Serikali imeingilia kati sakata la
uchaguzi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa kuamuru kufutwa kwa
katiba ya sasa ya shirikisho hilo na badala yake kuamuru itumike katiba
ya zamani (mwaka 2006) baada ya kubaini kuwa iliyopo ina kasoro nyingi.
Katika
taarifa yake kwa waandishi wa habari leo, Wizara ya Habari, Utamaduni,
Vijana na Michezo imeeleza kuwa katiba ya sasa ya TFF si halali.
Imeelezwa vilevile kuwa msajili wa vyama vya michezo aliyedaiwa
kuipitisha katiba hiyo ameondolewa.
Mchakato wa uchaguzi mkuu wa
TFF umesimamishwa kutokana na mgogoro mzito uliotokana na kuenguliwa
kiutata kwa wagombea kadhaa, wakiwamo Jamal Malinzi anayewania urais na
Michael Wambura anayetaka kugombea nafasi ya makamu wa rais.
Kamati
ya rufani ya TFF inayoongozwa na Iddi Mtiginjola ndiyo iliyozua balaa
lote la sasa baada ya kuwaengua kina Malinzi na mwishowe kumuacha makamu
wa sasa wa rais, Athumani Nyamlani abaki kuwa mgombea pekee.
Hata
hivyo, tayari mchakato wa uchaguzi huo uliozua mabishano makali
umeshasimamishwa na Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA) na maafisa wa
chombo hicho cha juu cha mchezo wa soka duniani wameshaanza kuwasili
kufuatilia kinachotokea nchini.
Uamuzi wa serikali wa kufuta
katiba ya sasa na kutaka itumike ya 2006 unampa ahueni kubwa Wambura
ambaye alishasema hadharani kuwa ataiburuza TFF mahakamani kama
isipoachana na katiba mpya na kufuata ya zamani; huku akitoa sababu
kadhaa za kupinga matumizi ya katiba mpya, mojawapo ikiwa ni kupitishwa
kwake kwa njia ya waraka wa barua pepe (e-mail) kwenda kwa wajumbe
badala ya kufuata maelekezo ya katiba yanayotaka mabadiliko kufanywa na
wajumbe kupitia mkutano mkuu.
Hata hivyo, kwa mujibu wa taratibu
za FIFA, ni marufuku kwa shughuli za soka kuingiliwa na serikali au
mahakama na nchi yoyote inayokwenda kinyume na taratibu hizo hujikuta
ikifungiwa kama ilivyowahi kutokea nchini Kenya.