Watu wawili wanahofiwa kupoteza maisha na wengine wengi kujeruhiwa
kutokana na mlipuko wa bomu lililolipuka kwenye mkutano wa CHADEMA
katika eneo la Soweto, kata ya Kaloleni jijini Arusha, wakati wa kufunga
kampeni za uchaguzi wa madiwani katika maeneo ya jiji hilo.
Waliojeruhiwa
wamekimbizwa katika hospitali za Seliani na Mount Meru ambapo baadhi ya
watu wamejitolea vyombo binafsi vya usafiri na wengine wanashirikiana
na Madaktari na Wauguzi wa hospitali hizo kutoa huduma ya kwanza.
Kamanda wa polisi mkoani humo, Liberatus Sabas yupo katika moja ya hospitali hizo.
Bomu
hilo linaelezwa kuwa lilipuka kwenye mkusanyiko wa watu meta chache
kutoka jukwa kuu, mwendo wa saa kumi na mbili na robo jioni wakati
mkutano huo ulipokuwa umekwisha na shughuli ya kukusanya michango
ikiendelea.
Viongozi wa juu wa CHADEMA, Freeman Mbowe na Godbless Lema walikuwepo na wameendelea kuwepo kwenye eneo hilo.
Polisi
wapo katika eneo hilo wakijitahidi kutuliza ghasia lakini inasemekana
upo upinzani mkubwa kutoka kwa wananchi wanaojaribu kuwafukuza, hali
iliyowalazimu kupiga mabomu ya machozi na kukamata watu kadhaa wakiwemo
viongozi wa CHADEMA. Mwandishi mmoja wa habari anaripotiwa kunyang’anywa
kamera yake baada kwa kupiga picha, hata baada ya kujitambulisha.
Watu
wenye hasira wanaripotiwa kuyashambulia na kuyaharibu baadhi ya magari
ya kutoa huduma ya kwanza (ambulance) kwa kuwa yalichelewa kufika
kuwaokoa majeruhi.
ILANI: Baadhi
ya picha zilizopachikwa hapo huenda zikagusa hisia ya mtizamaji,
tafadhali ikiwa huwezi kuvumilia kuona damu usibofye kitufye cha kuelekea mbele