WAKATI Mkutano Mkuu wa Nane wa Uchaguzi wa Umoja wa Vijana (UVCCM) 
ukimalizika, mmoja wa wagombea wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya 
chama hicho nafasi sita Tanzania Bara, Stanley Mdoe, ametiwa mbaroni na 
Polisi akibainika kuwa askari Polisi.
Askari
 huyo mwenye namba F 7961 wa cheo cha Konstebo, anatoka kituo cha Polisi
 Mvomero, Morogoro ambaye alibainika jana akijihusisha na siasa hata 
kuingia kinyang’anyiro cha kuwania ujumbe wa NEC kupitia Vijana.
Kwa
 mujibu wa habari zilizopatikana Morogoro, askari huyo alijitambulisha 
kwa baadhi ya wajumbe kuwa yeye ni mtoto wa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, 
Joel Bendera, akijiita Stanley Bendera.
Wapambe
 waliofuatana naye kutoka Morogoro wakiwa Dodoma waliarifu kuwa mgombea 
huyo alikamatwa juzi jioni akiwa amevalia sare za chama hicho akiomba 
kura kwa wajumbe ili wamchague kwa nafasi hiyo.
Hata
 hivyo, ilielezwa na baadhi ya wanachama waliofuatana naye na wengine 
wanaotambua kazi yake uaskari, waliwajulisha maofisa usalama waliokuwa 
eneo hilo nao kufikisha taarifa hizo Polisi na kukamatwa.
Kwa mujibu wa vyanzo vya habari, askari huyo alikuwa ameomba likizo isiyo na malipo, wakati wengine wakidai kuwa ameacha kazi.
Kamanda
 wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile akizungumzia tukio 
hilo alisema alipata taarifa ya kukamatwa kwa askari huyo Dodoma na 
kwamba wakati huo alikuwa akimtafuta kwa siku mbili kwa ajili ya 
shughuli za kikazi bila mafanikio.
“Sina
 uhakika kama askari huyu amejiingiza katika siasa ... nimetuma askari 
wengine kwenda Dodoma kufanya uchunguzi wa suala hilo,” alisema Kamanda 
Shilogile na kuongeza:
“Iwapo
 itabainika kuwa kweli, atachukuliwa hatua stahiki na kinidhamu 
kulingana na taratibu za kijeshi. Hata hivyo siwezi kuzungumzia suala la
 ugombeaji wake, sijathibitisha ukweli wake, isipokuwa hakuwa kazini kwa
 siku mbili na ni utovu wa nidhamu kwa Jeshi letu kutoonekana eneo la 
kazi,” alisema Kamanda Shilogile.
Kwa
 mujibu wa Kamanda, sheria za nchi na Katiba kuna vifungu vinavyohusu 
majeshi ya ulinzi na usalama vikitamka kuzuia na kupiga marufuku 
mwanajeshi kujihusisha na siasa.
Alisema
 iwapo jambo hilo litabainika, litakuwa limefanyika kinyume na kanuni na
 taratibu za kazi ya uaskari. Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Bendera, 
hakupatikana ofisini kwake wala kwa njia ya simu ya mkononi ili 
kufafanua kadhia hiyo.
Hata hivyo wasaidizi wake walidai kuwa yuko nje ya nchi kwa shughuli za kikazi.