![]()  | 
| Mwasisi wa Chadema Edwin Mtei (mwenye kofia) akizungumza kwenye mkutano wa siku tatu wa Baraza la Kanda ya Kaskazini ya chama hicho jijini Arusha juzi | 
Mkutano 
wa Baraza la Uongozi la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) 
Kanda ya Kaskazini juzi uligeuka ukumbi wa ngumi, baada ya Mwenyekiti wa
 chama hicho Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba kushushiwa kipigo.
Mwigamba 
alishushiwa kipigo hicho na baadhi ya viongozi wenzake wa chama kwa 
madai ya usaliti na tayari amesimamishwa uongozi kwa muda usiojulikana.
Kamanda 
wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas jana alithibitisha kutokea kwa
 vurugu hizo na viongozi hao wa Chadema kufikishana polisi.
Alikutwa 
na zahama hiyo mbele ya viongozi wakuu wa Chadema Taifa, Mwenyekiti, 
Freeman Mbowe na mwasisi wa chama hicho, Edwin Mtei katika Hoteli ya 
Coridal Spring.
Viongozi 
hao wamekuwa wakifanya ziara za aina hiyo nchi nzima, kuimarisha chama 
na kujipanga kwa ajili ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwakani na 
uchaguzi mkuu ujao wa Rais na wabunge mwaka 2015.
Habari 
kutoka ndani ya mkutano huo zinaeleza kuwa hatua hiyo ilifuatia tuhuma 
kwamba Mwigamba alituma ujumbe kwenye mtandao wa kijamii wa Jamii 
Forums, unaodaiwa kukichafua chama hicho.
Tukio 
hilo la aina yake lilitokea wakati viongozi wote wa juu wa chama hicho, 
wakiongozwa na Mbowe walipokuwa wakijadili mustakabali wa chama hicho, 
mkutano ambao ulihudhuriwa na wabunge karibu wote wa Chadema wa kanda 
hiyo.
Hata 
hivyo, wakati mijadala ikiendelea baadhi ya viongozi wa chama hicho, 
akiwamo Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Godbless Lema walimtuhumu 
Mwigamba kutuma ujumbe kwenye mtandao huo, uliokuwa ukizungumzia ufisadi
 ndani ya chama hicho, wakidai alitaka Mwenyekiti Mbowe kukubali 
kuchunguzwa.
Akizungumza
 na Mwananchi Jumapili jana, Mwigamba alisema kuwa baada ya Lema kutoa 
tuhuma hizo aliungwa mkono na viongozi wengine na vijana waliokuwa 
wameimarisha ulinzi, kumvamia na kuanza kumpiga pamoja na kumnyang'anya 
kwa nguvu kompyuta mpakato (Laptop), aliyokuwa nayo, kisha kumpeleka 
Kituo Kikuu cha Polisi, mjini Arusha.
"Wamenipiga
 sana na kuniweka ndani, ila nashukuru Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya ya 
Arusha (OCCID), alikuja na kunitoa saa 5:00 asubuhi," alisema Mwigamba.
Alisema 
kuwa leo katika mkutano wake na waandishi wa habari ataeleza yote 
yaliyotokea na hatua atakazochukua, kwa kuwa yeye ni kiongozi wa juu wa 
chama.
Hata hivyo, alieleza kwamba bado anashauriana na wanasheria wake kuona kama anaweza kuwachukulia hatua waliompinga.
Kauli ya polisi
Kamanda 
wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas alisema polisi wameona hakuna 
kosa la kisheria lililotokea hasa kutokana na malalamiko yaliyofikishwa 
kwao dhidi ya Mwigamba ya kukichafua chama kwenye mitandao.
"Hili 
suala la mitandao ni kubwa na lina taratibu zake sasa kusema tu 
umechafuliwa na iwe kesi nadhani uchunguzi unahitajika kwao, sisi 
tumeona haya ni mambo yao wanaweza kuyamaliza wao ndiyo sababu 
tulimwachia, Mwigamba," alisema Sabas.
Kosa analodaiwa kufanya Mwigamba
Akizungumzia
 sakata hilo jana, Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema alisema kwamba 
Mwigamba alibainika kutuma ujumbe kwenye mtandao wa Jamii Forums 
uliokichafua chama hicho, akieleza haikuwa mara yake ya kwanza kwa 
kiongozi huyo kufanya hivyo na kwamba walikuwa wakimfuatilia kwa muda 
mrefu.
"Kilichotokea
 ni hicho, vijana wa Red Brigade ndio waliomtoa ukumbini, baada ya 
kumbaini kukichafua chama, kwani laptop yake baada ya kuchunguzwa na 
wataalamu wetu walijiridhisha ni yeye ndiye aliyetuma ujumbe huo," 
alisema Lema.
Katibu wa
 Chadema Kanda ya Kaskazini, Amani Golugwa alitaja tuhuma zinazomkabili 
Mwigamba kuwa ni pamoja na kusema uongo, kupotosha taarifa za chama na 
kuchonganisha viongozi kupitia mtandao wa kijamii ya Jamii Forums.
Katika 
andiko lake kwenye mtandao, Mwigamba anadaiwa kuwatuhumu viongozi wa juu
 wa Chadema akiwamo Mwenyekiti wa Taifa, Freeman Mbowe na Katibu Mkuu, 
Dk Wilbrod Slaa kuwa wamechakachua katiba ya chama hicho kuhusu ukomo wa
 nafasi za uongozi ili kujinufaisha binafsi.
Golugwa 
alisema kuwa baada ya kubanwa kwenye kikao, Mwigamba alikiri kuandika na
 kurusha taarifa hizo kwenye mitandao, lakini alipotakiwa kukabidhi 
kompyuta yake ili ichunguzwe na wataalamu wa mawasiliano wa chama hicho 
aligoma, hali iliyozua tafrani kati yake na walinzi wa chama hicho (Red 
Brigade), waliolazimika kutumia nguvu kumdhibiti.
Purukushani zilivyotokea
Habari 
zaidi zinaeleza kuwa katika harakati za kutaka kumnyang'anya Mwigamba 
kompyuta yake, mwenyekiti huyo wa Chadema mkoani Arusha alianza 
kushambuliwa na baadhi ya viongozi wa Chadema, kabla ya kufanikiwa 
kumdhibiti.
Zinaeleza
 kuwa katika tukio hilo kulitokea pia kurushiana maneno na matusi ya 
nguoni kati yake na viongozi wengine wa chama hicho akiwamo Lema.
Baadaye Lema aliliambia gazeti hili kwamba katika purukushani hizo Mwigamba alimrushia ngumi ambayo hata hivyo aliikwepa.
Alisema kuwa wanakusudia kumfungulia kesi Mwigamba ya kukichafua chama chao katika mitandao ya kijamii.
Hata 
hivyo, alisema kikao chao kiliendelea jana bila ya vurugu zozote na 
kuweka mikakati ya kushinda majimbo yote ya Kanda ya Kaskazini mwaka 
2015 na kuchukua nchi katika uchaguzi huo ujao.
Adhabu kwa Mwigamba
Katika 
hatua nyingine Chadema, kimemsimamisha uongozi Mwigamba kwa tuhuma za 
kukisaliti, kukihujumu chama hicho na viongozi wake.
Akitangaza
 uamuzi huo mbele ya waandishi wa habari jijini Arusha jana, Mwenyekiti 
wa Chadema Kanda ya Kaskazini, Israel Natse alibainisha kuwa uamuzi wa 
kumsimamisha Mwigamba katika nyadhifa zote za uongozi ndani ya chama 
ulifikiwa na kikao cha Baraza la Uongozi wa Kanda ya Kaskazini 
kilichokutana juzi.
Alisema 
kuwa Mwigamba amesimamishwa kwa muda usiojulikana kupisha uchunguzi wa 
tuhuma dhidi yake na kuonya kuwa iwapo tuhuma zitathibitishwa, hatua 
nyingine za kinidhamu zitafuata kulingana na kanuni na katiba ya 
Chadema.
"Kwa sasa
 Mwigamba anatuhumiwa kuvunja sura ya kumi, kifungu cha 10.1 kifungu 
kidogo cha 8, 9 na 10 ya katiba ya Chadema inayozungumzia maadili ya 
uongozi," alisema Natse.
Akifafanua
 zaidi alisema kuwa sura na vifungu hivyo vinakataza kiongozi wa chama 
hicho kutoa tuhuma dhidi ya viongozi wenzake bila kufuata vikao halali 
vya kikanuni na kikatiba.
