwimbaji huyo alizushiwa kifo baada ya hali yake kuwa mbaya

Moja ya kibao kilichompatia umarufu kilijulikana kama Sitetereki "Mlinzi wa kweli ni Mungu aso hiyana na mtu sio wewe mlimwengu hunibabaishi kitu.....

Mwili wa Msanii huyo umeishatolewa hospitali tayari kwa maziko saa kumi jioni leo nyumbani kwa Baba yake Amani Fresh - Zanzibar

'INNALILAHI WAINNAILAIHI RRAJIUN' 


POLISI WAWILI WAKAMATWA WAKISAFIRISHA RISASI 3, 000

Polisi wawili wa Musoma, Mkoa wa Mara na Kibaha, Pwani wanashikiliwa kwa tuhuma za kukutwa wakisafirisha risasi 3,000 kutoka Musoma kwenda Dar es Salaam.

Wanaoshikiliwa kwa tuhuma hizo ni aliyekuwa mtunza chumba cha silaha Kikosi cha FFU Musoma na mwenzake mwenye cheo cha Koplo Wilaya ya Kibaha, Pwani. Inadaiwa walikamatwa Juni 2, mwaka huu saa 11:00 alfajiri.
Watuhumiwa wanashikiliwa Kituo cha Polisi Musoma na wamefunguliwa jalada MUS/RB/2465/013 wizi wa risasi 1,056, wanasubiri taratibu zingine za polisi.

Habari zinadai shehena hiyo ilisafirishwa kwa kutumia pikipiki hadi Kituo cha Mabasi, lakini polisi tayari walikuwa wameweka mtego baada ya kupata taarifa kuhusu wizi huo.

Taarifa kutoka vyanzo mbalimbali ikiwamo wahusika wa basi na nyumba moja ya kulala wageni iliyopo jirani na stendi, baadhi ya askari waliovaa kiraia walionekana maeneo hayo mapema.
Kwa mujibu wa habari za uhakika kutoka ndani ya polisi, Koplo huyo alikutwa na shehena hiyo karibu na kituo cha mabasi ya Kampuni ya Mohammed Trans, akijiandaa kuelekea Dar es Salaam ambako inasemekana wana wateja wao.
Inadaiwa koplo huyo aliomba ruhusa ya ugonjwa kazini kwake na kuitumia kusafiri hadi Musoma kuchukua mzigo huo, inadaiwa biashara yao hiyo ni ya muda mrefu na wana mtandao na watuwanaojihusisha na uhalifu.
Mtandao huo unadaiwa kuwagusa baadhi ya polisi Mkoa wa Tarime na Rorya, ambao huwauzia watu wanaojihusisha na uhalifu wa kutumia silaha.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Absalom Mwakyoma alipotafutwa kwa simu zake za mkononi licha ya kuitwa, hazikupokewa.

Hata hivyo, aliomba atumiwe ujumbe, licha ya kupelekewa huo ujumbe, hakujibu ingawa taarifa zinadai ameanza likizo ya kustaafu hivi karibuni.
Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Mara, Jafari Mohammed alipoulizwa kuhusu tukio hilo, alikanusha kufahamu suala hilo huku akigeuka kuwa mkali kwa mwandishi.
“Hilo mimi silijui, nani kakwambia wewe… askari kukutwa na risasi mfukoni ni jambo la kawaida huenda ni uzembe tunamshughulikia kwa uzembe,” alisema.

CHANZO: Mwananchi



 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU