Sheikh Farid Katikati ya Askari Magereza.
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Hellen Liwa amejitoa kusikiliza kesi ya ugaidi inayowakabili viongozi 23 wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar (JUMIKI).
Hakimu huyo amefikia uwamuzi huo baada ya wakili wa washtakiwa hao wa ugaidi, Abubakar Salim kumtaka ajitoe 
kuisikiliza kesi hiyo ili iweze kupangiwa hakimu mwingine ambaye atatoa 
uamuzi juu ya hoja zao walizozitoa mahakamani hapo Septemba 19,2014.
Salim 
aliiambia mahakama kuwa baada ya kushauriana na wateja wao na uamuzi 
uliotolewa na Jaji wa Mahakama Kuu, Dk Fauzi Twaib wakaona kuwa ni 
ukweli kuwa Hakimu Liwa alikwisha toa uamuzi wake juu ya hoja zao Oktoba
 Mosi, 2014 kuwa mahakama hiyo ya kisutu haina mamlaka ya kusikiliza hoja hizo.  
Alidai 
Mahakama Kuu katika uamuzi wake uliotolewa na Jaji Twaib umeelekeza kuwa
 Mahakama ya Kisutu inayo mamlaka ya kuzisikiliza hoja za washtakiwa hao
 wa ugaidi na hata kuzitolea uamuzi.
"Mahakama
 Kuu imeelekeza mawakili wa upande wa utetezi kama tutakuwa na hoja mpya
 ama  zile za awali tuzitoe kwenye mahakama hii ya Kisutu ili ziweze 
kutolewa maamuzi hivyo naona ni bora ujitoe tupate neno kutoka kwa 
hakimu mwingine."Alisisitiza kusema wakili huyo mahakamani hapo.
Wakili wa
 Serikali Mkuu, Benard Kongola alimuomba Hakimu Liwa asijitoe katika 
kuisikiliza kesi kwa madai sababu zilizotolewa na upande wa utetezi za 
kumtaka ajitoe hazina msingi.
Kongola 
alieleza kuwa uamuzi uliotolewa na Jaji Twaib aliamuru utekelezaji wa 
hoja za upande wa utetezi katika kesi hii ya ugaidi zisikilizwe na 
kutolewa uamuzi katika Mahakama ya Kisutu.
"Tukiendekeza
 hii tabia tutamaliza mahakimu wote wa mahakama hii tunasisitiza upande 
wa utetezi utoe sababu za msingi za wewe kujitoa."Alisema Kongola.
Akijibu 
hoja hizo, Wakili Salim alieleza kuwa ili haki ionekane inatendeka wewe 
Hakimu Liwa ujitoe ili hakimu mwingine atoe maamuzi wa hoja zetu.
Hakimu 
Liwa alisema ni kweli nilikwisha toa uamuzi wangu juu ya maombi ya 
washtakiwa lakini Mahakama Kuu imeona kivingine kuwa sijatumia mamlaka 
yangu vizuri nakubaliana na uamuzi huo.
Lakini 
uamuzi huo wa Jaji Twaib haukufafanua nini kifanyike, umetuacha hoi, ila
 alitoa angalizo kuwa ushahidi wa kesi hauwezi kutoka hewani na kwamba 
maelezo yaliyomo katika hati ya mashtaka ya kesi hiyo yapo sahihi.
"Kitu 
ambacho hata mimi nilikuwa nakishangaa ni hii hati ya mashtaka kuletwa 
Tanzania Bara badala ya Visiwani, lakini nilipoisoma sheria ya ugaidi 
nikabaini mtu anaweza kushtakiwa mahali popote." Alisema Hakimu 
Liwa.Alisisitiza kuwa kwa mujibu wa sheria Mahakama Kuu ndiyo yenye 
uwezo wa kuisikiliza kesi hii na siyo mahakama ya Kisutu hivyo yeye 
hawezi kusema kitu labda kesi ingekuwa imefikia kwenye mwenendo wa 
uhamishaji shauri (Committal Preceding).
Hatua 
hiyo inafikiwa baada ya upelelezi wa kesi kukamilika inahamishwa kutoka 
mahakama ya Kisutu kwenda Mahakama Kuu ambayo inamlaka ya kusikiliza 
kesi hizo.
"Mimi 
nimejifunza kitu hapa, kuwa mimi najua nini na wenzangu wanajua nini 
hivyo siwezi kuendelea na kesii haitakuwa haki najitoa."Aliongeza kusema
 Hakimu Liwa na akajitoa na kuiahirisha hadi Januari 13,2015 ili ipangwe
 kwa hakimu mwingine.
