Facebook Comments Box

Wednesday, August 28, 2013

YANGA WATOKA SARE NA COASTAL UNION: MWAMUZI ALAUMIWA KWA KUSHINDWA KUMUDU MCHEZO


Young Africans imetoka sare ya bao 1-1 dhidi ya timu ya Coastal Union kutoka mkoani Tanga kufuatia bao la kusawazisha la penati ya utata dakika ya 90 ya mchezo la kiungo Jerry Santo baada ya Didier Kavumbagu kuifungia Yanga bao la kwanza.
Coastal Union ambayo katika mchezo wake wa awali dhidi ya JKT Oljoro ilipata  ushindi wa bao 2-0, ilicheza mchezo mbovu tangu mwanzo mwa mchezo hali iliyopelekea mwamuzi Martin Sanya ashindwe kulimudu pambano.
Yanga iliuanza mchezo kwa kasi kwa lengo la kusaka bao la mapema lakini kutokua makini kwa washambuliaji wake Jerson Tegete, Didier Kaumbagu na Simon Msuva kuliifanya ishindwe kupata bao kwa dakika 45 za kipindi cha kwanza.
Haruna Moshi 'Boban'  na Said Nyosso walionyeshwa kadi za njano katika kipindi cha kwanza kufuatia kuwachezea ndivyo sivyo wachezaji wa Yanga, ambapo wachezaji hao wa Coastal walishindwa kuonyesha soka la uungwana.
Kipindi cha pili cha mchezo kilianza kwa Yanga kufanya mabadiliko kwa kuwaingiza Hussein Javu na Hamis Thabit waliochukua nafasi za Jerson Tegete na Salum Telela aliyeumia katika kipindi cha kwanza.
Mabadiliko hayo yaliongeza uhai kwa timu ya Yanga kwani katika dakika ya 69 mshambuliaji Didier Kavumbagu aliipatia Young Africans bao la kwanza akimalizia pasi safi ya mlinzi wa pembeni David Luhende aliyewazidi uwezo walinzi wa Coastal Union na kumpasia mfungaji.
Baada ya kupata bao hilo Yanga waliendelea kufanya mashambulizi kupitia kwa washambuliaji wake Hussein Javu na Didier Kavumbagu lakini walinzi wa waliendelea kucheza ndivyo sivyo kwa wachezaji wa Yanga kana kwamba wanacheza mchezo wa mateke na ngumi.
Katika hali iliyowastaabisha wengi mwamuzi alimpatia kadi nyekundu Saimon Msuva baada ya kuchezewa vibaya na mlinzi wa Coastal Abdi Banda, huku watu wakisubiria mwamuzi amuadhibu Banda alimpatia kadi Msuva na kiungo wa Coastal Crispin Odula.
Dakika ya 90 mwamuzi Martin Sanya aliipatia Coastal Union penati ya utata kufuatia kiungo Haruna Moshi 'Boban' kumdanganya mwamuzi kuwa mlinzi Nadir Haroub 'Cannavaro' ameunawa mpira ndani  ya eneo la hatari na penati hiyo ilipigwa na Jerry Santo na kuwapatia bao la kusawzisha.
Mpaka dakika 90 za mchezo zinamalizika Young Africans 1 - 1 Coastal Union.
Mara baada ya mchezo kocha mkuu wa Yanga Ernie Brandts amemtupia lawama mwamuzi wa mchezo Martin Sanya kwa kushindwa kuumudu mchezo na kusema katika mchezo wa  amekuwa mchezaji bora baada ya kushindwa kulimudu pambano.
Young Africans: 1.Ally Mustapha 'Barthez', 2.Juma Abdul, 3.David Luhende, 4.Nadir Haroub 'Cannavaro' 5.Mbuyu Twite, 6.Salum TelelaHamis Thabit , 7.Saimon Msuva, 8.Frank Domayo, 9.Didier Kavumbagu, 10.Jerson Tegete/Hussein Javu, 11.Haruna Niyonzima.
Coastal Union: 1.Shaban Hassan 'Kado', 2.Juma Hamada, 3.Abdi Banda, 4.Marcus Ndehele, 5.Juma Nyosso, 6.Jerry Santo, 7.Uhuru Seleman/Seleman Kassim, 8.Haruna Moshi 'Boban', 9.Lutimba Yayo/Kenneth Masumbuko, 10.Crispin Odula, 11.Danny Lyanga/Razack Khalfani


MSIMAMO WA LIGI KUU YA TANZANIA BAADA YA MECHI ZA LEO

Yanga 1 - 1 Coastal Union
Simba 1 - 0 JKT Oljoro
Mtibwa 1 -0 Kagera 0
Rhino Rangers 0 - 2 Azam FC
Mgambo 1 - 0 Ashanti United
 Mbeya City 2  - 1  Ruvu Shooting
JKT Ruvu 3 - 0 Prisons


PICHA YA LEO: WANAWAKE WANAWEZA

Mhandisi wa kike akikagua jengo kwa umakini na ufasaha



VIDEO: KAMA HUKUONA MAGOLI YA ARSENAL WALIVYO ITUNGUA FENERBACHE HAYA HAPA




104.5 RADIO IMAAN FM YARUDI HEWANI ILI KUKUTOA KWENYE GIZA NA KUKUPELEKA KWENYE MWANGA

Ustadh Ally Ajiraan akitoa maelezo baada ya RAdio Imaan kurudi hewani

Sheikh Hamza akiwa na Br Arif Nahdi studio baada ya radio Imaan kurudi hewani








Tuesday, August 27, 2013

ZITTO: SITOGOMBEA URAIS WALA UBUNGE 2015

Photo: Zitto: Sitogombea Urais wala Ubunge 2015

- Asema mwaka 2015, ndio mwaka wa mwisho kujihusisha na siasa ambapo dhamira yake ni kutafuta chuo ambacho ataweza kufundisha masomo ya uchumi na maliasili
- Adai ni bora akalime michikichi kuliko kuendelea kushiriki siasa...

Endelea kusoma zaidi => http://bit.ly/1cbWgRh
MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Bw. Zitto Kabwe (CHADEMA), amesema hafikirii kugombea urais kwa tiketi ya chama hicho wala ubunge katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2015.

Alisema mwaka 2015, ndio mwaka wa mwisho kujihusisha na siasa ambapo dhamira yake ni kutafuta chuo ambacho ataweza kufundisha masomo ya uchumi na maliasili.

Bw. Kabwe aliyasema hayo hivi karibuni katika mahojiano maalumu  siku chache baada ya viongozi 105 kutoka Vyuo Vikuu 30 nchini, kupendekeza majina ya wanasiasa wanaofaa kuwania urais mwaka 2015.

Jina la Bw. Kabwe, lilishika nafasi ya pili katika mchujo huo ambapo Mbunge wa Bumbuli, mkoani Tanga ambaye pia ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Bw. January Makamba, alishika nafasi ya kwanza kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mwanasiasa aliyeshika nafasi ya tatu katika mchujo huo alikuwa Mbunge wa Ubungo, Dar es Salaam, Bw. John Mnyika (CHADEMA).

"Hiki ni kipindi cha mwisho kwangu kujihusisha na siasa kwani nimechoka nazo, nitatafuta chuo nikafundishe na kama nitakosa ni bora nikalime michikichi... sihitaji urais," alisema.

Katika mkutano wa wanafunzi hao, walisema Bw. Makamba ana sifa zote za kuwa rais wa nchi kama atagombea nafasi hiyo mwaka 2015 ili aweze kulikomboa Taifa ambalo hivi sasa linakabiliwa na matukio mengi ya uvunjifu wa amani.

Wanafunzi hao walikwenda mbali zaidi na kuyataja baadhi ya matukio hayo kuwa ni pamoja na vurugu, kutekwa kwa watu wasio na hatia, kufanyiwa vitendo vya ukatili, kumwagiwa tindikali na kupungua kwa mtangamano wa kijamii.

Mwenyekiti wa mkutano huo ambao ulifanyika mkoani Morogoro ambaye pia ni Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Kampasi ya Mbeya, Bw. Theonest Theophil, alisema Bw. Makamba alipata kura 72 ambapo Bw. Kabwe alipata kura 20.

Bw. Theophil alisema sifa za kiongozi wanayemtaka kwanza awe kijana mwenye fikra mpya, atakayeleta matumaini mapya, kuwaunganisha Watanzania, asiyeendekeza siasa za kikanda, mdini na mkabila.

Sifa nyingine ni kiongozi mwadilifu asiye na rekodi ya kutuhumiwa mahali popote kwa vitendo viovu, mtulivu, mwenye busara na anayepima kauli zake.


PICHA: SAMAKI SAMAKI MBEZI - MAKONDE YATEKETEA KWA MOTO


Kiota cha starehe jijini Dar es Salaam maarufu kama Samaki Samaki tawi la Mbezi leo kimeteketea kwa moto.Moto huo umesababishwa na shoti ya umeme.





WANAUME WAWILI WAKUBALIANA KUOA MKE MMOJA


Mwendwa ni mmoja wa wanaume hao walioamua kugawana mke mmoja.

Wanaume wawili nchini Kenya wameibuka na mbinu isiyo ya kawaida ya kupata suluhu ya kupigania mwanamke ambaye wote wanampenda Wamesaini mkataba wakikubaliana kuishi nae kwa zamu.
Silvester Mwendwa ni mmoja wa wanaume hao. Ameeleza BBC kwanini binafsi anamuhusudu mwanamke huyo.
Mmoja ya wa wanaume hao alisema haoni ubaya wowote kwa yeye na mwenzake kumuoa mwanamke mmoja.
Amehoji sheria ya sasa inayoruhusu wanaume kuoa wanawake wengi na wakati huo huo kuharamisha mpango kama huo kwa kina mama.
Sylvester Mwendwa anasema wazazi wake wamekubali na mpango wake na wako tayari kumtolea mahari.
Wanaume hao wawili walikubali kumuoa mwanamke huyo baada ya kugundua kwamba kumbe wote wana uhusiano wa kimapenzi naye.
Na kumbe mwanamke huyo alikuwa ameahidiana na kila mmoja wao kwamba angelifunga nao ndoa bila ya wao kujuana.
Lakini walipogunduana , ilikuwa ni ugomvi wa mara kwa mara lakini mwanamke huyo alipoambiwa amchague mnmoja wao, alishindwa. Akasema anawapenda wote wawili.
Na baada ya hapo watatu hao waliafikiana kusaini mkataba ambao utaruhusu wanaume hao wawili kuishi na mwanamke huyo kama bwana na bibi ila kila mmoja wao atakuwa na wakati wake wa 'kwenda kumjulia hali.'
Vile vile mkataba huo unawashurutisha kugawana majukumu yote ya nyumbani ikiwa ni pamoja na kuwalea watoto na kutowabagua kwa kuwa wote watakuwa na haki sawa.
Hata hivyo kwa mujibu wa sheria za kenya ni haramu kwa mwanamke kuolewa na wanaume wawili na mkataba huo sasa umeibua mjadala mkali wa kisheria, huku sheria mpya ya ndoa ikitarajiwa kujadiliwa na kuidhinishwa bungeni.

CHANZO: BBC SWAHILI


CCM WAMFUKUZA UWANACHAMA MBUNGE WAO

Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete akiongoza kikao cha NEC, mjini Dodoma leo mchana. Kushoto ni Katibu Mkuu wa CCM Abdulrahman Kinana.


 HALMASHAURI Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) leo imemaliza kikao chake cha siku tatu chini ya Mwenyekiti wake, Rais Jakaya Kikwete ikiwa imeridhia mapendekezo kadhaa ya Kamati Kuu ya CCM, ikiwemo kumfuta uongozi Mbunge wa jimbo la Mjini Magharibi, Zanzibar, Mansor Yusuf Himid. 

 Kufuatia hatua hiyo, CCM itatoa taarifa kwa Spika wa Baraza la Wawakilishi kuondoa udhamini wake kwa mwanachama huyo kama Mjumbe wa Baraza hilo kwa jimbo la Kiembesamaki.

 Kikao hicho pia kimeridhia, uteuzi wa Makatibu wateule wapya wa Jumuia za CCM, za Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Jumuiya ya Wazazi na Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT).

 Hatua hiyo itamfanya Spika wa Baraza hilo kutangaza kiti cha jimbo hilo kuwa wazi na kuitishwa uchaguzi mdogo wa kugombea nafasi hiyo.

 Mjumbe wa kamati kuu ya halmashauri kuu ya CCM Taifa Daud, Ismail akizungumza na Zenji FM radio amesema kikao hicho kimefikia uamuzi huo baada ya kupokea madai ya mkoa wa Magharib kutaka mwanachama huyo afukuzwe kwa madai ya kupinga sera ya Serikali mbili ya Muungano inayoungwa mkono na CCM. 

 Hata hivyo Himid ambaey pia ni mjume wa kamati ya maridhiano Zanzibar, endapo hajaridhishwa na uamuzi wa kufukuzwa kwake anaweza kukata rufaa Mahakama Kuu kupinga uamuzi huo.

 Himid aliwahi kuwa Waziri asiekuwa na Wizara ya Maalum katika awamu ya saba ya uongozi inayongozwa na Dk Ali Mohammed Shein. Pia aliwahi kuwa Naibu Waziri wa Wizara ya Kilimo kabla ya kuwa Waziri wa Maji Ujenzi, Nishati na Ardhi katika Utawala wa rais Amani Abeid Karume. 

Himid alionekana kichocheo kutaka kuliondoa suala na mafuta na gesi asilia kwenye orodha ya Mambo ya Muungano pamoja na kuchukizwa na matatizo ya Muungano yanayoikandamiza Zanzibar. 

Hivi karibuni mwenyekiti wa Kamati ya Maridhiano, Mzee Hassan Moyo alisema kufukuzwa kwa Himid hakutathiri shughuli za Kamati hiyo katika kutetea Muungano wa mkataba. 

UTEUZI 

 Kikao hicho pia kimeridhia, uteuzi wa Makatibu wateule wapya wa Jumuiya za CCM, za Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Jumuia ya Wazazi na Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT). 

 Katika uteuzi huo mapendekezo hayo yaliyofanywa na Kamati Kuu ya CCM na kuridhiwa na NEC, kwa upande wa UVCCM ameteuliwa aliyekuwa Kaimu Katibu wa CCM mkoa wa Morogoro, Sixtus Mapunda na kwa upande wa Jumuia ya Wazazi ni Mjumbe wa NEC kutoka Pemba, Seif Shabani Mohamed, huku kwa upande wa UWT akiachwa Katibu Mkuu wa sasa, Amina Makilagi. 

Mapunda atachukua nafasi iliyokuwa imneshikiwa na Martine Shigela ambaye ameongoza UVCCM kwa miaka mitano sasa, na Seif Shabani Mohammed kutoka Pemba akichukua nafasi iliyokuwa ikishikiliwa na Hamis Suleiman Dadi ambaye pia amekuwa katika wadhifa kwa miaka mitano sasa. 

Pia, NEC imeridhia mapendekezo ya Kamati Kuu kwa ajili ya kuziba nafasi Makatibu wa CCM wa mikoa mitatu ya Morogoro, Kaskazini Pemba na Geita ambayo kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa imekuwa wazi kwa muda mrefu sasa kutrokana na sababu mbalimbali ikiwemo kifo. 

 Kufuatia mapendekezo hayo ya Kamati Kuu, ambayo yameridhiwa na NEC, walioteuliwa na mikoa yao ikiwa kwenye mabano ni Msaidizi Kitengo cha Uchaguzi, CCM Ofdisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Romuli Rojas John (Morogoro), aliyekuwa Katibu Katibu wa wilaya ya Mkinga, Kassim Mabrouk Mbarak (Kaskazini Pemba) na aliyekuwa Katibu wa CCM Igunga, Mary Maziku (Geita). 

Kuhusu sakata la madiwani wa Bukoba mjini, CCM imesema suala hilo, linaendelea kushughulikiwa ambapo baada ya kikao hicho cha NEC, Kamati kuu iliendelea kukutana na viongozi wa wilaya ya Bukoba, Mwenyekiti wa CCM na Katibu wa wilaya hiyo.

 Mapema kabla ya kikao cha NEC, Kamati Kuu ilikutana na Mbunge wa Bukoba mjini Khamis Kagasheki na Meya wa Manispaa ya Bukoba mjini na kuwahoji, wakati jana Kamati Kuu ilikutana na Mwenyekiti na Katibu wa CCM mkoa wa Kagera. 

 Taarifa Rasmi ya CCM ya majina ya Makatibu wa Wilaya walioteuliwa na NEC 

Ndugu Ashura Amanzi 
Ndugu Rukia Saidi Mkindu
Ndugu Elias J. Mpanda
Ndugu Jonathan M. Mabihya 
Ndugu Mulla Othman Zuberi 
Ndugu Jumanne Kapinga
Ndugu Ali Haji Makame
Ndugu Jacob G. Makune 
Ndugu Juma A. Mpeli
Ndugu Hawa Nanganjau
Ndugu Abdulrahman Shake 
Ndugu Subira Mohamed Ameir 
Ndugu Abdallah Shaban Kazwika 
Ndugu Juma Bakari Nachembe 
Ndugu Josephat Ndulango 
Ndugu Rajab Uhonde
Ndugu Abeid Maila 
Ndugu Mohamed Lawa 
Ndugu Mariam Sangito Kaaya 
Ndugu Bakar Lwasa Mfaume 
Ndugu Julius Peter 
Ndugu Jumanne Kitundu Mginga 
Ndugu Mathias Nyombi 
Ndugu Mohamed Hassan Moyo


Monday, August 26, 2013

HII NDIO TAREHE AMBAYO RADIO IMAAN ITARUDI HEWANI

Tv Imaan ikiwa kazini wakati wa sala ya Idd wakimuhoji Mwenyekiti wa Islamic Foundation Br Arif Nahdi

Mtaalam wa Mitambo wa Radio Imaan na Tv Imaan Muhammad Maembe akimuelekeza Mwenyekiti wa Islamic Foundation Br Arif Nahadi mitambo inavyofanya kazi katika jengo jipya la makao makuu ya Radio na Tv Imaan

Mwenyekiti wa Radio Imaan Br Arif Nahdi akikagua jengo jipya la Tv Imaan na Radio Imaan

Mwenyekiti wa Islamic Foundation Br Arif Nahdi akihojiwa na Radio MuM juu ya ujio wa Radio Imaan



SAKATA LA MADAWA YA KULEVYA: VIONGOZI NAO KUPEKULIWA KAMA ABIRIA WA KAWAIDA

KULIA: Uwanja wa ndege wa kimataifa wa Dar es Salaam. KUSHOTO: Dk Harrison Mwakyembe. 

Kuanzia sasa viongozi wote serikalini watakaopita kwenye viwanja vya ndege nchini, watakuwa wakikaguliwa kama abiria wengine, isipokuwa Rais, Makamu wake, Waziri Mkuu, Jaji Mkuu na Spika wa Bunge.
Waziri  wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe amesema ipo tabia ya  viongozi  wenye madaraka, kukiuka utaratibu na kupita   katika  viwanja vya ndege  bila kukaguliwa.Alisema kutokana na hali hiyo, amewaambia watumishi  wanaofanya kazi katika viwanja hivyo, hususan Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Julius Nyerere (JNIA) viongozi wasiokaguliwa ni Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Jaji Mkuu na Spika wa Bunge.

Alitoa msimamo huo wiki iliyopita  kupitia kipindi cha Jenerali on Monday, kinachorushwa na Televisheni ya Channel Ten. Alisema viongozi wengine wote, wakiwamo mabalozi na mawaziri lazima wakaguliwe.



Dk Mwakyembe alisema aliwaambia viongozi wasiopenda kukaguliwa, wasipande ndege. Alisema pamoja na baadhi kuona ni usumbufu, inawezekana wakajikuta wamesahau vitu hatari, kama vile risasi na wakaenda kugundulika nje ya nchi ikawa tatizo.

Alitoa mfano kwamba aliwahi kupigiwa simu na mmoja wa mabalozi, akilalamika kwamba vijana wake wamemkagua uwanja wa ndege. Alisema alimjibu kwamba wanatimiza wajibu wao.

Katika mahojiano yaliyojikita juu ya tatizo la  dawa za kulevya  nchini, Dk Mwakyembe alisisitiza  kwamba hatua alizoanza kuchukua kudhibiti upitishaji dawa hizo kwenye viwanja vya ndege, siyo moto wa kifuu wala nguvu ya soda.

 “Ninachokifanya hapa  ni kile ambacho kinapaswa kufanywa…na hili la dawa za kulevya katika viwanja vya ndege, nitalikomesha,” alisema. Alisisitiza kwamba udhibiti huo ni kwa viwanja vyote vya ndege nchini.

 Dk Mwakyembe alisema,  “kwa sasa mizigo yote inayoingia katika eneo hilo, lazima ikaguliwe, kwani huo sio mzaha, sio moto wa kifuu wala nguvu ya soda.”
Kwa mujibu wa Waziri, mizigo inayoingia imekuwa haikaguliwi. Alisema katika kutekeleza ukaguzi huo wa mizigo inayoingia, imenunuliwa  mitambo kwa  ajili hiyo.  Kuhusu wanaomeza dawa za kulevya,  alisema wamekuwa wakigundulika kutokana na ufuatiliaji kuanzia kwenye ndege.

Alitoa mfano kwamba  kwa sasa endapo abiria atapanda ndege katika uwanja wa ndege wa Dar es Salaam, mathalani kwenda Dubai, akipewa chai au pombe, akakataa kunywa,  kwa vyovyote huyo lazima akaguliwe zaidi.
Katika hilo, aliwaasa vijana wa Tanzania kujiepusha na hali hiyo, kwani pindi akishuka kwenye uwanja wowote, namba yake ya kiti itashikiliwa na atakaguliwa ipasavyo, kubaini kama amemeza dawa.

Hatua ya Mwakyembe kuamua kuvalia njuga dawa za kulevya, inatokana na kile ambacho kinaelezwa kuwa ni kuchafuka kwa Tanzania, kutokana na baadhi ya watanzania kukamatwa nje ya nchi, wakisafirisha dawa hizo, wakiwa wamezipitisha uwanja wa ndege.  Dk Mwakyembe alieleza kuwa hatua yake ya kuvalia njuga suala hilo, inaungwa mkono na serikali kwa ujumla. Hivi karibuni waziri huyo alifanya ziara ya ghafla  katika uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere na kubaini kuwa tatizo si vifaa vya ukaguzi, bali ni baadhi ya wafanyakazi wasio waadilifu. Msemaji Mkuu wa Serikali ambaye ni Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Assah Mwambene alisema hivi karibuni serikali imeanzisha mkakati wa kutokomeza wimbi la dawa za kulevya kwa kudhibiti viwanja vya ndege na sehemu mbalimbali za mipakani, zinazotumiwa kupitisha.
 


 

USISAHAU KU LIKE PAGE YETU