MSHAMBULIAJI wa Yanga, Said Bahanuzi
amesema anafikiri kwa sasa amerudi kwenye fomu isipokuwa tu kocha ndiye
anashindwa kumwamini kuanza kikosi cha kwanza.
Kocha wa Yanga, Mholanzi Ernie Brandts amekuwa akimtumia Bahanuzi kama mchezaji wa akiba tangu aliporejea uwanjani.
Bahanuzi aliyejiunga na Yanga msimu
huu akitokea Mtibwa Sugar ya Morogoro alikuwa anasumbuliwa na maamivu ya
nyama za paja aliyoyapata akiwa na timu ya Taifa Stars mwaka jana.
Katika mechi mbili za ligi ambazo nyota
huyo ametokea benchi zikiwa zimebaki dakika 15 kabla ya mchezo
kumalizika amefanikiwa kutoa pasi ya bao kila mechi.
Mchezo dhidi ya Mtibwa Sugar
uliopigwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam Bahanuzi ndiye
aliyetoa pasi kwa Hamis Kiiza kufunga bao la kusawazisha. Timu zote
mbili zilifungana bao 1-1.
Pia, mchezo wa African Lyon
uliochezwa Jumatano Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Bahanuzi akitokea
benchi alitoa pasi kwa Nizar Khalfan aliyefunga bao la tatu wakati Yanga
ikishinda 4-0.
Mara zote anapoingia mshambuliaji
huyo mwenye nguvu za miguu na uwezo wakufyatua mashuti makali, amekuwa
akiichangamsha safu ya ushambuliaji ya Yanga tofauti alivyokuwa benchi.
"Kwa sasa nafikiri nimerejea kwenye
fomu. Nafikiri kocha tu ndiye anashindwa kuniamini." alisema Bahanuzi
mwenye bao moja kwenye ligi alilofunga kwa penalti dhidi ya Simba Oktoba
3, mwaka jana.
"Nilikuwa nasumbuliwa na maumivu ya nyama za paja. Kwa sasa nafikiri hali yangu imeimarika kama awali." alisisitiza.
Kwa upande wake Ernie Brandts
alisema; "Siwezi kumchezesha dakika 90. Nadhani Bahanuzi ametoka kwenye
majeruhi. Kwa hiyo nimekuwa nikimpa dakika 15 za mwisho kutizama
maendeleo yake.
"Nafikiri ameimarika kwa mechi mechi ambazo nimemuona akicheza."