Utajiri, safari zake nje ya nchi vyatiliwa shaka
*Ahusishwa na mtandao hatari wa Masogange
KWA  mara ya kwanza tangu lilipoibuka sakata la watu maarufu kujihusisha
  ama  na utumiaji au usafirishaji wa dawa za kulevya, jina la  
mwanamuziki  anayeaminika kuwa na ukwasi mkubwa kwa sasa hapa nchini,  
Nasseeb  Abdulmaliki, maarufu zaidi kwa jina la Diamond, limeanza  
kutajwa kuwa ni  miongoni mwa vigogo wa dawa hizo.
Tayari mjadala mkubwa wa chini  chini umeibuka kwa watu mbalimbali  
wakiwemo mashabiki wake, na taarifa  ambazo zimelifikia MTANZANIA  
Jumatano kutoka vyanzo mbalimbali zimedai  kuwa, mwenendo wa maisha ya  
Diamond sasa unachunguzwa na baadhi ya  maofisa wa vyombo vya dola vya  
ulinzi na usalama.
Kutajwa kwa  jina la Diamond katika sakata hili, kunatiwa nguvu zaidi na
  mwenendo  binafsi wa maisha wa msanii huyo maarufu wa muziki wa kizazi
  kipya,  unaokwenda sambamba na ukwasi mkubwa alioupata katika kipindi 
 kifupi.    
Kama hiyo haitoshi, safari za nje ya nchi za mwanamuziki huyo   
unaohusisha ziara zake nchini Afrika Kusini na Uingereza, pia ni mambo  
 ambayo yamechochea wingu la mashaka lililofikia hatua ya jina lake   
kuingizwa katika mtandao huo ambao katika siku za karibuni, umewagusa   
pia baadhi ya watu wenye majina makubwa katika jamii.
Kuhusu  ziara hizo, kilicholeta mshtuko na dukuduku dhidi yake ni kuwapo
  kwa  taarifa kwamba, katika moja ya ziara hizo za nje ya nchi, Diamond
   alifikia hatua ya kusafiri akitumia chumba kinachotumiwa na wageni   
mashuhuri (VIP), badala ya njia ya wasafiri wa kawaida.
Mbali na  hilo, taarifa nyingine zinaeleza kwamba, mizigo ya msanii huyo
  ambaye  mara kadhaa amekuwa akisafiri na kundi la wacheza shoo wake,  
imekuwa  ikipita pasipo kupitishwa katika hatua za ukaguzi kwa namna ile
  ile  ilivyokuwa kwa mabinti wawili wa Kitanzania walionaswa nchini  
Afrika  Kusini baada ya kuruka mfumo wa ukaguzi wa JNIA. 
Aidha, ukaribu  wa kimahusiano kati ya Diamond na baadhi ya Watanzania  
wanaoishi nchini  Afrika Kusini na ambao majina yao pia yameanza  
kuhusishwa na biashara  hiyo ya mihadarati, ni jambo jingine ambalo  
limechochea harakati za  kufuatiliwa kwa karibu kwa nyendo za Diamond.
Taarifa zaidi  kutoka JNIA zinaeleza kwamba, miongoni mwa watu wanaoweza
  wakawa  wamemponza Diamond ni wale ambao walionekana kuwa karibu na  
Agness  Gerald ‘Masogange’ (25) na Melisa Edward (24), siku walipokuwa  
 wakisafiri kwenda Afrika Kusini kabla hawajanaswa katika uwanja wa 
Ndege   wa Oliver Thambo jijini Johannesburg nchini Afrika Kusini, 
wakiwa na   shehena ya dawa za kulevya.
Mwenendo wa watu hao unatiliwa shaka  kuwa huenda ni miongoni mwa  
wafanyabiashara wakubwa wa dawa za kulevya  wenye maskani yao nchini  
Afrika Kusini, kwa sababu mbali na ukaribu na  wasichana hao, pia  
walihusika kwa karibu kuusafirisha mwili wa  mwanamuziki Albert  
Mangwair, aliyefia huko huko Afrika Kusini ambaye  taarifa za kufa kwake
  ziligumbikwa na matumizi ya dawa za kulevya. 
Alipoulizwa  jana na MTANZANIA Jumatano kupitia simu yake ya kiganjani  
kuhusu  taarifa hizo na iwapo amekwishahojiwa na vyombo vya dola baada  
ya jina  lake kuanza kutajwa kuwa miongoni mwa orodha ya wasanii wa  
muziki  wanaosafirisha dawa za kulevya, Diamond alikiri kuwa na pesa za 
 kutosha  kuishi maisha anayoyataka, lakini akakana kujihusisha na  
biashara hiyo.
Akifafanua  tuhuma moja baada ya nyingine kwa mpangilio aliokuwa  
akiulizwa na  gazeti hili, Diamond alisema katika maisha yake, hajawahi 
 kujihusisha na  utumiaji au usafirishaji dawa za kulevya, lakini madai 
 hayo yamekuwa  yakitolewa dhidi yake na watu ambao hawajui siri ya  
mafanikio yake.
“Kazi  ngumu siku zote inalipa, sasa napata matunda ambayo yanatokana na
  kile  nilichokifanya, iweje watu wanitilie mashaka, Watanzania ni  
mashahidi  wangu wananiona navyochumia juani, nitaendelea kulia kivulini
  tu kwani  nakula kwa jasho langu.
“Siyo kweli kwamba mizigo yangu  haikukaguliwa na kama haikukaguliwa na 
 ingekuwa na kasoro, basi  Uingereza wangenitia hatiani, nilipita na  
nilikaguliwa.” Alisema  Diamond.
Alipoulizwa kuhusu taarifa za kuwa mwanamtandao wa kundi  la Masogange, 
 pia alikanusha kwa kueleza kuwa hata siku aliyosafiri  kwenda Afrika  
Kusini alikwenda peke yake uwanja wa ndege na kuongeza  kuwa alikwenda  
huko kwa shughuli za kimuziki, ambapo safari nzima  iligharimu zaidi ya 
 Dola 30,000 za Kimarekani.
“Afrika Kusini  nimekwenda kufanya kazi zangu na safari hiyo  
imenigharimu zaidi ya Dola  30,000, nilikwenda kurekodi nyimbo yangu  
mpya inayoitwa namba moja  ambayo itaanza kusikika hivi karibuni.
“Unajua Watanzania sasa  hivi wanajua mtu hawezi kufanikiwa au kupata  
maendeleo bila kuuza  ‘unga’, hili si sawa juhudi za mtu ndizo  
zinamfikisha alipo, na mimi  juhudi zangu ndio zinanifikisha hapa, watu 
 waache kunijadili vibaya.”  Alisema Diamond.
Kuibuka kwa taarifa hizi kumekuja ikiwa ni  takribani miezi miwili sasa 
 tangu Watanzania wawili, Agness Gerald  ‘Masogange’ (25) na Melisa  
Edward (24), waliokuwa na uhusiano wa karibu  na baadhi ya wanamuziki  
maarufu hapa nchini, kukamatwa nchini Afrika  Kusini wakiwa na dawa za  
kulevya aina ya Crystal Methamphetamine zenye  thamani ya Sh bilioni  
6.8.
Mbali na kuwa na uhusiano wa karibu na  wanamuziki, Edward anadaiwa kuwa
  alikuwa mfanyakazi katika mgahawa  mmoja maarufu jijini Dar es Salaam,
  unaomilikiwa na mmoja wa vijana  matajiri hapa nchini ambaye hata 
hivyo  gazeti hili halijafanikiwa  kumpata ili kufanya naye mahojiano.
Wakati huo huo, tayari hatua  za kinidhamu zimekwishaanza kuchukuliwa  
dhidi ya wafanyakazi wa JNIA  waliohusika kupitisha kilo 150 za dawa za 
 kulevya, ambao Waziri wa  Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, ametaja  
majina yao hivi karibuni na  kuonyesha kwa waandishi wa habari ushahidi 
 wa kuhusika kwao.
CHANZO:
JAMII FORUMS